Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kiongozi Wenu Ni Mmoja, Kristo”

“Kiongozi Wenu Ni Mmoja, Kristo”

“Kiongozi Wenu Ni Mmoja, Kristo”

“Msiitwe ‘viongozi,’ kwa maana Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.”—MT. 23:9, 10.

1. Mashahidi wa Yehova wanamtambua nani kuwa Kiongozi wao, na kwa nini?

MAKANISA yanayodai kuwa ya Kikristo yana viongozi wa kibinadamu, kama vile papa wa Roma, wazee na makasisi wa majimbo wa makanisa ya Othodoksi ya Mashariki, na viongozi wa dini nyingine. Mashahidi wa Yehova hawamtambui mwanadamu yeyote kuwa kiongozi wao. Wao si wanafunzi au wafuasi wa mwanadamu yeyote. Hilo linapatana na maneno haya ya kinabii ya Yehova kumhusu Mwana wake: “Tazama! Nimemtoa kuwa shahidi kwa vikundi vya mataifa, kuwa kiongozi na kamanda kwa vikundi vya mataifa.” (Isa. 55:4) Kutaniko la kimataifa la Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao, “kondoo wengine,” hawataki kiongozi mwingine ila tu yule ambaye Yehova amewapa. (Yoh. 10:16) Wanatii maneno haya ya Yesu: “Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.”—Mt. 23:10.

Mkuu wa Kiroho wa Israeli

2, 3. Mwana wa Mungu alifanya kazi gani katika Israeli?

2 Karne nyingi kabla ya kuanzishwa kwa kutaniko la Kikristo, Yehova alimtumia malaika kuwaongoza watu wake wa taifa la Israeli. Baada ya kuwatoa Waisraeli Misri, Yehova aliwaambia hivi: “Tazama, ninamtuma malaika mbele yako ili akuongoze barabarani na kukuingiza mahali ambapo nimetayarisha. Jiangalie kwa sababu yake na kuitii sauti yake. Usijiendeshe kwa kumwasi yeye, kwa maana hatawasamehe kosa lenu; kwa sababu jina langu limo ndani yake.” (Kut. 23:20, 21) Ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba malaika huyo ambaye ‘jina la Yehova lilikuwa ndani yake,’ alikuwa Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu.

3 Kabla ya kuzaliwa akiwa mwanadamu, inaonekana kwamba Mwana wa Mungu aliitwa Mikaeli. Katika kitabu cha Danieli, Mikaeli anaitwa ‘yule mkuu wa watu wa Danieli,’ Israeli. (Dan. 10:21) Mwanafunzi Yuda anaonyesha kwamba Mikaeli alihusika katika shughuli za Waisraeli kabla ya siku za Danieli. Baada ya kifo cha Musa, inaonekana kwamba Shetani alikusudia kuutumia mwili wa Musa ili kuendelea kwa njia fulani kujitafutia faida zake mwenyewe. Huenda alitaka kufanya hivyo kwa kuwachochea Waisraeli waabudu sanamu. Mikaeli aliingilia kati ili kuzuia jambo hilo lisitokee. Yuda anasema hivi: “Wakati Mikaeli, yule malaika mkuu alipokuwa na tofauti na Ibilisi na kubishana naye juu ya mwili wa Musa, yeye hakuthubutu kumhukumu kwa matukano, bali alisema: ‘Yehova na akukemee.’” (Yuda 9) Muda mfupi baadaye, kabla ya kuzingirwa kwa Yeriko, bila shaka Mikaeli, yule “mkuu wa jeshi la Yehova,” ndiye aliyemtokea Yoshua na kumhakikishia kwamba Mungu alikuwa pamoja naye. (Soma Yoshua 5:13-15.) Wakati roho mmoja mwovu mkuu alipojaribu kumzuia malaika kwenda kumpelekea nabii Danieli ujumbe fulani wa maana, Mikaeli, yule malaika mkuu, alimsaidia malaika huyo.—Dan. 10:5-7, 12-14.

Kiongozi Aliyetabiriwa Anafika

4. Ni unabii gani ambao ulitolewa kuhusu kuja kwa yule Masihi?

4 Kabla ya tukio hilo, Yehova alikuwa amemtuma malaika wake Gabrieli kwa nabii Danieli ili ampe unabii kuhusu kuja kwa “Masihi aliye Kiongozi.” (Dan. 9:21-25) * Kwa wakati unaofaa kabisa, mwishoni mwa mwaka wa 29 W.K., Yesu alibatizwa na Yohana. Roho takatifu ilimiminwa juu ya Yesu, na hivyo kumfanya kuwa Mtiwa-Mafuta, yaani, Kristo, yule Masihi. (Mt. 3:13-17; Yoh. 1:29-34; Gal. 4:4) Akiwa Masihi, Yesu angekuja kuwa Kiongozi asiye na kifani.

