Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Anayeweza Kuwakomboa Wale Wanaolilia Msaada?

Ni Nani Anayeweza Kuwakomboa Wale Wanaolilia Msaada?

Ni Nani Anayeweza Kuwakomboa Wale Wanaolilia Msaada?

“Ee Mungu, umpe mfalme maamuzi yako ya hukumu . . . Kwa maana atamkomboa maskini anayelilia msaada.”—ZAB. 72:1, 12.

1. Tunajifunza nini kuhusu rehema za Mungu kutokana na kisa cha Daudi?

MANENO hayo ambayo inaelekea yaliandikwa na Mfalme Daudi wa Israeli la kale, yanagusa moyo kama nini! Miaka mingi kabla ya kuandika maneno hayo, alijuta baada ya kufanya uzinzi na Bath-sheba. Wakati huo, Daudi alimwomba Mungu hivi: “Ufutilie mbali makosa yangu kulingana na wingi wa rehema zako. . . . Dhambi yangu iko mbele yangu daima. . . . Tazama! Nilizaliwa kwa maumivu nikiwa na kosa, na mama yangu alinichukua mimba katika dhambi.” (Zab. 51:1-5) Kwa rehema, Yehova anakumbuka kwamba tumerithi dhambi.

2. Zaburi ya 72 inaweza kutusaidia jinsi gani?

2 Yehova anaelewa hali yetu yenye kuhuzunisha. Hata hivyo, kama ilivyotabiriwa, Mfalme aliyetiwa mafuta na Mungu “atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini.” (Zab. 72:12, 13) Msaada huo utatolewa jinsi gani? Zaburi ya 72 inatueleza jinsi msaada utakavyotolewa. Wimbo huo ambao ulitungwa kuhusu ufalme wa Sulemani mwana wa Daudi, unaonyesha kimbele jinsi utawala wa Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, utakavyoondoa matatizo ya wanadamu.

Utawala wa Kristo Watabiriwa

3. Sulemani aliomba nini, na Mungu alimpa nini?

3 Baada ya kuamuru kwamba Sulemani awekwe kuwa mfalme, Daudi aliyekuwa amezeeka alimpa maagizo yaliyo wazi ambayo Sulemani aliyafuata kwa uaminifu. (1 Fal. 1:32-35; 2:1-3) Baadaye, Yehova alimtokea Sulemani katika ndoto na kumwambia: “Omba kile ninachopaswa kukupa.” Sulemani aliomba jambo moja tu: “Nawe umpe mtumishi wako moyo mtiifu ili awahukumu watu wako, atambue kati ya mema na mabaya.” Kwa sababu ya ombi la unyenyekevu la Sulemani, Mungu alimpa kile alichoomba na akamwongezea vitu vingine vingi.—1 Fal. 3:5, 9-13.

4. Utawala wa Sulemani ulielezwa jinsi gani na mtawala fulani aliyeishi wakati huo?

4 Kwa sababu ya baraka za Yehova, utawala wa Sulemani ulikuwa kipindi chenye amani nyingi sana na ufanisi ambao haujawahi kuwapo chini ya serikali yoyote duniani. (1 Fal. 4:25) Kati ya watu ambao walikuja kuona jinsi utawala wa Sulemani ulivyokuwa ni malkia wa Sheba pamoja na msafara wake mkubwa. Alimwambia Sulemani hivi: “Ni la kweli neno lile nililosikia katika nchi yangu . . . Sikuwa nimeambiwa hata nusu. Umezidi katika hekima na mafanikio, mambo yale niliyoyasikia.” (1 Fal. 10:1, 6, 7) Ingawa hivyo, Yesu alionyesha hekima nyingi hata zaidi, na kwa kufaa alisema hivi kujihusu: “Tazama! mtu mkuu kuliko Sulemani yuko hapa.”—Mt. 12:42.

