Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unawajali Wazazi Wasio na Wenzi wa Ndoa?

Je, Unawajali Wazazi Wasio na Wenzi wa Ndoa?

Je, Unawajali Wazazi Wasio na Wenzi wa Ndoa?

NI WATU wachache walio na shughuli nyingi na zinazohitaji wakati na nguvu kama vile wazazi wasio na wenzi wa ndoa. Wanakabili mambo mengi magumu. Lazima washughulikie majukumu mengi ya kutunza familia zao. Kando na kufanya kazi, inawapasa kununua vitu wanavyohitaji, kupika, kufanya usafi, na kulea watoto. Pia, wanahitaji kutunza afya ya watoto wao, kuwa na wakati wa burudani pamoja nao, na kuwategemeza kihisia, na ikiwezekana, kutenga wakati kwa ajili yao wenyewe.

Ingawa leo familia za mzazi mmoja zinaongezeka sana na zinazidi kuwa sehemu ya kawaida ya jamii, inaweza kuwa rahisi kuwasahau. Mama mmoja alikubaliana na jambo hilo na kusema: “Sikuwafikiria sana wazazi wasiokuwa na wenzi wa ndoa hadi mimi mwenyewe nilipojipata katika hali hiyo.” Unaweza kufanya nini ili kuonyesha kuwa unawafikiria wazazi hao? Je, unapaswa kuwajali? Acheni tuchunguze sababu tatu za kuwajali wazazi hao.

Sababu za Kuwajali

Wazazi wengi wasio na wenzi wa ndoa wanahitaji msaada. Mjane fulani mwenye umri wa miaka 41 na aliye na watoto wawili anasema, “Wakati fulani huwa sina hakika nifanye nini, na hujihisi nimelemewa na majukumu mengi.” Ujane, kuachwa na mwenzi, au hali nyingine mbaya huwaacha wazazi hao wakihisi kama mama mmoja alivyohisi. Alisema, “Tunaomba msaada na tunauhitaji haraka!”

Kuwajali kunachangia furaha yako. Je, umewahi kumsaidia mtu kubeba mzigo ambao ulikuwa mzito kwa mtu mmoja kuubeba peke yake? Ikiwa ndivyo, huenda ulihisi umeridhika kwa kujua kwamba umemsaidia mtu huyo. Vivyo hivyo, wazazi wasio na wenzi wa ndoa wanabeba mzigo ambao nyakati nyingine unaweza kuwa mzito mno kwa mtu kuubeba peke yake. Ikiwa utawasaidia kuubeba mzigo huo, basi utatambua ukweli wa maneno haya ya Zaburi 41:1: “Heri mtu anayewajali maskini.”—Biblia Habari Njema.

Ni jambo linalompendeza Mungu. Andiko la Yakobo 1:27 linasema hivi: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyotiwa unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kuwatunza mayatima na wajane katika dhiki yao.” Hilo linatia ndani kuwajali wazazi wasio na wenzi wa ndoa. * Andiko la Waebrania 13:16 linasema: “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.”

Tukiwa na sababu hizo tatu za kuwajali wazazi wasio na wenzi wa ndoa, hebu tuchunguze jinsi unavyoweza kuwasaidia na kuwa na hakika kwamba msaada unaotoa unafaa.

Tambua Mahitaji Yao

Huenda ikaonekana kuwa unalohitaji kufanya ni kumuuliza hivi mzazi asiye na mwenzi wa ndoa: “Ninaweza kukusaidia jinsi gani?” Hata hivyo, mara nyingi swali kama hilo halimsukumi mtu akueleze mahitaji yake. Kama tulivyoona, andiko la Zaburi 41:1 linatuhimiza ‘tuwajali maskini.’ Kitabu kimoja cha marejeo kinaeleza kuwa neno la Kiebrania lilinalotumika hapa linaweza kumaanisha “hatua ya kuchanganua mawazo tata na hivyo kutenda kwa hekima.”

Kwa hiyo, ili upate njia nzuri ya kumsaidia mzazi asiye na mwenzi wa ndoa, unahitaji kufikiria sana hali ngumu ambazo anakabili. Uwe macho na usichukulie mambo kijuujuu tu. Jiulize, ‘Ikiwa ningekabili hali kama yake, ni msaada gani ambao ningehitaji?’ Bila shaka, wazazi wengi wasio na wenzi wa ndoa watakwambia kuwa hata ujitahidi kadiri gani, huwezi kuelewa hali yao isipokuwa wewe mwenyewe uwe mzazi asiye na mwenzi. Hata hivyo, ukijitahidi unavyoweza kuelewa hali zao utakuwa katika hali nzuri ya ‘kutenda kwa kuwajali.’

Iga Mfano Mkamilifu wa Mungu

Inapohusu kuwajali wazazi wasio na wenzi wa ndoa, hakuna mtu ambaye amewahi kufanya hivyo kwa njia nzuri na kwa upendo mwingi zaidi kuliko Yehova Mungu. Maandiko mengi yanaonyesha jinsi Yehova Mungu anavyowajali wajane, wavulana wasio na baba, na hata wazazi wasio na wenzi wa ndoa. Kwa kuchunguza jinsi Mungu anavyohangaikia mahitaji ya watu hao wa hali ya chini, tunaweza kujifunza mambo mengi kuhusu jinsi ya kuwasaidia kwa njia inayofaa kabisa. Kuna mambo manne makuu ya kufikiria.