5. Kristo alitenda jinsi gani akiwa Kiongozi wakati wa huduma yake duniani?

5 Tangu mwanzo wa huduma yake duniani, Yesu alijithibitisha kuwa “Masihi aliye Kiongozi.” Baada ya siku chache tu, Yesu alianza kuwakusanya wanafunzi, na akafanya muujiza wake wa kwanza. (Yoh. 1:35–2:11) Wanafunzi wake walimfuata aliposafiri kotekote nchini, akihubiri habari njema ya Ufalme. (Luka 8:1) Aliwazoeza katika kazi ya kuhubiri na akawaongoza katika kuhubiri na kufundisha, na hivyo akawawekea mfano mzuri. (Luka 9:1-6) Wazee Wakristo leo wanapaswa kumwiga katika jambo hilo.

6. Kristo alijithibitisha katika njia gani kuwa Mchungaji na Kiongozi?

6 Yesu alionyesha sifa yake nyingine akiwa kiongozi kwa kujilinganisha na mchungaji mwenye upendo. Wachungaji wa mashariki wanawaongoza kihalisi wanyama wao. Katika kitabu kimoja (The Land and the Book), W. M. Thomson aliandika hivi: “Mchungaji anaenda mbele, si kuonyesha njia tu, bali kuona ikiwa njia hiyo inafaa na ni salama. . . . Akiwa na fimbo [yake] anawaongoza na kuwaelekeza wanyama kwenye malisho mazuri, naye anawalinda kutokana na maadui.” Akionyesha kwamba yeye ni Mchungaji wa kweli na Kiongozi, Yesu alisema hivi: “Mimi ndiye mchungaji mwema; mchungaji mwema huitoa nafsi yake kwa ajili ya kondoo. Kondoo wangu huisikiliza sauti yangu, nami ninawajua, nao wananifuata.” (Yoh. 10:11, 27) Kupatana na maneno yake, Yesu alikufa kifo cha kidhabihu kwa ajili ya kondoo wake, lakini Yehova “alimfufua ili awe kiongozi na Mwokozi.”—Mdo. 5:31, New Jerusalem Bible; Ebr. 13:20.

Mwangalizi wa Kutaniko la Kikristo

7. Yesu analiongoza kutaniko la Kikristo kupitia nini?

7 Muda mfupi kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliyefufuliwa aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mt. 28:18) Kwa uwezo wa Yehova, Yesu aliwapa wanafunzi wake roho takatifu ili iwatie nguvu katika kweli ya Kikristo. (Yoh. 15:26) Yesu aliwamiminia roho hiyo Wakristo wa mapema siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. (Mdo. 2:33) Kutaniko la Kikristo lilianzishwa wakati huo ambao roho takatifu ilimiminwa. Huko mbinguni, Yehova alimweka Mwana wake kuwa kiongozi juu ya kutaniko lote duniani. (Soma Waefeso 1:22; Kol. 1:13, 18.) Yesu analiongoza kutaniko la Kikristo kupitia roho takatifu ya Yehova, na ana malaika ambao ‘walitiishwa kwake.’—1 Pet. 3:22.

8. Katika karne ya kwanza, Kristo alitumia nani duniani ili kuwaongoza wanafunzi wake, na anatumia nani leo?

8 Pia, kupitia roho takatifu, Kristo alitoa “zawadi katika wanadamu,” wengine ‘wakiwa wachungaji na walimu’ katika kutaniko. (Efe. 4:8, 11) Mtume Paulo aliwahimiza hivi waangalizi Wakristo: “Jiangalieni ninyi wenyewe na kundi lote, ambalo roho takatifu imewaweka ninyi rasmi kuwa waangalizi kati yake, kulichunga kutaniko la Mungu.” (Mdo. 20:28) Kutaniko la Kikristo lilipoanza, waangalizi hao wote walikuwa wanaume waliotiwa mafuta kwa roho. Mitume na wazee wa kutaniko la Yerusalemu walikuwa baraza linaloongoza. Kristo aliwatumia kuongoza kundi lote la “ndugu” zake watiwa-mafuta duniani. (Ebr. 2:11; Mdo. 16:4, 5) Katika wakati huu wa mwisho, Kristo amemkabidhi “mali zake zote,” yaani, faida zake zote za Ufalme duniani, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” na mwakilishi wa mtumwa huyo, Baraza Linaloongoza, ambacho ni kikundi cha wanaume Wakristo watiwa-mafuta. (Mt. 24:45-47) Watiwa-mafuta na waandamani wenzao, kondoo wengine, wanatambua kwamba wanapofuata uongozi wa Baraza Linaloongoza la siku zetu, kwa kweli wanamfuata Kiongozi wao, Kristo.

