Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kiongozi Wetu Anayetenda kwa Bidii Leo

Kiongozi Wetu Anayetenda kwa Bidii Leo

Kiongozi Wetu Anayetenda kwa Bidii Leo

“Akaenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.”—UFU. 6:2.

1, 2. (a) Utendaji wa kifalme wa Kristo tangu mwaka wa 1914 unaonyeshwa jinsi gani katika Biblia? (b) Ni hatua gani ambazo Kristo amechukua tangu awekwe rasmi kuwa mfalme?

KRISTO aliwekwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi wa Yehova mwaka wa 1914. Tunawazia yeye ni nani leo? Je, tunawazia yeye ni mfalme mwenye kutafakari ambaye ameketi juu ya kiti chake cha ufalme, akitazama chini mara kwa mara ili kuona jinsi kutaniko lake linavyoendelea? Ikiwa tunawazia hivyo, tunapaswa kubadili maoni yetu. Katika Zaburi na katika kitabu cha Ufunuo anaonyeshwa akiwa mfalme mwenye nguvu aliye juu ya farasi, naye anaenda “akishinda na kukamilisha ushindi wake,” akiendelea ‘kufanikiwa’ mpaka mwisho.—Ufu. 6:2; Zab. 2:6-9; 45:1-4.

2 Hatua ya kwanza ya kifalme ambayo Kristo alichukua baada ya kuwekwa rasmi kuwa mfalme ni kumshinda yule “joka mkubwa na malaika zake.” Akiwa malaika mkuu Mikaeli, na akiongoza malaika wake, Kristo alimtupa Shetani na roho wake waovu kutoka mbingu takatifu na kuwazuilia kwenye ujirani wa dunia. (Ufu. 12:7-9) Kisha, katika daraka lake akiwa ‘mjumbe wa Yehova wa agano,’ Yesu alikuja pamoja na Baba yake kukagua hekalu la kiroho. (Mal. 3:1) Alizihukumu dini zinazodai kuwa za Kikristo, sehemu yenye kulaumika zaidi ya “Babiloni Mkubwa,” akazipata na hatia ya kumwaga damu na kufanya uzinzi wa kiroho pamoja na mfumo wa kisiasa wa ulimwengu huu.—Ufu. 18:2, 3, 24.

Kumsafisha Mtumwa Wake Aliye Duniani

3, 4. (a) Kristo alitimiza kazi gani akiwa “mjumbe” wa Yehova? (b) Ukaguzi wa hekalu ulifunua nini, na akiwa Kichwa cha kutaniko, Yesu alimweka nani rasmi?

3 Ukaguzi uliofanywa na Yehova na “mjumbe” wake ulifunua pia kwamba katika ua wa kidunia wa hekalu hilo la kiroho kuna kikundi cha Wakristo wa kweli, ambao hawakuwa sehemu ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Lakini, hata Wakristo hao watiwa-mafuta, au “wana wa Lawi,” walihitaji pia kusafishwa. Ilikuwa tu kama vile nabii Malaki alivyokuwa ametabiri: “[Yehova] ataketi kama msafishaji na mtakasaji wa fedha naye atawatakasa wana wa Lawi; naye atawasafisha kama dhahabu na kama fedha, nao watakuwa kwa Yehova watu wanaotoa toleo la zawadi katika uadilifu.” (Mal. 3:3) Yehova alimtumia ‘mjumbe wake wa agano,’ Kristo Yesu, kuwasafisha Waisraeli hao wa kiroho.