Kitulizo Chini ya Sulemani Mkuu Zaidi

5. Zaburi ya 72 inafunua nini, na inatoa habari gani kimbele?

5 Acheni sasa tuchunguze mistari fulani katika Zaburi ya 72 ili tujifunze kuhusu baraka zitakazokuwa chini ya utawala wa Yesu Kristo, yule Sulemani Mkuu Zaidi. (Soma Zaburi 72:1-4.) Zaburi hii inafunua jinsi Yehova anavyohisi kuhusu “utawala wa kifalme” wa Mwana wake, Yesu Kristo, yule “Mkuu wa Amani.” (Isa. 9:6, 7) Akiongozwa na Mungu, yule Sulemani Mkuu Zaidi ‘atawatetea wenye kuteseka na kuwaokoa wana wa maskini.’ Utawala wake utakuwa wa amani na uadilifu. Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha kimbele mambo ambayo yatatimizwa na Utawala wake unaokuja wa Miaka Elfu Moja.—Ufu. 20:4.

6. Yesu alionyesha kimbele baraka gani zitakazokuwa chini ya utawala wa Ufalme?

6 Fikiria matendo fulani ya Yesu Kristo ambayo yanatuonyesha kimbele yale ambayo atawafanyia wanadamu atakapotimiza Zaburi ya 72. Tuna kila sababu ya kuvutiwa na huruma nyingi ambayo aliwaonyesha watu waliokuwa wakiteseka. (Mt. 9:35, 36; 15:29-31) Kwa mfano, mtu fulani aliyekuwa akiteseka kwa sababu ya ukoma alimwendea Yesu na kumsihi hivi: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Yesu akamjibu hivi: “Ninataka. Takasika.” Na mara moja mwanamume huyo akaponywa! (Marko 1:40-42) Baadaye, Yesu alikutana na mjane ambaye mwana wake wa pekee alikuwa amekufa. Yesu “akamsikitikia” na kusema, “Inuka!” na mwana wake akainuka. Akawa hai tena!—Luka 7:11-15.

7, 8. Yesu alionyesha nguvu zake za kuponya katika njia gani mbalimbali?

7 Yehova alimpa Yesu nguvu za kufanya miujiza. Hilo lilionekana katika kisa cha “mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu kwa miaka kumi na miwili.” Ingawa “alikuwa ameumizwa sana na matabibu wengi na alikuwa ametumia mali zake zote,” kwa kweli hali yake iliendelea kuwa mbaya zaidi. Mwanamke huyo aliingia katikati ya umati na kumgusa Yesu—tendo ambalo lilivunja Sheria iliyohusu mtu mwenye ‘mtiririko wa damu.’ (Law. 15:19, 25) Yesu akatambua kwamba nguvu zilikuwa zimemtoka na hivyo akauliza ni nani aliyekuwa amemgusa. “Akiogopa na kutetemeka” mwanamke huyo “akaanguka chini mbele yake, akamwambia kweli yote.” Akitambua kwamba Yehova alikuwa amemponya mwanamke huyo, Yesu alimtendea kwa fadhili na kusema: “Binti yangu, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani, na uwe na afya njema kutokana na ugonjwa wako wenye kuhuzunisha.”—Marko 5:25-27, 30, 33, 34.

8 Nguvu za kuponya ambazo Yesu alipewa na Mungu ziliwaponya wagonjwa lakini pia zilikuwa na matokeo makubwa juu ya watazamaji. Kwa mfano, bila shaka wengi walifurahi sana walipoona Yesu akiwaponya watu kabla ya Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana. (Luka 6:17-19) Yohana Mbatizaji alipotuma wajumbe wawili ili kuhakikisha kwamba Yesu alikuwa ndiye Masihi, walimkuta Yesu ‘akiponya magonjwa na maradhi yenye kuhuzunisha na roho waovu, na kuwapa vipofu wengi uwezo wa kuona.’ Kisha Yesu akawaambia hivi wajumbe hao wawili: “Nendeni, mkamwambie Yohana yale mliyoona na kusikia: vipofu wanaona, vilema wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa na viziwi wanasikia, na wafu wanafufuliwa, maskini wanaambiwa ile habari njema.” (Luka 7:19-22) Bila shaka ujumbe huo ulimtia moyo sana Yohana!

