Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtegemee Yehova—Hakika Atakusaidia

Mtegemee Yehova—Hakika Atakusaidia

Mtegemee Yehova—Hakika Atakusaidia

Limesimuliwa na Edmund Schmidt

Muda mfupi kabla ya kufikishwa mahakamani huko New York mnamo Oktoba (Mwezi wa 10) 1943, nilikumbuka shauri lililo hapo juu. Nilipofikisha umri wa miaka 25, nilikuwa nimekwisha tumikia kifungo cha karibu miaka minne gerezani kwa sababu ya msimamo wangu wa Kikristo wa kutounga mkono vita. Kama wafuasi wa mapema wa Yesu, niliazimia ‘kumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’ (Matendo 5:29) Lakini kabla sijakusimulia jambo hilo, acha nieleze jinsi nilivyopata imani yenye nguvu katika Mungu.

NILIZALIWA Aprili 23, 1922, huko Cleveland, Ohio, Marekani, katika nyumba yetu iliyokuwa kwenye ghorofa ya kwanza juu ya duka la kuokea mikate la baba yangu. Miezi minne baadaye, baba yangu, Edmund, alihudhuria kusanyiko la Wanafunzi wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo) huko Cedar Point, karibu na Sandusky, kilomita 160 hivi kutoka nyumbani kwetu.

Katika kusanyiko hilo, wajumbe walihimizwa: “Tangazeni, tangazeni, tangazeni Mfalme [wa Mungu] na ufalme wake.” Jumapili (Siku ya Yenga) iliyofuata, Baba yangu alianza kushiriki katika kazi hiyo. Aliendelea kufanya hivyo kwa miaka 66 iliyofuata, hadi alipokufa mnamo Julai 4, 1988 (4/7/1988). Mama yangu, Mary, alikufa akiwa mwaminifu kwa Mungu mwaka wa 1981.

Naungana na Wazazi Wangu Katika Ibada

Familia yetu ilihudhuria mikutano iliyofanywa katika lugha ya Kipolishi huko Cleveland. Kila siku ya Jumamosi (Siku ya Posho) alasiri, wengi wetu sisi watoto tulihubiri nyumba kwa nyumba pamoja na wazazi wetu. Siku ya Jumapili , wazazi wetu walifurahia hotuba ya Biblia ndani ya jumba kuu la mahali petu pa kufanyia mikutano. Wakati huohuo, mwalimu wa Biblia mwenye ujuzi alitumia kitabu The Harp of God * kutufundisha Biblia tukiwa watoto 30 hivi. Punde si punde, mimi mwenyewe nilianza kuongoza mafunzo ya Biblia na kupata matokeo mazuri.

Mnamo Julai 1931, familia yetu, ambayo sasa ilitia ndani ndugu yangu mdogo Frank, tulihudhuria kusanyiko lingine la Wanafunzi wa Biblia. Wakati huu kusanyiko lilikuwa huko Columbus, karibu kilomita 160 kusini. Huo ndio wakati Wanafunzi wa Biblia walikubali kwa moyo wote jina linalotegemea Biblia, Mashahidi wa Yehova. (Isaya 43:10-12) Wakati huo, nilishiriki katika kazi ya kuhubiri ili kuwakaribisha watu waje kusikiliza hotuba ya msingi ambayo ingetolewa na J. F. Rutherford, ambaye wakati huo ndiye aliyekuwa akiongoza kazi ya Mashahidi wa Yehova. Tangu wakati huo, nimekuwa nikimtumikia Yehova Mungu kwa zaidi ya miaka 79 pamoja na watu wake.

