Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ninahisi Nimependelewa Sana”

“Ninahisi Nimependelewa Sana”

Barua Kutoka Haiti

“Ninahisi Nimependelewa Sana”

BAADA ya tetemeko la ardhi lililotokea nchini Haiti mnamo Januari 12, 2010 (12/1/2010), haikuwa rahisi kwangu kutazama uharibifu huo katika vyombo vya habari. Kisha, tarehe 20 ya mwezi huo, rafiki yangu mpendwa Carmen akanipigia simu na kupendekeza kwamba tuende Haiti tukafanye kazi ya kujitolea. Nilikuwa nimekutana na Carmen miaka kadhaa mapema wakati tulipokuwa tumejitolea kama wauguzi kwenye ujenzi wa Jumba la Ufalme. Tangu wakati huo, tumejitolea katika miradi mingine kadhaa na tumekuwa marafiki wakubwa.

Nilimweleza Carmen kwamba huenda nisiwe na nguvu za kimwili wala kihisia za kukabiliana na hali nchini Haiti. Alinikumbusha kwamba tumewahi kufanya kazi pamoja vizuri na tunaweza kutegemezana. Nilitiwa moyo na maneno yake, hivyo nikapiga simu kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova, huko Brooklyn, New York, na kuzungumza na ndugu aliyekuwa akisimamia mpango wa kutuma misaada nchini Haiti kutoka Marekani. Nilimwomba aandike jina langu kwenye orodha ya wajitoleaji. Nilimweleza kumhusu Carmen na kusema kwamba tungependa kufanya kazi pamoja. Ndugu huyo aliniambia kuwa hawezi kunihakikishia kwamba sote wawili tutakubaliwa kufanya kazi ya kujitolea au hata kufanya kazi pamoja.

Hivyo, niliendelea na shughuli zangu za kila siku, nikifikiri kwamba singeweza kukubaliwa kwenda Haiti. Siku nne baadaye, Jumatatu (Siku ya 1) tarehe 25, nilipigiwa simu kutoka Brooklyn na kuulizwa kama ningeweza kwenda Haiti—ikiwezekana siku iliyofuata! Sikuamini masikio yangu. Nilisema kwamba nitafanya yote niwezayo. Kwanza, niliomba likizo kazini. Kisha, nikawasiliana na Carmen, kumbe hakuwa amealikwa kwenda Haiti kwa sababu hajui Kifaransa. Nilifurahi na wakati huohuo nikawa na wasiwasi. Mnamo Januari 28, baada ya kufanikiwa kupata tiketi ya ndege, nilisafiri kutoka New York mpaka Santo Domingo, Jamhuri ya Dominika, ambayo inapakana na Haiti.

Shahidi mmoja kijana alikuja kunipokea kwenye uwanja wa ndege na kunipeleka kwa gari mpaka kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Jamhuri ya Dominika. Wauguzi wengine wawili kutoka Marekani walifika siku hiyo pia, na sote tukalala katika chumba kimoja. Asubuhi iliyofuata, tulisafiri kwa gari mpaka kwenye ofisi ya tawi ya Haiti, katika jiji la Port-au-Prince. Safari hiyo ilichukua muda wa saa saba na nusu.

Baada ya kuvuka mpaka na kuingia Haiti, tuliona uharibifu mkubwa. Lilikuwa jambo la kushangaza kwamba tetemeko la sekunde 35 tu lingeweza kusababisha uharibifu mkubwa hivyo katika nchi hiyo yenye kuvutia. Haikuwa rahisi kutazama uharibifu huo katika televisheni; sasa wazia jinsi nilivyohisi nilipouona kwa macho yangu. Nyumba nyingi, kutia ndani ikulu ya rais, ziliharibiwa, na nyingine zikawa marundo ya vifusi. Wenye nyumba hizo walikuwa wametumia wakati mwingi kuzijenga, lakini ziliharibiwa kwa sekunde chache tu. Niliendelea kutafakari kuhusu ukweli wa kwamba mambo muhimu katika maisha si vitu vya kimwili.

Tulipofika kwenye ofisi ya tawi, mpokezi wa wageni alituona tukiingia, naye akakimbia kutoka kwenye dawati lake hadi mlangoni na kutukumbatia kwa furaha. Alitushukuru kwa kuacha shughuli zetu za kibinafsi na kuenda kuwasaidia. Baada ya chakula cha mchana, tulienda kwenye Jumba la Kusanyiko lililokuwa limegeuzwa kuwa hospitali. Huko nilikutana na Mashahidi wengine waliokuwa wamejitolea, kutia ndani madaktari wawili kutoka Ujerumani ambao ni wenzi wa ndoa, msaidizi wao, na mzalishaji fulani kutoka Uswisi.

Nilianza kufanya kazi usiku huohuo. Kulikuwa na wagonjwa 18—Mashahidi na wengine ambao si Mashahidi. Wagonjwa hao walikuwa wamelalia magodoro kwenye sakafu ya Jumba la Kusanyiko. Madaktari na wauguzi Mashahidi waliwatibu wagonjwa wote bila kuwabagua na bila malipo.

Usiku huo mgonjwa mmoja, mwanamume mwenye umri wa miaka 80, alikufa. Mke wake, mimi, na dada niliyekuwa nikikaa naye kwenye chumba kimoja, tulikuwa kando yake. Kisha, mwanamke kijana anayeitwa Ketly akaanza kulia kwa maumivu. Mkono wake wa kulia ulikuwa umekatwa kwa sababu ya majeraha aliyopata katika tetemeko hilo. Shahidi aliyekuwa mwalimu wa Biblia wa Ketly, alikuwa ameketi kando yake. Alikuwa akilala kando ya Ketly katika Jumba la Kusanyiko karibu kila usiku.