Kristo Anaanzisha Kazi ya Kuhubiri

9, 10. Kristo aliongoza mambo jinsi gani katika kueneza habari njema ya Ufalme?

9 Tangu mwanzoni, Yesu mwenyewe aliongoza kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri na kufundisha. Aliweka utaratibu ambao ungefuatwa katika kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa wakaaji wa dunia. Wakati wa huduma yake, aliwaagiza hivi mitume wake: “Msiende katika barabara ya mataifa, na msiingie katika jiji la Wasamaria; bali, badala ya hivyo, nendeni kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. Mnapoenda, hubirini, mkisema, ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’” (Mt. 10:5-7) Walihubiri ujumbe huo kwa bidii kati ya Wayahudi na watu waliogeuzwa imani, hasa baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.—Mdo. 2:4, 5, 10, 11; 5:42; 6:7.

10 Baadaye, kupitia roho takatifu, Yesu alieneza kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme kwa Wasamaria na kisha kwa watu wengine wasio Wayahudi. (Mdo. 8:5, 6, 14-17; 10:19-22, 44, 45) Akiwa na nia ya kueneza habari njema katikati ya mataifa, Yesu mwenyewe alimchochea Sauli wa Tarso kuwa Mkristo. Yesu alimwagiza hivi mwanafunzi wake Anania: “Ondoka, uende kwenye barabara inayoitwa Nyoofu, na kwenye nyumba ya Yuda tafuta mtu anayeitwa jina Sauli, kutoka Tarso. . . . Ondoka uende, kwa sababu mtu huyu ni chombo kilichochaguliwa kwangu ili kupeleka jina langu kwa mataifa na vilevile kwa wafalme na wana wa Israeli.” (Mdo. 9:3-6, 10, 11, 15) “Mtu huyu” alikuja kuwa mtume Paulo.—1 Tim. 2:7.

11. Kristo alipanua jinsi gani kazi ya kuhubiri akitumia roho takatifu?

11 Wakati ulipofika wa kupanua kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme katikati ya mataifa yasiyo ya Kiyahudi, Paulo alipata mwongozo kutoka mbinguni wa kwenda katika Asia Ndogo na Ulaya kwa ajili ya safari za umishonari. Simulizi la Luka katika Matendo linasema hivi: “Walipokuwa [manabii na walimu Wakristo katika kutaniko la Antiokia ya Siria] wakimhudumia Yehova hadharani na kufunga, roho takatifu ikasema: ‘Kati ya watu wote wekeni kando Barnaba na Sauli kwa ajili yangu kwa kazi ambayo nimewaitia wao.’ Ndipo wakafunga na kusali na kuweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.” (Mdo. 13:2, 3) Yesu mwenyewe alimwita Sauli wa Tarso kuwa “chombo [Chake] kilichochaguliwa” ili kulipeleka jina Lake kwa mataifa; hivyo, nguvu hiyo mpya kwa kazi ya kutoa ushahidi ilitoka kwa Kristo, ambaye ni Kiongozi wa kutaniko. Wakati wa safari ya pili ya Paulo ya umishonari ilikuwa wazi kwamba Yesu alikuwa akitumia roho takatifu ili kuongoza kazi ya kuhubiri. Simulizi hilo linasema kwamba “roho ya Yesu,” yaani, Yesu alimwongoza Paulo na wasafiri wenzake kupitia roho takatifu, kuamua wakati na mahali ambapo wangeenda, na walipata maono ambayo yaliwaelekeza Ulaya.—Soma Matendo 16:6-10.

Uongozi wa Yesu Juu ya Kutaniko Lake

12, 13. Kitabu cha Ufunuo kinaonyesha jinsi gani kwamba Kristo anachunguza kwa makini mambo yanayotendeka katika kila kutaniko?