Huduma Yenye Matokeo Mazuri Licha ya Hali Ngumu

Kufikia mwaka wa 1933, dunia nzima ilikuwa inakabili Mshuko Mkubwa wa Kiuchumi. Huko Marekani, zaidi ya watu milioni 15, au mtu mmoja kati ya kila watu wanne alikuwa hana kazi. Majiji yaliishiwa na pesa na serikali haikuwa na uwezo wa kuwatunza wazee na maskini. Hata hivyo, ndugu na dada zetu Wakristo walisaidiana. Kila Jumapili, familia yetu ilibeba mikate na donati kwenye mkutano ili kuwagawia wengine. Mwishoni mwa mwezi, kiasi chochote cha pesa ambacho Baba alibaki nacho baada ya kulipia gharama mbalimbali, alikituma kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York. Alijua kwamba pesa hizo zingesaidia katika kazi ya kuchapisha vitabu vinavyotegemea Biblia.

Katika miaka hiyo, redio ilikuwa chombo muhimu sana katika huduma yetu. Zaidi ya vituo 400 vya redio vilitangaza moja kwa moja hotuba za Biblia zilizotolewa katika makusanyiko yetu. Katika miaka ya 1930, Mashahidi wa Yehova pia walitengeneza gramafoni na santuri katika kiwanda chao huko Brooklyn. Tulivitumia vifaa hivyo katika huduma yetu, na tuliripoti idadi ya watu wasio Mashahidi ambao walisikiliza hotuba hizo, na pia mara ambazo walizisikiliza.

Katika mwaka wa 1933, Adolf Hitler wa chama cha Nazi alianza kutawala nchini Ujerumani. Mashahidi wa Yehova katika nchi hiyo waliteswa sana kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono mambo ya kisiasa. (Yohana 15:19; 17:14) Kwa hiyo, wengi wao walifungwa magerezani au kupelekwa katika kambi za mateso, kwa sababu ya kukataa kushiriki katika mambo ya kisiasa au kumpigia Hitler saluti. Wengi waliuawa na wengine wakafanyishwa kazi ngumu mpaka wakafa. Kwa sababu ya kutendwa kikatili kwenye kambi hizo, wengi walikufa muda mfupi tu baada ya kuachiliwa. Watu wengi hawajui mateso ambayo Mashahidi wa Yehova walipata katika nchi nyingine, kutia ndani Marekani.

Mnamo mwaka wa 1940, tulihudhuria kusanyiko huko Detroit, Michigan. Nilibatizwa kwenye kusanyiko hilo mnamo Julai 28, ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova Mungu. Mwezi mmoja kabla ya kusanyiko hilo, Mahakama Kuu ya Marekani, ilikuwa imepitisha sheria ya kwamba kukataa kuipigia saluti bendera ni kuvunja sheria ya nchi, na ni kosa ambalo lingeweza kumfanya mwanafunzi afukuzwe shuleni. Mashahidi walishughulikia hali hiyo jinsi gani? Wengi wao walianzisha shule zao wenyewe ili kuwafundisha watoto wao. Shule hizo ziliitwa Shule za Ufalme.

Mnamo Septemba (Mwezi wa 9) 1939, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilikuwa vimeanza huko Ulaya, na wasiwasi kuhusu vita hivyo uliikumba Marekani yote. Vijana na vilevile watu wazima mbao hawakuelewa msimamo wetu wa kutounga mkono vita, waliwapiga na kuwatesa vijana Mashahidi. Iliripotiwa kwamba kuanzia mwaka wa 1940 hadi 1944, Mashahidi wa Yehova nchini Marekani walishambuliwa mara zaidi ya 2,500 na umati wa watu wenye jeuri. Mateso yaliongezeka hata zaidi wakati Japani iliposhambulia Pearl Harbor mnamo Desemba 7, 1941 (7/12/1941). Majuma machache mapema, nilikuwa nimeanza utumishi wa painia—kama ambavyo watumishi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova wanavyoitwa. Nilijiwekea pesa na kununua nyumba ya kukokotwa na gari ambayo ilikuwa na urefu wa mita 7, na baadhi yetu tulihamia Louisiana ili kuhubiri huko.

