Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Katika andiko la Mwanzo 6:3 tunasoma hivi: “Roho yangu haitavumiliana sikuzote na mwanadamu kwa kuwa yeye pia ni mwili. kwa hiyo siku zake zitakuwa miaka 120.” Je, Yehova alikuwa akiweka mpaka ili maisha ya wanadamu yawe tu na urefu wa miaka 120, na je, Noa alihubiri kwa muda huo kuhusu Gharika iliyokuwa ikija?

Jibu kwa sehemu zote mbili za swali hilo ni hapana.

Kabla ya Gharika, wanadamu wengi waliishi kwa karne nyingi. Noa alikuwa na umri wa miaka 600 Gharika ilipokuja, naye aliishi kwa miaka 950. (Mwa. 7:6; 9:29) Watu fulani waliozaliwa baada ya Gharika waliishi pia kwa miaka zaidi ya 120, Arpakshadi alikufa akiwa na miaka 438 naye Shela miaka 433. (Mwa. 11:10-15) Hata hivyo, kufikia siku za Musa, urefu wa maisha ya kawaida ulipungua kufikia miaka 70 au 80. (Zab. 90:10) Kwa hiyo, andiko la Mwanzo 6:3 halikuwa likiweka mpaka ili maisha ya kawaida ya wanadamu yawe yenye urefu wa miaka 120 tu.

Basi, je, maneno ya mstari huo ni maneno ambayo Mungu alimwambia Noa ili awaonye wengine kuhusu uharibifu ambao ungekuja baada ya miaka 120? Hapana. Mungu alizungumza na Noa mara kwa mara. Tunasoma hivi katika mstari wa 13 wa simulizi hilo: “Mungu akamwambia Noa: ‘Mwisho wa wote wenye mwili umekuja mbele zangu, kwa maana dunia imejaa jeuri.’” Katika miaka iliyofuata, Noa alimaliza kazi kubwa ya kujenga safina, na wakati huo: “Yehova akamwambia Noa: ‘Ingia ndani ya safina, wewe pamoja na nyumba yako yote.’” (Mwa. 6:13; 7:1) Na kuna pindi nyingine ambazo Yehova alimjulisha Noa mambo fulani ya hakika.—Mwa. 8:15; 9:1, 8, 17.

Hata hivyo, andiko la Mwanzo 6:3 lina wazo tofauti; halitaji Noa, wala halisemi kwamba Mungu alikuwa akizungumza naye. Maneno hayo yanaweza kuonwa kuwa maneno rahisi yaliyoonyesha azimio au kusudi la Mungu. (Linganisha Mwanzo 8:21.) Ni muhimu kukumbuka kwamba katika rekodi ya historia kuhusu mambo yaliyotukia kabla ya Adamu kuwapo, tunapata maneno kama haya: “Mungu akaendelea kusema.” (Mwa. 1:6, 9, 14, 20, 24) Bila shaka, Yehova hakuwa akizungumza na mwanadamu fulani duniani, kwa kuwa mwanadamu hakuwa ameumbwa.

Kwa hiyo, ni jambo la akili kukata kauli kwamba andiko la Mwanzo 6:3 linaonyesha azimio la Mungu la kukomesha mfumo huo mwovu wa mambo duniani. Yehova alitoa tangazo la hukumu la kwamba angefanya hivyo baada ya miaka 120, ingawa Noa hakuwa amejua hilo. Lakini kwa nini aliweka wakati wa kufanya hivyo? Kwa nini alingoja?

Mtume Petro anaeleza sababu: “Subira ya Mungu ilipokuwa ikingoja katika siku za Noa, safina ilipokuwa ikijengwa, ambayo ndani yake watu wachache, yaani, nafsi nane, walichukuliwa salama kupitia maji.” (1 Pet. 3:20) Ndiyo, Mungu alipoazimia kuhusu miaka 120, kuna mambo ambayo bado yalihitaji kufanywa. Miaka 20 hivi baadaye, Noa na mke wake wakaanza kupata watoto. (Mwa. 5:32; 7:6) Wana wao watatu walikua na baadaye wakaoa, na hivyo familia ikaongezeka kufikia “nafsi nane.” Kisha, walipaswa kujenga safina, kazi ambayo haikuwa rahisi tukifikiria ukubwa wa safina na ukubwa wa familia ya Noa. Ndiyo, subira ya Mungu kwa miaka 120 iliruhusu mambo hayo yatimizwe na kuandaa njia ya kuokoa uhai, na kuwawezesha wanadamu wanane waaminifu ‘wachukuliwe salama kupitia maji.’

Biblia haitaji waziwazi mwaka ambao Yehova alimjulisha Noa kwamba Gharika ingekuja. Kwa kuwa wana wa Noa walikuwa wamezaliwa, wakakua, na kuoa, labda miaka 40 au 50 ilibaki kabla ya Gharika. Kisha Yehova akamwambia Noa hivi: “Mwisho wa wote wenye mwili umekuja mbele zangu.” Alisema pia kwamba Noa alipaswa kujenga safina kubwa na kuingia ndani yake pamoja na familia yake. (Mwa. 6:13-18) Katika makumi ya miaka iliyobaki, Noa alifanya mengi zaidi ya kuweka mfano wa uadilifu kupitia maisha yake. Alitumika akiwa “mhubiri wa uadilifu” ambaye alipaswa kutangaza ujumbe wa moja kwa moja wa onyo—Mungu alikuwa ameazimia kuwaharibu watu ambao hawakuwa wakimwogopa wakati huo. Noa hakujua mapema uharibifu huo ungekuja mwaka gani, lakini bila shaka alijua kwamba ungekuja. Na bila shaka unajua kwamba ulikuja.—2 Pet. 2:5.