Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endeleeni Kuutafuta Kwanza “Uadilifu Wake”

Endeleeni Kuutafuta Kwanza “Uadilifu Wake”

Endeleeni Kuutafuta Kwanza “Uadilifu Wake”

“Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.”—MT. 6:33.

1, 2. Uadilifu wa Mungu ni nini, na unategemea nini?

“BASI, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme.” (Mt. 6:33) Leo, Mashahidi wa Yehova wanajua vizuri sana himizo hilo ambalo lilitolewa na Yesu Kristo katika Mahubiri yake ya Mlimani. Katika kila sehemu ya maisha yetu, tunajitahidi kuonyesha kwamba tunapenda serikali hiyo ya Ufalme na tunataka kuwa washikamanifu kwa serikali hiyo. Lakini ni lazima pia tukumbuke sehemu ya pili ya himizo hilo, yaani, “na uadilifu wake.” Uadilifu wa Mungu ni nini, na inamaanisha nini kuutafuta kwanza?

2 Maneno ya lugha ya awali yaliyotafsiriwa kuwa “uadilifu” yanaweza pia kutafsiriwa kuwa “haki” au “unyoofu.” Kwa hiyo, uadilifu wa Mungu ni unyoofu kulingana na viwango na sheria zake mwenyewe za maadili. Akiwa Muumba, Yehova ana haki ya kuweka viwango vya mema na mabaya, mambo yanayofaa na yasiyofaa. (Ufu. 4:11) Hata hivyo, uadilifu wa Mungu si orodha ya sheria na maagizo makali yasiyo na mwisho. Badala yake, uadilifu huo unategemea utu wa Yehova na sifa yake kuu ya haki, pamoja na sifa zake nyingine kuu, yaani, upendo, hekima, na nguvu. Basi, uadilifu wa Mungu unahusiana na mapenzi na kusudi lake. Uadilifu huo unatia ndani mambo anayotazamia yatimizwe na wale wanaotamani kumtumikia.

3. (a) Inamaanisha nini kuutafuta kwanza uadilifu wa Mungu? (b) Kwa nini tunaishi kulingana na viwango vya Yehova vya uadilifu?

3 Inamaanisha nini kuutafuta kwanza uadilifu wa Mungu? Kwa ufupi, inamaanisha kufanya mapenzi ya Mungu ili kumpendeza. Kuutafuta uadilifu wake kunatia ndani kujitahidi kuishi kulingana na sheria zake za maadili na viwango vyake vikamilifu bali si kulingana na viwango vyetu wenyewe. (Soma Waroma 12:2.) Njia hiyo ya maisha inahusisha uhusiano wetu wenyewe pamoja na Yehova. Haimaanishi kutii sheria zake kwa sababu tunaogopa kuadhibiwa. Badala yake, upendo wetu kwa Mungu unatuchochea tujitahidi kumpendeza kwa kuishi kulingana na viwango vyake, bali si kujiwekea viwango vyetu wenyewe. Tunatambua kwamba hilo ndilo jambo linalofaa ambalo tunapaswa kufanya, na kwamba tuliumbwa ili tufanye hivyo. Ni lazima tuupende uadilifu kama Yesu Kristo, Mfalme wa Ufalme wa Mungu alivyoupenda.—Ebr. 1:8, 9.

4. Kwa nini ni jambo la maana sana kuutafuta uadilifu wa Mungu?

4 Ni jambo la maana kadiri gani kuutafuta uadilifu wa Yehova? Fikiria jambo hili la hakika: Jaribu la kwanza katika shamba la Edeni lilitegemea ikiwa Adamu na Hawa wangekubali haki ya Yehova ya kuweka viwango au wangekataa. (Mwa. 2:17; 3:5) Walikataa na hivyo wakatuletea mateso na kifo tukiwa wazao wao. (Rom. 5:12) Kwa upande mwingine, Neno la Mungu linasema hivi: “Anayefuatilia uadilifu na fadhili zenye upendo atapata uzima, uadilifu na utukufu.” (Met. 21:21) Ndiyo, tukitafuta kwanza uadilifu wa Mungu tutakuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova ambao utatusaidia kupata wokovu.—Rom. 3:23, 24.