Mateso Kusini mwa Marekani

Wakaaji wa eneo hilo walituruhusu kuegesha gari letu katika shamba fulani la matunda karibu na jiji la Jeanerette. Jumamosi moja tuliamua kufanya mahubiri ya barabarani, lakini mkuu wa polisi akawatuma askari wake waje kutukamata na kutufungia katika ukumbi wa jiji. Kundi la watu wapatao 200 hivi lilikusanyika nje, na polisi wakatuachilia bila ulinzi wowote. Tulifurahi kundi hilo lilipofungua njia na kuturuhusu kupita. Siku iliyofuata, tulienda Baton Rouge, jiji kubwa lililokuwa karibu, kuwaeleza Mashahidi wenzetu kile kilichotokea.

Tuliporudi Jeanerette, tulikuta ujumbe umebandikwa kwenye mlango wa gari letu uliosema: “Tafadhali, naomba tukutane katika kambi ya wafanyakazi wa mafuta.” Ujumbe huo ulikuwa na jina, “E. M. Vaughn.” Tulikutana na Bw. Vaughn, naye akatukaribisha kula mlo pamoja naye na mke wake. Alisema kwamba alikuwa kati ya umati wa watu uliokuwa umekusanyika siku ya Jumamosi, na kwamba kama kungalikuwa na tatizo angalitutetea tusishambuliwe na umati huo. Tulimshukuru kwa kututia moyo na kututegemeza.

Siku iliyofuata, askari polisi wakiwa na silaha walitukamata na kuharibu vitabu vyetu. Walichukua ufunguo wa nyumba yetu iliyokokotwa na gari na kunifunga kifungo cha upweke kwa siku 17. Nilipewa chakula kidogo sana. Bw. Vaughn alijitahidi kutusaidia, lakini hakufanikiwa. Tulipokuwa tumefungwa, kundi la watu lilipora vitu vyetu na kuteketeza kila kitu tulichokuwa nacho kutia ndani nyumba yetu ya kukokotwa na gari. Wakati huo, sikujua kwamba Yehova alikuwa akinitayarisha kwa ajili ya yale ambayo muda si mrefu ningeyakabili.

Nafungwa Kaskazini mwa Marekani

Mwezi mmoja baada ya kurudi kaskazini, niliwekwa rasmi kuwa painia wa pekee ili nitumike pamoja na Mashahidi wengine huko Olean, New York. Nikiwa huko, serikali ilitaka nijiandikishe kwa ajili ya utumishi wa kijeshi, lakini niliruhusiwa kutojiandikisha kwa msingi wa dhamiri yangu. Hata hivyo, baada ya kuchunguzwa afya ya mwili na akili, karatasi yangu ilipigwa muhuri ulioonyesha kwamba nilifaa kupata mafunzo ya kijeshi.

Niliendelea na utumishi wa painia kwa mwaka mwingine mmoja hivi. Kisha, mnamo 1943, kwa sababu nilikataa kuacha huduma yangu na kujiunga na mafunzo ya kijeshi, Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI) lilinikamata na kuniagiza niripoti mahakamani huko Syracuse, New York, wiki iliyofuata ili nijibu mashtaka. Nilishtakiwa na kesi yangu ikapangwa kusikilizwa baada ya siku mbili.

Nilijitetea mwenyewe mahakamani. Katika mikutano yetu ya Kikristo, sisi vijana tulipata mazoezi ya jinsi tunavyoweza kutetea haki zetu za kisheria mahakamani na jinsi ya kujiendesha vizuri tukiwa huko. Nilikumbuka vizuri ushauri uliotajwa mwanzoni mwa makala haya. Hata waendesha mashtaka fulani walilalamika kwamba Mashahidi walijua mengi zaidi kuhusu sheria kuliko wao! Hata hivyo, hakimu alisema nina hatia. Hakimu aliponiuliza ikiwa nina jambo lingine zaidi la kusema, nilisema tu, “Leo taifa linahukumiwa mbele ya Mungu kutokana na jinsi linavyowatendea watumishi wake.”

