Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Sasa Ndio Wakati Unaokubalika Hasa”

“Sasa Ndio Wakati Unaokubalika Hasa”

“Sasa Ndio Wakati Unaokubalika Hasa”

“Tazama! Sasa ndio wakati unaokubalika hasa. Tazama! Sasa ndiyo siku ya wokovu.”—2 KOR. 6:2.

1. Kwa nini tunahitaji kutambua kila wakati kazi ambayo tunapaswa kufanya?

“KUNA wakati uliowekwa wa kila kitu, hata kuna wakati wa kila jambo chini ya mbingu.” (Mhu. 3:1) Sulemani alikuwa akiandika kuhusu umuhimu wa kutambua wakati unaofaa zaidi wa kufanya shughuli yoyote ile iliyo ya maana sana, kama vile kulima, kusafiri, kufanya biashara, au kuwasiliana na wengine. Hata hivyo, kila wakati, sisi pia tunahitaji kutambua kazi ya maana zaidi ambayo ni lazima tuifanye. Kwa maneno mengine, ni lazima tujue vizuri mambo ambayo tunapaswa kutanguliza.

2. Tunajua jinsi gani kwamba Yesu alipokuwa akihubiri, alitambua vizuri kabisa wakati aliokuwa akiishi?

2 Alipokuwa duniani, Yesu alitambua vizuri kabisa alikuwa akiishi wakati gani na kile ambacho alihitaji kufanya. Kwa kuwa alitambua waziwazi mambo aliyohitaji kutanguliza, Yesu alijua kwamba wakati uliongojewa kwa muda mrefu wa kutimizwa kwa unabii mwingi kuhusu Masihi ulikuwa umefika. (1 Pet. 1:11; Ufu. 19:10) Alikuwa na kazi ya kufanya ili kujitambulisha waziwazi kwamba yeye ndiye yule Masihi aliyeahidiwa. Alipaswa kutoa ushahidi kamili kuhusu kweli ya Ufalme na kuwakusanya wale ambao wangekuwa warithi wa wakati ujao pamoja naye katika Ufalme. Na ilikuwa lazima aweke msingi wa kutaniko la Kikristo ambalo lingetimiza kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi mpaka miisho ya dunia.—Marko 1:15.

3. Kutambua wakati aliokuwa akiishi kulimchochea Yesu kutenda jinsi gani?

3 Kutambua jambo hilo kulimchochea Yesu kufanya mapenzi ya Baba yake kwa bidii. Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Kwa kweli, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo mwombeni Bwana wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Luka 10:2; Mal. 4:5, 6) Kati ya wanafunzi wake, Yesu aliwachagua 12 kwanza kisha 70, akawapa maagizo hususa, na akawatuma kuhubiri ujumbe wenye kusisimua: “Ufalme wa mbinguni umekaribia.” Kuhusu Yesu mwenyewe, tunasoma hivi: “Alipokuwa amemaliza kuwapa maagizo wanafunzi wake kumi na wawili, aliondoka akafundishe na kuhubiri katika majiji yao.”—Mt. 10:5-7; 11:1; Luka 10:1.

4. Paulo alimwiga Yesu Kristo katika njia gani?

4 Yesu alikuwa kielelezo kikamilifu cha bidii na ujitoaji kwa wafuasi wake wote. Mtume Paulo alionyesha jambo hilo alipowahimiza hivi waamini wenzake: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Kor. 11:1) Paulo alimwiga Kristo katika njia gani? Kwanza kabisa ni kwa kufanya yote aliyoweza ili kuhubiri habari njema. Katika barua ambazo Paulo aliyaandikia makutaniko, tunapata maneno kama “msiwe wavivu katika kazi zenu,” “mtumikieni Yehova,” “sikuzote mkiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana,” na “lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova.” (Rom. 12:11; 1 Kor. 15:58; Kol. 3:23) Paulo hakusahau kamwe jinsi alivyokutana na Bwana Yesu Kristo alipokuwa njiani kwenda Damasko na maneno ya Yesu ambayo inaelekea mwanafunzi Anania alimwambia: “Mtu huyu ni chombo kilichochaguliwa kwangu ili kupeleka jina langu kwa mataifa na vilevile kwa wafalme na wana wa Israeli.”—Mdo. 9:15; Rom. 1:1, 5; Gal. 1:16.

