Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwimbieni Yehova!

Mwimbieni Yehova!

Mwimbieni Yehova!

“Nitampigia Mungu wangu muziki maadamu nipo.”—ZAB. 146:2.

1. Ni nini kilichomchochea kijana Daudi kutunga zaburi fulani?

DAUDI alipokuwa kijana alitumia saa nyingi sana katika maeneo yaliyokuwa karibu na Bethlehemu akichunga makundi ya baba yake. Alipokuwa akichunga kondoo, Daudi angeweza kuona kazi za ajabu za Yehova za uumbaji, kama vile mbingu zenye nyota, “wanyama wa porini,” na “ndege wa mbinguni.” Aliguswa moyo sana na mambo aliyoona hivi kwamba alichochewa kutunga nyimbo zinazogusa moyo za kumsifu Muumba wa vitu hivyo vizuri ajabu. Nyimbo nyingi ambazo Daudi alitunga zinapatikana katika kitabu cha Zaburi. *Soma Zaburi 8:3, 4, 7-9.

2. (a) Muziki unaweza kuwa na matokeo gani kwa mtu? Toa mfano. (b) Tunaweza kujifunza nini kuhusu uhusiano wa Daudi pamoja na Yehova kutokana na Zaburi 34:7, 8 na Zaburi 139:2-8?

2 Inaelekea kwamba Daudi aliboresha ustadi wake akiwa mwanamuziki katika kipindi hicho cha maisha yake. Kwa kweli, baada ya muda alikuwa mwanamuziki stadi sana hivi kwamba alialikwa ili ampigie kinubi Mfalme Sauli. (Met. 22:29) Muziki wa Daudi ulimtuliza mfalme huyo aliyekuwa akiteseka moyoni, kama vile ambavyo mara nyingi muziki mzuri unawatuliza watu hata leo. Kila mara Daudi alipoanza kupiga kinubi chake, ‘Sauli alipata faraja na mambo yakamwendea vema.’ (1 Sam. 16:23) Nyimbo ambazo zilitungwa na mwanamuziki na mtungaji huyo wa nyimbo aliyemwogopa Mungu zimekuwa na faida mpaka leo. Hebu fikiria jambo hili! Leo, miaka zaidi ya 3,000 baada ya Daudi kuzaliwa, mamilioni ya watu wenye hali mbalimbali wanaoishi katika sehemu zote za dunia wanasoma kwa ukawaida zaburi za Daudi ili wapate faraja na tumaini.—2 Nya. 7:6; soma Zaburi 34:7, 8; 139:2-8; Amo. 6:5.

Muziki Unatimiza Sehemu ya Maana Katika Ibada ya Kweli

3, 4. Katika siku za Daudi, ni mipango gani iliyofanywa ya kuimba muziki mtakatifu?

3 Daudi alikuwa na kipawa, na alitumia kipawa chake kwa njia bora zaidi iwezekanavyo, yaani, kumtukuza Yehova. Baada ya kuwekwa kuwa mfalme wa Israeli, Daudi alipanga ili utumishi wa maskani utie ndani muziki mtamu. Zaidi ya asilimia kumi ya Walawi wote waliotumika katika maskani, yaani, Walawi 4,000, walipewa mgawo wa “kutoa sifa,” na 288 ‘walizoezwa nyimbo kwa Yehova, wote wakiwa wajuzi.’—1 Nya. 23:3, 5; 25:7.

4 Daudi mwenyewe alitunga nyimbo nyingi kati ya zile ambazo Walawi waliimba. Ni wazi kwamba Waisraeli wote ambao walipata pendeleo la kuwapo wakati zaburi za Daudi zilipoimbwa waliguswa moyo sana na nyimbo walizosikia. Baadaye, sanduku la agano lilipoletwa Yerusalemu, ‘Daudi aliwaambia wakuu wa Walawi wawaweke ndugu zao waimbaji wakiwa na vyombo vya nyimbo, vinanda na vinubi na matoazi, wakipiga kwa sauti ili sauti ya kushangilia itokee.’—1 Nya. 15:16.

