Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Bwana Wetu Mwenye Enzi Kuu!

Yehova Ni Bwana Wetu Mwenye Enzi Kuu!

Yehova Ni Bwana Wetu Mwenye Enzi Kuu!

“Nimeweka kimbilio langu katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”—ZAB. 73:28.

1. Kulingana na maneno ya Paulo katika 1 Wakorintho 7:31, inaonekana alikuwa akizungumza kuhusu nini?

“TAMASHA ya ulimwengu huu inabadilika,” akasema mtume Paulo. (1 Kor. 7:31) Inaonekana kwamba Paulo alikuwa akilinganisha ulimwengu na jukwaa, ambalo lina waigizaji wa drama wanaocheza sehemu zao mbalimbali, sehemu nzuri au mbaya mpaka tamasha inapobadilika.

2, 3. (a) Tatizo linalokabili utawala wa Yehova linaweza kulinganishwa na nini? (b) Tutachunguza maswali au maulizo gani?

2 Leo, drama ya maana zaidi inaendelea kuchezwa, na inakuhusu wewe pia! Drama hiyo inahusiana hasa na kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova Mungu. Drama hiyo inaweza kufananishwa na hali fulani ambayo inaweza kuwa katika nchi fulani. Kwa upande mmoja, kuna serikali halali ambayo inadumisha utaratibu. Na kwa upande mwingine, kuna kikundi cha wahalifu ambao wanatawala kwa udanganyifu, jeuri, na mauaji. Kikundi hicho haramu kinatatiza serikali halali na pia kinajaribu ushikamanifu wa raia wote kwa serikali hiyo.

3 Kuna hali kama hiyo katika ulimwengu wote. Kuna serikali halali ya “Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova.” (Zab. 71:5) Lakini sasa wanadamu wanatishwa na kikundi cha wahalifu kinachoongozwa na “yule mwovu.” (1 Yoh. 5:19) Kikundi hicho kinatatiza serikali halali ya Mungu na kinajaribu ushikamanifu wa watu wote kuelekea utawala wake halali. Hali hiyo ilianza jinsi gani? Kwa nini Mungu anairuhusu? Tunaweza kufanya nini kuhusu hali hiyo tukiwa mtu mmoja-mmoja?

Mambo Yanayohusika Katika Drama Hiyo

4. Drama ya ulimwenguni pote inayoendelea inatia ndani masuala gani mawili yanayohusiana?

4 Drama hiyo ya ulimwenguni pote inayoendelea inatia ndani masuala mawili yanayohusiana: Suala la enzi kuu ya Yehova na suala la utimilifu wa wanadamu. Katika Maandiko, mara nyingi Yehova anaitwa “Bwana Mwenye Enzi Kuu.” Kwa mfano, akimtegemea kabisa Yehova, mtunga-zaburi aliimba hivi: “Nimeweka kimbilio langu katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” (Zab. 73:28) “Enzi kuu” ni uwezo wa juu zaidi katika mamlaka au utawala. Mtawala mwenye enzi kuu ana mamlaka ya juu kabisa. Kuna sababu nzuri za kumwona Yehova Mungu kuwa Mwenye Mamlaka ya Juu Zaidi.—Dan. 7:22.

5. Kwa nini tunapaswa kuchochewa kuunga mkono enzi kuu ya Yehova?

5 Akiwa Muumba, Yehova Mungu ni Mwenye Enzi Kuu ya dunia na ulimwengu wote. (Soma Ufunuo 4:11.) Pia, Yehova ni Mwamuzi, Mpaji-Sheria, na Mfalme wetu, kwa sababu ana mamlaka yote ya kuhukumu, kutunga sheria, na ya kutawala serikali ya ulimwenguni pote. (Isa. 33:22) Kwa kuwa Mungu ndiye chanzo cha uhai wetu na tunamtegemea yeye, tunapaswa kumwona kuwa Bwana wetu Mwenye Enzi Kuu. Tutachochewa kuunga mkono cheo chake cha juu zaidi tukikumbuka sikuzote kwamba “Yehova amekifanya imara kiti chake cha ufalme mbinguni; nao ufalme wake mwenyewe umetawala juu ya kila kitu.”—Zab. 103:19; Mdo. 4:24.

