Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kusanyiko Karibu na Ufuo

Kusanyiko Karibu na Ufuo

Barua Kutoka Grenada

Kusanyiko Karibu na Ufuo

MTU hupata shangwe isiyo na kifani anapopewa mgawo wa kutumika akiwa mmishonari katika nchi ya kigeni. Kama mtoto anayekodoa macho akitaka kujua jambo fulani, huenda ukaanza kuwaza kuhusu watu utakaokutana nao na mambo utakayojionea katika mgawo wako.

Mimi na mke wangu tulipopokea mgawo wa kuwa wamishonari nchini Grenada, katika eneo la pwani lenye fuo 45 hivi zenye kupendeza sana, tulitamani sana kuona jinsi fuo hizo zilivyo. Kumbe karibuni tungekuwa na siku yenye kufurahisha katika mojawapo ya fuo hizo. Furaha hiyo ilihusiana hasa na watu tuliokutana nao, bali si kuota jua wala kufurahia mchezo wa kuteleza juu ya mawimbi.

Kutoka nyumbani kwetu mpaka Grand Anse Beach ni mwendo mfupi kwa kutumia gari, lakini safari hiyo inafurahisha na kupendeza kama nini! Barabara imejipindapinda na hivyo inatuwezesha kuona mandhari zenye kuvutia sana. Pia kuna milima iliyo na miti yenye rangi ya kijani kibichi. Tunapoendelea na safari yetu kwenye barabara hiyo tunaona milima, misitu ya mvua, maporomoko ya maji na mandhari yenye kuvutia ya upeo wa bahari. Bila shaka, hiyo ndiyo sababu watalii kutoka kotekote ulimwenguni wanakuja kutembelea eneo hili! Mandhari hiyo inapendeza sana hivi kwamba lazima dereva awe mwangalifu asije akasababisha aksidenti. Barabara hizo zenye kujipindapinda ni nyembamba sana kiasi kwamba nyakati nyingine una shaka kama magari mawili yataweza kupishana bila kugongana.

Hatimaye, tulifika kwenye jengo la Trade Center lililo kwenye barabara ya Grand Anse Beach, ambapo kusanyiko lilifanywa. Muda si muda, Mashahidi wa Yehova karibu 600 walikusanyika ili kupokea maagizo ya Biblia na kufurahia ushirika wa Kikristo. Siku hiyo ilikuwa ya maana sana hasa kwa Lesley na mke wake Daphne walio na umri wa miaka 70 hivi. Lesley alibatizwa siku hiyo. Daphne aliyebatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova mwaka wa 1958, alikuwa akingojea kwa hamu kuona mume wake akibatizwa pia.

Ubatizo, yaani, kuzamishwa kabisa ndani ya maji, una maana kubwa kwa Mashahidi. Mtu huchukua hatua hiyo baada ya kupata ujuzi sahihi wa kweli za Biblia na kuanza kuzifuata maishani mwake. Ubatizo ni tangazo la hadharani la kuonyesha kuwa mtu amejitoa kwa Yehova Mungu.

Niliombwa nitoe hotuba inayotegemea Biblia kuhusu ubatizo. Mwishoni mwa hotuba hiyo, Lesley na watu wengine wawili ambao pia walitaka kubatizwa, walisimama. Lesley alikuwa amevaa shati nyeupe zuri na tai na pia alitabasamu sana. Niliwauliza swali hili: “Je, umetubu dhambi zako na kujiweka wakfu kwa Yehova ili kufanya mapenzi yake?” Ungetambua unyofu na azimio lao wakati walipojibu kutoka moyoni, “Ndiyo!”

Niliguswa moyo sana hasa kwa sababu nilijua maisha ya Lesley. Kwa muda mrefu alikataa kujifunza Biblia. Kisha, yeye na mke wake wakatembelea kisiwa kingine. Walipokuwa kisiwani humo, waliamua kila mtu ahudhurie ibada katika dini yake. Lesley alimwambia Daphne hivi: “Wewe, nenda kwenye kanisa lako, nami nitaenda kwenye kanisa langu.”

Lesley alimpeleka Daphne kwa gari hadi kwenye Jumba la Ufalme, naye akaenda kwenye kanisa moja la Kianglikana lililokuwa karibu. Ibada ilipoisha alirudi kwenye Jumba la Ufalme kumchukua Daphne. Alipofika katika jumba hilo alikaribishwa kwa uchangamfu na watu wenye kumjali ingawa walikuwa hawajawahi kukutana naye. Jambo hilo lilimgusa Lesley. Katika kanisa lake hakuna mtu aliyeongea naye. Lesley alimwambia hivi Daphne: “Sitarudi katika kanisa hilo tena. Hakuna mtu aliyeongea nami, hata kasisi mwenyewe. Hakuna mtu alinisalimu. Niliingia na nikatoka bila yeyote kuongea nami.” Lesley aliamua kuliacha kabisa kanisa hilo.

Lesley alianza kujifunza kwa bidii Neno la Mungu. Na sasa alikuwa tayari kubatizwa. Tuliandamana na watu hao watatu waliotaka kubatizwa hadi baharini. Kwa kuwa bahari ilikuwa karibu sana, hakukuwa na haja ya kuwa na kidimbwi cha ubatizo kama inavyofanywa kwenye makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Tulihitaji tu kuvuka barabara.

Ufuo wa Grand Anse Beach ulio na urefu wa kilomita tatu hivi unapendeza na una mchanga mweupe na maji ya rangi ya bluu ambayo huwa vuguvugu mwaka mzima. Watalii walishangaa sana kuona kikundi cha watu wakielekea baharini, wanaume wakiwa wamevaa shati na tai, nao wanawake wakiwa wamevaa mavazi yao yenye kupendeza. Lesley alikuwa amebadili mavazi yake na alikuwa amevaa T-shati na suruali fupi. Hebu wazia jinsi Daphne alivyohisi alipomwona mume wake akibatizwa baada ya miaka 50! Jua la adhuhuri liling’aa sana kama tu tabasamu lake. Hata watalii walijiunga nasi kufurahia siku hiyo. Pia walipiga makofi wakati kila mmoja wa watu hao alipobatizwa.

Anga ya bluu, mchanga mweupe wa baharini, na mawimbi yanayopigapiga ufuo taratibu, ni mandhari ambayo inamletea Muumba sifa. Yehova alipata sifa hata zaidi wakati watu hao watatu walipotoka ndani ya maji baada ya kubatizwa. Tulifurahia zaidi kuwaona watu hao kuliko vile tulivyofurahia kupigwa na jua. Kwa kweli, hiyo ilikuwa siku ya pekee sana. Kwa Lesley na Daphne, hiyo ilikuwa ndiyo siku nzuri zaidi maishani mwao.