Nilimkaribia Ketly, nikitaka sana kumpunguzia maumivu, lakini Ketly hakuwa na maumivu ya kimwili tu. Alinieleza kuwa alikuwa katika nyumba ya rafiki yake wakati tetemeko lilipotokea. Hawakujua ni nini kilichokuwa kikiendelea. Walianza kukimbia kuelekea barazani, wakiwa wameshikana mikono, wakati ukuta ulipowaangukia na kuwafunika chini ya kifusi. Alimwita rafiki yake, lakini hakuitika. Alisema alijua mara moja kwamba rafiki yake amekufa. Sehemu fulani ya mwili wa rafiki yake ilikuwa imemlalia Ketly hadi waokoaji walipofika saa nne baadaye. Ketly alipoteza mkono wake wote wa kulia.

Usiku wangu wa kwanza hapo, Ketly alikuwa akifikiria matukio hayo kila alipojaribu kulala. Aliniambia hivi huku akilia: “Ninajua Maandiko yanavyosema kuhusu siku za mwisho na matetemeko ya ardhi. Ninajua tuna tumaini zuri la wakati ujao. Ninajua ninapaswa kushukuru kuwa hai. Lakini, hebu jiweke katika hali yangu sasa. Siku moja kila kitu ni shwari maishani mwako, kisha ghafula unajikuta katika hali kama hii.” Kwa kuwa singeweza kumsaidia, nilimkumbatia tu na kuanza kulia. Tuliendelea kulia mpaka alipolala.

Kila siku, daktari mmoja na wauguzi wawili, walitumwa kwenda kuwasaidia watu waliokuwa wakihitaji kutibiwa. Nilitumwa katika mji wa Petit Goave, umbali wa karibu saa mbili hivi kutoka Port-au-Prince. Nilienda na wajitoleaji wengine wawili—muuguzi kutoka Florida na daktari kutoka Ufaransa. Tulifika saa 3:30 asubuhi, tukashusha vifaa vyetu, na kuviingiza katika Jumba la Ufalme. Watu walikuwa wameambiwa kuhusu ziara yetu, hivyo waliketi na kutusubiri tufike.

Tulianza kufanya kazi mara moja. Kulikuwa na joto kali, na watu waliokuwa wanahitaji matibabu walizidi kuongezeka. Tulifanya kazi bila kupumzika hadi saa tisa hivi alasiri. Sote watatu tulitoa chanjo kwa watu 114 na kutoa ushauri wa kitiba kwa watu 105 siku hiyo. Nilikuwa nimechoka lakini mwenye furaha kwa kuwa tuliwasaidia watu waliokuwa na uhitaji.

Kwa ujumla, nilikaa Haiti kwa majuma mawili nikifanya kazi ya kutoa msaada. Karibu kila usiku, nilifanya zamu ya saa 12 katika Jumba la Kusanyiko. Lilikuwa jukumu kubwa sana, ambalo sikuwa nimewahi kulishughulikia kabla ya hapo. Hata hivyo, nilijihisi kuwa nimependelewa na kubarikiwa kufanya kazi Haiti. Ninafurahi sana kwamba niliweza kuwapa faraja na msaada watu wa Haiti, ambao wameteseka sana.

Kuna mambo mengi tunayoweza kujifunza kutoka kwao. Kwa mfano, mmoja kati ya wagonjwa niliowashughulikia ni Eliser, kijana mwenye umri wa miaka 15, ambaye mguu wake mmoja ulihitaji kukatwa. Niligundua kwamba angehifadhi chakula chake ili ale na Jimmy, ambaye alikuwa akilala kando yake. Alinieleza kwamba si wakati wote Jimmy alikuwa akila nyumbani kabla ya kuja jioni. Mfano wa Eliser ulinisaidia kuelewa kwamba hatuhitaji kuwa matajiri, wala kuwa na afya nzuri, ili kuwagawia wengine tulicho nacho.

Wajitoleaji niliofanya kazi nao walikuwa na mtazamo kama huo pia. Mjitoleaji mmoja hakuwa anajisikia vizuri na mwingine alikuwa na maumivu ya mgongo. Hata hivyo, wote walitanguliza mahitaji ya wagonjwa badala ya starehe zao wenyewe. Hilo lilinitia moyo kuendelea kufanya kazi. Mara kwa mara, sote tulihisi tumechoka kihisia, kiakili, na kimwili, lakini tulitegemezana na kusonga mbele. Hayo ni mambo ambayo sitayasahau kamwe! Ninashukuru sana kuwa sehemu ya tengenezo la Wakristo safi ambao wana fadhili, upendo, na roho ya kujidhabihu.

Kabla sijaondoka Haiti, wagonjwa wawili ambao mikono yao ya kulia ilikuwa imekatwa, waliweza kuniandikia barua za shukrani, ambazo waliniomba nizisome nikiwa ndani ya ndege. Nilifanya vivyo hivyo. Barua hizo zilinigusa moyo sana, na sikuweza kujizuia kutokwa na machozi.

Tangu niliporudi nyumbani, nimekuwa nikiwasiliana na baadhi ya marafiki zangu wapya niliowapata nchini Haiti. Urafiki imara unaundwa na kujaribiwa wakati wa hali ngumu na matatizo. Nina hakika kwamba urafiki wetu unaweza kustahimili jaribu lolote lile wakati ujao. Ninahisi kuwa nimependelewa sana.