5, 6. (a) Kwa nini muziki ulikaziwa sana uangalifu wakati wa utawala wa Daudi? (b) Tunajua jinsi gani kwamba katika Israeli la kale muziki ulionwa kuwa wa maana katika ibada?

5 Kwa nini muziki ulikaziwa sana uangalifu katika siku za Daudi? Je, ni kwa sababu tu mfalme alikuwa mwanamuziki? Hapana, kulikuwa na sababu nyingine ambayo ilifunuliwa karne nyingi baadaye wakati Mfalme Hezekia aliyekuwa mwadilifu alipoanzisha tena utumishi katika hekalu. Tunasoma hivi katika andiko la 2 Mambo ya Nyakati 29:25: “Akawaweka [yaani, Hezekia] Walawi katika nyumba ya Yehova, wakiwa na matoazi, na vinanda na vinubi, kulingana na amri ya Daudi na ya Gadi mwonaji wa mfalme na ya nabii Nathani, kwa maana amri hiyo ilikuwa kulingana na mkono wa Yehova kupitia manabii wake.”

6 Ndiyo, kupitia manabii wake, Yehova aliwaagiza waabudu wake wamsifu kwa nyimbo. Pia, waimbaji kutoka katika kabila la kikuhani hawakupewa migawo ambayo Walawi wengine walitakiwa wafanye ili wawe na wakati wa kutosha wa kutunga nyimbo na inaelekea sana, ili pia wafanye mazoezi.—1 Nya. 9:33.

7, 8. Ni jambo gani ambalo ni la maana zaidi kuliko ustadi inapohusu kuimba nyimbo zetu za Ufalme?

7 Huenda ukasema, “Inapohusu muziki, bila shaka siwezi kuhesabiwa kuwa kati ya waimbaji stadi ambao waliimba katika maskani!” Lakini si wanamuziki wote Walawi waliokuwa waimbaji stadi. Kulingana na andiko la 1 Mambo ya Nyakati 25:8, kulikuwa pia na ‘wenye kujifunza.’ Pia, ni vizuri kukumbuka kwamba huenda kulikuwa na wanamuziki na waimbaji fulani ambao walikuwa stadi sana kutoka katika makabila mengine ya Israeli, lakini Yehova aliwapa Walawi mgawo wa kushughulikia muziki. Tunaweza kuwa na hakika kwamba iwe walikuwa ‘wajuzi,’ yaani, waimbaji stadi, au ‘wenye kujifunza,’ Walawi wote waaminifu walitimiza kazi hiyo kwa moyo wote.

8 Daudi alipenda muziki naye alikuwa mwanamuziki stadi. Lakini je, Mungu anapendezwa tu na kipawa au uwezo wetu? Daudi aliandika hivi kwenye Zaburi 33:3: “Fanyeni yote mnayoweza katika kumpigia vinanda pamoja na vigelegele vya shangwe.” Ujumbe uko wazi: Jambo la maana ni ‘kufanya yote tunayoweza’ katika kumsifu Yehova.

Sehemu Ambayo Muziki Ulitimiza Baada ya Siku za Daudi

9. Eleza mambo ambayo huenda ungeona na kusikia ikiwa ungehudhuria sherehe ya kuzindua hekalu wakati wa utawala wa Sulemani.

