Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaweza Kuwasiliana na Viumbe wa Roho?

Je, Unaweza Kuwasiliana na Viumbe wa Roho?

Je, Unaweza Kuwasiliana na Viumbe wa Roho?

MUNGU MWEZA YOTE amewapa viumbe fulani wa roho majukumu fulani. Kwa mfano, amempa Yesu Kristo jukumu la kuitawala dunia, na amewaweka malaika waaminifu waelekeze kazi ya kutangaza habari njema. (Ufunuo 14:6) Lakini, kuhusiana na sala, mambo ni tofauti. Hajampa yeyote jukumu la kusikiliza sala. Sala zetu zinapaswa kuelekezwa kwa Mungu peke yake.

Yehova ni “msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Anasikiliza sala zetu na kuzijibu. Kuhusu sala, mtume Yohana aliwaandikia watumishi wengine wa Yehova hivi: “Hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, [Mungu] hutusikia. Zaidi ya hayo, tukijua kwamba yeye hutusikia kwa habari ya jambo lolote tunaloomba, tunajua tutapata mambo yaliyoombwa kwa kuwa tumeyaomba kwake.”—1 Yohana 5:14, 15.

Malaika waaminifu hawataki tujaribu kuwasiliana nao wala kuelekeza sala zetu kwao. Wanaelewa na wanaunga mkono mpango wa Mungu kuhusu sala, ambao nyakati nyingine unawahusisha. Kwa njia gani? Wakati nabii Danieli aliposali kwa Yehova kuhusu uharibifu wa Yerusalemu, Mungu alijibu sala ya Danieli kwa kumtuma malaika Gabrieli akiwa na ujumbe wenye kutia moyo.—Danieli 9:3, 20-22.

Je, Tunaweza Kuwasiliana na Wafu?

Je, inafaa kuwasiliana na wafu? Kuna hadithi nyingi kuhusu watu wanaodai kuwa walizungumza na roho za wafu. Kwa mfano, mwanamke fulani wa Ireland aliambiwa na mtu anayewasiliana na pepo kuwa usiku uliotangulia mtu huyo alikuwa amezungumza na Fred, mume wake. Lakini Fred alikuwa amekufa majuma kadhaa yaliyopita. Mtu huyo aliendelea kumweleza yale ambayo “Fred” alisema, mambo ambayo mke wa Fred aliamini ni yeye tu aliyeyajua. Ingekuwa rahisi kwa mke wa Fred kuamua kuwa Fred alikuwa hai katika ulimwengu wa roho na kwamba alikuwa akijaribu kuzungumza naye kupitia mtu huyo asiyemjua. Hata hivyo, uamuzi huo ungepingana na yale ambayo Biblia inasema waziwazi kuhusu hali ya wafu.—Ona sanduku chini.

Hivyo basi, tunaweza kusema nini kuhusu hadithi kama hizo? Mbinu moja ya udanganyifu ambayo mashetani wanatumia ni kujifanya kuwa watu waliokufa, na katika kisa kilichotajwa, walijifanya kuwa Fred. Wakiwa na nia gani? Kuwakegeusha watu wasifuate mafundisho ya Biblia na kudhoofisha imani na tumaini lao katika Yehova. Bila shaka, Shetani na mashetani huwapotosha watu kwa “kila tendo lenye nguvu na ishara za uwongo na mambo ya ajabu na pamoja na kila udanganyifu usio wa uadilifu kwa wale wanaoangamia.”—2 Wathesalonike 2:9, 10.

Kwa hakika, kuna watu wanaowasiliana na pepo na pia washirika wao ambao wanaamini kabisa kuwa wanawasiliana na wafu. Lakini ukweli ni kwamba kama wanawasiliana na yeyote, basi wanawasiliana na viumbe wa roho ambao wanampinga Yehova. Vivyo hivyo, kuna wale wanaoamini kimakosa kwamba wanamwabudu Mungu. Mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika onyo hili zito: “Vitu ambavyo mataifa huvitoa dhabihu wao huvitoa dhabihu kwa roho waovu, na si kwa Mungu.”—1 Wakorintho 10:20, 21.

Kwa kuwa tunajua kwamba tunaweza kusali kwa Aliye Mkuu Zaidi, anayetupenda na kutujali, haifai kusali kwa kiumbe mwingine yeyote. Biblia inatupa uhakikisho huu: “Kwa habari ya Yehova, macho yake yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.”—2 Mambo ya Nyakati 16:9.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Kwa kuwa tunajua kwamba tunaweza kusali kwa Aliye Mkuu Zaidi, ambaye anatupenda na kutujali, haifai kusali kwa kiumbe mwingine yeyote.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Kweli au Si Kweli?

KWELI: SHETANI NI KIUMBE HALISI

“Shetani mwenyewe huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru.”—2 Wakorintho 11:14.

“Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.”—1 Petro 5:8.

“Yeye ambaye huendelea kufanya dhambi hutokana na Ibilisi, kwa sababu Ibilisi amekuwa akifanya dhambi tangu mwanzo.”—1 Yohana 3:8.

“Basi, jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.”—Yakobo 4:7.

“Ibilisi . . . alikuwa muuaji alipoanza, naye hakusimama imara katika kweli, kwa sababu kweli haimo ndani yake. Anaposema uwongo, yeye husema kulingana na mwelekeo wake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.”—Yohana 8:44.

SI KWELI: BAADA YA KUFA WATU WOTE WANAENDA KATIKA MAKAO YA ROHO

“Kwa jasho la uso wako utakula mkate mpaka utakaporudi katika udongo, kwa kuwa ulitolewa katika huo. Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.”—Mwanzo 3:19.

“Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.”—Mhubiri 9:5.

“Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote, kwa maana hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi, mahali unapokwenda.”—Mhubiri 9:10.

“Roho yake hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; Siku hiyo mawazo yake hupotea.”—Zaburi 146:4.

KWELI: MALAIKA WAAMINIFU WANATUJALI

“Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa, na yeye huwaokoa.”—Zaburi 34:7; 91:11.

“Je, wao [malaika] wote si roho kwa ajili ya utumishi wa watu wote, waliotumwa kuhudumu kwa ajili ya wale watakaorithi wokovu?”—Waebrania 1:14.

“Nikamwona malaika mwingine akiruka katikati ya mbingu, naye alikuwa na habari njema ya milele ili aitangaze kuwa habari za furaha kwa wale wanaokaa duniani, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu, akisema kwa sauti kubwa: ‘Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu.’”—Ufunuo 14:6, 7.

SI KWELI: YESU NI SAWA NA MUNGU

“Nataka mjue kwamba kichwa cha kila mwanamume ni Kristo; nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume; nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.”—1 Wakorintho 11:3.

“Vitu vyote vitakapokuwa vimetiishwa kwake, ndipo Mwana mwenyewe atakapojitiisha pia kwa Yeye aliyevitiisha vitu vyote kwake, ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.”—1 Wakorintho 15:28.

“Kwa kweli kabisa ninawaambia ninyi, Mwana hawezi kufanya hata jambo moja kwa uamuzi wake mwenyewe, ila tu lile analomwona Baba akifanya.”—Yohana 5:19.