Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Kulikuwa na Bustani ya Edeni?

Je, Kweli Kulikuwa na Bustani ya Edeni?

Je, Kweli Kulikuwa na Bustani ya Edeni?

JE, UNAJUA ile hadithi kuhusu Adamu na Hawa na bustani ya Edeni? Watu wengi ulimwenguni wanaijua. Tunakutia moyo uisome hadithi hiyo. Utaipata katika andiko la Mwanzo 1:26–3:24. Huu ndio muhtasari wa hadithi hiyo:

Yehova Mungu * anamuumba mwanadamu kutokana na mavumbi na kumwita Adamu, kisha anamweka katika bustani iliyo katika eneo linaloitwa Edeni. Mungu mwenyewe ndiye mpandaji wa bustani hii. Imetunzwa vizuri, na ina miti mingi yenye kupendeza inayozaa matunda. Katikati ya bustani hii kuna “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” Mungu anawakataza wanadamu wasile matunda ya mti huo, akisema kuwa wasipotii watapatwa na kifo. Baada ya muda, Yehova anamuumba Hawa, msaidizi wa Adamu, kutokana na ubavu mmoja wa Adamu. Mungu anawapa kazi ya kutunza butani na kuwaambia wazaane na kuijaza dunia.

Hawa anapokuwa peke yake, nyoka anaongea naye, akimshawishi ale matunda aliyokatazwa akidai kuwa Mungu amemdanganya na anamnyima kitu fulani kizuri, kitakachomfanya awe kama Mungu. Anashawishika na kula matunda ya mti huo. Baadaye, Adamu anajiunga naye kutomtii Mungu. Yehova anachukua hatua na kutangaza hukumu juu ya Adamu, Hawa, na nyoka. Baada ya wanadamu kufukuzwa kutoka katika bustani hiyo ya kiparadiso, malaika wanailinda njia ya kuingia humo.

Wakati fulani lilikuwa jambo la kawaida kwa wasomi, watu wenye akili, na wanahistoria kukubali kuwa matukio katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo ni ya kweli na yalitukia. Siku hizi, watu wengi wanatilia shaka mambo hayo. Lakini wana sababu gani za kutilia shaka simulizi la Mwanzo kuhusu Adamu, Hawa, na bustani ya Edeni? Acheni tuchunguze sababu nne kuu.

1. Je, bustani ya Edeni ilikuwa mahali halisi?

Kwa nini watu wana shaka kuhusu jambo hilo? Huenda falsafa ilichangia kuwapo kwa shaka hizo. Kwa karne nyingi, wanatheolojia walikuwa wakifikiria kuwa bustani ya Mungu bado ilikuwa mahali fulani. Hata hivyo, kanisa liliathiriwa na wanafalsafa Wagiriki kama Plato na Aristotle, walioamini kuwa hakuna kitu kikamilifu duniani. Ukamilifu ungeweza kupatikana mbinguni pekee. Kwa hiyo, wanatheolojia wakakata kauli kuwa lazima Paradiso ya kwanza iwe ilikuwa karibu na mbinguni. * Wengine walisema kuwa bustani hiyo ilikuwa juu ya mlima mrefu sana hivi kwamba haingeweza kuathiriwa na dunia iliyopotoka; wengine walisema ilikuwa katika Ncha ya Kaskazini au Ncha ya Kusini; nao wengine walisema ilikuwa karibu na au juu ya mwezi. Haishangazi kuwa simulizi kuhusu bustani ya Edeni lilianza kuonekana kama jambo la kuwaziwa tu. Wasomi fulani wa kisasa wanasema kuwa habari kuhusu mahali ambapo Edeni ilikuwa ni upuuzi mtupu, wakisisitiza kuwa hakujawahi kuwapo na mahali kama hapo.