4 Hata hivyo, Kristo aliwakuta Wakristo haohao waaminifu waliotiwa mafuta wakifanya yote wawezayo ili kuwaandalia watu wa nyumba ya imani chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Kuanzia mwaka wa 1879 na kuendelea, katika hali zinazofaa na zisizofaa, walikuwa wakitangaza kweli za Biblia kuhusu Ufalme wa Mungu kupitia gazeti hili. Yesu alikuwa ametabiri kwamba wakati ambapo ‘angefika’ kuwakagua watumishi wake wa nyumbani wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo,” angemkuta mtumwa fulani akiwaandalia watumishi hao “chakula chao kwa wakati unaofaa.” Angemtangaza mtumwa huyo kuwa mwenye furaha na ‘angemweka juu ya mali zake zote’ duniani. (Mt. 24:3, 45-47) Akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Kristo amemtumia ‘mtumwa huyo mwaminifu na mwenye busara’ kusimamia mambo ya Ufalme Wake duniani. Ameandaa mwongozo kwa ‘watumishi wa nyumbani,’ watiwa-mafuta na waandamani wao, “kondoo wengine,” kupitia Baraza Linaloongoza.—Yoh. 10:16.

Kuvuna Dunia

5. Ni utendaji gani wa kifalme ambao mtume Yohana aliona katika maono?

5 Katika maono, mtume Yohana aliona jambo lingine ambalo Mfalme wa Kimasihi angefanya katika “siku ya Bwana,” baada ya kuwekwa kuwa mfalme mwaka wa 1914. Yohana aliandika hivi: “Nikaona, na, tazama! wingu jeupe, na mtu fulani kama mwana wa binadamu ameketi juu ya wingu lile, mwenye taji la dhahabu juu ya kichwa chake na mundu mkali mkononi mwake.” (Ufu. 1:10; 14:14) Yohana alimsikia malaika mmoja kutoka kwa Yehova akimwambia Mvunaji huyo atie ndani mundu wake kwa sababu “mavuno ya dunia yameiva kabisa.”—Ufu. 14:15, 16.

6. Yesu alisema ni hali gani ambayo ingetokea katika wakati wa mwisho?

6 ‘Mavuno hayo ya dunia’ yanatukumbusha mfano wa Yesu wa ngano na magugu. Yesu alijifananisha na mtu mmoja aliyepanda mbegu za ngano katika shamba lake akitazamia kuvuna ngano nzuri iliyokomaa, ambayo inafananisha “wana wa ufalme,” yaani, Wakristo wa kweli watiwa-mafuta ambao watatawala pamoja naye katika Ufalme wake. Lakini usiku, adui mmoja, “Ibilisi,” alikuja na kupanda magugu katika shamba hilo, “wana wa yule mwovu.” Mpandaji aliwaagiza wafanyakazi wake waache ngano na magugu yakue pamoja mpaka wakati wa mavuno, kwenye “umalizio wa mfumo wa mambo.” Wakati huo, angewatuma malaika wake watenganishe ngano na magugu.—Mt. 13:24-30, 36-41.

7. Kristo anatimiza jinsi gani kazi ya “mavuno ya dunia”?

7 Katika kutimiza maono ambayo Yohana alipewa, Yesu amekuwa akiongoza kazi ya mavuno ya ulimwenguni pote. “Mavuno ya dunia” yalianza na kukusanywa kwa mabaki ya wale “wana wa ufalme” 144,000 ambao ni “ngano” inayotajwa katika mfano wa Yesu. Tofauti kati ya Wakristo wa kweli na Wakristo wa uwongo ilionekana wazi zaidi baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, na jambo hilo limechangia kutimizwa kwa sehemu ya pili ya “mavuno ya dunia,” yaani, kukusanywa kwa kondoo wengine. Hao kondoo wengine si “wana wa ufalme,” badala yake, ni “umati mkubwa” wa raia wanaojitiisha kwa kupenda chini ya Ufalme huo. Wanavunwa kutoka kati ya “vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha.” Wanajitiisha chini ya Ufalme wa Kimasihi, ambao unafanyizwa na Kristo Yesu na wale “watakatifu” 144,000 ambao watakuwa pamoja naye katika serikali hiyo ya kimbingu.—Ufu. 7:9, 10; Dan. 7:13, 14, 18.