Hatari ya Kujiona Wenyewe Kuwa Waadilifu

5. Tunapaswa kuepuka hatari gani?

5 Akiwaandikia Wakristo huko Roma, mtume Paulo alikazia hatari ambayo sisi sote tunahitaji kuepuka ikiwa tunataka kufanikiwa katika kuutafuta kwanza uadilifu wa Mungu. Paulo alisema hivi kuhusu Wayahudi wenzake: “Nawatolea ushahidi kwamba wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi; kwa maana, kwa sababu ya kukosa kujua uadilifu wa Mungu bali wakitafuta kujiwekea uadilifu wao wenyewe, hawakujitiisha kwa uadilifu wa Mungu.” (Rom. 10:2, 3) Kulingana na Paulo, waabudu hao hawakuelewa uadilifu wa Mungu kwa sababu walikuwa na bidii sana wakijaribu kujiwekea viwango vyao wenyewe vya uadilifu. *

6. Tunapaswa kuepuka mtazamo gani, na kwa nini?

6 Njia moja ambayo tunaweza kuanguka katika mtego huo ni kuuona utumishi wetu kwa Yehova kuwa mashindano, tukijilinganisha na wengine. Mtazamo huo unaweza kwa urahisi kutufanya tujitumaini kupita kiasi kwa sababu ya uwezo wetu. Lakini kwa kweli, tukitenda hivyo, tutakuwa tunausahau uadilifu wa Yehova. (Gal. 6:3, 4) Nia nzuri ambayo inapaswa kutuchochea kufanya mambo yanayofaa ni upendo wetu kwa Yehova. Tukijaribu kwa njia yoyote ile kuthibitisha uadilifu wetu wenyewe tutakuwa tukipinga dai letu la kwamba tunampenda Yehova.—Soma Luka 16:15.

7. Yesu alizungumzia jinsi gani tatizo la kujiona wenyewe kuwa waadilifu?

7 Yesu alihangaishwa na watu “waliokuwa wakiamini kwamba walikuwa waadilifu na kuwaona wale wengine kama si kitu.” Alizungumza kuhusu tatizo la kujiona wenyewe kuwa waadilifu kwa kusimulia mfano huu: “Watu wawili walipanda kuingia hekaluni ili kusali, mmoja alikuwa Farisayo na yule mwingine alikuwa mkusanya-kodi. Yule Farisayo akasimama na kuanza kusali mambo haya akisema moyoni, ‘Ee Mungu, ninakushukuru ya kuwa mimi si kama wale watu wengine, wanyang’anyi, wasio waadilifu, wazinzi, au hata kama mkusanya-kodi huyu. Mimi hufunga mara mbili kwa juma, mimi hutoa sehemu ya kumi ya vitu vyote ninavyojipatia.’ Lakini yule mkusanya-kodi akiwa amesimama umbali fulani hakutaka hata kuinua macho yake kuelekea mbinguni, bali alikuwa akipiga-piga kifua chake, akisema, ‘Ee Mungu, unirehemu mimi mtenda-dhambi.’” Yesu akamalizia kwa kusema: “Ninawaambia ninyi, Mtu huyu alishuka kwenda nyumbani kwake akiwa amethibitishwa kuwa mwadilifu zaidi kuliko yule mwingine; kwa sababu kila mtu anayejiinua atafedheheshwa, bali yule anayejinyenyekeza atainuliwa.”—Luka 18:9-14.

Hatari Nyingine—Kuwa “Mwadilifu Kupita Kiasi”

8, 9. Inamaanisha nini kuwa “mwadilifu kupita kiasi,” na matokeo yanaweza kuwa nini tukiwa hivyo?

8 Hatari nyingine ambayo tunapaswa kuepuka inaelezwa katika andiko la Mhubiri 7:16: “Usiwe mwadilifu kupita kiasi, wala kujionyesha kuwa na hekima kupita kiasi. Kwa nini ujiletee ukiwa?” Mwandikaji huyo wa Biblia aliyeongozwa na roho takatifu anaendelea kusema maneno haya katika mstari wa 20, ili kutuonyesha sababu ya kuepuka mtazamo huo: “Kwa maana hakuna mwanadamu aliye mwadilifu duniani ambaye huendelea kufanya mema na asifanye dhambi.” Mtu ambaye ni “mwadilifu kupita kiasi” anaweka viwango vyake mwenyewe vya uadilifu na kuwahukumu wengine akitumia viwango hivyo. Hata hivyo, anasahau kwamba kwa kufanya hivyo, anainua viwango vyake juu kuliko viwango vya Mungu na hivyo kujithibitisha kuwa asiye mwadilifu machoni pa Mungu.

