Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

4 Tusali Kuhusu Nini?

4 Tusali Kuhusu Nini?

Sala

4 Tusali Kuhusu Nini?

IMETAJWA kuwa sala inayorudiwa-rudiwa sana kati ya sala zote za Wakristo. Iwe hilo ni kweli au si kweli, sala ya kielelezo ya Yesu, ambayo nyakati nyingine inaitwa Sala ya Bwana au ya Baba Yetu, ndiyo sala ambayo wengi hawaielewi. Watu wengi huirudia-rudia kila siku. Lakini Yesu hakukusudia sala hiyo itumiwe kwa njia hiyo. Kwa nini tunasema hivyo?

Muda mfupi tu kabla ya kufundisha sala hiyo, Yesu alisema: “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena.” (Mathayo 6:7) Je, Yesu alikuwa akipinga maneno yake mwenyewe kwa kufundisha sala ambayo ingekaririwa na kurudiwa-rudiwa? Bila shaka, hapana! Badala yake, Yesu alikuwa akitufundisha mambo tunayopaswa kutaja na kuyatanguliza tunaposali. Acheni tuchunguze kwa makini yale aliyosema katika sala hiyo iliyoandikwa katika Mathayo 6:9-13.

“Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.”

Hivyo, Yesu alikuwa akiwakumbusha wafuasi wake kuwa sala zote zinapaswa kuelekezwa kwa Baba yake, Yehova. Lakini unajua ni kwa nini jina la Mungu ni la maana sana na kwa nini linapaswa kutakaswa, au kufanywa takatifu?

Tangu mwanzo wa historia ya mwanadamu, mambo mengi ya uwongo yamesemwa kuhusu jina takatifu la Mungu. Adui ya Mungu, Shetani, alimwita Yehova Mtawala mwongo na mwenye ubinafsi ambaye hana haki ya kuutawala uumbaji Wake. (Mwanzo 3:1-6) Wengi wameunga mkono madai ya Shetani, wakifundisha kwamba Mungu hana upendo na hana huruma. Pia wanakana kwamba kuna Muumba. Wengine wamelishambulia jina la Mungu, Yehova, kwa kuliondoa katika tafsiri fulani za Biblia na kuwakataza watu wasilitumie.

Biblia inaonyesha kwamba Mungu atarekebisha ukosefu huo wote wa haki. (Ezekieli 39:7) Kwa kufanya hivyo, atatimiza mahitaji yako yote na kutatua matatizo yako. Atafanya hivyo jinsi gani? Maneno yanayofuata katika sala ya Yesu yanatoa jibu.

“Ufalme wako na uje.”

Leo, viongozi wa kidini wamechanganyikiwa sana kuhusiana na Ufalme wa Mungu. Hata hivyo, kama wasikilizaji wa Yesu walivyojua, manabii wa Mungu walikuwa wametabiri tangu zamani kwamba Masihi, Mkombozi aliyechaguliwa na Mungu, angetawala katika Ufalme ambao ungeubadili ulimwengu. (Isaya 9:6, 7; Danieli 2:44) Ufalme huo utatakasa jina la Mungu kwa kufunua uwongo wa Shetani na kisha kumwondoa Shetani na kazi zake zote. Utaondoa vita, magonjwa, njaa, na hata kifo. (Zaburi 46:9; 72:12-16; Isaya 25:8; 33:24) Unaposali Ufalme wa Mungu uje, unasali kwamba ahadi hizo zote zitimie.

“Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”

Maneno ya Yesu yanaonyesha kwamba mapenzi ya Mungu yatatimizwa hapa duniani kama yanavyotimizwa mbinguni, makao ya Mungu. Imethibitika kwamba mapenzi ya Mungu hayawezi kuzuiwa yasitimizwe mbinguni; huko, Mwana wa Mungu alipigana vita na Shetani na malaika zake, na kuwatupa hapa duniani. (Ufunuo 12:9-12) Ombi hili la tatu, kama tu yale maombi mawili ya kwanza katika sala ya kielelezo, linatusaidia kukazia uangalifu wetu jambo lililo muhimu hata zaidi, yaani, mapenzi ya Mungu, bali si mapenzi yetu. Ni kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu tu ndiko kunakoweza kuwaletea viumbe wake wote mambo mema. Hivyo, hata mwanadamu mkamilifu Yesu alimwambia Baba yake: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.”—Luka 22:42.

“Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii.”

Pia, Yesu alionyesha kwamba tunaweza kusali kuhusu mahitaji yetu. Hakuna ubaya wowote kusali kwa Mungu kuhusu mahitaji yetu ya kila siku. Kwa kweli, kufanya hivyo kunatukumbusha kwamba Yehova ndiye “huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:25) Biblia inafunua kwamba yeye ni mzazi mwenye upendo ambaye hufurahia kuwapa watoto wake kile wanachohitaji. Hata hivyo, kama mzazi mwenye upendo, Mungu hawezi kuwapa watu wake vitu ambavyo havitawaletea faida yoyote.

“Utusamehe madeni yetu.”

Je, kweli kuna deni lolote ambalo Mungu anakudai? Je, kweli unahitaji akusamehe deni hilo? Watu wengi leo hawaelewi dhambi ni nini wala hawaelewi uzito wake. Lakini Biblia inafundisha kwamba dhambi ndiyo chanzo cha matatizo yetu, kwa sababu ndiyo inayosababisha kifo cha wanadamu. Kwa kuwa tumezaliwa katika dhambi, mara kwa mara sote tunatenda dhambi, na tunategemea msamaha wa Mungu ili tuweze kuishi milele wakati ujao. (Waroma 3:23; 5:12; 6:23) Inatuliza kujua maneno haya ya Biblia: “Wewe, Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe.”—Zaburi 86:5.

“Utukomboe kutokana na yule mwovu.”

Je, unajua ni kwa nini unahitaji sana ulinzi wa Mungu? Wengi hawataki kuamini kwamba Shetani, “yule mwovu,” yupo. Lakini Yesu alifundisha kwamba Shetani ni kiumbe halisi, hata akamwita “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31; 16:11) Shetani ameupotosha ulimwengu huu anaoutawala, na anatamani sana kukupotosha ili usiweze kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Baba yako, Yehova. (1 Petro 5:8) Hata hivyo, Yehova ana nguvu zaidi kuliko Shetani na anafurahia kuwalinda wale wanaompenda.

Bila shaka, mambo ambayo tumezungumzia katika sala ya kielelezo ya Yesu, hayatii ndani kila jambo linalopaswa kutajwa katika sala. Kumbuka andiko la 1 Yohana 5:14 linatuambia hivi kumhusu Mungu: “Hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” Hivyo, usifikiri kwamba mahangaiko yako ni madogo sana hivi kwamba hupaswi kumweleza Mungu katika sala.—1 Petro 5:7.

Hata hivyo, namna gani kuhusu mahali na wakati wa kusali? Je, ni muhimu kufikiria mambo hayo?