6. Utimilifu ni nini?

6 Ili kuunga mkono enzi kuu ya Yehova, ni lazima tudumishe utimilifu wetu kwa Yehova. “Utimilifu” ni maadili bora au kamili. Mtu anayeshika utimilifu ni mtu mnyoofu na asiye na lawama. Mzee wa ukoo Ayubu alikuwa hivyo.—Ayu. 1:1.

Jinsi Drama Hiyo Ilivyoanza

7, 8. Shetani alipinga jinsi gani haki ya Yehova ya kutawala akiwa mwenye enzi kuu?

7 Miaka 6,000 hivi iliyopita, kiumbe mmoja wa roho alipinga haki ya Yehova ya kutawala akiwa mwenye enzi kuu. Tamaa ya kichoyo ya kutaka kuabudiwa ilichochea maneno na matendo ya kiumbe huyo mwasi. Aliwashawishi wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, wasiwe washikamanifu kwa enzi kuu ya Mungu na akajaribu kulichafua jina la Yehova kwa kudai kwamba Yehova alisema uwongo. (Soma Mwanzo 3:1-5.) Mwasi huyo akaja kuwa yule Adui mkubwa, Shetani (Mpinzani), Ibilisi (Mchongezi), nyoka (mdanganyifu), na joka (mwenye kumeza).—Ufu. 12:9.

8 Shetani mwenyewe alijifanya kuwa mtawala mpinzani. Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova angekabiliana jinsi gani na tatizo hilo? Je, angewaharibu papo hapo waasi hao watatu, yaani, Shetani, Adamu, na Hawa? Bila shaka, alikuwa na nguvu za kufanya hivyo, na tendo hilo lingeonyesha ni nani mwenye nguvu zaidi. Hilo pia lingethibitisha kwamba Yehova alikuwa amesema kweli kuhusu adhabu ya kuvunja sheria yake. Kwa nini Mungu hakutenda hivyo?

9. Shetani alitilia shaka nini?

9 Kwa kusema uwongo na kuwashawishi Adamu na Hawa wamwasi Mungu, Shetani alitilia shaka haki ya Yehova ya kutaka wanadamu wamtii. Zaidi ya hayo, kwa kuwashawishi wanadamu wawili wa kwanza wasimtii Mungu, Shetani pia alitilia shaka ushikamanifu wa viumbe wote wenye akili. Kama ilivyoonyeshwa katika kisa cha Ayubu, ambaye alikuwa mshikamanifu kwa enzi kuu ya Yehova, Shetani alidai kwamba anaweza kuwashawishi wanadamu wote wamwasi Mungu.—Ayu. 2:1-5.

10. Kwa kuruhusu muda upite kabla ya kutetea enzi yake kuu, Mungu ameruhusu nini?

10 Kwa kuruhusu muda upite kabla ya kutetea enzi yake kuu, Yehova amempa Shetani wakati wa kuthibitisha dai lake. Pia, Mungu amewapa wanadamu nafasi ya kuonyesha ushikamanifu wao kwa enzi yake. Ni nini ambacho kimetukia baada ya karne nyingi kupita? Shetani ameanzisha kikundi chenye nguvu cha wahalifu. Mwishowe, Yehova atamharibu Ibilisi na kikundi hicho, na kuthibitisha waziwazi kwamba Mungu ana haki ya kutawala. Yehova Mungu alikuwa na hakika kabisa kuwa matokeo yangekuwa mazuri hivi kwamba alitabiri hilo wakati uasi ulipotokea katika Edeni.—Mwa. 3:15.