Uongozi Katika Makutaniko

8, 9. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Kristo haoni tu mwenendo wa kutaniko lote kwa ujumla, bali pia anaona mwenendo wa kila mshiriki wa kutaniko? (b) Kama inavyoonyeshwa kwenye ukurasa wa 26, ni ‘mambo gani mazito ya Shetani’ ambayo tunapaswa kuepuka?

8 Tuliona katika habari iliyotangulia jinsi ambavyo Kristo alikuwa akichunguza kwa makini hali ya kiroho ya kila kutaniko katika karne ya kwanza W.K. Katika siku zetu, akiwa Mfalme anayetawala ambaye amepewa “mamlaka yote mbinguni na duniani,” Kristo Kiongozi wetu anatenda kwa bidii akiwa kichwa cha makutaniko ulimwenguni pote na cha waangalizi wa makutaniko hayo. (Mt. 28:18; Kol. 1:18) Yehova ‘amemfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko’ la watiwa-mafuta. (Efe. 1:22) Akiwa kichwa cha kutaniko, hakuna jambo linalotokea katika kutaniko lolote kati ya makutaniko zaidi ya 100,000 ya Mashahidi wa Yehova ambalo haoni.

9 Yesu alituma ujumbe huu kwa wazee wa kutaniko la kale la Thiatira: “Haya ndiyo mambo ambayo Mwana wa Mungu anasema, yeye ambaye macho yake ni kama mwali wa moto, . . . ‘Mimi nayajua matendo yako.’” (Ufu. 2:18, 19) Aliwakemea washiriki wa kutaniko hilo kwa sababu ya maisha yao mapotovu na ya anasa kwa kuwaambia hivi: “Mimi ndiye ninayechunguza figo na mioyo, nami nitawapa ninyi mmoja-mmoja kulingana na matendo yenu.” (Ufu. 2:23) Maneno hayo yanaonyesha kwamba Kristo haoni tu mwenendo wa kutaniko lote kwa ujumla, bali pia anaona mwenendo wa kila mshiriki wa kutaniko. Yesu aliwapongeza Wakristo katika Thiatira “ambao hawakujua ‘mambo mazito ya Shetani.’” (Ufu. 2:24) Leo pia anawathamini vijana na wazee, ambao hawajiingizi ndani ya “mambo mazito ya Shetani” kupitia Intaneti au michezo ya video yenye jeuri au kufuata mawazo mapotovu ya wanadamu. Anafurahi kama nini kuona Wakristo wengi leo wakijitahidi na kujidhabihu kadiri wanavyoweza ili kufuata mwongozo wake katika sehemu zote za maisha yao!

10. Ni nini kinachoonyesha kwamba Kristo anawaongoza wazee wa kutaniko, lakini ni mpango gani ambao wanahitaji kutambua?

10 Kristo anaongoza kwa upendo makutaniko yake duniani kupitia wazee waliowekwa rasmi. (Efe. 4:8, 11, 12) Katika karne ya kwanza, waangalizi wote walikuwa wanaume waliozaliwa kwa roho. Katika kitabu cha Ufunuo wanafananishwa na nyota zilizo katika mkono wa kuume wa Kristo. (Ufu. 1:16, 20) Leo, wazee wa makutaniko mengi ni washiriki wa kondoo wengine. Wanawekwa rasmi baada ya sala na chini ya mwongozo wa roho takatifu, hivyo tunaweza kusema kwamba wao pia wanaongozwa na Kristo, au wako chini ya mkono wake ambao unaongoza. (Mdo. 20:28) Hata hivyo, wanatambua kwamba Kristo anatumia kikundi kidogo cha wanaume Wakristo watiwa-mafuta wakiwa Baraza Linaloongoza ili kuwaongoza na kuwaelekeza wanafunzi wake duniani.—Soma Matendo 15:6, 28-30.

