Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtoto Wako Atasema Nini?

Mtoto Wako Atasema Nini?

Mtoto Wako Atasema Nini?

WAZAZI: Katika ukurasa wa 16-20 wa toleo la Januari 15, 2010, tulizungumza kuhusu kuwa na vipindi vya mazoezi pamoja na watoto wenu. Habari hii inatoa mapendekezo yanayoweza kuwasaidia kuwatayarisha watoto wenu wadogo kupambana na matatizo shuleni. Mkipenda, mnaweza kuwa na vipindi hivyo vya mazoezi wakati wa jioni ya Ibada ya Familia yenu.

WATOTO ambao ni Mashahidi wa Yehova wanakabiliana na matatizo mengi. Mara nyingi wanafunzi wenzao wanawauliza kwa nini hawashiriki katika utendaji mbalimbali, kama vile kuisalimu au kuipigia bendera saluti, kusherehekea sikukuu za kuzaliwa, na kushiriki katika miradi ya wakati wa likizo. Ikiwa mwana au binti yako ataulizwa maswali kama hayo, mtoto wako atajibu jinsi gani?

Watoto fulani Wakristo wanasema tu hivi: “Siwezi kufanya hivyo. Dini yangu hainiruhusu.” Watoto hao wanapaswa kupongezwa kwa sababu ya kuchukua msimamo imara. Huenda jibu lao likawazuia wanafunzi wenzao kuwauliza maswali zaidi. Hata hivyo, Biblia inatuhimiza ‘tuwe tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hutaka kutoka kwetu sababu’ ya mambo tunayoamini. (1 Pet. 3:15) Kufanya hivyo kunamaanisha mengi zaidi ya kusema tu, “Siwezi kufanya hivyo.” Hata ikiwa wengine hawakubaliani nasi, huenda wengine wao wakapenda kujua sababu zinazotuongoza kufanya maamuzi hayo.

Vijana wengi ambao ni Mashahidi wamewaeleza wanafunzi wenzao masimulizi ya Biblia wakitumia vitabu kama vile Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. Masimulizi hayo yanaweza kusaidia kuonyesha kwa nini watoto wa Mashahidi wanafanya au hawafanyi mambo fulani. Wanafunzi fulani wanasikiliza kwa makini hadithi hizo za Biblia, na mafunzo mengi ya Biblia yameanzishwa kwa njia hiyo. Huenda wanafunzi wengine wakaona kwamba ni vigumu kusikiliza hadithi yote ya Biblia. Bila maelezo kamili, huenda masimulizi fulani ya Biblia yakawa magumu sana kueleweka kwa watoto wanaoenda shuleni. Msichana mwenye umri wa miaka 11 anayeitwa Minhee alipoalikwa na rafiki yake kwenye sherehe ya sikukuu ya kuzaliwa, alimwambia rafiki yake hivi: “Biblia haituambii tusherehekee sikukuu za kuzaliwa. Yohana Mbatizaji ambaye anatajwa katika Biblia, aliuawa wakati wa sikukuu ya kuzaliwa.” Hata hivyo, Minhee anakumbuka kwamba inaonekana rafiki yake hakuelewa jibu lake.

Nyakati nyingine, kuna faida ya kumwonyesha mwanafunzi mwenzako picha au simulizi katika vitabu vyetu. Namna gani ikiwa wasimamizi wa shule wanasema kwamba hawangependa watoto wawaonyeshe wanafunzi wenzao vitabu vya kidini? Je, watoto wetu wanaweza kutoa ushahidi kwa njia inayofaa hata bila kichapo chochote? Unaweza kuwasaidia jinsi gani watoto wako ili wajitetee?

Muwe na Vipindi vya Mazoezi

Kuna faida ya kuwa na vipindi vya mazoezi nyumbani huku wazazi wakiigiza sehemu ya wanafunzi shuleni. Watoto wanapojaribu kutetea imani yao, wazazi wanapaswa kuwapongeza kwa sababu ya jitihada zao na kuwaonyesha jinsi wanavyoweza kuboresha njia yao ya kutoa sababu na kwa nini inafaa kufanya hivyo. Kwa mfano, wapendekezee watumie maneno ambayo yataeleweka kwa wanafunzi wa umri wao. Joshua, mtoto wa kiume mwenye umri wa miaka tisa, anasema kwamba wanafunzi wenzake hawakuelewa maneno kama “dhamiri” na “ushikamanifu.” Hivyo, alilazimika kutumia maneno rahisi ili kuzungumza nao.—1 Kor. 14:9.