9 Wakati wa utawala wa Sulemani, muziki ulitimiza sehemu ya maana katika ibada safi. Wakati wa kuzinduliwa kwa hekalu, kulikuwa na kikundi kamili cha kupiga muziki, na kilitia ndani watu 120 waliopiga tarumbeta. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 5:12.) Biblia inatuambia kwamba ‘wapiga-tarumbeta [ambao wote walikuwa makuhani] na waimbaji walikuwa kama mtu mmoja kwa kutokeza sauti moja isikike katika kumsifu na kumshukuru Yehova, “kwa maana yeye ni mwema, kwa maana fadhili zake zenye upendo ni za mpaka wakati usio na kipimo.”’ Mara tu baada ya kupaaza sauti hiyo ya shangwe, “nyumba ile ikajaa wingu,” kuonyesha kwamba Yehova aliikubali. Ilisisimua na kustaajabisha kama nini kusikia sauti za tarumbeta hizo zote pamoja na maelfu ya waimbaji wakiimba kwa upatano kama mtu mmoja!—2 Nya. 5:13.

10, 11. Ni nini kinachoonyesha kwamba Wakristo wa mapema walitumia muziki katika ibada?

10 Wakristo wa mapema walitumia pia muziki katika ibada. Bila shaka, waabudu wa karne ya kwanza hawakukutana katika maskani au katika mahekalu, bali katika nyumba za watu. Mara nyingi walikutana chini ya hali ngumu kwa sababu ya mateso na mambo mengine. Hata hivyo, Wakristo hao walimsifu Mungu kwa nyimbo.

11 Mtume Paulo aliwahimiza hivi ndugu zake Wakristo huko Kolosai: “Endeleeni . . . kuonyana kwa zaburi, sifa kwa Mungu, nyimbo za kiroho kwa neema.” (Kol. 3:16) Baada ya Paulo na Sila kutupwa gerezani, walianza ‘kusali na kumsifu Mungu kwa wimbo,’ ingawa hawakuwa na kitabu cha nyimbo. (Mdo. 16:25) Ikiwa ungetupwa gerezani, ungeweza kukumbuka na kuimba nyimbo zetu ngapi za Ufalme?

12. Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunathamini nyimbo zetu za Ufalme?

12 Kwa kuwa muziki unatimiza sehemu ya maana sana katika ibada yetu, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninaonyesha uthamini unaofaa kwa muziki huo? Je, ninajitahidi kabisa kufika katika mikutano na makusanyiko kwa wakati ili nijiunge na ndugu na dada zangu katika kuimba wimbo wa kwanza, na je, ninaimba kwa sauti na hisia? Je, ninawasaidia watoto wangu kuona kwamba wimbo unaoimbwa kati ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi au kati ya hotuba ya watu wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi si wakati wa mapumziko au wakati wa kutoka nje bila sababu, labda ili tu kunyoosha miguu yao?’ Kuimba ni sehemu ya ibada yetu. Ndiyo, sisi sote tunaweza kuunganisha sauti zetu na kumsifu Yehova, iwe sisi ni ‘wajuzi’ au ‘wenye kujifunza.’—Linganisha na 2 Wakorintho 8:12.

Nyakati Zinabadilika, Mahitaji Yanabadilika

13, 14. Kuna faida gani ya kuimba kwa moyo wote katika mikutano ya kutaniko? Toa mfano.

13 Miaka zaidi ya 100 iliyopita, gazeti Zion’s Watch Tower lilieleza moja ya sababu zinazofanya nyimbo zetu za Ufalme ziwe za maana sana. Lilisema hivi: “Kuimba kuhusu kweli ni njia nzuri ya kuifanya itie mizizi katika akili na mioyo ya watu wa Mungu.” Maneno mengi ya nyimbo zetu yanategemea Maandiko, kwa hiyo, kujifunza maneno ya nyimbo fulani ni njia bora ya kukazia kabisa kweli hiyo ndani ya mioyo yetu. Mara nyingi, watu wanaohudhuria kwa mara ya kwanza mikutano yetu wanaguswa moyo sana wanaposikia kutaniko likiimba kutoka moyoni.