9 Kuwa “mwadilifu kupita kiasi,” au kama tafsiri fulani za Biblia zinavyosema, kuwa “mwadilifu sana” au kuwa na “haki kupita kipimo,” kunaweza hata kutufanya tuwe na shaka kuhusu jinsi Yehova anavyoshughulikia mambo. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba ikiwa tunatilia shaka maamuzi ya Yehova kwamba si ya haki, kwa kweli, tunaanza kuweka viwango vyetu vya uadilifu juu kuliko viwango vya Yehova. Ni kana kwamba tunamshtaki Yehova na kumhukumu kulingana na viwango vyetu wenyewe vya mema na mabaya. Lakini Yehova ndiye mwenye haki ya kuweka viwango vya uadilifu, sisi hatuna haki hiyo!—Rom. 14:10.

10. Kama ilivyokuwa katika kisa cha Ayubu, ni jambo gani ambalo linaweza kufanya tumhukumu Mungu?

10 Ingawa hakuna yeyote kati yetu ambaye angependa kumhukumu Mungu, hali yetu ya kutokamilika inaweza kufanya tumhukumu. Ni rahisi kufanya hivyo tunapoona jambo ambalo tunafikiri kwamba si la haki au ikiwa sisi wenyewe tunapatwa na mateso. Hata mwanamume mwaminifu Ayubu alifanya kosa hilo. Mwanzoni ilisemwa kwamba Ayubu alikuwa mtu “asiye na lawama na mnyoofu, na mwenye kumwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya.” (Ayu. 1:1) Lakini Ayubu alipatwa na misiba iliyofuatana ambayo aliona kwamba haikuwa ya haki. Hilo lilimfanya Ayubu atangaze “nafsi yake mwenyewe kuwa adilifu badala ya Mungu.” (Ayu. 32:1, 2) Maoni ya Ayubu yalihitaji kurekebishwa. Kwa hiyo, hatupaswi kushangaa ikiwa nyakati nyingine tunajikuta katika hali kama hiyo. Hali hiyo ikitokea, ni nini ambacho kinaweza kutusaidia kurekebisha fikira zetu?

Mara Nyingi Hatuna Habari Kamili

11, 12. (a) Tunapohisi kwamba jambo fulani si la haki, tunahitaji kukumbuka nini? (b) Kwa nini huenda mtu akahisi kwamba mfano wa Yesu wa wafanyakazi katika shamba la mizabibu unaonyesha jambo lisilo la haki?

11 Jambo la kwanza tunalopaswa kukumbuka ni kwamba mara nyingi hatuna habari kamili. Ndivyo ilivyokuwa katika kisa cha Ayubu. Hakujua kuhusu mikutano iliyofanywa mbinguni ya wana wa kimalaika wa Mungu wakati ambapo Shetani alimshtaki kwa uwongo. (Ayu. 1:7-12; 2:1-6) Ayubu hakujua kwamba kwa kweli matatizo yake yalisababishwa na Shetani. Na kwa kweli, hatuwezi hata kuwa na hakika kwamba Ayubu alijua Shetani ni nani! Kwa hiyo, alifikiria kimakosa kwamba matatizo yake yalisababishwa na Mungu. Ndiyo, ni rahisi kufanya uamuzi mbaya ikiwa hatuna habari kamili.

12 Kwa mfano, fikiria mfano wa Yesu wa wafanyakazi katika shamba la mizabibu. (Soma Mathayo 20:8-16.) Katika mfano huo Yesu anaeleza kuhusu mwenye nyumba ambaye anawalipa wafanyakazi wake wote mshahara unaolingana, iwe walifanya kazi siku nzima au kwa muda wa saa moja tu. Wewe unahisi namna gani kuhusu jambo hilo? Je, alitenda kwa haki? Labda moja kwa moja unawahurumia wafanyakazi ambao walifanya kazi kwa siku nzima katika jua kali. Huenda ukahisi kwamba bila shaka walistahili kulipwa mshahara mkubwa zaidi! Kulingana na maoni hayo, mwenye nyumba huyo anaweza kuonwa kuwa mtu asiye na upendo na asiyetenda kwa haki. Hata jibu lake kwa wafanyakazi hao waliolalamika linaweza kuonwa kuwa utumizi mbaya wa mamlaka. Lakini je, tuna habari kamili?