“Wakati Unaokubalika Hasa”

5. Ni nini kilichomchochea Paulo kutimiza huduma yake kwa bidii?

5 Tunaposoma kitabu cha Matendo, tunaona waziwazi ujasiri na bidii ambayo Paulo alionyesha katika kutimiza huduma yake. (Mdo. 13:9, 10; 17:16, 17; 18:5) Paulo alitambua umuhimu wa kipindi alichoishi. Alisema hivi: “Tazama! Sasa ndio wakati unaokubalika hasa. Tazama! Sasa ndiyo siku ya wokovu.” (2 Kor. 6:2) Mwaka wa 537 K.W.K., ulikuwa wakati uliokubalika kwa wahamishwa Wayahudi huko Babiloni kurudi katika nchi yao. (Isa. 49:8, 9) Lakini katika andiko hilo Paulo alikuwa akizungumza kuhusu nini? Mistari mingine katika andiko hilo inatusaidia kuelewa jambo ambalo alikuwa akifikiria.

6, 7. Ni heshima gani kubwa ambayo Wakristo watiwa-mafuta wamepewa leo, na ni nani wanaofanya kazi pamoja na watiwa-mafuta hao?

6 Mwanzoni mwa barua yake, Paulo alisema kuhusu heshima kubwa ambayo yeye pamoja na Wakristo wenzake watiwa-mafuta walipewa. (Soma 2 Wakorintho 5:18-20.) Alieleza kwamba waliitwa na Mungu kwa ajili ya kusudi hususa, ili kutimiza “huduma ya upatanisho,” kuwaomba watu ‘wapatanishwe pamoja na Mungu.’ Hilo lilimaanisha kuwa tena na urafiki mzuri au kujipatanisha tena na Mungu.

7 Tangu uasi katika bustani ya Edeni, wanadamu wote wametengwa mbali na Yehova. (Rom. 3:10, 23) Hali hiyo ya kutengwa mbali na Mungu imewatumbukiza wanadamu wote kwa ujumla katika giza la kiroho, na hivyo kusababisha mateso na kifo. Paulo aliandika hivi: “Tunajua kwamba uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja mpaka sasa.” (Rom. 8:22) Lakini Mungu amechukua hatua ili kuwahimiza, yaani, ‘kuwaomba,’ watu warudi, au wajipatanishe tena naye. Hiyo ndiyo huduma ambayo Paulo na Wakristo wenzake watiwa-mafuta walikabidhiwa siku hizo. ‘Wakati huo unaokubalika’ unaweza kuthibitika kuwa “siku ya wokovu” kwa wale wanaomwamini Yesu. Wakristo wote watiwa-mafuta na waandamani wao wa “kondoo wengine,” ambao wanafanya kazi pamoja nao, wanaendelea kuwaalika watu wafaidike katika “wakati unaokubalika.”—Yoh. 10:16.

8. Nini kinachofanya mwito wa kujipatanisha na Mungu uwe wa pekee?

8 Kile kinachofanya mwito wa kujipatanisha na Mungu uwe wa pekee zaidi ni kwamba hata ingawa upande mmoja tu ndio uliovunja uhusiano huo—kwa sababu ya uasi wa mwanadamu katika Edeni—Mungu mwenyewe alichukua hatua ya kurekebisha uhusiano huo. (1 Yoh. 4:10, 19) Alifanya nini? Paulo alijibu hivi: “Mungu kupitia Kristo alikuwa akiupatanisha ulimwengu kwake mwenyewe, bila kuwahesabia makosa yao, naye alitukabidhi sisi lile neno la upatanisho.”—2 Kor. 5:19; Isa. 55:6.

9. Paulo alifanya nini ili kuonyesha kwamba alithamini rehema ya Mungu?

9 Kwa kuandaa fidia au dhabihu ya ukombozi, Yehova alifungua njia ili wale wanaoamini waweze kusamehewa makosa yao na kuwa tena na urafiki pamoja naye au kujipatanisha tena naye. Zaidi ya hayo, alituma wajumbe wake kuwahimiza watu kila mahali wafanye amani pamoja naye maadamu wangeweza kufanya hivyo. (Soma 1 Timotheo 2:3-6.) Akielewa mapenzi ya Mungu na kutambua wakati ambao alikuwa akiishi, Paulo alijitoa mwenyewe kwa bidii katika “huduma ya upatanisho.” Mapenzi ya Yehova hayajabadilika. Leo pia bado anawaomba watu wajipatanishe naye. Maneno ya Paulo “sasa ndio wakati unaokubalika hasa” na “sasa ndiyo siku ya wokovu” bado yanatuhusu leo. Yehova ni Mungu mwenye rehema na huruma kama nini!—Kut. 34:6, 7.

‘Usikose Kusudi Lake’

10. “Siku ya wokovu” imemaanisha nini kwa Wakristo watiwa-mafuta, wa wakati uliopita na wa sasa?