14 Jioni moja mwaka wa 1869, C. T. Russell alikuwa akirudi nyumbani kutoka kazini aliposikia watu wakiimba katika jumba fulani lililokuwa chini ya ardhi. Wakati huo katika maisha yake, alikuwa amekata tamaa kwamba hangepata kamwe kweli kumhusu Mungu. Hivyo, alikuwa ameamua kujiingiza kabisa katika mambo yake ya kibiashara, huku akijiambia kwamba ikiwa angepata pesa, angeweza kuwatimizia watu mahitaji yao ya kimwili hata kama hangeweza kuwasaidia kiroho. Ndugu Russell aliingia ndani ya jumba hilo chafuchafu lenye mavumbi na kugundua kwamba ibada ya kidini ilikuwa ikifanyiwa humo. Aliketi na kusikiliza. Baadaye aliandika kwamba mambo aliyosikia usiku huo, “kwa mwongozo wa Mungu, yalitosha kutia nguvu tena imani [yake] iliyokuwa ikiyumbayumba kuhusu uhakika wa kwamba Biblia iliandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu.” Ona kwamba mwanzoni Ndugu Russell alivutiwa kuingia katika mkutano huo aliposikia watu wakiimba.

15. Ni marekebisho gani katika uelewaji ambayo yalitokeza uhitaji wa kuandika upya kitabu cha nyimbo?

15 Kadiri wakati unavyopita, uelewaji wetu wa Maandiko unazidi kuboreshwa. Andiko la Methali 4:18 linasema hivi: “Njia ya waadilifu ni kama nuru inayong’aa, inayozidi kuongezeka mpaka mchana mkamilifu.” Bila shaka, nuru inayoongezeka inatokeza marekebisho katika njia ‘tunayoimba kuhusu ile kweli.’ Katika muda wa miaka 25 ambayo imepita, Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingi wamefurahia kutumia kitabu cha nyimbo chenye kichwa Mwimbieni Yehova Sifa. * Katika miaka iliyofuata tangu kitabu hicho kilipochapishwa kwa mara ya kwanza, nuru imekuwa ikiongezeka kuhusu mambo mbalimbali, na maneno fulani ambayo yalitumiwa katika kitabu hicho cha nyimbo hayatumiki tena. Kwa mfano, siku hizi hatusemi “taratibu mpya” badala yake tunasema “ulimwengu mpya.” Na sasa tunasema kwamba jina la Yehova “litatakaswa,” bali si “kutetewa.” Ni wazi kwamba kumekuwa na uhitaji wa kurekebisha kitabu chetu cha nyimbo kwa sababu ya mafundisho.

16. Kitabu chetu kipya cha nyimbo kitatusaidia jinsi gani kufuata shauri la Paulo katika Waefeso 5:19?

16 Kwa sababu hiyo na sababu nyinginezo, Baraza Linaloongoza lilikubali kitabu kipya cha nyimbo chenye kichwa Mwimbieni Yehova kichapishwe. Idadi ya nyimbo katika kitabu chetu kipya imepunguzwa kufikia 135. Kwa kuwa kuna nyimbo chache zaidi za kujifunza, tunaweza kushika akilini maneno ya nyimbo fulani mpya. Hilo linapatana na shauri la Paulo katika Waefeso 5:19.—Soma.

Unaweza Kuonyesha Uthamini Wako

17. Ni mawazo gani yanayoweza kutusaidia tusiogope kuaibika wakati kutaniko linapoimba?

17 Je, tunapaswa kuogopa kuimba kwa sauti katika mikutano ya Kikristo kwa sababu tunaogopa kuaibika? Fikiria jambo hilo kwa njia hii: Je, si ni kweli kwamba “sisi sote hujikwaa mara nyingi” tunapozungumza? (Yak. 3:2) Hata hivyo, hatuogopi kumsifu Yehova nyumba kwa nyumba eti kwa sababu maneno yetu si makamilifu. Basi kwa nini, tuogope kumsifu Mungu kwa nyimbo kwa sababu sauti zetu si kamilifu? Yehova, “aliyekifanya kinywa kwa ajili ya mwanadamu,” anafurahi kusikiliza tunapotumia sauti zetu kuimba sifa zake.—Kut. 4:11.

