Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Yesu Anavyoutukuza Uadilifu wa Mungu

Jinsi Yesu Anavyoutukuza Uadilifu wa Mungu

Jinsi Yesu Anavyoutukuza Uadilifu wa Mungu

“Mungu alimweka [Kristo] kuwa toleo la kupatanisha kupitia imani katika damu yake. Ilikuwa hivyo ili kuonyesha wazi uadilifu wake mwenyewe.”—ROM. 3:25.

1, 2. (a) Biblia inafundisha nini kuhusu hali ya wanadamu? (b) Ni maswali gani yatakayozungumziwa katika habari hii?

SIMULIZI la Biblia kuhusu uasi katika bustani ya Edeni linajulikana sana. Sisi sote tunapatwa na matokeo ya dhambi ya Adamu kama inavyoelezwa na maneno haya: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Rom. 5:12) Hata tukijitahidi kadiri gani kufanya yaliyo sawa, tunafanya makosa, na hivyo tunahitaji msamaha wa Mungu. Hata mtume Paulo alilalamika hivi: “Lile jema ninalotaka silifanyi, bali lile baya nisilotaka ndilo ninalozoea kulifanya. Maskini mimi!”—Rom. 7:19, 24.

2 Kwa kuwa kiasili sisi sote ni wenye dhambi, ni jambo la akili kujiuliza maswali haya ya maana: Iliwezekana jinsi gani Yesu wa Nazareti azaliwe bila kurithi dhambi, na kwa nini alibatizwa? Maisha ya Yesu yalitukuza uadilifu wa Yehova jinsi gani? Na swali la maana zaidi ni hili: Kifo cha Kristo kilitimiza nini?

Uadilifu wa Mungu Unatiliwa Shaka

3. Shetani alimdanganya Hawa jinsi gani?

3 Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walikataa kwa upumbavu enzi kuu ya Yehova na wakakubali kutawaliwa na “yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani.” (Ufu. 12:9) Ona jinsi hilo lilivyotukia. Shetani alitilia shaka uadilifu wa njia ya Yehova Mungu ya kutawala. Alifanya hivyo kwa kumuuliza Hawa hivi: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” Hawa alirudia kutaja amri ya Mungu iliyokuwa wazi ya kwamba hawakupaswa kugusa mti fulani, ili wasife. Kisha Shetani akamshtaki Mungu kuwa mwongo. “Hakika hamtakufa,” akasema Ibilisi. Akamdanganya Hawa ili aamini kwamba Mungu alikuwa amewaficha kitu fulani kizuri na kwamba kwa kula tunda hilo, Hawa angekuwa kama Mungu, na kuwa na uhuru wa kujiamulia mambo.—Mwa. 3:1-5.

4. Wanadamu walikuja jinsi gani kuwa chini ya utawala wa mpinzani Shetani?

4 Kwanza, Shetani alidai kwamba wanadamu wangekuwa na furaha zaidi kwa kuishi bila kumtegemea Mungu. Badala ya kuunga mkono uadilifu wa enzi kuu ya Mungu, Adamu alimsikiliza mke wake na akajiunga naye katika kula tunda lililokatazwa. Hivyo, Adamu akapoteza msimamo wake mkamilifu machoni pa Yehova na akatuleta chini ya nira yenye ukatili ya dhambi na kifo. Wakati huohuo, wanadamu walikuja kuwa chini ya utawala wa mpinzani Shetani, ambaye ni “mungu wa ulimwengu huu.”—2 Kor. 4:4; King James Version; Rom. 7:14.

5. (a) Yehova alithibitika jinsi gani kuwa mwaminifu kwa neno lake? (b) Ni tumaini gani ambalo Mungu aliwapa wazao wa Adamu na Hawa?