9. Miujiza ya Yesu ilionyesha kimbele mambo gani?

9 Ni kweli kwamba kitulizo ambacho Yesu aliwapa watu waliokuwa wakiteseka wakati wa huduma yake duniani kilikuwa cha muda mfupi tu. Watu ambao aliponya au kufufua walikufa baadaye. Hata hivyo, miujiza ambayo Yesu alifanya alipokuwa duniani ilionyesha kimbele kitulizo cha kudumu ambacho wanadamu watafurahia chini ya utawala wake wa Kimasihi.

Paradiso Itaenea Duniani Pote Hivi Karibuni!

10, 11. (a) Baraka za Ufalme zitadumu kwa muda gani, na utawala wa Yesu utakuwa namna gani? (b) Ni nani atakayekuwa pamoja na Kristo katika Paradiso, na ataweza jinsi gani kuishi milele?

10 Hebu wazia jinsi maisha yatakavyokuwa katika Paradiso duniani. (Soma Zaburi 72:5-9.) Waabudu wa Mungu wa pekee wa kweli watafurahia maisha katika Paradiso kwa muda wote ambao jua na mwezi utakuwapo, ndiyo, milele! Mfalme Yesu Kristo atathibitika kuwa mwenye kuburudisha, ‘kama mvua juu ya majani yaliyofyekwa na manyunyu mengi yanayolowesha dunia.’

11 Unapofikiria utimizo wa zaburi hiyo, je, huguswi moyo na tumaini la kuishi milele katika dunia iliyo paradiso? Kwa kweli, mtenda-maovu aliyekuwa ametundikwa alisisimka Yesu alipomwambia hivi: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43) Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Yesu, mwanamume huyo atarudishwa kwenye uhai tena. Ikiwa atajitiisha chini ya utawala wa Kristo, ataishi milele duniani akiwa na afya kamilifu na furaha.

12. Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, watu wasio waadilifu ambao watafufuliwa watakuwa na nafasi gani?

12 Chini ya utawala wa yule Sulemani Mkuu Zaidi, Yesu Kristo, “mwadilifu atachipuka,” yaani, atasitawi au atafanikiwa. (Zab. 72:7) Wakati huo, upendo na utunzaji mwororo wa Kristo utakuwa mwingi, kama vile ulivyokuwa alipokuwa duniani. Katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa, hata “wasio waadilifu” ambao watafufuliwa, watapewa kwa upendo nafasi ya kujipatanisha na viwango vya Yehova na kuishi. (Mdo. 24:15) Bila shaka, wale watakaokataa kutenda kulingana na matakwa ya Mungu hawataruhusiwa kuendelea kuishi na kuvuruga amani na utulivu katika ulimwengu mpya.

13. Utawala wa Ufalme utaenea kwa kadiri gani, na kwa nini amani yake haitavurugwa kamwe?

13 Maneno haya yanaonyesha jinsi utawala wa Sulemani Mkuu Zaidi utakavyoenea duniani pote: “Atakuwa na raia kutoka bahari mpaka bahari na kutoka ule Mto [Efrati] mpaka miisho ya dunia. Wakaaji wa maeneo yasiyo na maji watainama mbele yake, na adui zake watayaramba mavumbi.” (Zab. 72:8, 9) Ndiyo, Yesu Kristo atatawala dunia yote. (Zek. 9:9, 10) Wale ambao wanathamini utawala wake na baraka zake “watainama” wakijitiisha kwa kupenda. Kwa upande mwingine, watenda-dhambi wasiotubu watakatiliwa mbali, hata ikiwa wana “umri wa miaka mia moja.” (Isa. 65:20) Watu hao “watayaramba mavumbi.”

