Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Umoja wa Kikristo Unamletea Mungu Utukufu

Umoja wa Kikristo Unamletea Mungu Utukufu

Umoja wa Kikristo Unamletea Mungu Utukufu

‘Mjitahidi sana kuushika umoja wa roho.’—EFE. 4:3.

1. Wakristo wa karne ya kwanza huko Efeso walimletea Mungu utukufu jinsi gani?

UMOJA wa kutaniko la Kikristo katika jiji la kale la Efeso ulimletea utukufu Mungu wa kweli, Yehova. Inaonekana kwamba ndugu fulani Wakristo katika kituo hicho cha kibiashara chenye utajiri walikuwa matajiri waliomiliki watumwa, na wengine walikuwa watumwa na labda maskini sana. (Efe. 6:5, 9) Wengine walikuwa Wayahudi ambao walijifunza kweli katika muda wa miezi mitatu ambayo mtume Paulo alikuwa akitoa hotuba katika sinagogi lao. Zamani, wengine wao walikuwa wakiabudu Artemi na walikuwa na zoea la kufanya ufundi wa uchawi. (Mdo. 19:8, 19, 26) Ni wazi kwamba Ukristo wa kweli uliwaunganisha watu wa malezi mbalimbali. Paulo alitambua kwamba umoja wa kutaniko ulimletea Yehova utukufu. Mtume huyo aliandika hivi: “Kwake kuwe na utukufu kwa njia ya kutaniko.”—Efe. 3:21.

2. Ni nini kilichohatarisha umoja wa Wakristo huko Efeso?

2 Hata hivyo, umoja uliobarikiwa wa kutaniko la Efeso ulikabili hatari. Paulo aliwaonya hivi wazee: “Kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Mdo. 20:30) Pia, ndugu fulani hawakuwa wameacha kabisa roho inayosababisha migawanyiko ambayo Paulo alionya kwamba ‘inatenda katika wana wa kutotii.’—Efe. 2:2; 4:22.

Barua Inayokazia Umoja

3, 4. Barua ya Paulo kwa Waefeso inakazia jinsi gani umoja?

3 Paulo alitambua kwamba ili Wakristo waendelee kushirikiana kwa upatano, ni lazima kila mmoja wao ajitahidi kabisa kudumisha umoja. Mungu alimwongoza Paulo kupitia roho takatifu kuwaandikia Waefeso barua ambayo ilikazia umoja. Kwa mfano, Paulo aliandika kuhusu kusudi la Mungu la “kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo.” (Efe. 1:10) Pia, aliwafananisha Wakristo na mawe mbalimbali yanayotumiwa kujenga jengo. “Jengo lote likiunganishwa pamoja kwa upatano, linakua liwe hekalu takatifu kwa ajili ya Yehova.” (Efe. 2:20, 21) Zaidi ya hayo, Paulo alikazia umoja wa Wakristo Wayahudi na wasio Wayahudi na pia akawakumbusha ndugu hao kwamba wote waliumbwa na Mungu. Alimwita Yehova, ‘Baba, ambaye kila familia mbinguni na duniani hupata jina kutokana naye.’—Efe. 3:5, 6, 14, 15.

4 Tunapochunguza sura ya 4 ya Waefeso, tutaona kwa nini jitihada zinahitajiwa ili kudumisha umoja, jinsi Yehova anavyotusaidia kuungana, na mitazamo ambayo itatusaidia kudumisha umoja wetu. Kwa nini usisome sura nzima ili ufaidike zaidi na funzo hili?

Kwa Nini Umoja Unahitaji Jitihada Nyingi?

5. Kwa nini malaika wa Mungu wanamtumikia kwa umoja, lakini kwa nini ni vigumu zaidi kwetu kudumisha umoja?

5 Paulo aliwasihi ndugu zake Waefeso ‘wajitahidi sana kuushika umoja wa roho.’ (Efe. 4:3) Ili kuelewa kwa nini jitihada zinahitajiwa katika jambo hilo, fikiria hali ya malaika wa Mungu. Hakuna vitu viwili vilivyo hai duniani ambavyo vinafanana kabisa, kwa hiyo tunaweza kukata kauli kwamba Yehova amembariki kila mmoja kati ya mamilioni ya malaika wake kwa kumuumba akiwa na utu wa kipekee. (Dan. 7:10) Hata hivyo, wanaweza kumtumikia Yehova kwa umoja kwa sababu wote wanamsikiliza na kufanya mapenzi yake. (Soma Zaburi 103:20, 21.) Malaika waaminifu wana sifa tofauti-tofauti kama Wakristo walivyo na sifa tofauti-tofauti, lakini Wakristo wana udhaifu mbalimbali pia. Udhaifu huo unaweza kufanya iwe vigumu zaidi kudumisha umoja.