5 Kupatana na neno lake lisilokosea, Yehova alitoa hukumu ya kifo kwa Adamu na Hawa. (Mwa. 3:16-19) Lakini hilo halikumaanisha kwamba kusudi la Mungu lilikuwa limeshindwa. Hapana! Alipokuwa akiwahukumu Adamu na Hawa, Yehova aliwapa tumaini zuri ajabu wazao wao ambao wangezaliwa baadaye. Alifanya hivyo kwa kutangaza kusudi lake la kutokeza “uzao” ambao Shetani angeuumiza au kuutia jeraha kwenye kisigino. Hata hivyo, Uzao huo ulioahidiwa ungepona jeraha hilo la kisigino nao ‘ungemponda Shetani kichwa.’ (Mwa. 3:15) Biblia inaeleza zaidi kuhusu habari hiyo kwa kusema yafuatayo kumhusu Yesu Kristo: “Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alifunuliwa, yaani, ili azivunje kazi za Ibilisi.” (1 Yoh. 3:8) Lakini mwenendo na kifo cha Yesu vilitukuza jinsi gani uadilifu wa Mungu?

Maana ya Ubatizo wa Yesu

6. Tunajua jinsi gani kwamba Yesu hakurithi dhambi kutoka kwa Adamu?

6 Akiwa mtu mzima, Yesu alilingana kabisa na Adamu alipokuwa mkamilifu. (Rom. 5:14; 1 Kor. 15:45) Hilo linamaanisha kwamba Yesu alipaswa kuzaliwa akiwa mkamilifu. Jambo hilo liliwezekana jinsi gani? Malaika Gabrieli alimweleza hivi waziwazi Maria, mama ya Yesu: “Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu za Aliye Juu Zaidi zitakufunika. Kwa sababu hiyo pia kile kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35) Mapema katika maisha ya Yesu, inaelekea Maria alimfunulia Yesu mambo fulani kuhusu kuzaliwa kwake. Hivyo, pindi moja Maria na Yosefu, baba mlezi wa Yesu, walipompata Yesu ndani ya hekalu la Mungu, mtoto huyo mchanga aliwauliza hivi: “Je, hamkujua kwamba ni lazima niwe katika nyumba ya Baba yangu?” (Luka 2:49) Bila shaka, tangu akiwa na umri mchanga, Yesu alijua kwamba yeye ni Mwana wa Mungu. Hivyo, jambo la maana zaidi kwake lilikuwa ni kuutukuza uadilifu wa Mungu.

7. Yesu alikuwa na vitu gani vyenye thamani?

7 Yesu alionyesha kwamba alipendezwa sana na mambo ya kiroho kwa kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya ibada. Akitumia akili yake kamilifu, inaelekea alielewa kila jambo alilosikia na kusoma katika Maandiko ya Kiebrania. (Luka 4:16) Alikuwa pia na kitu kingine chenye thamani, yaani, mwili mkamilifu wa kibinadamu ambao ungeweza kutolewa dhabihu kwa ajili ya wanadamu. Alipobatizwa, Yesu alikuwa akisali na huenda alikuwa akitafakari kuhusu maneno ya kinabii ya Zaburi 40:6-8.—Luka 3:21; soma Waebrania 10:5-10. *

8. Kwa nini Yohana Mbatizaji alijaribu kumzuia Yesu asibatizwe?

8 Mwanzoni, Yohana Mbatizaji alitaka kumzuia Yesu asibatizwe. Kwa nini? Kwa sababu Yohana alikuwa akiwabatiza Wayahudi katika maji ili kuonyesha kwamba walikuwa wametubu dhambi waliyotenda kwa kuvunja ile Sheria. Akiwa mtu wa karibu wa ukoo wa Yesu, inaelekea Yohana alijua kwamba Yesu alikuwa mwadilifu na hivyo hakuhitaji kutubu. Yesu alimhakikishia Yohana kwamba ilifaa abatizwe. Yesu akaeleza hivi: “Katika njia hiyo inafaa kwetu kufanya yote yaliyo ya uadilifu.”—Mt. 3:15.