13. Tunaweza kuona mfano wa Yesu wa wafanyakazi katika shamba la mizabibu kwa njia gani nyingine?

13 Acheni tuchunguze mfano huo kwa njia nyingine. Bila shaka, mwenye nyumba katika mfano huo alitambua kwamba wanaume hao wote walihitaji kulisha familia zao. Katika siku za Yesu, watu waliofanya kazi katika mashamba walilipwa mshahara kila siku. Familia zao zilitegemea mshahara waliolipwa kila siku. Ukiwa na wazo hilo akilini, sasa fikiria hali ya wale ambao mwenye nyumba aliwapata wakati wa alasiri na ambao walifanya kazi kwa muda wa saa moja tu. Labda hawangeweza kulisha familia zao kwa mshahara wa saa moja tu; hata hivyo, walikuwa tayari kufanya kazi na walikuwa wamengoja kwa siku nzima ili wapewe kazi. (Mt. 20:1-7) Halikuwa kosa lao kutoruhusiwa kufanya kazi kwa siku nzima. Hakuna jambo lolote linaloonyesha kwamba walijaribu kuepuka kimakusudi kufanya kazi. Hebu fikiria kama ungelazimika kungoja siku nzima, ukijua kwamba wengine wanategemea mshahara ambao utalipwa siku hiyo. Ungefurahi kama nini ikiwa ungepata kazi—na ungesisimka kama nini kupokea mshahara wa kutosha kulisha familia yako!

14. Ni somo gani la maana ambalo tunajifunza kutokana na mfano wa shamba la mizabibu?

14 Sasa acheni tuchunguze tena hatua ambayo yule mwenye nyumba alichukua. Hakumlipa mtu yeyote mshahara wa chini. Badala yake, aliwatendea wafanyakazi wote kama watu walio na haki ya kupata riziki. Huenda ikaonekana kwamba kwa sababu hakukuwa na upungufu wa wafanyakazi, mwenye nyumba ndiye aliyekuwa na uhuru wa kuamua, hata hivyo, hakuwanyanyasa kwa kuwalipa mshahara mdogo kuliko mshahara waliostahili kupata. Wafanyakazi wake wote walirudi nyumbani wakiwa na pesa za kutosha kulisha familia zao. Kufikiria habari hizo za ziada kunaweza kutusaidia kubadili maoni yetu kuhusu hatua ambayo mwenye nyumba huyo alichukua. Alifanya uamuzi wa upendo na hakutumia vibaya mamlaka yake. Tunaweza kujifunza somo gani? Kwamba tukichunguza mambo fulani tu bila kuwa na habari kamili tunaweza kukata kauli isiyofaa haraka-haraka. Kwa kweli, mfano huo unakazia ubora wa uadilifu wa Mungu, ambao hautegemei maagizo ya kisheria na ikiwa tu wanadamu wanastahili kupata kitu fulani.

Maoni Yetu Yanaweza Kuwa Yamepotoka au Kuwa na Mipaka

15. Kwa nini maoni yetu kuhusu haki yanaweza kupotoshwa au kuwa na mipaka?

15 Jambo la pili ambalo tunapaswa kukumbuka tunapokabili hali ambayo tunaona haki haikufuatwa ni kwamba maoni yetu yanaweza kuwa yamepotoka au kuwa na mipaka. Yanaweza kupotoshwa na kutokamilika, ubaguzi, au utamaduni. Maoni yetu pia yanaweza kuwa na mipaka kwa sababu hatuna uwezo wa kutambua na kujua nia na mambo ambayo kwa kweli yako katika mioyo ya watu. Tofauti na sisi, Yehova na Yesu hawana mipaka kama hiyo.—Met. 24:12; Mt. 9:4; Luka 5:22.

16, 17. Kwa nini huenda Yehova hakufuata sheria yake kuhusu uzinzi katika dhambi ya Daudi na Bath-sheba?