Wanafunzi fulani wa shule wanaouliza swali wanaweza kuacha kuonyesha upendezi ikiwa watapewa jibu lenye maneno mengi. Kwa kuwahusisha katika mazungumzo na kuwaonyesha sababu, vijana Mashahidi wanaweza kuwachochea waendelee kupendezwa. Haneul, msichana mwenye umri wa miaka kumi, anasema, “Wanafunzi wenzangu wanapenda mazungumzo, hawapendi kuelezwa mambo.” Ili muwe na mazungumzo, uliza maswali, na kisha usikilize kwa makini maoni ya kibinafsi yanayotolewa.

Mazungumzo yanayofuata yanaonyesha jinsi watoto Wakristo wanavyoweza kuzungumza na wanafunzi wenzao. Si lazima mtoto ashike akilini maneno yaliyo katika mazungumzo hayo, kwa sababu watoto wanatofautiana, na hali tofauti zinashughulikiwa kwa njia tofauti. Kwa hiyo, mtoto ambaye ni Shahidi anapaswa kuwa na mawazo hayo akilini, aeleze kwa maneno yake, kisha aseme mawazo hayo kwa njia inayofaana na hali na inayowafaa wanafunzi wenzake. Ikiwa una watoto wanaoenda shuleni, jaribu kuigiza mazungumzo haya pamoja nao.

Kuwazoeza watoto ni jambo linalohitaji wakati na bidii. Wazazi Wakristo wanapaswa kuwafundisha watoto wao kanuni za Biblia na kuwashawishi kuishi kulingana na kanuni hizo.—Kum. 6:7; 2 Tim. 3:14.

Katika jioni inayofuata ya Ibada yenu ya Familia, jaribuni kufanya mazoezi ya mazungumzo yaliyoonyeshwa hapa. Ona jinsi mazoezi hayo yanavyoweza kuwa na matokeo mazuri. Kumbuka kwamba kusudi si kuweka akilini majibu au maneno fulani. Hata mnaweza kuigiza hali fulani zaidi ya mara moja, ukitoa majibu tofauti na kuona jinsi watoto wako wanavyoshughulikia hali mbalimbali. Wanapojaribu kueleza msingi wa imani yao, wasaidie wasitawishe usawaziko na busara. Baada ya muda, utawafundisha watoto wako jinsi ya kutetea mambo wanayoamini mbele ya wanafunzi wenzao, majirani, na walimu wao pia.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4, 5]

SHEREHE ZA SIKUKUU YA KUZALIWA

Mary: John, ningependa kukukaribisha kwenye sherehe ya sikukuu yangu ya kuzaliwa.

John: Asante Mary kwa kunikumbuka. Tafadhali niambie kwa nini utakuwa na karamu ya sikukuu ya kuzaliwa?

Mary: Ili nikumbuke siku yangu ya kuzaliwa. Kwani wewe husherehekei siku yako ya kuzaliwa?

John: Hapana, sisherehekei.

Mary: Kwa nini? Familia yetu ilifurahi nilipozaliwa.

John: Familia yetu ni kama familia yenu. Wao pia walifurahi nilipozaliwa. Lakini sifikirii kwamba hiyo ni sababu ya kunifanya nisherehekee siku hiyo kila mwaka. Wakati wa karamu za sikukuu za kuzaliwa, wengi wanafikiri kwamba wao ndio watu wa maana zaidi. Lakini Mungu ndiye mtu wa maana zaidi, sivyo? Na je, hatupaswi kumshukuru kwa sababu alitupatia uhai?

Mary: Unamaanisha kwamba sipaswi kuwa na karamu ya sikukuu yangu ya kuzaliwa?

