Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana—Mtatumia Maisha Yenu Jinsi Gani?

Vijana—Mtatumia Maisha Yenu Jinsi Gani?

Vijana—Mtatumia Maisha Yenu Jinsi Gani?

“Jinsi ninavyoelekeza ngumi zangu ni ili nisiwe nikipiga hewa.”—1 KOR. 9:26.

1, 2. Ili ufanikiwe unapokua kuelekea kuwa mtu mzima, unahitaji kuwa na nini?

IKIWA unapanga kusafiri kwenye njia ambayo huijui, huenda ukahitaji kubeba ramani na dira. Ramani itakusaidia kujua mahali ulipo na itakusaidia kuchagua njia inayofaa. Dira itakusaidia kubaki kwenye njia inayofaa. Hata hivyo, ramani na dira haziwezi kukusaidia ikiwa hujui mahali unapoenda. Ili usitembee bila mwelekeo, unapaswa kujua waziwazi mahali unapoenda.

2 Unakabili hali kama hiyo unapoendelea kukua kuelekea kuwa mtu mzima. Tayari una dira na ramani inayotegemeka. Biblia ni ramani inayoweza kukusaidia kujua njia unayopaswa kuchagua. (Met. 3:5, 6) Dhamiri yako ikizoezwa vizuri, inaweza kukusaidia sana kubaki kwenye njia inayofaa. (Rom. 2:15) Inaweza kuwa kama dira. Hata hivyo, ili ufanikiwe maishani, unahitaji pia kujua mahali unapoelekea. Unapaswa kuwa na miradi iliyo wazi.

3. Katika 1 Wakorintho 9:26, Paulo anataja faida gani za kujiwekea miradi?

3 Mtume Paulo alionyesha faida za kujiwekea miradi na kujitahidi kuifikia alipoandika hivi: “Jinsi ninavyokimbia si bila uhakika; jinsi ninavyoelekeza ngumi zangu ni ili nisiwe nikipiga hewa.” (1 Kor. 9:26) Ikiwa una miradi, unaweza kukimbia ukiwa na uhakika. Baada ya muda, utahitaji kufanya maamuzi fulani ya maana sana kuhusu ibada, kazi ya kimwili, ndoa, familia, na kadhalika. Ingawa hivyo, huenda nyakati nyingine ukahisi kwamba umechanganyikiwa unapopewa mapendekezo mbalimbali. Lakini ukijiwekea miradi mapema, na kutegemea kweli na kanuni zinazopatikana katika Neno la Mungu unapofanya maamuzi, hutashawishiwa kufuata njia isiyofaa.—2 Tim. 4:4, 5.

4, 5. (a) Ni nini ambacho kinaweza kutokea usipojiwekea miradi? (b) Kwa nini maamuzi unayofanya yanapaswa kuongozwa na tamaa ya kumpendeza Mungu?

4 Ikiwa hutajiwekea miradi, inaelekea kwamba marafiki wako na walimu watakushawishi kufanya mambo ambayo wanahisi kwamba yanakufaa. Bila shaka, hata ukiwa na miradi fulani, huenda wengine wakapendekeza ufuate maoni yao. Unaposikiliza mapendekezo yao, jiulize, ‘Je, miradi ambayo wanataja itanisaidia kumkumbuka Muumba wangu nikiwa bado kijana au itanikengeusha nisifanye hivyo?’—Soma Mhubiri 12:1.

5 Kwa nini maamuzi unayofanya maishani yanapaswa kuongozwa na tamaa ya kumpendeza Mungu? Sababu moja ni kwamba Yehova alitupatia kila kitu kizuri tulicho nacho. (Yak. 1:17) Kwa kweli, kila mtu anapaswa kumshukuru Yehova. (Ufu. 4:11) Je, kuna njia bora zaidi ya kuonyesha kwamba una shukrani kuliko kumkumbuka Yehova unapojiwekea miradi? Acheni tuchunguze miradi inayofaa na mambo ambayo ni lazima ufanye ili uifikie.

Unaweza Kujiwekea Miradi Gani?

6. Ni mradi gani wa kwanza ulio wa maana ambao unaweza kujiwekea, na kwa nini?

6 Kama ilivyotajwa katika habari iliyotangulia, mradi wa kwanza ulio wa maana ambao unaweza kujiwekea ni kujithibitishia mwenyewe kwamba mambo yanayosemwa katika Biblia ni ya kweli. (Rom. 12:2; 2 Kor. 13:5) Huenda vijana wenzako wanaamini mageuzi au mafundisho mbalimbali ya kidini ambayo ni ya uwongo kwa sababu wameambiwa na wengine kwamba wanapaswa kuamini mambo hayo. Hata hivyo, hupaswi kuamini jambo kwa sababu tu mtu fulani anataka uamini. Kumbuka, Yehova anataka umtumikie kwa akili yako yote. (Soma Mathayo 22:36, 37.) Baba yetu wa mbinguni anataka ujenge imani yako juu ya mambo yaliyothibitishwa.—Ebr. 11:1.