Anatujali kwa Huruma

14, 15. Tunajua jinsi gani kwamba Yesu anaelewa hisia za wanadamu na kwamba “atamkomboa maskini anayelilia msaada”?

14 Wanadamu wenye dhambi wako katika hali ya kusikitisha na wanahitaji sana msaada. Lakini tuna tumaini. (Soma Zaburi 72:12-14.) Yesu, yule Sulemani Mkuu Zaidi, anatuhurumia kwa sababu anaelewa hali yetu ya kutokamilika. Zaidi ya hayo, Yesu aliteseka kwa ajili ya uadilifu, na Mungu alimruhusu apambane na majaribu akiwa peke yake. Kwa kweli, Yesu aliteseka sana kihisia hivi kwamba “jasho lake likawa kama matone ya damu yakianguka chini”! (Luka 22:44) Baadaye akiwa kwenye mti wa mateso, alilia hivi kwa sauti: “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?” (Mt. 27:45, 46) Ingawa aliteseka sana, na hata ingawa Shetani alijitahidi kabisa kumfanya amwache Yehova, Yesu alithibitika kuwa mwaminifu kwa Yehova Mungu.

15 Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu anaona uchungu tunaohisi na kwamba “atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi.” Akiwa mwenye upendo na mwenye kujali kama Baba yake, Yesu ‘atawasikiliza maskini’ na ‘atawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye atafunga sehemu zao zenye maumivu.’ (Zab. 69:33; 147:3) Yesu anaweza “kuusikitikia udhaifu wetu” kwa sababu “amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe.” (Ebr. 4:15) Ni jambo zuri kama nini kujua kwamba Mfalme Yesu Kristo anatawala sasa mbinguni na anatazamia kwa hamu kuwaletea wanadamu wanaoteseka kitulizo!

16. Kwa nini Sulemani aliwahurumia raia wake?

16 Kwa kuwa Sulemani alikuwa na hekima na ufahamu, bila shaka ‘alimsikitikia mtu wa hali ya chini.’ Pia, maisha yake yalikuwa na matukio ya kusikitisha na kufadhaisha. Ndugu yake Amnoni alimlala kinguvu dada yake Tamari, na Absalomu ndugu ya Sulemani akaamuru Amnoni auawe kwa sababu ya uhalifu huo. (2 Sam. 13:1, 14, 28, 29) Absalomu alijaribu kunyakua kiti cha ufalme cha Daudi, lakini mapinduzi hayo hayakufaulu, naye akauawa na Yoabu. (2 Sam. 15:10, 14; 18:9, 14) Baadaye, Adoniya ndugu ya Sulemani alijaribu kunyakua ufalme. Ikiwa angefaulu, bila shaka Sulemani angeuawa. (1 Fal. 1:5) Tunajua kwamba Sulemani alielewa jinsi wanadamu wanavyoteseka na hilo linaonekana wazi katika maneno aliyosema katika sala wakati wa kuzinduliwa kwa hekalu la Yehova. Mfalme Sulemani alisali hivi kuhusu raia wake: “Wanajua kila mmoja wao pigo lake na maumivu yake mwenyewe . . . Nawe [Yehova] usamehe na kumpa kila mmoja kulingana na njia zake zote.”—2 Nya. 6:29, 30.

17, 18. Ni maumivu gani ambayo watumishi fulani wa Mungu wamekabiliana nayo, na ni nini ambacho kimewasaidia?

17 ‘Maumivu yetu wenyewe’ yanaweza kusababishwa na matukio fulani ya wakati uliopita katika maisha yetu. Mary, * Shahidi wa Yehova ambaye ana umri wa miaka 30 na kitu, anaandika hivi: “Nina kila sababu ya kuwa na furaha, lakini mara kwa mara mambo niliyofanya zamani yananiletea hisia za aibu na zenye kuchukiza. Hisia hizo zinanifanya nihuzunike sana, na kulia, ni kana kwamba mambo hayo yote yalitendeka jana. Kumbukumbu zilizotia mizizi bado zinanifanya nilemewe sana na hisia za kwamba sifai na nina hatia.”

