Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

3 Tusali Jinsi Gani?

3 Tusali Jinsi Gani?

Sala

3 Tusali Jinsi Gani?

KUHUSIANA na sala, mapokeo mengi ya kidini yanakazia mambo kama vile jinsi ya kukaa unaposali, maneno yanayotumiwa, na taratibu fulani za kidini. Hata hivyo, Biblia inatusaidia kutokazia fikira mambo hayo na badala yake kufikiria kwa uzito swali hili, “Tunapaswa kusali jinsi gani?”

Biblia inasema kwamba watumishi waaminifu wa Mungu walisali wakiwa mahali tofauti-tofauti na katika mkao tofauti. Walisali kimyakimya au kwa sauti ikitegemea hali. Walisali wakiangalia juu mbinguni au wakiwa wamesujudu. Badala ya kutumia sanamu, rozari, au vitabu vya sala, walisali kutoka moyoni kwa maneno yao wenyewe. Ni nini kilichofanya sala zao zisikilizwe na Mungu?

Kama ilivyoelezwa katika makala iliyotangulia, walielekeza sala zao kwa Mungu mmoja tu, Yehova. Kuna jambo lingine muhimu. Tunasoma hivi katika 1 Yohana 5:14: “Huu ndio uhakika ambao tunao kwake, kwamba, hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” Sala zetu zinapaswa kupatana na mapenzi ya Mungu. Hilo linamaanisha nini?

Ili kusali kulingana na mapenzi ya Mungu, tunahitaji kujua mapenzi yake ni nini. Kwa hiyo, kujifunza Biblia ni muhimu ili kuboresha sala zetu. Je, hilo linamaanisha kwamba ili Mungu asikilize sala zetu ni lazima tuwe wasomi wa Biblia? Hapana. Lakini Mungu anatazamia tujifunze mapenzi yake na tujitahidi kuyaelewa, na kuishi kupatana na yale tunayojifunza. (Mathayo 7:21-23) Tunahitaji kusali kulingana na yale tunayojifunza.

Kadiri tunavyojifunza kumhusu Yehova na mapenzi yake, ndivyo imani yetu inavyozidi kukomaa. Hilo ni jambo lingine muhimu linaloweza kutusaidia kuboresha sala zetu. Yesu alisema: “Mambo yote mnayoomba katika sala, mkiwa na imani, mtapokea.” (Mathayo 21:22) Kuwa na imani hakumaanishi kuamini lolote bila kufikiri. Badala yake, kunamaanisha kuamini jambo fulani ambalo hata ingawa halionekani, kuna uthibitisho ulio wazi unaounga mkono jambo hilo. (Waebrania 11:1) Biblia ina uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba Yehova ambaye hatuwezi kumwona ni halisi, anategemeka, na yuko tayari kujibu sala za wale wanaomwamini. Zaidi ya hayo, nyakati zote tunaweza kuomba tuongezewe imani, na Yehova anapenda kutupa kile tunachohitaji.—Luka 17:5; Yakobo 1:17.

Ona pendekezo lingine muhimu kuhusu jinsi ya kusali. Yesu alisema: “Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Kwa hiyo, Yesu ndiye njia ambayo tunaweza kuitumia kumfikia Baba, Yehova. Hivyo, Yesu aliwaambia wafuasi wake wasali katika jina lake. (Yohana 14:13; 15:16) Hilo halimaanishi kuwa tunapaswa kusali kwa Yesu. Badala yake, tunasali katika jina la Yesu, tukikumbuka kwamba tunaweza tu kumfikia Baba yetu mkamilifu na mtakatifu kwa sababu ya Yesu.

Wafuasi wa karibu wa Yesu walimsihi hivi: “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali.” (Luka 11:1) Bila shaka, kama ambavyo tumeona, hawakuwa wakiomba wafundishwe mambo ya msingi tu. Badala yake walitaka kujua mengi—kwa maneno mengine walikuwa wakiuliza, ‘Tunapaswa kusali kuhusu nini?’

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Sala ambazo Mungu anasikiliza ni zile zinazopatana na mapenzi yake, zinazotolewa kwa imani, na katika jina la Yesu