10 Watu wa kwanza kufaidika na fadhili hizo zisizostahiliwa ni wale waliokuwa “katika muungano na Kristo.” (2 Kor. 5:17, 18) Kwa watu hao, “siku ya wokovu” ilianza Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Kuanzia wakati huo na kuendelea, watu hao wamekabidhiwa kazi ya kutangaza “neno la upatanisho.” Leo, mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta bado wanaendelea kutimiza “huduma ya upatanisho.” Wanatambua kwamba malaika wanne ambao mtume Yohana aliona katika maono ya kinabii ‘wanazishika sana zile pepo nne za dunia, ili upepo wowote usivume juu ya dunia.’ Kwa hiyo, bado ni “siku ya wokovu” na “wakati unaokubalika hasa.” (Ufu. 7:1-3) Kwa sababu hiyo, tangu mwanzoni mwa karne ya 20, mabaki ya watiwa-mafuta wamekuwa wakijitoa wenyewe kwa bidii kutimiza kazi ya “huduma ya upatanisho” kwenye sehemu za mbali zaidi za dunia.

11, 12. Mwanzoni mwa karne ya 20, Wakristo watiwa-mafuta walionyesha jinsi gani kwamba walitambua umuhimu wa wakati waliokuwa wakiishi? (Ona picha kwenye ukurasa wa 15.)

11 Kwa mfano, kama kinavyosema kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, mwanzoni mwa karne ya 20, “C. T. Russell na washirika wake waliamini kwa nguvu sana kwamba walikuwa katika wakati wa mavuno na kwamba watu walihitaji kusikia kweli zenye kuweka watu huru.” Walifanya nini kuhusu hilo? Wakitambua kwamba walikuwa katika wakati wa mavuno, “wakati unaokubalika hasa,” ndugu hao hawakutosheka tu kuwaalika watu kwenye ibada fulani ya kidini. Tayari makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walikuwa wakifanya hivyo kwa muda mrefu sana. Badala yake, Wakristo hao watiwa-mafuta walianza kutumia njia nyingine zinazofaa za kueneza habari njema. Kati ya njia hizo, walitumia kwa hekima teknolojia ya kisasa ili kuendeleza kazi yao.

12 Ili kueneza habari njema ya Ufalme, kikundi hicho kidogo cha wahudumu wenye bidii kilitumia trakti, vijitabu, magazeti, na vitabu. Pia, walitayarisha hotuba na habari mbalimbali ili zichapishwe katika maelfu ya magazeti ya ulimwengu. Walifanya vipindi vinavyozungumzia Maandiko katika vituo vya redio vya kitaifa na vya kimataifa. Walitayarisha na kutumia sinema yenye picha na sauti, hata kabla ya watengenezaji wa sinema kutengeneza sinema za aina hiyo kwa ajili ya watu wote. Bidii hiyo isiyopungua ilikuwa na matokeo gani? Leo, kuna watu milioni saba hivi ambao wamekubali na kushiriki katika kazi ya kutangaza ujumbe huu: “Mpatanishwe pamoja na Mungu.” Kwa kweli, watumishi hao wa mapema wa Yehova walikuwa vielelezo vizuri vya bidii ingawa walikabili matatizo fulani maishani.

13. Tunapaswa kuchukua kwa uzito kusudi gani la Mungu?

13 Maneno ya Paulo “sasa ndio wakati unaokubalika hasa” bado ni ya kweli. Sisi ambao tumeonja fadhili zisizostahiliwa za Yehova tunashukuru kwamba tumepewa nafasi ya kusikia na kukubali ujumbe wa upatanisho. Badala ya kuhisi kwamba tumetosheka, tunachukua kwa uzito maneno ya Paulo yafuatayo: “Tunawasihi ninyi pia msipokee fadhili zisizostahiliwa za Mungu kisha mkose kusudi lake.” (2 Kor. 6:1) Kusudi la fadhili zisizostahiliwa za Mungu ni ‘kuupatanisha ulimwengu kwake mwenyewe’ kupitia Kristo.—2 Kor. 5:19.

14. Ni nafasi gani zinazojitokeza katika nchi nyingi?

14 Wanadamu wengi, ambao wamepofushwa na Shetani, bado wametengwa mbali na Mungu na hawajui kusudi la fadhili zisizostahiliwa za Mungu. (2 Kor. 4:3, 4; 1 Yoh. 5:19) Hata hivyo, hali za ulimwengu zinazozidi kuwa mbaya zimewafanya watu wengi wakubali ujumbe wetu wanapoonyeshwa kwamba kutengwa mbali na Mungu ndicho chanzo cha maovu na mateso ya wanadamu. Hata katika nchi ambazo watu wengi hawakuwa wakipendezwa na kazi yetu ya kuhubiri, wengi sasa wanakubali habari njema na wanachukua hatua ili kujipatanisha na Mungu. Basi, je, tunaelewa kwamba huu ndio wakati ambao tunapaswa kuwa na bidii zaidi katika kutangaza himizo hili: “Mpatanishwe pamoja na Mungu”?