9. Ubatizo wa Yesu ulimaanisha nini?

9 Akiwa mwanadamu mkamilifu, Yesu angeweza kukata kauli kwamba yeye, kama Adamu, alikuwa na uwezo wa kuzaa jamii ya wanadamu wakamilifu. Hata hivyo, Yesu hakutamani kamwe maisha hayo kwa sababu hayo hayakuwa mapenzi ya Yehova kumwelekea. Mungu alikuwa amemtuma Yesu duniani ili atimize daraka la Uzao ulioahidiwa, au Masihi. Hilo lilitia ndani Yesu kudhabihu uhai wake mkamilifu wa kibinadamu. (Soma Isaya 53:5, 6, 12.) Bila shaka, ubatizo wa Yesu ulikuwa na maana tofauti na ubatizo wetu. Yesu hakujiweka wakfu kwa Yehova kwa sababu alikuwa tayari mshiriki wa taifa la Israeli ambalo lilikuwa wakfu kwa Mungu. Badala yake, ubatizo wa Yesu ulimaanisha kwamba alijitoa mwenyewe kufanya mapenzi ya Mungu kama ilivyoonyeshwa katika Maandiko kumhusu Masihi.

10. Kufanya mapenzi ya Mungu kama Masihi kulitia ndani nini, na Yesu alihisi jinsi gani kuhusu hilo?

10 Mapenzi ya Yehova kumhusu Yesu yalitia ndani kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, kufanya wanafunzi, na kuwatayarisha kwa ajili ya kazi ya wakati ujao ya kufanya wanafunzi. Kujitoa kwa Yesu kulitia ndani pia kuwa tayari kuvumilia mateso na kifo cha kikatili ili kuunga mkono enzi kuu yenye uadilifu ya Yehova Mungu. Kwa sababu Yesu alimpenda kwelikweli Baba yake wa mbinguni, alipendezwa kufanya mapenzi ya Mungu na aliona kutoa mwili wake uwe dhabihu kuwa jambo lenye kuridhisha sana. (Yoh. 14:31) Pia, alifurahi kujua kwamba thamani ya uhai wake mkamilifu ingeweza kutolewa kwa Mungu kuwa fidia au dhabihu ya ukombozi ili kutununua kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo. Je, Mungu alikubali hatua ya Yesu ya kujitoa ili atimize madaraka hayo makubwa? Bila shaka, alikubali!

11. Yehova alionyesha jinsi gani kwamba alimkubali Yesu kuwa Masihi aliyeahidiwa, au Kristo?

11 Waandikaji wote wanne wa Injili wanatoa ushahidi kuhusu maneno ya waziwazi ya Yehova Mungu ya kumkubali Yesu alipokuwa akitoka ndani ya maji ya Mto Yordani. Yohana Mbatizaji alitoa ushahidi huu: “Niliona roho ikishuka kama njiwa kutoka mbinguni, nayo ikakaa juu [ya Yesu] . . . Nami nimeona, na nimetoa ushahidi kwamba huyo ndiye Mwana wa Mungu.” (Yoh. 1:32-34) Zaidi ya hayo, katika pindi hiyo Yehova alitangaza hivi: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.”—Mt. 3:17; Marko 1:11; Luka 3:22.

Mwaminifu Mpaka Kifo

12. Yesu alifanya nini kwa muda wa miaka mitatu na nusu baada ya ubatizo wake?

12 Kwa muda wa miaka mitatu na nusu iliyofuata, Yesu alijitoa kabisa katika kuwafundisha watu kumhusu Baba yake na uadilifu wa enzi kuu ya Mungu. Alichoka kwa sababu alisafiri kwa miguu katika Nchi yote ya Ahadi, lakini hakuna jambo ambalo lingeweza kumzuia kutoa ushahidi kamili kuhusu ile kweli. (Yoh. 4:6, 34; 18:37) Yesu aliwafundisha wengine kuhusu Ufalme wa Mungu. Na kwa kuwaponya wagonjwa kimuujiza, kulisha umati wenye njaa, na hata kuwafufua wafu, Yesu alionyesha mambo ambayo Ufalme ungewatimizia wanadamu.—Mt. 11:4, 5.