16 Acheni tuchunguze kisa cha uzinzi kati ya Daudi na Bath-sheba. (2 Sam. 11:2-5) Kulingana na Sheria ya Musa, wote wawili walistahili kuuawa. (Law. 20:10; Kum. 22:22) Ingawa Yehova aliwaadhibu, hakuwatendea kulingana na sheria yake mwenyewe. Je, Yehova alitenda kwa njia isiyo ya haki? Je, alimwonyesha Daudi upendeleo na kuvunja viwango Vyake mwenyewe vya uadilifu? Wasomaji fulani wa Biblia wamehisi hivyo.

17 Hata hivyo, Yehova aliwapa sheria hiyo kuhusu uzinzi waamuzi wasio wakamilifu, ambao hawangeweza kusoma mioyo. Ingawa walikuwa na mipaka, sheria hiyo iliwawezesha kufuata kiwango kilekile walipotoa hukumu. Kinyume na hilo, Yehova anaweza kusoma mioyo. (Mwa. 18:25; 1 Nya. 29:17) Hivyo, hatupaswi kutazamia kwamba Yehova angezuiwa na sheria ambayo alitunga kwa ajili ya waamuzi wasio wakamilifu. Ikiwa angefuata sheria hiyo, je, hilo halingekuwa sawa na kumlazimisha mtu aliye na uwezo mzuri wa kuona avae miwani ambayo imetengenezwa kwa ajili ya watu walio na tatizo la kutoona vizuri? Yehova angeweza kusoma moyo ya Daudi na pia wa Bath-sheba na kuona kwamba walikuwa wametubu kikweli. Tukifikiria jambo hilo, tunaweza kusema kwamba Yehova aliwahukumu inavyofaa, kwa njia ya huruma na ya upendo.

Endelea Kuutafuta Uadilifu wa Yehova

18, 19. Ni nini ambacho kitatusaidia tusimhukumu kamwe Yehova tukitumia viwango vyetu wenyewe vya uadilifu?

18 Kwa hiyo, ikiwa nyakati nyingine tunaona jambo ambalo tunahisi kwamba Yehova hakutenda kwa haki, iwe tunasoma jambo hilo katika simulizi la Biblia au tunakabiliana nalo katika maisha yetu, acheni tusimhukumu kamwe Mungu tukitumia viwango vyetu wenyewe vya uadilifu. Kumbuka kwamba mara nyingi hatuna habari kamili na kwamba maoni yetu yanaweza kupotoshwa au kuwa na mipaka. Usisahau kamwe kwamba “ghadhabu ya mwanadamu haitokezi uadilifu wa Mungu.” (Yak. 1:19, 20) Kwa kufanya hivyo, mioyo yetu haitawahi kamwe ‘kuwa na ghadhabu juu ya Yehova.’—Met. 19:3.

19 Kama Yesu, acheni sikuzote tukubali kwamba Yehova peke yake ndiye aliye na haki ya kuweka viwango kuhusu mambo yaliyo ya uadilifu na mema. (Marko 10:17, 18) Jitahidi kupata “ujuzi sahihi” au “ujuzi wa kweli” kuhusu viwango vyake. (Rom. 10:2; 2 Tim. 3:7, Union Version) Kwa kukubali viwango hivyo na kupatanisha maisha yetu na mapenzi ya Yehova, tunaonyesha kwamba tunatafuta kwanza “uadilifu wake.”—Mt. 6:33.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kulingana na msomi mmoja, neno la lugha ya awali ambalo lilitafsiriwa kuwa “kujiwekea” linaweza pia kumaanisha ‘kusimamisha mnara wa ukumbusho.’ Hivyo, Wayahudi hao kwa kweli walikuwa wakisimamisha mnara wa mfano wa ukumbusho ili wajiletee sifa badala ya kumletea Mungu sifa.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini ni jambo la maana kuutafuta uadilifu wa Yehova?

• Ni hatari gani mbili ambazo tunapaswa kuepuka?

• Tunaweza jinsi gani kuutafuta kwanza uadilifu wa Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Tunajifunza somo gani kutokana na mfano wa Yesu wa wanaume wawili waliosali katika hekalu?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je, lilikuwa jambo lisilo la haki kuwalipa wafanyakazi walioingia kazini saa kumi na moja mshahara uliolingana na wa wale waliofanya kazi siku nzima?