Nilihukumiwa kifungo cha miaka minne katika gereza la Chillicothe, Ohio. Huko nilipewa kazi ya kuwa mwandishi wa ofisa wa gereza. Baada ya majuma machache, mpelelezi maalumu kutoka Washington D.C. alikuja ofisini kwetu na kusema kwamba walikuwa wakimchunguza Hayden Covington. Ndugu Covington alikuwa mwanasheria aliyewawakilisha Mashahidi wa Yehova, na alijulikana kuwa mmoja kati ya wanasheria bora nchini Marekani.

Mpelelezi huyo alisema kwamba anahitaji mafaili ya wafungwa wawili—Danny Hurtado na Edmund Schmidt. Mkubwa wangu akajibu: “Hata Bw. Schmidt mwenyewe ndiye huyu hapa.” Mpelelezi huyo alikuwa ametumwa kisiri, lakini mara moja akatambua kwamba siri hiyo imefichuka. Hivyo, muda si muda nikabadilishiwa kazi na kupelekwa jikoni.

Upainia, Betheli, na Ndoa

Mnamo Septemba 26, 1946, niliachiliwa kwa msamaha wenye masharti, na kuendelea na upainia, wakati huo nikitumika katika Kutaniko la Highland Park huko California. Baadaye, mnamo Septemba 1948, tamaa yangu ya muda mrefu ilitimizwa. Nilialikwa kutumika kama mwokaji mikate katika makao makuu (Betheli) huko Brooklyn, mahali ambapo vitabu vya Biblia vinavyotumiwa kwa ajili ya kazi yetu ya kuhubiri ulimwenguni pote vinachapishwa. Niliacha kazi ya kupika donati katika mkahawa mmoja huko Glendale na kuhamia Betheli.

Miaka saba baadaye, mnamo 1955, makusanyiko kadhaa ya kimataifa yalifanywa barani Ulaya. Familia yangu ilinilipia nauli ili nihudhurie makusanyiko hayo. Nilifurahia kusanyiko huko London, Paris, Rome, na hasa lile lililofanywa Nuremberg, Ujerumani, ambapo zaidi ya watu 107,000 walihudhuria katika uwanja ambao wakati fulani Hitler alikagua kwa kujigamba vikosi vyake vya kijeshi. Katika kusanyiko hilo kulikuwa na baadhi ya Mashahidi ambao Hitler alikuwa ameapa kuwaangamiza. Lilikuwa jambo lenye kuchangamsha moyo kama nini kukusanyika pamoja na ndugu hao!

Katika kusanyiko la Nuremberg, nilikutana na kumpenda mshichana Shahidi Mjerumani—Brigitte Gerwien. Tulioana mwaka mmoja hivi baadaye na nikarudi Glendale kuishi karibu na wazazi wangu. Mwana wetu wa kwanza Tom, alizaliwa mwaka 1957, wa pili Don, akazaliwa mwaka 1958, na binti yetu Sabena, akazaliwa mwaka 1960.

Maisha Yenye Kuridhisha Sana

Watu fulani wameniuliza kama nimewahi kujuta kwa sababu ya kupigwa na kufungwa kwa ajili ya kumtumikia Mungu. Kinyume cha hilo, ninamshukuru Yehova kwamba nilipata pendeleo la kumtumikia nikiwa pamoja na wengi wa watumishi wake waaminifu. Ninatumaini kwamba mambo ambayo nimejionea yatawatia moyo wengine wamkaribie Mungu hata zaidi na kutomwacha kamwe.

Watumishi wengi wa Mungu wameteswa sana kwa sababu ya kumtumikia. Lakini, je, hatukuambiwa tutazamie mambo hayo? Biblia inasema, “wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Hata hivyo, maneno ya Zaburi 34:19 yamethibitika kuwa kweli: “Mwadilifu ana misiba mingi, lakini Yehova humkomboa kutoka katika yote hiyo”!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Tukihubiri huko Louisiana, miaka ya mapema ya 1940

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikioka mikate kwa ajili ya wafanyakazi wa makao makuu

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikiwa na mke wangu Brigitte