11. Wanadamu wengi wamefanya nini kuhusiana na enzi kuu ya Yehova?

11 Wanadamu wengi wameonyesha imani na kudumisha utimilifu wao kwa enzi kuu ya Yehova na kutakaswa kwa jina lake. Wanadamu hao wanatia ndani Abeli, Enoko, Noa, Abrahamu, Sara, Musa, Ruthu, Daudi, Yesu, wanafunzi wa mapema wa Kristo, na mamilioni ya watu wanaoshika utimilifu leo. Watu kama hao ambao wanaunga mkono enzi kuu ya Mungu wanashiriki katika kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo na katika kuondoa suto ambayo Ibilisi ameleta juu ya jina la Yehova kwa kujigamba kwamba anaweza kuwashawishi wanadamu wote wamwasi Mungu.—Met. 27:11.

Matokeo ya Drama Hiyo ni Hakika

12. Tunaweza jinsi gani kuwa na hakika kwamba Mungu hatavumilia uovu milele?

12 Tunaweza kuwa na hakika kwamba hivi karibuni Yehova atatetea enzi yake kuu. Hatavumilia uovu milele, na tunajua kwamba tunaishi katika siku za mwisho. Yehova alichukua hatua ya kuwaharibu waovu wakati wa Gharika. Aliharibu Sodoma na Gomora, na Farao na majeshi yake. Sisera na jeshi lake, na Senakeribu na vikosi vyake vya Waashuru hawakufanikiwa kumshinda Aliye Juu Zaidi. (Mwa. 7:1, 23; 19:24, 25; Kut. 14:30, 31; Amu. 4:15, 16; 2 Fal. 19:35, 36) Hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova Mungu hataruhusu jina lake lidharauliwe milele wala hataruhusu Mashahidi wake watendewe vibaya milele. Zaidi ya hayo, sasa tunaona uthibitisho wa ishara ya kuwapo kwa Yesu na ya umalizio wa mfumo huu mwovu wa mambo.—Mt. 24:3.

13. Tunaweza jinsi gani kuepuka kuharibiwa pamoja na maadui wa Yehova?

13 Ili tuepuke kuharibiwa pamoja na maadui wa Mungu, ni lazima tuthibitishe ushikamanifu wetu kwa enzi kuu ya Yehova. Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? Kwa kuendelea kujitenga na utawala wa kihalifu wa Shetani na kukataa kuogopeshwa na watumishi wake. (Isa. 52:11; Yoh. 17:16; Mdo. 5:29) Tukifanya hivyo, ndipo tu tunapoweza kutetea enzi kuu ya Baba yetu wa mbinguni na kutumaini kulindwa wakati Yehova atakapoondoa suto juu ya jina lake na kuonyesha kwamba yeye ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote.

14. Ni habari gani zinazofunuliwa katika sehemu mbalimbali za Biblia?

14 Habari zaidi kuhusu wanadamu na enzi kuu ya Yehova zinaelezwa katika Biblia yote. Sura tatu za kwanza zinatueleza kuhusu uumbaji na kutumbukia kwa mwanadamu katika dhambi, nazo sura tatu za mwisho zinaeleza kuhusu kurudishwa kwa wanadamu kwenye ukamilifu. Kurasa za katikati zinatoa habari zaidi kuhusu hatua mbalimbali zilizochukuliwa na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova ili kutimiza kusudi lake kwa ajili ya wanadamu, dunia, na ulimwengu wote. Kitabu cha Mwanzo kinaonyesha jinsi Shetani alivyoingia katika ulimwengu na pia uovu, na sehemu ya mwisho ya kitabu cha Ufunuo inaonyesha jinsi uovu utakavyoondolewa, jinsi Ibilisi atakavyoharibiwa, na jinsi mapenzi ya Mungu yatakavyotendeka duniani kama ilivyo mbinguni. Kwa kweli, Biblia inafunua kinachosababisha dhambi na kifo na inaonyesha jinsi vitakavyoondolewa duniani, na badala yake watu wanaoshika utimilifu waishi milele wakiwa na shangwe nyingi sana.