6. Ni mitazamo gani itakayotusaidia kufurahia kushirikiana na ndugu ambao wana udhaifu tofauti na wetu?

6 Ni rahisi kwa watu wasio wakamilifu kukosana wanapojaribu kushirikiana. Kwa mfano, namna gani ikiwa ndugu mpole ambaye mara nyingi anachelewa kufika anamtumikia Yehova akishirikiana na ndugu ambaye hachelewi lakini ambaye anakasirika haraka? Huenda kila mmoja wao akahisi kwamba mwenzake anajiendesha kwa njia isiyofaa lakini labda anasahau kwamba yeye pia anajiendesha kwa njia fulani isiyofaa. Ndugu wawili kama hao wanaweza kutumika pamoja jinsi gani kwa umoja? Ona jinsi mitazamo ambayo Paulo alipendekeza katika maneno yake yanayofuata inavyoweza kuwasaidia. Kisha ufikirie jinsi tunavyoweza kudumisha umoja kwa kusitawisha mitazamo hiyo. Paulo aliandika hivi: “[Mimi] nawasihi ninyi mtembee kwa kuustahili . . . mkiwa na unyenyekevu kamili wa akili na upole, mkiwa na ustahimilivu, mkivumiliana katika upendo, mkijitahidi sana kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.”—Efe. 4:1-3.

7. Kwa nini ni jambo la maana kujitahidi kuwa na umoja na Wakristo wengine wasio wakamilifu?

7 Kujifunza kumtumikia Mungu kwa umoja pamoja na watu wengine wasio wakamilifu ni jambo la maana kwa sababu kuna kikundi au mwili mmoja tu wa waabudu wa kweli. “Kuna mwili mmoja, na roho moja, kama vile mlivyoitwa katika tumaini moja mliloitiwa; Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja; Mungu mmoja na Baba wa watu wote.” (Efe. 4:4-6) Roho ya Yehova na baraka zake ziko juu ya ule ushirika mmoja wa ndugu ambao Mungu anatumia. Hata ikiwa mtu fulani katika kutaniko anatukasirisha, tunaweza kwenda mahali gani pengine? Hatuwezi kusikia maneno ya uzima wa milele mahali pengine popote.—Yoh. 6:68.

Wale Ambao Ni “Zawadi Katika Wanadamu” Wanadumisha Umoja

8. Kristo anatumia nani ili kutusaidia kupata nguvu za kushinda uvutano unaosababisha migawanyiko?

8 Akitumia zoea fulani ambalo askari-jeshi walikuwa nalo nyakati za kale, Paulo alionyesha jinsi Yesu alivyotoa “zawadi katika wanadamu” ili kusaidia kuunganisha kutaniko. Askari-jeshi aliyeshinda vitani angeweza kumchukua mtu mateka kutoka nchi nyingine na kumleta nyumbani ili awe mtumwa wake na kumsaidia mke wake kazi. (Zab. 68:1, 12, 18) Vivyo hivyo, ushindi wa Yesu juu ya ulimwengu ulimsaidia kupata watumwa wengi walio tayari kumtumikia. (Soma Waefeso 4:7, 8.) Aliwatumia jinsi gani mateka hao wa mfano? “Alitoa wengine kuwa mitume, wengine kuwa manabii, wengine kuwa waeneza-injili, wengine kuwa wachungaji na walimu, kwa kusudi la kuwarekebisha upya watakatifu, kwa ajili ya kazi ya huduma, kwa ajili ya kuujenga mwili wa Kristo, mpaka sisi sote tuufikie umoja katika imani.”—Efe. 4:11-13.

9. (a) Wale ambao ni “zawadi katika wanadamu” wanasaidia jinsi gani kudumisha umoja wetu? (b) Kwa nini kila mshiriki wa kutaniko anapaswa kuchangia umoja wa kutaniko?

