Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

1 Kwa Nini Tusali?

1 Kwa Nini Tusali?

Sala

1 Kwa Nini Tusali?

SALA. Kuna mambo machache katika Biblia yanayopendwa na ambayo husababisha udadisi mwingi kama vile sala. Fikiria maswali saba ambayo yanaulizwa kwa ukawaida kuhusu sala, na kisha ujiunge nasi ili kuchunguza majibu yanayopatikana katika Biblia. Makala hizi zimeandaliwa ili kukusaidia uanze kusali au uboreshe sala zako.

ULIMWENGUNI pote, watu wa kila utamaduni na dini husali. Wanasali wakiwa peke yao au wakiwa kikundi. Wanasali wakiwa katika makanisa, mahekalu, masinagogi, misikiti, au mahali penginepo pa ibada. Wanatumia mikeka ya kusalia, rozari, magurudumu ya sala, sanamu, vitabu vya sala, au sala ambazo zimeandikwa katika vibao vidogo ambavyo huning’inizwa ukutani.

Sala inawafanya wanadamu wawe tofauti na viumbe vingine vyote duniani. Ni kweli kwamba kwa kadiri fulani tunafanana na wanyama. Kama tu wanyama, tunahitaji chakula, hewa, na maji. Pia tunazaliwa, tunaishi, na kisha tunakufa. (Mhubiri 3:19) Lakini wanadamu pekee ndio wanaosali. Kwa nini?

Labda jibu rahisi ni kwamba tuna uhitaji wa kusali. Kwa ujumla sala huonwa kuwa njia ya wanadamu ya kuwasiliana na ulimwengu wa roho, kuwasiliana na chochote ambacho watu hukiona kuwa kitakatifu na chenye kudumu. Biblia inaonyesha kwamba tuliumbwa tukiwa na tamaa ya mambo hayo. (Mhubiri 3:11) Wakati fulani Yesu Kristo alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

Ni jambo linalopatana na akili kwamba ‘uhitaji wa kiroho’ ndio unaofanya watu wawe na majengo makubwa na vifaa vya ibada vya kale, na kutumia saa nyingi katika sala. Bila shaka, watu fulani hujitegemea au kuwategemea wanadamu wenzao ili kutosheleza mahitaji yao ya kiroho. Je, huoni kwamba wanadamu hawana uwezo wa kutosheleza uhitaji huo kikamili? Sisi ni dhaifu sana, maisha yetu ni mafupi, na hatuna uwezo wa kujua wakati ujao. Mtu anayeweza kutimiza uhitaji huo, lazima awe mwenye hekima, mwenye nguvu zaidi, na anayedumu kwa muda mrefu zaidi kuliko sisi. Ni mahitaji gani hayo ya kiroho ambayo yanatusukuma tusali?

Fikiria hili: Je, umewahi kutamani kupata mwongozo, hekima, au majibu ya maswali yanayoonekana kuwa hayawezi kujibiwa na mwanadamu? Je, umewahi kuhisi kwamba unahitaji faraja baada ya kupata msiba mkubwa, au unahitaji kupata mwongozo wa kufanya uamuzi mzito, au kusamehewa baada ya kulemewa na hisia za hatia?

Kulingana na Biblia, hizo zote ni sababu nzuri zinazoweza kumfanya mtu asali. Biblia ndicho kitabu kinachotegemeka zaidi kuhusiana na suala hili, na kina sala za wanaume na wanawake wengi waaminifu. Walisali ili wapate faraja, mwongozo, msamaha, na majibu ya maswali magumu.—Zaburi 23:3; 71:21; Danieli 9:4, 5, 19; Habakuki 1:3.

Hata ingawa sala hizo zilitofautiana, zilikuwa na jambo fulani linalofanana. Wote waliotoa sala walitambua jambo fulani muhimu ambalo lilifanya sala zao zijibiwe, na ambalo linapuuzwa na watu leo. Walijua walipaswa kusali kwa nani.