15. Ni lazima sisi binafsi tufanye nini ili tufaidike wakati drama inayohusu enzi kuu inapofikia mwisho?

15 Hivi karibuni tamasha ya ulimwengu huu itabadilika kabisa. Pazia la drama ya karne nyingi inayohusu enzi kuu litateremshwa. Shetani ataondolewa kwenye jukwaa na mwishowe ataharibiwa, na bila shaka mapenzi ya Mungu yatashinda. Lakini ili tufaidike na yote hayo na kufurahia baraka nyingi zilizotabiriwa katika Neno la Mungu, ni lazima tuunge mkono enzi kuu ya Yehova sasa. Hatuwezi tu kusimama bila kuunga mkono upande wowote. Ili tuweze kusema: “Yehova yuko upande wangu,” ni lazima tubaki upande wake.—Zab. 118:6, 7.

Tunaweza Kudumisha Utimilifu!

16. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba wanadamu wanaweza kudumisha utimilifu kwa Mungu?

16 Tunaweza kuunga mkono enzi kuu ya Yehova na kudumisha utimilifu wetu, kwa sababu mtume Paulo aliandika hivi: “Hakuna jaribu ambalo limewapata ninyi ila lile lililo kawaida kwa watu. Lakini Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.” (1 Kor. 10:13) Ni nini chanzo cha jaribu linalotajwa na Paulo, na Mungu anatufanyia jinsi gani njia ya kutokea?

17-19. (a) Waisraeli walishindwa na jaribu gani jangwani? (b) Kwa nini tunaweza kudumisha utimilifu wetu kwa Yehova?

17 Kama mambo yaliyowapata Waisraeli jangwani yanavyoonyesha, “jaribu” linakuja kupitia hali ambazo zinaweza kutushawishi tuvunje sheria ya Mungu. (Soma 1 Wakorintho 10:6-10.) Waisraeli wangeweza kushinda jaribu, lakini walitamani “mambo mabaya” Yehova alipowapa kimuujiza kware ambao wangekula kwa mwezi mzima. Hata ingawa watu hawakuwa wamekula nyama kwa muda fulani, Mungu alikuwa amewapa mana ya kutosha ya kula. Hata hivyo, walishindwa na jaribu la kuwa na pupa isiyozuilika walipokuwa wakiokota kware hao.—Hes. 11:19, 20, 31-35.

18 Mapema, Musa alipokuwa akipokea Sheria juu ya Mlima Sinai, Waisraeli walianza kuabudu sanamu, wakajiingiza katika ibada ya ndama na raha za kimwili. Jaribu hilo halikuzuiwa kwa sababu kiongozi wao aliyeonekana hakuwepo. (Kut. 32:1, 6) Kabla tu ya kuingia katika Nchi ya Ahadi, maelfu ya Waisraeli walishawishiwa na wanawake Wamoabu, na wakafanya uasherati pamoja nao. Katika pindi hiyo, maelfu ya Waisraeli walikufa kwa sababu ya dhambi yao. (Hes. 25:1, 9) Nyakati nyingine, Waisraeli walishindwa na jaribu la kunung’unika kwa uasi, na pindi moja walisema vibaya kumhusu Musa na pia Mungu mwenyewe! (Hes. 21:5) Waisraeli hata walinung’unika baada ya kuharibiwa kwa Kora, Dathani, Abiramu, na marafiki wao wengine waliokuwa waovu, wakifikiri kimakosa kwamba uharibifu wa waasi hao haukuwa wa haki. Matokeo ni kwamba, Waisraeli 14,700 waliuawa kwa tauni iliyotoka kwa Mungu.—Hes. 16:41, 49.

