Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kaini Alipata Wapi Mke Wake?

Kaini Alipata Wapi Mke Wake?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Kaini Alipata Wapi Mke Wake?

▪ “Ikiwa Adamu na Hawa walikuwa na wana wawili, Kaini na Abeli, mke wa Kaini alitoka wapi?” Ingawa mara nyingi wachambuzi wa Biblia huuliza swali hilo ili tu kuwavuruga watu, Biblia ina habari za kutosha kujibu swali hilo kwa njia inayofaa.

Katika Mwanzo sura ya 3 na ya 4 tunapata habari zifuatazo: (1) Hawa alikuwa “mama ya kila mtu anayeishi.” (2) Muda fulani ulipita kuanzia wakati Kaini alipozaliwa mpaka wakati alipotoa dhabihu ambayo ilikataliwa na Mungu. (3) Baada ya kufukuzwa na kuwa “mwenye kutanga-tanga na mkimbizi,” Kaini alikuwa na wasiwasi kwamba huenda ‘mtu yeyote akakutana naye’ na kujaribu kumuua. (4) Mungu aliweka ishara ya kumlinda Kaini, jambo lililoonyesha kwamba ndugu au dada zake, au watu wengine wa ukoo wangejaribu kumuua. (5) “Baadaye” Kaini alilala na mke wake “katika nchi ya Ukimbizi.”—Mwanzo 3:20; 4:3, 12, 14-17.

Kutokana na habari hizo, tunaweza kusema kwamba mke wa Kaini, ambaye haijulikani alizaliwa wakati gani, alikuwa mzao wa Hawa. Andiko la Mwanzo 5:4 linasema kwamba katika miaka 930 ambayo Adamu aliishi, ‘alizaa wana na mabinti.’ Bila shaka, Biblia haisemi waziwazi kwamba mke wa Kaini alikuwa binti ya Hawa. Hata hivyo, kwa kuwa mke wa Kaini anatajwa baada ya Kaini kufukuzwa, jambo hilo linaonyesha kwamba wakati wa kutosha ulikuwa umepita na angeweza kuwa mmoja wa wajukuu wa Adamu na Hawa. Kwa hiyo, tafsiri ya Biblia The Amplified Old Testament inasema tu kwamba mke wa Kaini alikuwa “mmoja wa watoto wa Adamu.”

Mfafanuzi wa Biblia wa karne ya 19 Adam Clarke, alionelea kwamba hatua ya Mungu ya kuweka ishara kwa sababu Kaini aliogopa kuuawa, ilitokana na kuwapo kwa vizazi kadhaa vya wazao wa Adamu—vizazi vingi vya kutosha “kuanzisha vijiji kadhaa.”

Wazo la kwamba Kaini alimwoa dada yake au mzao wa baadaye wa Adamu kupitia mmoja wa wana au mabinti zake, ni jambo lisilokubalika katika jamii fulani leo. Sababu ni kuwa jamii hizo huliona hilo kuwa jambo lisilokubalika au huogopa kwamba litasababisha kasoro za kimaumbile. Hata hivyo, F. LaGard Smith anasema hivi katika kitabu The Narrated Bible in Chronological Order: “Inaelekea kwamba ndugu na dada hao wa karibu walioana ingawa ndoa kama hiyo ingeonekana kuwa jambo lisilofaa katika vizazi vya baadaye.” Inafaa kuzingatia kwamba ngono kati ya watu wa ukoo haikukatazwa waziwazi mpaka Musa alipopokea sheria za Mungu kwa ajili ya taifa la Israeli mwaka wa 1513 K.W.K.—Mambo ya Walawi 18:9, 17, 24.

Leo, maelfu ya miaka imepita tangu wazazi wetu wa kwanza wapoteze ukamilifu wao. Huenda matatizo yanayotokana na chembe za urithi leo hayangewapata. Isitoshe, uchunguzi wa hivi karibuni, kama ule uliochapishwa katika jarida Journal of Genetic Counseling, unaonyesha kwamba watoto wanaozaliwa katika ndoa kati ya binamu wa karibu, hawana kasoro nyingi za urithi kama inavyowaziwa na wengi. Kwa kweli, hayo hayangekuwa mambo yenye kutia wasiwasi mwingi siku za Adamu au hata kabla ya siku za Noa. Kwa hiyo, tunaweza kukata kauli kwamba mke wa Kaini alikuwa mmoja kati ya watu wake wa ukoo.