9 Wakiwa wachungaji wenye upendo, wazee hao ambao ni “zawadi katika wanadamu” wanasaidia kudumisha umoja wetu. Kwa mfano, mzee wa kutaniko akiona ndugu wawili ‘wakichochea mashindano juu ya mtu na mwenzake,’ anaweza kusaidia sana kudumisha umoja katika kutaniko kwa kuwapa shauri la faragha, ili ‘kuwarekebisha upya katika roho ya upole.’ (Gal. 5:26–6:1) Wakiwa walimu, wazee hao ambao ni “zawadi katika wanadamu” wanatusaidia kujenga imani yenye nguvu inayotegemea mafundisho ya Biblia. Hivyo, wanadumisha umoja na kutusaidia kufikia ukomavu wa Kikristo. Paulo aliandika kwamba kusudi ni “ili tusiwe tena watoto wachanga, tukirushwa huku na huku kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho kupitia udanganyifu wa watu, kwa njia ya ujanja katika kutunga kosa.” (Efe. 4:13, 14) Kila Mkristo anapaswa kuchangia umoja wa undugu wetu, kama vile tu ambavyo kila kiungo cha mwili wetu kinavyojenga viungo vingine kwa kuandaa kile kinachohitajiwa.—Soma Waefeso 4:15, 16.

Sitawisha Mitazamo Mipya

10. Mwenendo mpotovu unaweza kuhatarisha umoja wetu namna gani?

10 Je, uliona kwamba sura ya nne ya barua ya Paulo kwa Waefeso inaonyesha kwamba kuonyesha upendo kwa matendo ndio ufunguo wa kupata umoja tukiwa Wakristo wakomavu? Kisha, inataja mambo ambayo yanahusika katika kuonyesha upendo. Kwanza, ili mtu afuate njia ya upendo ni lazima aepuke kabisa uasherati na mwenendo mpotovu. Paulo aliwahimiza ndugu zake ‘wasiendelee tena kutembea kama vile mataifa wanavyotembea pia.’ Watu hao walikuwa ‘wameishiwa na ufahamu wote wa maadili,’ na “walijitoa wenyewe ili kuwa na mwenendo mpotovu.” (Efe. 4:17-19) Ulimwengu wenye maadili mapotovu ambamo tunaishi unahatarisha umoja wetu. Watu wanafanya mizaha kuhusu uasherati, wanaimba nyimbo kuhusu uasherati, wanatazama uasherati ili kujiburudisha, na wanafanya uasherati katika siri au waziwazi. Lakini, hata kuchezeana kimapenzi, yaani, kutenda kana kwamba unavutiwa kingono na mtu mwingine ambaye hukusudii kumuoa, kunaweza kukutenganisha na Yehova na kutaniko. Kwa nini? Kwa sababu kufanya hivyo kunaongoza kwa urahisi sana katika uasherati. Pia, kuchezeana kimapenzi ambako kunamwongoza mtu aliyefunga ndoa kutumbukia katika uzinzi kunaweza kuwatenganisha kikatili watoto na wazazi wao na wenzi wasio na hatia na wenzi wao wa ndoa. Kwa kweli, zoea hilo linatenganisha watu! Si ajabu kwamba Paulo aliandika hivi: “Ninyi hamkujifunza Kristo kuwa hivyo”!—Efe. 4:20, 21.

11. Biblia inawatia moyo Wakristo wafanye badiliko gani?

11 Paulo alikazia kwamba tunapaswa kuacha njia za kufikiri zinazovuruga umoja na badala yake tusitawishe mitazamo ambayo inatuwezesha kuishi kwa upatano na wengine. Alisema hivi: “Mnapaswa kuuondolea mbali utu wa zamani unaolingana na mwenendo wenu wa kwanza na ambao unaharibiwa kulingana na tamaa zake [za utu wa zamani] za udanganyifu; . . . mnapaswa kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yenu, na mnapaswa kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.” (Efe. 4:22-24) Tunaweza jinsi gani ‘kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yetu’? Tukitafakari na kuthamini mambo tunayojifunza kutoka katika Neno la Mungu na kutokana na mifano mizuri ya Wakristo wakomavu, na tukijitahidi sana, tunaweza kuvaa utu mpya “ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu.”

Sitawisha Njia Mpya za Kuzungumza

12. Kusema kweli kunadumisha umoja jinsi gani, na kwa nini ni vigumu kwa wengine kusema kweli?

12 Ni jambo la maana kwa wale ambao ni mwili mmoja katika familia au katika kutaniko kusema kweli. Kuongea kwa unyoofu, kwa fadhili, na waziwazi, kunaweza kuwaunganisha watu. (Yoh. 15:15) Lakini namna gani ikiwa mtu anamdanganya ndugu yake? Ndugu yake akitambua hilo, kifungo cha kuaminiana kati yao kitadhoofika. Basi, unaweza kuelewa kwa nini Paulo aliandika hivi: “Semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake, kwa sababu sisi ni viungo vya mtu na mwenzake.” (Efe. 4:25) Inaweza kuwa vigumu kwa mtu kuanza kusema kweli ikiwa amezoea kusema uwongo, na labda alianza kusema uwongo akiwa mtoto. Lakini Yehova anathamini jitihada za mtu huyo za kubadilika na atamsaidia.

