Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mazungumzo Pamoja na Jirani Roho Takatifu Ni Nini?

Mazungumzo Pamoja na Jirani Roho Takatifu Ni Nini?

Mazungumzo Pamoja na Jirani Roho Takatifu Ni Nini?

MASHAHIDI WA YEHOVA hufurahia kuzungumza kuhusu Biblia pamoja na jirani zao. Je, una swali lolote la Biblia ambalo limekuwa likikutatiza? Je, kuna jambo lolote ambalo Mashahidi wa Yehova wanaamini au kufanya ambalo ungependa kulifahamu zaidi? Ikiwa ndivyo, basi unapokutana tena na Shahidi wa Yehova usikose kumwuliza. Yeye atafurahi kuzungumzia jambo hilo pamoja nawe.

Mazungumzo yaliyo hapa chini yanaonyesha jinsi Shahidi wa Yehova anavyoweza kuzungumza na jirani yake. Hebu tuwazie kwamba Shahidi anayeitwa Joshua amemtembelea mwanamume anayeitwa Daniel nyumbani kwake.

Unamaanisha Nini Unaposema “Roho Mtakatifu”?

Daniel: Nimesikia kwamba nyinyi Mashahidi wa Yehova si Wakristo kwa sababu hamwamini roho mtakatifu.

Joshua: Kwanza, ningependa kukuhakikishia kwamba sisi ni Wakristo. Nimekuja kwako asubuhi ya leo kwa sababu ninamwamini Yesu Kristo. Yeye ndiye anayewaamuru wafuasi wake wahubiri. Lakini hebu nikuulize, unamaanisha nini unaposema “roho mtakatifu”?

Daniel: Ninamaanisha yule mtu wa tatu katika Utatu, msaidizi ambaye Yesu aliahidi atatutumia. Msaidizi huyo ni muhimu sana kwangu. Ninataka kuhisi kwamba roho mtakatifu anatenda kazi katika maisha yangu.

Joshua: Hayo ndiyo maoni ya watu wengi kuhusu roho takatifu. Wakati fulani uliopita nilipata nafasi ya kuchunguza yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu jambo hilo. Ikiwa una dakika chache, nitafurahi kukuonyesha yale niliyojifunza.

Daniel: Ndio, nina dakika kadhaa.

Joshua: Jina langu ni Joshua. Na wewe unaitwa nani?

Daniel: Naitwa Daniel na nimefurahi kukujua.

Joshua: Nimefurahi kukujua pia, Daniel. Ili nisitumie wakati wako mwingi, nitazungumzia jambo moja tu kuhusiana na habari hii. Ulitaja kwamba roho takatifu ndiye msaidizi ambaye Yesu alituahidi. Ninakubaliana nawe. Lakini je, unamaanisha kwamba roho takatifu ni mtu na yeye ni sawa na Mungu?

Daniel: Naam, hivyo ndivyo nilivyofundishwa.

Je, Roho Takatifu Ni Mtu?

Joshua: Acha tuchunguze simulizi fulani katika Biblia ambalo litatusaidia kuona ikiwa roho takatifu ni mtu au si mtu. Huenda unafahamu mistari hii. Tunasoma hivi katika Matendo 2:1-4: “Basi siku ya sherehe ya Pentekoste ilipokuwa ikiendelea walikuwa wote pamoja mahali pale pale, na ghafula kukatokea kutoka mbinguni kelele kama ile ya upepo wenye nguvu unaovuma, nao ukaijaza nyumba yote ambamo walikuwa wameketi. Nao wakaona ndimi kama za moto, nazo zikagawanyika huku na huku, na mmoja ukaketi juu ya kila mmoja wao, nao wote wakajazwa roho takatifu wakaanza kusema katika lugha tofauti, kama vile roho ilivyokuwa ikiwawezesha kusema.”

Daniel: Ninalifahamu vizuri simulizi hilo.

Joshua: Hivyo, unaonaje Daniel, mtu anaweza kujazwa na mtu mwingine?

Daniel: Haiwezekani.

Joshua: Hebu tusome mstari mwingine katika sura hiyohiyo—mstari wa 17. Sehemu ya kwanza ya mstari huo inasema: “‘Katika siku za mwisho,’ Mungu asema, ‘Nitaimimina sehemu ya roho yangu juu ya kila namna ya mwili.’” Daniel, hebu nikuulize, Mungu anaweza kumimina sehemu ya Mungu aliye sawa naye?

Daniel: Hapana.

Joshua: Yohana Mbatizaji alitumia njia tofauti kufafanua kuhusu kujazwa na roho takatifu. Ufafanuzi huo unapatikana katika Mathayo 3:11. Tafadhali ungependa kusoma mstari huo?

Daniel: “Mimi ninawabatiza ninyi kwa maji kwa sababu ya toba yenu; lakini yule anayekuja nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, ambaye viatu vyake mimi sistahili kuvivua. Huyo atawabatiza ninyi kwa roho takatifu na kwa moto.”

Joshua: Asante. Umeona Yohana Mbatizaji alisema roho takatifu ingetumiwa kufanya nini?

Daniel: Alitaja kuhusu kubatizwa kwa roho takatifu.

Joshua: Ni kweli. Ona pia kwamba alitaja kuhusu kubatizwa kwa moto. Ni wazi kwamba moto si mtu. Je, unafikiri mstari huo unaonyesha kwamba roho takatifu ni mtu?

Daniel: Hapana.

Joshua: Kwa hiyo, maandiko ambayo tumechunguza yanaonyesha kwamba roho takatifu si mtu.

Daniel: Hilo ni kweli.

Ni Katika Njia Gani Roho Takatifu Ni “Msaidizi”?