Wasikilize kwa makini

Katika Sheria ambayo Yehova alilipa taifa la Israeli la kale, alitangaza kuwa ‘hangekosa kukisikia kilio’ cha mtu wa hali ya chini. (Kutoka 22:22, 23) Unaweza kuiga jinsi gani mfano huo mzuri? Mara nyingi, wazazi wasio na wenzi wa ndoa wanahisi wakiwa wapweke sana, kwa kuwa nyumbani hakuna mtu mwingine mzima wanayeweza kuzungumza naye. Mzazi mmoja asiye na mwenzi wa ndoa alisema hivi kwa huzuni: “Watoto wanapolala, wakati mwingine mimi hushindwa kujizuia nisilie. Upweke ninaohisi ni mwingi sana hivi kwamba nyakati nyingine inakuwa vigumu sana kuvumilia.” Inapofaa, je, unaweza kuwa tayari ‘kukisikia kilio’ cha mzazi kama huyo ambaye anahitaji kuelezea hisia zake? Ukifanya hivyo wakati na mahali panapofaa, unaweza kumsaidia sana kukabiliana na matatizo yake.

Watie moyo kwa maneno yako

Yehova aliongoza kwa roho yake kuandikwa kwa nyimbo takatifu, au zaburi, ambazo Waisraeli wangeimba nyakati za ibada. Hebu wazia jinsi wajane Waisraeli na wavulana wasio na baba walivyotiwa moyo walipoimba zaburi hizo zilizoongozwa na roho ya Mungu ambazo ziliwakumbusha kuwa Yehova ni “baba” na “mwamuzi” wao, na kwamba atawapa kitulizo. (Zaburi 68:5; 146:9) Hata sisi tunaweza kumfariji mzazi asiye na mwenzi wa ndoa kwa maneno ambayo atayakumbuka miaka mingi baadaye. Ruth, ambaye ni mzazi asiye na mwenzi wa ndoa, bado anakumbuka sana wakati baba fulani mwenye uzoefu alipomwambia maneno yafuatayo miaka 20 iliyopita: “Unafanya kazi nzuri ya kulea wavulana wako wawili. Endelea na moyo huohuo.” Ruth anaeleza: “Maneno hayo yalinisaidia sana.” Kwa kweli, “maneno yenye fadhili ni dawa nzuri” na yanaweza kumtia moyo mzazi asiye na mwenzi zaidi ya vile tunavyoweza kufahamu. (Methali 15:4, Contemporary English Version) Je, unaweza kufikiria maneno hususa na yenye kutia moyo ambayo unaweza kumwambia mzazi asiye na mwenzi?

Toa msaada inapohitajika

Sheria ambayo Yehova alilipa taifa la Israeli la kale ilitia ndani mpango wa kuwapa wajane na wavulana wasio na baba chakula katika njia ambayo haingewavunjia heshima. Kupitia mpango huo, watu hao wa hali ya chini walikuwa na chakula cha kutosha ‘kula na kujishibisha.’ (Kumbukumbu la Torati 24:19-21; 26:12, 13) Sisi pia, kwa busara na heshima, tunaweza kuisaidia familia ya mzazi mmoja yenye uhitaji. Je, unaweza kuipelekea chakula au bidhaa za kutumia nyumbani? Je, una nguo ambazo mzazi asiye na mwenzi wa ndoa au watoto wake wanaweza kutumia? Au je, unaweza kumsaidia kwa kumpa pesa ambazo anaweza kununulia vitu ambavyo familia yake inahitaji?

Shirikiana nao

Yehova aliamuru kuwa wavulana wasio na baba na wajane washirikishwe katika sherehe za kila mwaka za taifa, ili waweze kufurahia ushirika pamoja na Waisraeli wengine. Hata, waliambiwa: ‘Mtashangilia.’ (Kumbukumbu la Torati 16:10-15) Leo pia, Wakristo wanahimizwa “[wa]karibishane,” na kuwa na ushirika wenye furaha. (1 Petro 4:9) Hivyo, kwa nini usiikaribishe familia ya mzazi mmoja nyumbani kwako kwa ajili ya mlo? Huhitaji kuandaa vitu vingi. Yesu alipofurahia ushirika katika nyumba za rafiki zake, alisema, “Mambo machache ndiyo yanayohitajiwa, au moja tu.”—Luka 10:42.

Jitihada Zako Zitathaminiwa

Kathleen, ambaye alilea watoto watatu bila mwenzi wa ndoa, anasema kuwa hatasahau shauri hili lenye hekima, “Usitazamie chochote; thamini kila kitu.” Kama Kathleen, wazazi wengi wasio na wenzi wa ndoa wanatambua kuwa wana jukumu la kuwalea watoto wao. Kwa hiyo, hawatazamii watu wengine wawafanyie yale wanayopaswa kufanya. Hata hivyo, hakuna shaka kuwa watathamini msaada wowote wanaopokea. Unaweza kuchangia hali yao nzuri na furaha yako mwenyewe kwa kuwafikiria wazazi wasio na wenzi wa ndoa, ukiwa na hakika kuwa Yehova Mungu “atakulipa kwa tendo jema.”—Methali 19:17, BHN.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ingawa maneno “mzazi asiye na mwenzi wa ndoa” hayapatikani katika Biblia, maneno “mjane” na “mvulana asiye na baba” yametumika sana. Hilo linamaanisha kwamba hata nyakati za Biblia, kulikuwa na wazazi wasio na wenzi wa ndoa.—Isaya 1:17.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Unakumbuka mara ya mwisho ulipoikaribisha familia ya mzazi mmoja ilikuwa lini? Je, unaweza kujaribu kufanya hivyo?