18. Toa mapendekezo yanayoweza kutusaidia kujifunza maneno ya nyimbo zetu.

18 CD zenye kichwa Mwimbieni Yehova—Muziki wa Kuimbwa zimetayarishwa katika lugha mbalimbali. CD hizo zina nyimbo mpya ambazo zimeimbwa kwa vyombo vya muziki na pia kikundi cha waimbaji. Kusikiliza muziki huo kunafurahisha sana. Sikiliza muziki huo mara nyingi; ukifanya hivyo utajifunza haraka maneno ya nyimbo chache mpya. Nyingi kati ya nyimbo hizo zina maneno ambayo yametungwa kwa njia ya kwamba unapoimba mstari mmoja, inakuwa rahisi zaidi kuimba mstari unaofuata. Basi unaposikiliza CD hizo, kwa nini usijaribu kuimba ukifuatana na waimbaji? Ukielewa vizuri maneno na muziki huo nyumbani, bila shaka utaweza kuimba kwa uhakika zaidi kwenye Jumba la Ufalme.

19. Ni hatua gani zinazohusika katika kutayarisha nyimbo zetu za Ufalme zinazopigwa kwa vyombo vya muziki?

19 Ni rahisi kupuuza muziki tunaofurahia katika makusanyiko yetu ya pekee, makusanyiko ya mzunguko, na makusanyiko ya wilaya. Kazi nyingi inahusika katika kutayarisha muziki huo. Baada ya muziki kuchaguliwa, ni lazima mpangilio utakaofuatwa na kikundi cha wanamuziki uandikwe kwa uangalifu ili muziki huo upigwe na kikundi hicho cha Watchtower chenye washiriki 64. Kisha, wanamuziki hao wanatumia saa nyingi sana wakijifunza muziki huo ili waweze kufanya mazoezi na mwishowe kurekodi muziki huo katika studio zetu huko Patterson, New York. Kumi kati ya ndugu na dada hao hawaishi nchini Marekani. Wote wanaona kwamba ni pendeleo kushiriki katika kutayarisha muziki mtamu kwa ajili ya mikutano na makusanyiko yetu. Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini jitihada zao za upendo. Mwenyekiti katika makusanyiko yetu anapotuomba tuketi, acheni tuketi bila kuchelewa na kusikiliza kwa makini muziki ambao umetayarishwa kwa upendo sana.

20. Umeazimia kufanya nini?

20 Yehova anakazia uangalifu nyimbo zetu za sifa. Ni za maana kwake. Tunaweza kuufanya moyo wake ushangilie kwa kuimba kwa sauti na kwa moyo wetu wote kila mara tunapokutana ili kuabudu. Ndiyo, iwe sisi ni waimbaji stadi au wenye kujifunza, acheni ‘tumwimbie Yehova’!—Zab. 104:33.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Inapendeza kwamba karne kumi baada ya kifo cha Daudi, kundi kubwa la malaika liliwatangazia wachungaji kuzaliwa kwa Masihi. Wachungaji hao walikuwa wakichunga makundi yao katika maeneo yaliyo karibu na Bethlehemu.—Luka 2:4, 8, 13, 14.

^ fu. 15 Nyimbo zote 225 zilikuwa zimetafsiriwa katika lugha zaidi ya 100.

Ungesema Nini?

• Ni mifano gani katika nyakati za Biblia inayoonyesha kwamba muziki unatimiza sehemu ya maana katika ibada yetu?

• Kuna uhusiano gani kati ya kutii amri ya Yesu kwenye Mathayo 22:37 na kushiriki kwa moyo wote katika kuimba nyimbo za Ufalme?

• Taja njia fulani za kuonyesha kwamba tunathamini ifaavyo nyimbo zetu za Ufalme.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Je, unawazuia watoto wako wasitoke nje bila sababu wakati wa wimbo?

[Picha katika ukurasa wa 24]

Je, mnajifunza maneno ya nyimbo zetu mpya nyumbani?