13. Yesu alifundisha nini kuhusu sala?

13 Badala ya kujitafutia sifa kwa sababu ya mafundisho yake na kazi za kuponya, Yesu aliweka mfano mzuri sana kwa kuelekeza kwa unyenyekevu sifa zote kwa Yehova. (Yoh. 5:19; 11:41-44) Yesu alituonyesha pia mambo ya maana zaidi ambayo tunapaswa kutaja katika sala zetu. Sala zetu zinapaswa kutia ndani maombi ya kwamba jina la Mungu, Yehova, “litakaswe” au kuonwa kuwa takatifu, na kwamba enzi kuu ya Mungu yenye uadilifu ichukue nafasi ya utawala mwovu wa Shetani ili ‘mapenzi ya Mungu yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.’ (Mt. 6:9, 10) Pia, Yesu alitutia moyo tutende kulingana na sala hizo kwa “kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu].”—Mt. 6:33.

14. Ingawa Yesu alikuwa mkamilifu, kwa nini alihitaji kujitahidi ili kutimiza daraka lake katika kusudi la Mungu?

14 Wakati wa kifo chake cha kidhabihu ulipokuwa ukikaribia, Yesu alianza kuhisi mkazo zaidi kwa sababu ya daraka zito alilokuwa nalo. Sifa na kusudi la Baba yake lilitegemea jinsi ambavyo Yesu angevumilia mashtaka ya uwongo na kifo cha kikatili. Siku tano kabla ya kifo chake, Yesu alisali hivi: “Sasa nafsi yangu inataabika, nami nitasema nini? Baba, niokoe kutoka katika saa hii. Hata hivyo, ndiyo sababu nimekuja kwenye saa hii.” Baada ya kueleza hisia hizo za kibinadamu ambazo ni za kawaida, bila uchoyo Yesu alikazia fikira zake jambo la maana zaidi na kusali hivi: “Baba, litukuze jina lako.” Papo hapo, Yehova alijibu hivi: “Nimelitukuza na pia nitalitukuza tena.” (Yoh. 12:27, 28) Ndiyo, Yesu alikuwa tayari kuvumilia jaribu kubwa zaidi la utimilifu ambalo mwanadamu yeyote amewahi kupata. Lakini bila shaka kusikia maneno hayo ya Baba yake wa mbinguni, kulimpa Yesu uhakika wenye nguvu kwamba angefanikiwa kuitukuza na kuitetea enzi kuu ya Yehova. Na kwa kweli alifanikiwa!

Yale Ambayo Kifo cha Yesu Kilitimiza

15. Kabla tu ya kifo chake, kwa nini Yesu alisema: “Imetimizwa”?

15 Alipokuwa akining’inia kwenye mti wa mateso na akiwa karibu kuvuta pumzi yake ya mwisho kwa uchungu sana, Yesu alisema hivi: “Imetimizwa!” (Yoh. 19:30) Kwa muda wa miaka mitatu na nusu tangu alipobatizwa mpaka alipokufa, Yesu alitimiza mambo makubwa kama nini kwa msaada wa Mungu! Yesu alipokufa, kulikuwa na tetemeko kubwa la nchi, na ofisa-jeshi Mroma aliyesimamia kuuawa kwake alichochewa kusema: “Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.” (Mt. 27:54) Ni wazi kwamba ofisa-jeshi huyo aliona Yesu akidhihakiwa kwa sababu alidai kwamba yeye ni Mwana wa Mungu. Ingawa aliteseka sana, Yesu alidumisha utimilifu wake na kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo mwovu sana. Kuhusu kila mtu anayeunga mkono enzi kuu ya Mungu, Shetani alidai hivi: “Mtu atatoa kila kitu alicho nacho ili kuokoa uhai wake.” (Ayu. 2:4, Complete Jewish Bible) Kwa kubaki mwaminifu, Yesu alionyesha kwamba Adamu na Hawa wangeweza kubaki waaminifu chini ya jaribu lao ambalo lilikuwa rahisi zaidi. Jambo la maana hata zaidi ni kwamba kupitia maisha na kifo chake, Yesu aliunga mkono na kutukuza uadilifu wa enzi kuu ya Yehova. (Soma Methali 27:11.) Je, kuna jambo lingine zaidi ambalo kifo cha Yesu kimetimiza? Ndiyo bila shaka!