7, 8. (a) Ili utie nguvu imani yako, unaweza kujiwekea miradi gani ambayo unaweza kufikia kwa muda mfupi? (b) Matokeo yatakuwa nini ukifikia miradi fulani ya muda mfupi?

7 Ili utie nguvu imani yako, kwa nini usijiwekee miradi fulani ambayo unaweza kuifikia kwa kipindi kifupi? Kwa mfano, unaweza kujiwekea mradi wa kusali kila siku. Ili utaje mambo hususa katika sala zako na kuepuka kurudia-rudia mambo, unaweza kuandika au kuweka akilini jambo fulani ambalo limetendeka siku hiyo unalotaka kutaja katika sala zako. Pia, hakikisha kwamba hutaji tu matatizo ambayo ulikabiliana nayo bali pia mambo uliyofurahia. (Flp. 4:6) Mradi mwingine ni kusoma Biblia kila siku. Je, unajua kwamba ukisoma kurasa nne hivi kila siku, utamaliza kusoma Biblia nzima kwa mwaka mmoja tu? * Andiko la Zaburi 1:1, 2 linasema hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye . . . mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku.”

8 Mradi wa tatu unaoweza kujiwekea ambao unaweza kufikia kwa kipindi kifupi ni kutayarisha jibu ambalo utatoa katika kila mkutano wa kutaniko. Mwanzoni, unaweza kusoma andiko au jibu lako. Baada ya muda, unaweza kujiwekea mradi wa kujibu kwa maneno yako mwenyewe. Kwa kweli, kila mara unapojibu unamtolea Yehova zawadi. (Ebr. 13:15) Baada ya kufikia miradi fulani kati ya hiyo, utakuwa na uhakika zaidi, na vilevile utamthamini Yehova zaidi, kisha utakuwa tayari kujiwekea miradi ya muda mrefu.

9. Ikiwa wewe bado si mhubiri wa Ufalme, unaweza kujiwekea miradi gani ya muda mrefu?

9 Unaweza kujiwekea miradi gani ya muda mrefu? Ikiwa bado hujaanza kutangaza habari njema hadharani, unaweza kujiwekea mradi wa muda mrefu wa kustahili kuwa mhubiri wa Ufalme. Baada ya kufikia mradi huo wenye kuheshimika, utahitaji kujitahidi kuhubiri kwa ukawaida na kwa ustadi, bila kukosa kamwe kuhubiri kwa mwezi hata mmoja. Pia, utahitaji kujifunza kutumia Biblia katika huduma. Ukifanya hivyo, inaelekea utaanza kufurahia zaidi kazi ya kuhubiri. Kisha unaweza kuongeza muda unaotumia katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba au hata kujitahidi kuongoza funzo la Biblia. Ukiwa mhubiri ambaye hajabatizwa, je, kuna mradi bora zaidi ambao unaweza kujiwekea kuliko kustahili kubatizwa na kuwa Shahidi aliyejiweka wakfu kwa Yehova Mungu?

10, 11. Vijana waliobatizwa wanaweza kujiwekea miradi gani ya muda mrefu?

10 Ikiwa tayari wewe ni mtumishi aliyebatizwa wa Yehova, hapa pana miradi fulani ya muda mrefu ambayo unaweza kujitahidi kufikia. Huenda pindi kwa pindi ukapenda kusaidia makutaniko kuhubiri maeneo ambayo hayahubiriwi kwa ukawaida. Unaweza pia kuamua kutumia nguvu zako na afya yako nzuri kufanya kazi ya upainia msaidizi au upainia wa kawaida. Makumi ya maelfu ya mapainia wenye furaha watakuambia kwamba utumishi wa wakati wote ni njia yenye kuthawabisha sana ya kumkumbuka Muumba wako wakati wa ujana wako. Hiyo ni miradi ambayo unaweza kufikia ukiwa bado unaishi nyumbani. Kutaniko lenu pia litafaidika ukifikia miradi hiyo.

11 Miradi mingine ya muda mrefu inaweza kukupa nafasi ya kutumika mbali na kutaniko lenu. Kwa mfano, unaweza kupanga kutumikia katika eneo au nchi nyingine ambayo ina uhitaji mkubwa. Huenda pia ukataka kusaidia katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme au ofisi za tawi katika nchi za kigeni. Unaweza hata kuingia katika utumishi wa Betheli au kuwa mmishonari. Bila shaka, mradi wa kwanza wa maana ambao utahitaji kufikia kabla ya kufikia miradi mingine ya muda mrefu ambayo imetajwa ni mradi wa kubatizwa. Ikiwa bado hujabatizwa, chunguza mambo unayohitaji kufanya ili ufikie mradi huo wa maana katika maisha yako.