John: Huo ni uamuzi wako Mary. Lakini kwa nini usifikirie jambo hili? Ingawa watu wengi wanapenda kupokea zawadi za sikukuu ya kuzaliwa, Biblia inasema kwamba kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea. Badala ya kujikazia fikira sisi wenyewe wakati wa sikukuu yetu ya kuzaliwa, je, halingekuwa jambo zuri kumshukuru Mungu, kuwafikiria wengine, na kuwatendea mema?

Mary: Sijawahi kamwe kufikiria jambo hilo. Kwa hiyo, wazazi wako hawakupi zawadi zozote?

John: Bila shaka wananipa. Lakini wazazi wangu hawangoji mpaka sikukuu yangu ya kuzaliwa ifike. Wananipa zawadi mara nyingi kadiri wanavyopenda. Lakini Mary, ungependa kujua jinsi sherehe za sikukuu ya kuzaliwa zilivyoanza?

Mary: Tafadhali niambie.

John: Kesho nitakusimulia hadithi yenye kusisimua kuhusu karamu fulani ya sikukuu ya kuzaliwa ambayo ilifanywa zamani.

KUPIGIA BENDERA SALUTI

Gail: Claire, kwa nini huipigii bendera saluti?

Claire: Asante sana Gail kwa kuuliza swali hilo. Lakini kwanza acha nikuulize kwa nini wewe unaipigia bendera saluti?

Gail: Ninaipigia saluti kwa sababu ninapenda nchi yangu.

Claire: Gail, ninajua unampenda mama yako. Lakini humpigii mama yako saluti, sivyo?

Gail: Ni kweli. Unajua ninaipigia bendera saluti kwa sababu ninaiheshimu. Wewe huheshimu bendera?

Claire: Ninaiheshimu. Lakini hatupigii saluti kila kitu na kila mtu ambaye tunamheshimu, sivyo?

Gail: Ni kweli, ninamheshimu mwalimu wetu, lakini simpigii saluti. Basi, sijui ni kwa nini ninaipigia bendera saluti.

Claire: Gail, watu wengi wanafikiri kwamba bendera inawakilisha nchi yao. Wanapopigia bendera saluti wanamaanisha kwamba wako tayari kufanya jambo lolote kwa ajili ya nchi yao. Lakini mimi sihisi hivyo. Siwezi kutoa uhai wangu kwa ajili ya nchi yangu kwa sababu Mungu ndiye aliyenipa uhai. Nimeamua kumpa uhai wangu. Kwa hiyo, ingawa ninaiheshimu bendera, siipigii saluti.

Gail: Nimeelewa.

Claire: Hata hivyo, Gail, ninafurahi kwamba ulitaja jambo hilo. Na ikiwa ungependa kujua kwa nini ninafanya au sifanyi mambo fulani, niulize tu. Biblia inasema kwamba zamani mfalme fulani wa Babiloni aliwaamuru watu wainamie sanamu. Watu fulani walikataa kuinama, hata ingawa jambo hilo lilihatarisha uhai wao.

Gail: Ni kweli? Ni nini kilichowapata?

Claire: Nitakuambia kuwahusu wakati wa mapumziko ya mchana.

SIASA KATIKA SHULE

Mike: Tim, unafikiri ni nani anayepaswa kuwa kiongozi wa darasa letu?

Tim: Siungi mkono mwanafunzi yeyote anayetaka kuwa kiongozi.

Mike: Kwa nini?

Tim: Tayari nina kiongozi bora zaidi. Nikiwa Mkristo, nimeahidi kumfuata Yesu. Kwa hiyo, siwezi kumchagua kiongozi mwingine. Lakini je, unajua ni kwa nini ninafikiri kwamba yeye ndiye Kiongozi bora kabisa?

Mike: Hapana, sitaki kujua.

Tim: Basi, ikiwa siku moja utataka kujua, nitafurahi kukuambia.

[Picha]

“John, ningependa kukukaribisha kwenye sherehe ya sikukuu yangu ya kuzaliwa”

[Picha katika ukurasa wa 3]

“Kwa nini huipigii bendera saluti?”