Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Mtume Paulo alimaanisha nini kwa maneno “maandamano yenye shangwe”?

Paulo aliandika hivi: “Mungu . . . hutuongoza katika maandamano yenye shangwe ya ushindi kwa kushirikiana na Kristo naye huifanya harufu ya ujuzi juu yake yeye ifahamike kupitia sisi kila mahali! Kwa maana kwa Mungu sisi ni harufu tamu ya Kristo katikati ya wale wanaookolewa na katikati ya wale wanaoangamia; kwa hawa wa mwisho ni harufu inayotoka katika kifo mpaka kifo, kwa wale wa kwanza ni harufu inayotoka katika uzima mpaka uzima.”—2 Wakorintho 2:14-16.

Paulo alikuwa akirejelea zoea la Waroma la kumfanyia sherehe za maandamano jemadari ambaye alikuwa amewashinda maadui wa Taifa. Katika sherehe za maandamano kama hizo, kulikuwa na maonyesho ya hadharani ya wafungwa wa vita pamoja na nyara zilizokusanywa vitani na ng’ombe-dume ambao wangetolewa kama dhabihu huku jemadari aliyepata ushindi pamoja na jeshi lake wakisifiwa na raia. Maandamano hayo yalipoisha, ng’ombe-dume hao walichinjwa na huenda wengi wa wafungwa hao waliuawa.

Kitabu kimoja cha marejeo (The International Standard Bible Encyclopedia) kinasema kuwa maneno “harufu tamu ya Kristo” yanayotumiwa kuonyesha kuwa watu fulani wangekufa na wengine kuendelea kuishi, ‘huenda yanatokana na zoea la Waroma la kuvukiza uvumba wakati wa maandamano hayo. Harufu ya uvumba ambayo iliwakilisha ushindi kwa jemadari na jeshi lake, iliwakumbusha wale wafungwa, kuhusu kifo ambacho huenda kingewapata.’ *

Ni nini kilichomaanishwa na “mahali pa juu” ambapo panatajwa mara kwa mara katika Maandiko ya Kiebrania?

Wakati wana wa Israeli walipokuwa karibu kuingia katika Nchi ya Ahadi, Yehova aliwaambia waondolee mbali mahali pote pa ibada ya Wakanaani ambao waliishi huko. Aliwaamuru hivi: “Mutaharibu mawe yao yote ya kuchorwa sanamu, na kuharibu sanamu zao zote za kuyeyusha, na kuharibu pahali pao pa juu [au, mahali pa juu] pote.” (Hesabu 33:52, Zaire Swahili Bible) Vituo hivyo vya ibada ya uwongo vilikuwa juu ya milima katika sehemu zilizo wazi au jukwaa zilizojengwa mahali penginepo kama vile chini ya miti au kwenye majiji. (1 Wafalme 14:23; 2 Wafalme 17:29; Ezekieli 6:3) Vituo hivyo vilikuwa na madhabahu, nguzo takatifu, sanamu, vinara vya uvumba, au vitu vingine vilivyotumiwa katika ibada ya uwongo.

Kabla ya kujengwa kwa hekalu huko Yerusalemu, Waisraeli walimwabudu Yehova katika sehemu zilizokubalika ambazo pia zinaitwa mahali pa juu katika Maandiko. Nabii wa Mungu Samweli alitoa dhabihu kwenye “mahali pa juu,” katika jiji lisilotajwa jina lililokuwa katika nchi ya Sufu. (1 Samweli 9:11-14) Hata hivyo, baada ya hekalu kujengwa wafalme kadhaa ambao walikuwa waaminifu kwa Yehova walijaribu kuondoa “mahali pa juu” nchini Israeli.—2 Wafalme 21:3; 23:5-8, 15-20; 2 Mambo ya Nyakati 17:1, 6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kwa maelezo kuhusu maana ya kiroho ya mfano huo wa Paulo, ona Mnara wa Mlinzi, Novemba 15, 1990 (15/11/1990), ukurasa 27.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Sehemu ya mchoro ukionyesha maandamano yenye shangwe ya Waroma katika karne ya pili W.K.

[Hisani]

Photograph taken by courtesy of the British Museum

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mabaki ya nguzo takatifu, Gezeri