18 Watumishi wengi wa Mungu wanapambana na hisia kama hizo, lakini ni nini kinachoweza kuwasaidia kupata nguvu wanazohitaji ili wavumilie? Mary anasema hivi: “Sasa familia ya kiroho na marafiki wa kweli wananiletea furaha. Pia, ninajitahidi kukazia fikira ahadi za Yehova kuhusu wakati ujao, na nina hakika kwamba vilio vyangu vya kuomba msaada vitageuzwa na kuwa vigelegele vya shangwe.” (Zab. 126:5) Tunahitaji kuweka tumaini letu katika uandalizi wa Mungu wa kutoa Mwana wake, Mtawala wake aliyechaguliwa. Ilitabiriwa hivi kumhusu: “Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri, nayo damu yao itakuwa na thamani machoni pake.” (Zab. 72:13, 14) Hilo linatia moyo kama nini!

Ulimwengu Mpya Wenye Vitu Vingi Uko Mbele Yetu

19, 20. (a) Kama inavyoonyeshwa kwenye Zaburi ya 72, utawala wa Ufalme utaondoa tatizo gani? (b) Ni nani anayestahili kusifiwa kwanza kwa sababu ya utawala wa Kristo, na unahisi namna gani kuhusu yale ambayo utawala huo utatimiza?

19 Jaribu tena kuwazia wakati ujao wa wanadamu wanyoofu katika ulimwengu mpya wa Mungu chini ya utawala wa yule Sulemani Mkuu Zaidi. Tunaahidiwa hivi: “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani. Juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” (Zab. 72:16) Kwa kuwa si jambo la kawaida kukuza nafaka juu ya milima, maneno hayo yanakazia jinsi dunia itakavyozaa mazao mengi. Mazao yake ‘yatakuwa kama katika Lebanoni,’ eneo lililozalisha mazao mengi sana wakati wa utawala wa Sulemani. Hebu fikiria hili! Hakutakuwa tena na upungufu wa chakula, hakuna mtu atakayekosa chakula cha kujenga mwili, wala hakuna mtu atakayekuwa na njaa! Wakati huo, watu wote watafurahia “karamu ya vyakula vinono vilivyotiwa mafuta.”—Isa. 25:6-8; 35:1, 2.

20 Ni nani atakayesifiwa kwa ajili ya baraka hizo zote? Kwanza kabisa ni Mfalme wa Milele na Mtawala wa Ulimwengu Wote, Yehova Mungu. Kwa kweli, wakati huo sote tutaimba pamoja kwa shangwe sehemu ya mwisho ya wimbo huu mtamu unaochangamsha moyo: “Jina lake [la Mfalme Yesu Kristo] na liweko mpaka wakati usio na kipimo; jina lake na liongezeke mbele ya jua, na kupitia yeye na wajibariki; mataifa yote na yamtangaze kuwa mwenye furaha. Na abarikiwe Yehova Mungu, Mungu wa Israeli, ambaye peke yake anafanya kazi za ajabu. Na jina lake tukufu na libarikiwe mpaka wakati usio na kipimo, nao utukufu wake na uijaze dunia yote. Amina na Amina.”—Zab. 72:17-19.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Jina limebadilishwa.

Ungesema Nini?

Zaburi ya 72 ilitabiri nini kimbele?

• Yule Sulemani Mkuu Zaidi ni nani, na utawala wake utaenea kadiri gani?

• Wewe binafsi unavutiwa na nini kuhusiana na baraka zilizotabiriwa katika Zaburi ya 72?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Ufanisi uliofurahiwa wakati wa utawala wa Sulemani ulionyesha nini kimbele?

[Picha katika ukurasa wa 32]

Tuna kila sababu ya kujitahidi kabisa ili tuishi katika Paradiso chini ya utawala wa yule Sulemani Mkuu Zaidi