Kufikia Mradi wa Kubatizwa

12. Vijana fulani wanabatizwa kwa sababu gani, na kwa nini sababu hizo hazitoshi?

12 Unaweza kueleza jinsi gani kusudi la kubatizwa? Huenda wengine wakafikiri kwamba kubatizwa kunawalinda wasifanye dhambi. Wengine wanaweza kufikiri kwamba wanapaswa kubatizwa kwa sababu vijana wenzao wamebatizwa. Huenda vijana wengine wakataka kuwapendeza wazazi wao. Hata hivyo, ubatizo haupaswi kuwa mkataba au makubaliano ambayo yanakuzuia kufanya mambo ambayo ungependa kufanya kisiri; wala hupaswi kubatizwa kwa sababu ya kusukumwa na wengine. Unapaswa kubatizwa wakati unapoelewa kabisa mambo yanayohusika katika kuwa Shahidi wa Yehova na unapokuwa na hakika kwamba uko tayari na ungependa kuchukua daraka hilo.—Mhu. 5:4, 5.

13. Kwa nini unapaswa kubatizwa?

13 Sababu moja inayofanya mtu abatizwe ni kwamba Yesu aliwaamuru wafuasi wake ‘wafanye wanafunzi na kuwabatiza.’ Pia, aliweka mfano kwa kubatizwa. (Soma Mathayo 28:19, 20; Marko 1:9.) Zaidi ya hayo, ubatizo ni hatua ya maana kwa wale ambao wangependa kuokolewa. Baada ya kutaja kwamba Noa alijenga safina ambamo yeye pamoja na familia yake walilindwa wakati wa Gharika, mtume Petro alisema hivi: “Lile ambalo linalingana na hili linawaokoa ninyi sasa pia, yaani, ubatizo, . . . kupitia ufufuo wa Yesu Kristo.” (1 Pet. 3:20, 21) Ingawa hivyo, hilo halimaanishi kwamba ubatizo ni kama bima au malipo ya kukusaidia wakati msiba unapotokea. Badala yake, unabatizwa kwa sababu unampenda Yehova na unataka kumtumikia kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zako zote.—Marko 12:29, 30.

14. Kwa nini huenda wengine wakasitasita kubatizwa, lakini una uhakikisho gani?

14 Huenda wengine wakasitasita kubatizwa kwa sababu wanaogopa kwamba huenda watatengwa na ushirika baadaye. Je, unaogopa kwa sababu hiyo? Ikiwa ndivyo, wakati mwingine si vibaya kuwa na woga kama huo. Woga huo unaweza kumaanisha unaelewa kwamba kuwa Shahidi wa Yehova ni daraka zito. Je, huenda kuna sababu nyingine? Labda bado hujasadiki kwamba kuishi kulingana na viwango vya Mungu ndiyo njia bora zaidi ya maisha. Ikiwa ndivyo ilivyo, kufikiria matokeo mabaya ambayo yanawapata wale wanaopuuza viwango vya Biblia kunaweza kukusaidia kufanya uamuzi. Kwa upande mwingine, inawezekana kwamba unapenda viwango vya Mungu lakini huamini kwamba unaweza kuishi kulingana navyo. Kwa kweli, hiyo inaweza kuwa ishara nzuri kwa sababu inaonyesha kwamba wewe ni mnyenyekevu. Kwa wazi, Biblia inasema kwamba mioyo ya wanadamu wote wasio wakamilifu ni yenye hila. (Yer. 17:9) Lakini unaweza kufanikiwa ikiwa utaendelea ‘kujilinda kulingana na neno la Mungu.’ (Soma Zaburi 119:9.) Hata ikiwa unasitasita kubatizwa kwa sababu fulani, unahitaji kutatua mahangaiko na wasiwasi huo. *

15, 16. Unaweza kujua jinsi gani kwamba uko tayari kubatizwa?

15 Hata hivyo, unaweza kujua jinsi gani kwamba uko tayari kubatizwa? Njia moja ni kujiuliza maswali kama haya: ‘Je, ninaweza kuwaeleza wengine mafundisho ya msingi ya Biblia? Je, ninashiriki katika huduma hata wakati ambapo wazazi wangu hawashiriki? Je, ninajitahidi kuhudhuria mikutano yote ya Kikristo? Je, ninaweza kukumbuka nyakati fulani hususa ambazo nilishinda msongo wa marafiki? Je, nitaendelea kumtumikia Yehova hata kama wazazi wangu na marafiki wataacha kumtumikia? Je, nimesali kuhusu uhusiano wangu pamoja na Mungu? Na je, kweli nimejiweka wakfu kwa Yehova bila masharti kupitia sala?’

