Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Msikiaji wa Sala”

“Msikiaji wa Sala”

Mkaribie Mungu

“Msikiaji wa Sala”

1 MAMBO YA NYAKATI 4:9, 10

JE, KWELI Yehova Mungu hujibu sala za unyofu za waabudu waliojitoa kwake? Simulizi la Biblia kuhusu mtu asiyejulikana sana aitwaye Yabesi, linaonyesha kuwa Yehova kwa kweli ni “msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Simulizi hilo fupi linapatikana mahali ambapo mtu hangetazamia kulipata—katika orodha za kiukoo zinazopatikana mwanzoni mwa kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati. Acheni tuchunguze 1 Mambo ya Nyakati 4:9, 10.

Mambo yote tunayojua kumhusu Yabesi yanapatikana katika mistari hiyo miwili. Kulingana na mstari wa 9, mama yake ‘alimwita jina Yabesi, akisema: “Nimemzaa kwa maumivu.”’ a Kwa nini alichagua jina hilo? Je, alimzaa mwana huyo kwa maumivu makali zaidi kuliko ilivyo kawaida? Je, labda alikuwa mjane aliyehuzunika kwamba mumewe hakuwa hai kumwona mtoto wao mchanga? Biblia haijibu maswali hayo. Lakini siku moja mama huyo angekuwa na sababu ya kujivunia mtoto wake. Huenda ndugu za Yabesi walikuwa watu wenye kuheshimika, lakini “Yabesi a[liku]ja kuheshimika kuliko ndugu zake.”

Yabesi alipenda kusali. Alianza sala yake kwa kuomba baraka za Mungu. Kisha, akaomba mambo matatu yanayoonyesha alikuwa na imani thabiti.

Kwanza, Yabesi alimwomba Mungu, akisema: “Upanue eneo langu.” (Mstari wa 10) Mtu huyu mwenye kuheshimika hakuwa mnyakuzi wa ardhi, aliyetamani vitu vya watu wengine. Huenda ombi lake lilihusu watu hasa, bali si ardhi. Huenda alikuwa akiomba eneo lake lipanuliwe kwa amani ili apate nafasi ya kutosha kwa ajili ya waabudu wa Mungu wa kweli. b

Pili, Yabesi aliomba ‘mkono’ wa Mungu uwe pamoja naye. Mkono huo wa mfano unamaanisha nguvu za Mungu, ambazo anatumia kuwasaidia waabudu wake. (1 Mambo ya Nyakati 29:12) Ili ajibiwe maombi ya moyo wake, Yabesi alimtegemea Mungu ambaye mkono wake si mfupi kuwaelekea wale wanaomwamini.—Isaya 59:1.

Tatu, Yabesi aliomba hivi: “Uniokoe kutoka katika msiba, ili huo usipate kunidhuru.” Huenda maneno “usipate kunidhuru” yanadokeza kwamba Yabesi aliomba, si aepuke msiba, bali alindwe ili asihuzunishwe wala asishindwe na matokeo ya uovu.

Sala ya Yabesi ilionyesha kuwa alihangaikia ibada ya kweli na alimwamini na kumtumaini Msikiaji wa sala. Yehova alifanya nini? Simulizi hili fupi linamalizia kwa maneno: “Basi Mungu akatimiza yale ambayo yeye alikuwa ameomba.”

Msikiaji wa sala hajabadilika. Yeye hufurahia sala za waabudu wake. Wale wanaomwamini na kumtumaini wanaweza kuwa na uhakika huu: “Hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.”—1 Yohana 5:14.

[Maelezo ya Chini]

a Jina Yabesi linatokana na neno linaloweza kumaanisha “maumivu.”

b Katika Targumi, au tafsiri za Wayahudi za Maandiko Matakatifu yaliyofafanuliwa, maneno ya Yabesi yametafsiriwa hivi: “Nibariki kwa kunipa watoto, na upanue mipaka yangu kwa kunipa wanafunzi.”