Joshua: Mwanzoni ulitaja kuhusu “msaidizi.” Yesu alitaja kwamba roho takatifu ni “msaidizi” kwenye Yohana 14:26. Hebu tusome andiko hilo pamoja: “Msaidizi, roho takatifu, ambayo Baba atatuma katika jina langu, hiyo itawafundisha ninyi mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia.” Watu fulani wanafikiri kuwa andiko hilo linathibitisha wazo la kwamba roho takatifu ni mtu, ambaye atawasaidia na kuwafundisha.

Daniel: Ndiyo, hivyo ndivyo ninavyoamini.

Joshua: Lakini je, inawezekana kwamba Yesu alikuwa akizungumza kwa njia ya mfano? Ona jambo ambalo Yesu alisema kuhusu hekima, katika Luka 7:35: “Hata hivyo, hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa watoto wake wote.” Je, ungesema kwamba hekima ni mtu, aliye na watoto?

Daniel: Hapana. Hapo alikuwa akizungumza kwa njia ya mfano.

Joshua: Ni kweli. Yesu alikuwa akimaanisha kwamba hekima huonekana kupitia matunda yake. Mara nyingi Biblia hutumia usemi wa mfano unaoitwa tashihisi—yaani, kuzungumzia kitu kisicho na uhai kana kwamba kina uhai. Mara nyingi sisi hutumia semi za mfano katika mazungumzo yetu. Kwa mfano, asubuhi kama ya leo ambapo jua limeangaza, ni kawaida mtu kusema, “Fungua pazia ili mwangaza wa jua uingie,” sivyo?

Daniel: Bila shaka.

Joshua: Je, ungekuwa unamaanisha kwamba mwangaza wa jua ni mtu ambaye anaweza kuingia ndani ya nyumba yako kama mgeni?

Daniel: Hapana. Huo ni usemi wa mfano.

Joshua: Kwa hiyo, Yesu aliposema kwamba roho takatifu ni msaidizi, au mwalimu, je, inawezekana alikuwa akitumia usemi wa mfano?

Daniel: Nafikiri hivyo. Hilo linapatana na maandiko uliyosoma kwamba roho takatifu ilimwagwa na kwamba watu walibatizwa kwa roho hiyo. Lakini ikiwa roho takatifu si mtu, ni nini?

Roho Takatifu Ni Nini?

Joshua: Kwenye Matendo 1:8, Yesu anatuambia roho takatifu ni nini. Ungependa kusoma mstari huo?

Daniel: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”

Joshua: Ona kwamba Yesu anahusianisha roho takatifu na nguvu. Na kulingana na mistari tuliyotangulia kusoma, unafikiri nguvu hiyo inatoka wapi?

Daniel: Inatoka kwa Mungu, Baba.

Joshua: Ni kweli. Roho takatifu ndiyo nguvu ileile ambayo Mungu alitumia kuumba ulimwengu. Mstari wa pili wa Biblia unazungumza kuhusu nguvu hiyo. Andiko la Mwanzo 1:2 linasema: “Nguvu za utendaji za Mungu zilikuwa zikienda huku na huku juu ya uso wa maji.” Neno la Kiebrania linalotafsiriwa hapa kuwa “nguvu za utendaji” linatafsiriwa pia kuwa “roho.” Roho hiyo ni nguvu zisizoonekana za utendaji ambazo Mungu hutumia kutimiza kusudi lake na kufunua mapenzi yake. Acha nikuonyeshe andiko lingine moja tu—Luka 11:13. Tafadhali, ungependa kusoma mstari huu?

Daniel: “Ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!”

Joshua: Ikiwa Baba aliye mbinguni ndiye mwenye mamlaka juu ya roho takatifu, na anawapa wale wanaomwomba, je, roho takatifu inaweza kuwa sawa na Baba?

Daniel: Hapana. Nimeelewa unachosema.

Joshua: Sitaki kutumia wakati wako mwingi, Daniel. Ulisema kwamba una dakika chache tu. Lakini acha nikuulize swali la mwisho. Kutokana na maandiko ambayo tumesoma, ungesema roho takatifu ni nini?

Daniel: Ni nguvu za utendaji za Mungu.

Joshua: Ni kweli. Na kulingana na Yohana 14:26, Yesu alipozungumza kuhusu roho takatifu kuwa msaidizi, au mwalimu, alikuwa akitumia usemi wa mfano unaoitwa tashihisi.

Daniel: Sikujua hilo.

Joshua: Kuna jambo lenye kufariji sana ambalo tunajifunza kutokana na maneno ya Yesu.

Daniel: Jambo gani hilo?

Joshua: Tunaweza kumwomba Mungu roho yake takatifu ili itusaidie tunapopatwa na hali ngumu. Tunaweza pia kuomba roho yake itusaidie tujifunze ukweli kumhusu.

Daniel: Hilo ni jambo zuri. Nitalifikiria.

Joshua: Kabla sijaondoka, ningependa pia ufikirie jambo hili lingine. Kwa kuwa roho takatifu ni nguvu za utendaji za Mungu, basi tunakubaliana kwamba Mungu anaweza kuitumia kutimiza jambo lolote analotaka.

Daniel: Bila shaka.

Joshua: Hivyo basi, kwa nini hajatumia nguvu hizo zisizo na mipaka kumaliza matatizo na uovu wote tunaoona leo ulimwenguni? Umewahi kujiuliza swali hilo? a

Daniel: Nimewahi kujiuliza.

Joshua: Je, itakuwa sawa nikirudi juma lijalo wakati kama huu tuzungumzie jambo hilo?

Daniel: Nitafurahi sana. Tuonane wakati huo.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa habari zaidi, ona sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.