16 Ubatizo ni hatua inayobadili maisha na inapaswa kuchukuliwa kwa uzito. Je, umekomaa vya kutosha kufikiria hatua hiyo kwa uzito? Kukomaa kunamaanisha mengi zaidi ya kuweza tu kutoa hotuba nzuri jukwaani au maelezo mazuri wakati wa mikutano. Unahitaji kuwa na uwezo wa kufanya maamuzi yanayotegemea uelewaji wa kanuni za Biblia. (Soma Waebrania 5:14.) Ikiwa katika maisha yako umefikia hatua ambayo unaweza kufanya hivyo, basi mbele yako kuna pendeleo kubwa zaidi kuliko yote—pendeleo la kumtumikia Yehova kwa moyo wote na kuishi kwa njia inayoonyesha kwamba kwa kweli umejiweka wakfu kwake.

17. Ni nini ambacho kitakusaidia kukabiliana na majaribu ambayo unaweza kupata baada ya kubatizwa?

17 Mara tu baada ya kubatizwa, unaweza kuwa na bidii sana ya kumtumikia Mungu. Hata hivyo, baada ya muda huenda ukakabiliana na matatizo ambayo yatajaribu imani na uthabiti wako. (2 Tim. 3:12) Usihisi kwamba unapaswa kukabiliana na majaribu hayo ukiwa peke yako. Waombe wazazi wako mashauri. Tafuta msaada kutoka kwa Wakristo wakomavu katika kutaniko. Dumisha urafiki pamoja na wale ambao watakutegemeza. Usisahau kamwe kwamba Yehova anakujali, na atakupatia nguvu unazohitaji ili ukabiliane na hali yoyote ile ambayo inaweza kutokea.—1 Pet. 5:6, 7.

Unaweza Jinsi Gani Kufikia Miradi Yako?

18, 19. Unaweza kufaidika jinsi gani kwa kuchunguza mambo unayotanguliza?

18 Hata ingawa una nia nzuri kabisa, je, unahisi kwamba huna wakati wa kutosha kamwe kufanya mambo unayotaka kufanya na ambayo unahitaji kufanya? Ikiwa ndivyo, unapaswa kuchunguza mambo unayotanguliza. Kwa mfano: Chukua ndoo ya plastiki na uweke mawe kadhaa makubwa ndani yake. Kisha ujaze ndoo hiyo kwa mchanga. Sasa una ndoo iliyojaa mawe na mchanga. Sasa ondoa mawe na mchanga katika ndoo hiyo lakini usitupe mawe na mchanga huo. Sasa, tia mchanga huo ndani ya ndoo kwanza, kisha ujaribu kuweka yale mawe ndani ya ndoo hiyohiyo. Hakuna nafasi ya kuweka mawe. Kwa nini? Kwa sababu ulitia mchanga kwanza ndani ya ndoo.

19 Unakabili tatizo kama hilo unapopanga jinsi ya kutumia wakati wako. Ukitanguliza mambo kama vile burudani, hutakuwa kamwe na wakati wa kutosha katika maisha yako wa kufanya mambo makubwa, yaani, mambo ya kiroho. Lakini ukifuata himizo la Biblia la ‘kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi,’ utaona kwamba una wakati wa kufanya mambo ya Ufalme na pia wakati wa burudani.—Flp. 1:10.

20. Unapaswa kufanya nini ukipata mahangaiko na mashaka unapojitahidi kufikia miradi yako?

20 Unapojitahidi kufikia miradi yako, kutia ndani ubatizo, huenda nyakati nyingine ukawa na mahangaiko na mashaka. Unapohisi hivyo, “mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” (Zab. 55:22) Kwa sasa, una nafasi ya kushiriki katika kazi ya maana na yenye kusisimua zaidi katika historia ya wanadamu, kampeni ya kuhubiri na kufundisha ulimwenguni pote. (Mdo 1:8) Unaweza kuamua kuangalia tu wengine wakifanya kazi hiyo. Au unaweza kuamua kushiriki katika kazi hiyo. Usisitesite kutumia vipawa vyako katika kuendeleza kazi ya Ufalme. Hutajuta kamwe kumtumikia ‘Muumba wako katika siku za ujana wako.’—Mhu. 12:1.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 2009 (1/8/2009), ukurasa wa 15-18.

Ungesema Nini?

• Kwa nini unapaswa kujiwekea miradi?

• Ni miradi gani inayofaa ambayo unapaswa kujitahidi kufikia?

• Ni mambo gani ambayo yanahusika katika kufikia mradi wa ubatizo?

• Kuchunguza mambo unayotanguliza kunaweza kukusaidia jinsi gani kufikia miradi yako?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Je, una mradi wa kusoma Biblia kila siku?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ni nini kitakachokusaidia kufikia mradi wa kubatizwa?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Unajifunza somo gani kutokana na mfano huu?