“Njoo, Bwana Yesu”

11. Kwa nini tuna hamu ya kuona Kiongozi wetu akija upesi?

11 Katika ufunuo ambao mtume Yohana alipewa, Yesu alisema mara nyingi kwamba alikuwa akija upesi. (Ufu. 2:16; 3:11; 22:7, 20) Bila shaka, alikuwa akisema kuhusu kuja kwake ili kutekeleza hukumu juu ya Babiloni Mkubwa na sehemu inayobaki ya mfumo mwovu wa mambo wa Shetani. (2 The. 1:7, 8) Akiwa na hamu ya kuona matukio yote mazuri ajabu yaliyotabiriwa yakitimia, mtume Yohana aliyezeeka alisema hivi: “Amina! Njoo, Bwana Yesu.” Sisi ambao tunaishi mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo tunatamani pia kuona Kiongozi na Mfalme wetu akija katika mamlaka ya Ufalme kulitakasa jina la Baba yake na kuitetea enzi Yake kuu.

12. Ni kazi gani ambayo Kristo atakamilisha kabla ya pepo za uharibifu kuachiliwa?

12 Kabla ya Yesu kuja kuliharibu tengenezo linaloonekana la Shetani, watiwa-mafuta wanaobaki kati ya wale 144,000 ambao ni washiriki wa Israeli wa kiroho watatiwa muhuri wa mwisho. Biblia inasema waziwazi kwamba pepo za uharibifu juu ya mfumo wa Shetani hazitaachiliwa kabla ya kazi hiyo ya kuwatia muhuri wale 144,000 kukamilika.—Ufu. 7:1-4.

13. Kristo ataonyesha wazi jinsi gani kuwapo kwake wakati wa sehemu ya kwanza ya ile “dhiki kuu”?

13 “Kuwapo” kwa Kristo tangu mwaka wa 1914 hakujatambuliwa na wakaaji wengi wa dunia. (2 Pet. 3:3, 4) Hata hivyo, hivi karibuni ataonyesha wazi kuwapo kwake atakapotekeleza hukumu za Yehova juu ya sehemu mbalimbali za mfumo wa mambo wa Shetani. Uharibifu wa “yule mtu wa uasi-sheria,” yaani, makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, utakuwa uthibitisho ulio wazi kabisa wa “ufunuo wa kuwapo kwake.” (Soma 2 Wathesalonike 2:3, 8.) Utakuwa uthibitisho ulio wazi kwamba Kristo anatenda akiwa Hakimu au Mwamuzi aliyewekwa rasmi na Yehova. (Soma 2 Timotheo 4:1.) Kuharibiwa kwa sehemu yenye kulaumika zaidi ya Babiloni Mkubwa kutakuwa ndio mwanzo wa uharibifu kamili wa hiyo milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo yenye uovu. Yehova atatia ndani ya mioyo ya viongozi wa kisiasa wazo la kumharibu kahaba huyo wa kiroho. (Ufu. 17:15-18) Hiyo itakuwa sehemu ya kwanza ya ile “dhiki kuu.”—Mt. 24:21.

14. (a) Kwa nini sehemu ya kwanza ya ile dhiki kuu itafupishwa? (b) “Ishara ya Mwana wa binadamu” itamaanisha nini kwa watu wa Yehova?

14 Yesu alisema kwamba siku za dhiki hiyo zitafupishwa “kwa sababu ya wale waliochaguliwa,” yaani, mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta ambao bado wako duniani. (Mt. 24:22) Yehova hataruhusu shambulizi hilo la kuiharibu dini ya uwongo liwafagilie mbali Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao, kondoo wengine. Yesu aliongeza kwamba “baada ya ile dhiki ya siku hizo,” kutakuwa na ishara katika jua, mwezi, na nyota, “ndipo ishara ya Mwana wa binadamu itakapoonekana mbinguni.” Hilo litafanya mataifa ya dunia ‘yajipige-pige yenyewe kwa kuomboleza.’ Haitakuwa hivyo kwa watiwa-mafuta, ambao wana tumaini la kuishi mbinguni, na waandamani wao, ambao wana tumaini la kuishi duniani. Wao ‘watasimama wima na kuinua vichwa vyao, kwa sababu ukombozi wao utakuwa umekaribia.’—Mt. 24:29, 30; Luka 21:25-28.

