Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Kuna Viumbe wa Roho?

Je, Kweli Kuna Viumbe wa Roho?

Je, Kweli Kuna Viumbe wa Roho?

Huko Ulaya, mwanamke mzee anaingia kanisani akiwa na rozari mkononi, na anapiga magoti kwa heshima mbele ya sanamu ya Maria. Barani Afrika, familia inamwaga pombe fulani kali kwenye kaburi la mtu wa ukoo aliyeheshimiwa. Huko Amerika, mwanamume kijana anafunga na kutafakari, akitumaini kuwa ataweza kuwasiliana na malaika ambaye anaamini ndiye mlinzi wake. Barani Asia, kasisi anateketeza vitu ambavyo vimetengenezwa kwa karatasi za rangi mbalimbali kama toleo kwa roho za mababu waliokufa.

WATU wanaofanya mambo hayo wanafanana katika njia gani? Wote wanaamini kuwa kuna viumbe wenye akili walio katika makao ya roho ambao wanaweza kuwasiliana na wanadamu, na ambao wana uvutano mkubwa katika maisha yao. Bila shaka, imani hiyo si jambo geni wala lenye kushangaza. Kinachoshangaza ni kuwa watu wana maoni yanayotofautiana kuhusu viumbe wa roho.

Waislamu wanamwabudu Mungu mmoja—Allah. Watu katika Jumuiya ya Wakristo wanasema kwamba Mungu ni Utatu, unaofanyizwa na Mungu Baba, Mungu Mwana, na Mungu Roho Mtakatifu. Wahindu wanaamini kuwa kuna miungu ya kiume na ya kike zaidi ya elfu moja. Watu wengine wanasema kwamba roho hukaa katika wanyama, miti, miamba, na mito fulani. Nao wengine huathiriwa na vitabu, sinema, vipindi vya televisheni kuhusu malaika, mashetani, pepo, majini, na miungu ya kiume na ya kike.

Leo watu wana maoni mengi tofauti-tofauti na yanayopingana kuhusu miungu mbalimbali, na pia kuhusu jinsi ya kuwasiliana nayo. Si jambo linalopatana na akili kusema kuwa njia zote za kuwasiliana na miungu hiyo ni sawa. Hebu fikiria mfano huu: Kabla ya kupiga simu, tunahitaji kujua mtu tunayempigia simu na pia tunahitaji kuwa na hakika kwamba mtu huyo yupo na atakubali kuzungumza nasi. Ingekuwa ni kazi bure kujaribu kuwasiliana na mtu wa kuwaziwa tu. Isitoshe, lingekuwa jambo la hatari hata zaidi kuwasiliana na mtu mdanganyifu.

Kwa hiyo basi, ni nani hasa wanaokaa katika makao ya roho? Biblia inajibu swali hilo na pia inaeleza ni nani tunayepaswa kuwasiliana naye, na majibu tunayoweza kutazamia. Tafadhali endelea kusoma na huenda ukashangaa kuona yale ambayo Biblia inafunua.