19 Hakuna jaribu lolote kati ya majaribu ambayo yametajwa hapo juu ambalo Waisraeli hawangeweza kushinda. Waisraeli walishindwa na jaribu kwa sababu walipoteza imani na wakamsahau Yehova, wakasahau jinsi alivyowatunza kwa upendo, na kwamba njia zake ni za haki. Kama Waisraeli, majaribu tunayokabiliana nayo ni yale ambayo yanawapata wanadamu wengine pia. Tukijitahidi sana kushinda majaribu na kumtegemea Mungu ili atutegemeze, tunaweza kudumisha utimilifu wetu. Tunaweza kuwa na hakika kuhusu jambo hilo kwa sababu “Mungu ni mwaminifu” na haruhusu ‘tujaribiwe kupita tunavyoweza kuhimili.’ Yehova hatuachi kamwe kwa kuruhusu tupatwe na hali ambazo zinafanya iwe vigumu kwa wanadamu kufanya mapenzi yake.—Zab. 94:14.

20, 21. Tunapojaribiwa, Mungu anafanya “njia ya kutokea” jinsi gani?

20 Yehova anafanya “njia ya kutokea” kwa kututia nguvu ili tushinde jaribu. Kwa mfano, watesaji wanaweza kututesa kimwili ili kujaribu kufanya tuikane imani yetu. Mateso kama hayo yanaweza kufanya tulegeze msimamo wetu ili kuepuka kupigwa zaidi, kuteswa, au labda kuuawa. Hata hivyo, kulingana na maneno ya Paulo yaliyoongozwa na roho ya Mungu na ambayo yanatupa uhakikisho katika 1 Wakorintho 10:13, tunajua kwamba hali inayosababisha jaribu ni ya muda tu. Yehova hataruhusu hali hiyo iendelee hivi kwamba tushindwe kubaki waaminifu kwake. Mungu anaweza kuitia nguvu imani yetu na kutupatia nguvu za kiroho tunazohitaji ili kudumisha utimilifu wetu.

21 Yehova anatutegemeza kupitia roho yake takatifu. Roho hiyo inatukumbusha pia mawazo ya Kimaandiko ambayo tunahitaji ili kushinda jaribu. (Yoh. 14:26) Kwa hiyo, hatudanganywi kufuata mwenendo mbaya. Kwa mfano, tunaelewa masuala yanayohusiana ya enzi kuu ya Yehova na utimilifu wa wanadamu. Wakiwa na ujuzi huo, watu wengi wamesaidiwa na Mungu kubaki waaminifu mpaka kifo. Lakini si kifo kilichowafanyia njia ya kutokea; Yehova ndiye aliyewasaidia kuvumilia mpaka mwisho bila kushindwa na jaribu. Yehova anaweza kutusaidia vivyo hivyo. Kwa kweli, anatumia pia malaika wake waaminifu ili kutusaidia wakiwa watumishi wa watu wote ‘wanaotumwa kuhudumu kwa ajili ya wale watakaorithi wokovu.’ (Ebr. 1:14) Kama habari inayofuata inavyoonyesha, ni wale tu wanaoshika utimilifu ndio wanaoweza kutumaini kupata pendeleo lenye shangwe la kuunga mkono enzi kuu ya Mungu milele. Tunaweza kuwa kati yao ikiwa tunashikamana na Yehova akiwa Bwana wetu Mwenye Enzi Kuu.

Ungesema Nini?

• Kwa nini tunapaswa kumtambua Yehova kuwa Bwana wetu Mwenye Enzi Kuu?

• Kudumisha utimilifu wetu kwa Mungu kunamaanisha nini?

• Tunajua jinsi gani kwamba hivi karibuni Yehova atatetea enzi yake kuu?

• Kulingana na 1 Wakorintho 10:13, kwa nini tunaweza kudumisha utimilifu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 24]

Shetani aliwashawishi Adamu na Hawa wasiwe washikamanifu kwa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 26]

Azimia kuunga mkono enzi kuu ya Yehova