15. Ni kazi gani ambayo Kristo atafanya anapokuja?

15 Kabla ya kukamilisha ushindi wake, Mwana wa binadamu anakuja kwa njia nyingine. Alitabiri hivi: “Wakati Mwana wa binadamu atakapofika katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote yatakusanyika mbele yake, naye atawatenganisha watu, mmoja kutoka kwa mwenzake, kama vile mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi. Naye atawaweka kondoo kwenye mkono wake wa kuume, lakini mbuzi kwenye mkono wake wa kushoto.” (Mt. 25:31-33) Unabii huo unahusu kuja kwa Kristo akiwa Hakimu ili kuwatenganisha watu wa “mataifa yote” katika vikundi viwili: “kondoo,” yaani, wale ambao watakuwa wamewaunga mkono kwa bidii ndugu wa kiroho wa Kristo (Wakristo watiwa-mafuta walio duniani) na “mbuzi,” yaani, wale “wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.” (2 The. 1:7, 8) Kondoo, wanaosemwa kuwa “waadilifu,” watapata “uzima wa milele” duniani, lakini mbuzi “watakatiliwa mbali milele,” yaani, wataharibiwa.—Mt. 25:34, 40, 41, 45, 46.

Yesu Anakamilisha Ushindi Wake

16. Kristo Kiongozi wetu atakamilisha ushindi wake jinsi gani?

16 Baada ya hesabu kamili ya wafalme-makuhani wenzake kutiwa muhuri na kondoo kutambuliwa na kuwekwa kwenye mkono wake wa kuume wa wokovu, Kristo anaweza kuendelea “kukamilisha ushindi wake.” (Ufu. 5:9, 10; 6:2) Akiongoza jeshi lenye nguvu la malaika na, bila shaka, akiwa pamoja na ndugu zake waliofufuliwa, Kristo atauharibu mfumo wote wa Shetani wa kisiasa, kijeshi, na kibiashara duniani. (Ufu. 2:26, 27; 19:11-21) Ushindi wa Kristo utakamilika wakati atakapouharibu mfumo mwovu wa Shetani. Kisha atamtupa Shetani na roho waovu ndani ya abiso kwa muda wa miaka elfu moja.—Ufu. 20:1-3.

17. Wakati wa Utawala wa ile Miaka Elfu Moja, Kristo atawaongoza kondoo wengine kwenye nini, na tunapaswa kuazimia kufanya nini?

17 Akizungumza kuhusu “umati mkubwa” wa kondoo wengine, ambao wataokoka ile dhiki kuu, mtume Yohana alitabiri kwamba “Mwana-Kondoo, aliye katikati ya kile kiti cha ufalme, atawachunga, na kuwaongoza kwenye chemchemi za maji ya uzima.” (Ufu. 7:9, 17) Ndiyo, wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja, Kristo ataendelea kuwaongoza kondoo wengine, ambao wanasikiliza kwelikweli sauti yake, naye atawaongoza kwenye uzima wa milele. (Soma Yohana 10:16, 26-28.) Na tuazimie kuendelea kumfuata kwa uaminifu Kiongozi wetu na mfalme sasa na mpaka katika ulimwengu mpya wa Yehova ulioahidiwa!

Kwa Kupitia

• Kristo alichukua hatua gani baada ya kuwekwa kuwa mfalme?

• Kristo anatumia nani duniani ili kuongoza makutaniko?

• Kiongozi wetu Kristo atakuja katika njia gani nyingine?

• Kristo ataendelea kutuongoza jinsi gani katika ulimwengu mpya?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Uharibifu wa mfumo mwovu wa Shetani utaonyesha wazi kuwapo kwa Kristo