16, 17. (a) Kwa nini mashahidi wa Yehova walioishi kabla ya Ukristo waliweza kuwa na msimamo wa uadilifu mbele zake? (b) Yehova alithawabisha uaminifu wa Mwana wake jinsi gani, na Bwana Yesu Kristo anaendelea kufanya nini?

16 Watumishi wengi wa Yehova waliishi kabla ya Yesu kuja duniani. Walikuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Mungu na walipewa tumaini la ufufuo. (Isa. 25:8; Dan. 12:13) Lakini Mungu mtakatifu, Yehova, angeweza kuwabariki wanadamu wenye dhambi katika njia hiyo ya ajabu sana kwa msingi gani halali? Biblia inaeleza hivi: “Mungu alimweka [Yesu Kristo] kuwa toleo la kupatanisha kupitia imani katika damu yake. Ilikuwa hivyo ili kuonyesha wazi uadilifu wake mwenyewe, kwa sababu alikuwa akizisamehe dhambi zilizotokea wakati uliopita wakati Mungu alipokuwa akivumilia kwa subira; ili kuonyesha wazi uadilifu wake mwenyewe katika majira haya yaliyopo, ili awe mwadilifu hata anapomtangaza kuwa mwadilifu mtu aliye na imani katika Yesu.”—Rom. 3:25, 26. *

17 Yehova alimthawabisha Yesu kwa kumfufua na kumpa cheo kikubwa zaidi kuliko kile alichokuwa nacho kabla ya kuja duniani. Sasa Yesu ana uhai usioweza kufa akiwa kiumbe wa roho mwenye utukufu. (Ebr. 1:3) Akiwa Kuhani Mkuu na Mfalme, Bwana Yesu Kristo anaendelea kuwasaidia wafuasi wake wautukuze uadilifu wa Mungu. Na tunashukuru kama nini kwamba Baba yetu wa mbinguni, Yehova, ni Mthawabishaji wa wote wanaofanya hivyo na kumtumikia kwa ushikamanifu wakimwiga Mwana wake!—Soma Zaburi 34:3; Waebrania 11:6.

18. Tutazungumzia nini katika habari inayofuata?

18 Wanadamu wote waaminifu kuanzia Abeli walikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kwa sababu waliamini na kuutumaini kabisa Uzao ulioahidiwa. Yehova alijua kwamba Mwana wake angedumisha utimilifu wake na kwamba kifo chake kingekuwa kifuniko kikamilifu cha “dhambi ya ulimwengu!” (Yoh. 1:29) Kifo cha Yesu kinawafaidi pia watu wanaoishi leo. (Rom. 3:26) Kwa hiyo, fidia au dhabihu ya ukombozi ya Kristo inaweza kukuletea baraka gani? Habari inayofuata itazungumzia jambo hilo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Katika andiko hilo mtume Paulo anarudia maneno ya Zaburi 40:6-8 kulingana na tafsiri ya Kigiriki ya Septuajinti, ambayo inataja maneno “ulinitayarishia mwili.” Maneno hayo hayapatikani katika hati zilizopo za Maandiko ya kale ya Kiebrania.

^ fu. 16 Ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” kwenye ukurasa wa 6 na 7.

Ungesema Nini?

• Uadilifu wa Mungu ulitiliwa shaka jinsi gani?

• Ubatizo wa Yesu ulimaanisha nini?

• Kifo cha Yesu kilitimiza nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Je, unajua ubatizo wa Yesu ulimaanisha nini?