Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ametupa Uhuru wa Kuchagua

Ametupa Uhuru wa Kuchagua

Mkaribie Mungu

Ametupa Uhuru wa Kuchagua

2 WAFALME 18:1-7

WAZAZI wanapaswa kuwawekea watoto wao mfano mzuri. Mfano mzuri wa wazazi unaweza kuwasaidia watoto kuwa na sifa nzuri na kufanya maamuzi ya hekima maishani. Jambo la kusikitisha ni kwamba wazazi wengi huwawekea watoto wao mfano mbaya. Je, hilo linamaanisha kwamba watoto kama hao hawawezi kufanikiwa? Tunapata jibu lenye kutia moyo sana—Yehova Mungu ametupa sisi sote zawadi ya uhuru wa kuchagua. Fikiria kisa cha Hezekia, kinachopatikana katika 2 Wafalme 18:1-7.

Hezekia alikuwa “mwana wa Ahazi mfalme wa Yuda.” (Mstari wa 1) Ahazi aliwaongoza raia zake waache ibada safi ya Yehova. Mfalme huyo mwovu aliabudu Baali, na kufuata desturi za ibada hiyo za kutoa watu dhabihu. Alisababisha kifo cha ndugu mmoja au hata zaidi wa Hezekia. Ahazi aliifunga milango ya hekalu na “akajitengenezea madhabahu katika kila pembe katika Yerusalemu.” Mfalme huyo ‘alimtia uchungu Yehova.’ (2 Mambo ya Nyakati 28:3, 24, 25) Kwa kweli Hezekia alikuwa na baba mbaya sana. Hata hivyo, je, Hezekia angerudia makosa ya baba yake?

Mara baada ya kutwaa madaraka kutoka kwa Ahazi, mara moja Hezekia alianza kuonyesha kwamba hakuathiriwa na malezi mabaya ya baba yake. Hezekia “akaendelea kufanya yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova.” (Mstari wa 3) Hezekia alimtegemea Yehova, na “baada yake hapakuwa na yeyote kama yeye kati ya wafalme wote wa Yuda.” (Mstari wa 5) Katika mwaka wa kwanza wa utawala wake, mfalme huyo kijana alianza kufanya marekebisho ya ibada yaliyotia ndani kuondolewa kwa mahali pa juu, mahali ambapo sanamu za kipagani zilikuwa zikiabudiwa. Hekalu lilifunguliwa tena, na ibada safi ikarudishwa. (Mstari wa 4; 2 Mambo ya Nyakati 29:1-3, 27-31) Hezekia “a[li]endelea kushikamana na Yehova . . . , na Yehova akawa pamoja naye.”—Mstari wa 6, 7.

Ni nini kilichomsaidia Hezekia asifuate mfano mbaya wa baba yake? Je, inawezekana kwamba mama yake, Abiya—ambaye hatuna habari nyingi kumhusu—alimwekea mwana wake kielelezo kizuri? Je, mfano mzuri wa Isaya, ambaye alianza huduma yake ya kutoa unabii kabla Hezekia kuzaliwa, ulikuwa na uvutano mzuri juu ya mwana huyo wa mfalme? * Biblia haisemi. Vyovyote vile, jambo moja ni hakika: Hezekia aliamua kufuata mwenendo ambao ulikuwa tofauti kabisa na ule wa baba yake.

Mfano mzuri wa Hezekia unamtia moyo yeyote ambaye huenda amekabili matatizo utotoni kwa sababu ya malezi mabaya. Hatuwezi kubadili wakati uliopita wala mambo mabaya yaliyotupata wakati huo. Lakini mambo hayo hayamaanishi kwamba hatuwezi kufanikiwa. Tunaweza kuwa na wakati ujao wenye furaha ikitegemea maamuzi tunayofanya sasa. Kama Hezekia, tunaweza kuchagua kumpenda na kumwabudu Mungu wa kweli, Yehova. Kufanya hivyo, kutatuwezesha kuishi maisha yenye kuridhisha sasa na tunaweza kupata uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Tunamshukuru Mungu wetu mwenye upendo kama nini kwa kutupa kila mmoja wetu zawadi yenye thamani—uhuru wa kuchagua!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Isaya alitoa unabii kuanzia karibu mwaka 778 K.W.K. hadi karibu mwaka 732 K.W.K. Hezekia alianza kutawala mwaka 745 K.W.K., akiwa na umri wa miaka 25.