Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Edeni—Je, Ndio Makao ya Kwanza ya Mwanadamu?

Edeni—Je, Ndio Makao ya Kwanza ya Mwanadamu?

Edeni—Je, Ndio Makao ya Kwanza ya Mwanadamu?

WAZIA ukiwa katika bustani. Hakuna pilikapilika nyingi wala kelele nyingi kama inavyokuwa mijini. Bustani hii ni kubwa, na hakuna kitu kinachotatiza amani humo. Zaidi ya hayo, huna wasiwasi na husumbuliwi na magonjwa, mizio, wala maumivu yoyote. Hisi zako zinafanya kazi na unafurahia mazingira.

Kwanza, macho yako yanaona maua ya rangi mbalimbali, kisha kijito chenye maji yanayometameta, na nyasi na mimea mingi ya kijani kibichi inayopigwa na jua. Unahisi upepo mwororo ukipiga ngozi yako na harufu nzuri ya maua. Unasikia sauti ya majani yanayotikiswa na upepo, sauti ya maji yanayotiririka juu ya mawe, ndege wakiimba kwa sauti zenye kupendeza, na sauti za wadudu wakifanya kazi yao. Unapotafakari kuhusu mandhari hiyo, je, hutamani kuwa mahali kama hapo?

Wanadamu ulimwenguni pote wanaamini kuwa binadamu wa kwanza waliishi katika mazingira kama hayo. Kwa karne nyingi, washiriki wa dini ya Kiyahudi, jumuiya ya Wakristo, na Waislamu wamefundishwa kuhusu bustani ya Edeni, mahali ambapo Mungu aliwaweka Adamu na Hawa. Kulingana na Biblia, walifurahia maisha yenye amani. Walikuwa na amani kati yao wenyewe, pamoja na wanyama, na pamoja na Mungu, ambaye kwa fadhili aliwapa tumaini la kuishi milele katika mazingira hayo yenye kupendeza.—Mwanzo 2:15-24.

Wahindi pia wana maoni fulani kuhusu paradiso ya nyakati za kale. Wabudha wanaamini kuwa viongozi wao wakuu wa kiroho watafufuka wakati ambapo ulimwengu utakuwa kama paradiso. Nazo dini nyingi za Kiafrika zina hadithi zinazofanana sana na ile hadithi kuhusu Adamu na Hawa.

Bila shaka, wazo hilo la paradiso linapatikana katika dini na mapokeo mengi ya wanadamu. Mwandishi mmoja alitaja hivi: “Jamii nyingi zinaamini kwamba kulikuwa na paradiso mapema katika historia ya mwanadamu. Paradiso hiyo ilikuwa na wanadamu wakamilifu, yenye uhuru, amani, furaha, vitu vingi, na isiyokuwa na mkazo wala ugomvi. . . . Imani hiyo ilifanya watu kwa ujumla watamani sana paradiso iliyopotea na hivyo kutafuta mbinu ya kuipata tena.”

Je, inawezekana kuwa hadithi na mapokeo hayo yalikuwa na chanzo kimoja? Je, inawezekana kwamba mawazo ya “watu kwa ujumla” yameathiriwa na tukio fulani halisi? Je, kweli miaka mingi iliyopita kulikuwa na bustani ya Edeni, na je, Adamu na Hawa walikuwa watu halisi?

Watu wanaochambua Biblia wanapinga jambo hilo. Katika kizazi hiki cha kisayansi, watu wengi wanaamini kuwa masimulizi hayo ni hadithi tu. Kwa kushangaza, hata watu fulani wa dini wana maoni kama hayo. Viongozi wengi wa dini wanaendeleza imani hiyo ya kutokuwapo kwa bustani ya Edeni. Wanasema kuwa hakujawahi kuwa na mahali kama hapo na kwamba simulizi hilo ni sitiari, hadithi, hekaya, au mfano tu.

Bila shaka, Biblia ina mifano mbalimbali. Yesu mwenyewe alitoa mifano ambayo ni maarufu sana. Hata hivyo, Biblia inataja simulizi la Edeni, si kama mfano, bali kama historia, iliyo wazi na rahisi kueleweka. Lakini, ikiwa mambo yanayotajwa hayakutukia, je, Biblia nzima inaweza kutumainiwa? Acheni tuchunguze kwa nini watu fulani wana shaka kuhusu bustani ya Edeni na ikiwa wana sababu nzuri za kuwa na shaka. Kisha, tutachunguza kwa nini simulizi hili ni muhimu kwa kila mmoja wetu.