15. Badala ya kuhubiri ujumbe unaowafurahisha watu, tunataka watu kila mahali wajue nini?

15 Kazi yetu si kuwaambia tu watu kwamba ikiwa watamrudia Mungu, atawasaidia kutatua matatizo yao yote na watajihisi vizuri zaidi. Watu wengi ambao wanaenda kanisani wanatafuta tu jambo hilo, na makanisa yana hamu kubwa ya kutimiza tamaa hiyo. (2 Tim. 4:3, 4) Hilo si kusudi la huduma yetu. Habari njema tunayohubiri ni kwamba Yehova yuko tayari kusamehe makosa kupitia Kristo kwa sababu ya upendo wake. Kwa hiyo, watu ambao walikuwa wametengwa mbali na Mungu wanaweza kuwekwa huru na kupatanishwa tena na Mungu. (Rom. 5:10; 8:32) Hata hivyo, ‘wakati huu unaokubalika hasa,’ unakaribia haraka mwisho wake.

“Wakeni Roho”

16. Ni nini kilichomsaidia Paulo kuwa na bidii na ujasiri?

16 Hivyo basi, tunaweza jinsi gani kusitawisha na kudumisha bidii yetu kwa ajili ya ibada ya kweli? Huenda kiasili wengine ni wenye haya au ni wanyamavu na huenda ikawa vigumu kwao kuonyesha waziwazi hisia zao au kujieleza kwa urahisi. Hata hivyo, ni vizuri kukumbuka kwamba bidii si kuonyesha tu hisia kwa nje au kusisimka; wala haitegemei utu wa mtu. Paulo alionyesha jinsi ya kusitawisha na kudumisha bidii alipowahimiza Wakristo wenzake hivi: “Wakeni roho.” (Rom. 12:11) Roho ya Yehova ilimsaidia sana mtume huyo kuonyesha ujasiri na uvumilivu katika kazi ya kuhubiri. Kuanzia wakati alipoitwa na Yesu mpaka kufikia kifungo chake cha mwisho na kuuawa kwa ajili ya imani huko Roma, yaani, kipindi cha miaka zaidi ya 30, Paulo hakupunguza bidii yake. Sikuzote alimtegemea Mungu, ambaye kupitia roho takatifu alimpa Paulo nguvu alizohitaji. Paulo alisema hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” (Flp. 4:13) Tunaweza kufaidika kama nini tukijifunza kutokana na mfano wake!

17. Tunaweza ‘kuwaka roho’ jinsi gani?

17 Neno linalotafsiriwa ‘kuwaka’ linamaanisha hasa “kuchemka.” (Kingdom Interlinear) Ili birika la maji liendelee kuchemka, ni lazima moto uendelee kuwaka. Vivyo hivyo, ili ‘kuwaka roho,’ tunahitaji mtiririko unaoendelea daima wa roho ya Mungu. Njia ya kupata roho hiyo ni kutumia maandalizi yote ambayo Yehova anatoa ili kututia nguvu kiroho. Hilo linamaanisha kuchukua kwa uzito ibada yetu ya familia na ya kutaniko, yaani, kufanya kwa ukawaida funzo la kibinafsi na la familia, kusali kwa ukawaida, na kukutana kwa ukawaida na Wakristo wenzetu. Hilo litatusaidia kuwa na “moto” ambao utaendelea “kutuchemsha” na hivyo tutaendelea ‘kuwaka roho.’—Soma Matendo 4:20; 18:25.

18. Tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu, tunapaswa kukazia fikira kusudi gani?

18 Mtu aliyejiweka wakfu ni yule ambaye anakazia kabisa fikira kusudi moja na hakengeushwi kwa urahisi au kuvunjika moyo na kuacha kufuatia kusudi hilo. Tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu, kusudi letu ni kufanya jambo lolote ambalo Yehova anataka tufanye, kama alivyofanya Yesu. (Ebr. 10:7) Mapenzi ya Yehova leo ni kwamba watu wengi iwezekanavyo wajipatanishe naye. Kwa hiyo, acheni tumwige Yesu na Paulo kwa kuwa wenye bidii katika kazi hii ya maana sana na ya haraka inayopaswa kufanywa leo.

Je, Unakumbuka?

• Ni nini iliyokuwa “huduma ya upatanisho” ambayo Paulo na Wakristo wengine watiwa-mafuta walikabidhiwa?

• Mabaki ya watiwa-mafuta wameutumia vizuri jinsi gani “wakati unaokubalika hasa”?

• Wahudumu Wakristo wanaweza jinsi gani ‘kuwaka roho’?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Paulo hakusahau kamwe jinsi alivyokutana na Bwana Yesu Kristo