12 Yesu alichunguza kwa makini mambo yaliyokuwa yakitendeka katika makutaniko ya wafuasi wake watiwa-mafuta katika karne ya kwanza W.K. Alijua vizuri sana hali ya kiroho ya kila kutaniko. Jambo hilo linaonekana wazi hasa tunaposoma Ufunuo sura ya 2 na ya 3. Anataja makutaniko saba yaliyo katika Asia Ndogo. (Ufu. 1:11) Tuna kila sababu ya kuamini kwamba alijua pia hali ya kiroho ya makutaniko mengine ya wafuasi wake yaliyokuwa duniani wakati huo.—Soma Ufunuo 2:23.

13 Yesu aliyapongeza makutaniko mengine kwa sababu ya uvumilivu wao, uaminifu chini ya majaribu, ushikamanifu kwa neno lake, na kwa kuwakataa waasi-imani. (Ufu. 2:2, 9, 13, 19; 3:8) Kwa upande mwingine, alitoa mashauri makali kwa makutaniko fulani kwa sababu upendo wao kumwelekea ulikuwa umepoa, pia yaliruhusu ibada ya sanamu, uasherati, na madhehebu kati yao. (Ufu. 2:4, 14, 15, 20; 3:15, 16) Akiwa mwangalizi wa kiroho mwenye upendo, hata kwa wale ambao aliwashauri kwa ukali, Yesu alisema hivi: “Wale wote ninaowapenda, mimi huwakaripia na kuwatia nidhamu. Kwa hiyo uwe mwenye bidii na utubu.” (Ufu. 3:19) Ingawa alikuwa mbinguni, Yesu alikuwa akiyaongoza makutaniko ya wanafunzi wake duniani kupitia roho takatifu. Mwishoni mwa ujumbe mbalimbali kwa makutaniko hayo, alisema hivi: “Yeye aliye na sikio na asikie yale ambayo roho inayaambia makutaniko.”—Ufu. 3:22.

14-16. (a) Yesu amejithibitisha jinsi gani kuwa Kiongozi mwenye ujasiri wa watu wa Yehova duniani? (b) Kumekuwa na matokeo gani kwa sababu ya Yesu kuwa “pamoja” na wanafunzi wake “siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo”? (c) Tutazungumzia nini katika habari inayofuata?

14 Tumeona kwamba Mikaeli (Yesu) alijithibitisha kuwa Kiongozi wa Israeli ambaye ni malaika mwenye nguvu. Baadaye, Yesu alikuwa Kiongozi mwenye ujasiri na Mchungaji mwenye upendo wa wanafunzi wake wa mapema. Wakati wa huduma yake duniani, aliongoza katika kazi ya kuhubiri. Na baada ya kufufuliwa, aliongoza moja kwa moja kazi ya kueneza habari njema ya Ufalme.

15 Kupitia roho takatifu, mwishowe Yesu angepanua kazi ya kutoa ushahidi mpaka kwenye miisho ya dunia. Kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8; soma 1 Petro 1:12.) Chini ya mwongozo wa Kristo, ushahidi mkubwa ulitolewa katika karne ya kwanza.—Kol. 1:23.

16 Lakini Yesu mwenyewe alionyesha kwamba kazi hiyo ingeendelea mpaka wakati wa mwisho. Baada ya kuwaamuru wafuasi wake wahubiri na kufanya wanafunzi kutoka katika mataifa yote, Yesu aliwaahidi hivi: “Mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20) Tangu apewe mamlaka ya kifalme mwaka wa 1914, Kristo yupo “pamoja” na wanafunzi wake kuliko wakati mwingine wowote naye anatenda akiwa Kiongozi wao. Habari inayofuata itazungumzia utendaji wake mwingi tangu mwaka wa 1914.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kwa habari zaidi kuhusu unabii huo, ona sura ya 11 ya kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!

Kwa Kupitia

• Mwana wa Mungu alijithibitisha jinsi gani kuwa Kiongozi mwenye kutenda kwa bidii katika Israeli?

• Kristo analiongoza kutaniko lake duniani kwa njia gani?

• Kristo ameongoza jinsi gani kazi ya kueneza habari njema?

• Ni nini kinachoonyesha kwamba Kristo anachunguza kwa makini hali ya kiroho ya kila kutaniko?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

“Ninamtuma malaika mbele yako”

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kristo anatumia “zawadi katika wanadamu” ili kulichunga kundi lake kama alivyofanya zamani