13. Kuondolea mbali matukano kunahusisha nini?

13 Yehova anatufundisha kudumisha heshima na umoja katika kutaniko na katika familia kwa kuweka mipaka thabiti kuhusiana na njia yetu ya kusema. “Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu . . . Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.” (Efe. 4:29, 31) Njia moja ya kuepuka kusema maneno yenye kuudhi ni kusitawisha mtazamo wenye heshima zaidi kuelekea wengine. Kwa mfano, mtu anayemtukana mke wake anapaswa kujitahidi kubadili mtazamo wake kumwelekea, hasa anapojifunza jinsi Yehova anavyowaheshimu wanawake. Mungu hata anawatia mafuta kwa roho takatifu wanawake fulani, na kuwapa tumaini la kutawala wakiwa wafalme pamoja na Kristo. (Gal. 3:28; 1 Pet. 3:7) Vivyo hivyo, mwanamke ambaye ana tabia ya kumpigia kelele mume wake anapaswa kuchochewa kubadilika anapojifunza jinsi Yesu alivyojizuia alipochokozwa.—1 Pet. 2:21-23.

14. Kwa nini kuonyesha hasira ni hatari?

14 Matukano yanahusiana sana na kutozuia hasira. Jambo hilo pia linaweza kuwatenganisha watu ambao ni viungo vya mwili mmoja. Hasira ni kama moto. Inaweza kwa urahisi kupita mipaka na kusababisha msiba. (Met. 29:22) Ni lazima mtu ambaye ana sababu nzuri ya kukasirika azuie hasira yake kwa uangalifu ili aepuke kuharibu mahusiano yenye thamani. Wakristo wanapaswa kujitahidi kuwa wenye kusamehe, na hawapaswi kuweka kinyongo moyoni na kuzungumza tena kuhusu jambo hilo. (Zab. 37:8; 103:8, 9; Met. 17:9) Paulo aliwashauri hivi Waefeso: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.” (Efe. 4:26, 27) Kutozuia hasira kunaweza kumpa Ibilisi nafasi ya kusababisha migawanyiko na hata mizozano ndani ya kutaniko.

15. Kuchukua kitu ambacho si chetu kunaweza kuwa na matokeo gani?

15 Kuheshimu mali ya wengine kunachangia umoja katika kutaniko. Tunasoma hivi: “Mwizi asiibe tena.” (Efe. 4:28) Kwa ujumla, watu wa Yehova wamesitawisha hali ya kuaminiana. Ikiwa Mkristo angetumia vibaya hali hiyo ya kuaminiana kwa kuchukua kitu ambacho si chake, angeharibu umoja huo unaoleta furaha.

Kumpenda Mungu Kunatuunganisha

16. Tunaweza kutumia jinsi gani usemi wenye kujenga ili kutia nguvu umoja wetu?

16 Kuna umoja katika kutaniko la Kikristo kwa sababu wote wanachochewa kumpenda Mungu kwa kuwatendea wengine kwa njia ya upendo. Kuthamini fadhili za Yehova kunatuchochea kujitahidi kabisa kufuata shauri hili: “[Semeni] neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa. . . . Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.” (Efe. 4:29, 32) Yehova anawasamehe kwa fadhili watu wasio wakamilifu kama sisi. Je, sisi pia hatupaswi kuwasamehe wengine tunapoona udhaifu wao?

17. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kabisa kudumisha umoja?

17 Umoja wa watu wa Mungu unamletea Yehova utukufu. Roho yake inatuchochea kwa njia mbalimbali kudumisha umoja. Bila shaka, hatungependa kukataa mwongozo wa roho. Paulo aliandika hivi: “Msiwe mkiihuzunisha roho takatifu ya Mungu.” (Efe. 4:30) Umoja ni hazina ambayo inastahili kulindwa. Unawaletea shangwe wote ambao wana umoja na unamletea Yehova utukufu. “Kwa hiyo, iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo.”—Efe. 5:1, 2.

Ungesema Nini?

• Ni mitazamo gani inayodumisha umoja kati ya Wakristo?

• Mwenendo wetu unaweza jinsi gani kudumisha umoja katika kutaniko?

• Usemi wetu unaweza kutusaidia jinsi gani kushirikiana na wengine?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Watu wa malezi mbalimbali wameunganishwa pamoja

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, unaelewa hatari za kuchezeana kimapenzi?