Hata hivyo, Biblia haielezi kuhusu bustani ya Edeni kwa njia hiyo. Katika Mwanzo 2:8-14, tunajifunza mambo kadhaa kuhusu eneo hilo. Bustani hiyo ilikuwa mashariki ya eneo linaloitwa Edeni. Maji katika bustani hiyo yalitoka katika mto ambao ulikuwa chanzo cha mito minne. Majina ya mito hiyo yote minne yanatajwa na pia maelezo mafupi kuhusu mahali ilikoelekea. Wasomi wengi wametamani sana kujua habari kuhusu eneo la Edeni, hivyo wengi wao wametumia sehemu hii ya Biblia kujaribu kutafuta eneo hilo la kale liko mahali gani. Hata hivyo, wasomi hao wametoa maoni mengi tofauti-tofauti kuhusu eneo hilo. Je, hilo linamaanisha kuwa maelezo halisi kuhusu eneo la Edeni, bustani hiyo, na mito yake ni uwongo au ni hadithi tu?

Wazia: Matukio ya simulizi la bustani ya Edeni yaliyotokea miaka 6,000 hivi iliyopita. Musa ndiye aliyeandika simulizi hilo, na huenda alitumia masimulizi yaliyopitishwa kwa mdomo au hata maandishi fulani yaliyokuwapo wakati huo. Hata hivyo, Musa aliandika simulizi hilo miaka 2,500 hivi baada ya matukio hayo. Tayari matukio katika Edeni yalikuwa historia ya kale. Je, baada ya karne nyingi kupita, huenda alama hizo kuu kama mito imebadili mikondo yake? Uso wa dunia unabadilika kila mara. Eneo ambapo bustani ya Edeni ilikuwa linaathiriwa sana na matetemeko ya ardhi—asilimia 17 ya matetemeko yote duniani, yanatukia katika eneo hilo. Katika maeneo kama hayo, mabadiliko katika uso wa dunia ni jambo la kawaida. Zaidi ya hayo, huenda Gharika ya siku za Noa ilibadili uso wa eneo hilo katika njia ambazo hatuwezi kuzielewa leo. *

Hata hivyo, kuna mambo machache ya hakika tunayojua: Simulizi la kitabu cha Mwanzo linataja kuwa bustani ya Edeni ilikuwa mahali halisi. Mito miwili kati ya mito minne inayotajwa katika simulizi hilo—Efrati na Tigri, au Hidekeli—bado ipo hadi leo, na baadhi ya vyanzo vyake viko karibu-karibu. Simulizi hilo linataja majina ya maeneo ambapo mito hiyo ilipitia na hata inataja kihususa maliasili zinazojulikana sana katika eneo hilo. Habari hizo ziliwasaidia Waisraeli wa kale waliosoma simulizi hilo kuelewa mambo mengi.

Je, hadithi na hekaya zinawasaidia watu kuelewa mambo vizuri? Au huwa zinakosa mambo hususa ambayo yanaweza kuthibitishwa kwa urahisi kuwa ya kweli au ya uwongo, au hata kukanushwa? Hadithi nyingi huanza hivi: “Hapo zamani za kale katika nchi moja ya mbali.” Lakini, historia hutoa habari hususa, kama lifanyavyo simulizi kuhusu Edeni.

2. Je, tunaweza kuamini kuwa Mungu alimuumba Adamu kutokana na mavumbi na Hawa kutokana na ubavu mmoja wa Adamu?

Wanasayansi wa kisasa wamethibitisha kuwa mwili wa mwanadamu una elementi fulani—kama vile hidrojeni, oksijeni, na kaboni—ambazo zinapatikana katika udongo. Lakini elementi hizo zilikusanywa kwa njia gani na kuwa mwili wa kiumbe hai?

Wanasayansi wengi wanataja kuwa uhai ulijitokeza wenyewe, ukianzia na viumbe visivyo tata na kubadilika polepole, na baada ya mamilioni ya miaka ukawa tata hata zaidi. Hata hivyo, maneno “visivyo tata” yanaweza kupotosha kwa kuwa viumbe vyote vilivyo hai—hata chembe ndogo zisizoweza kuonekana kwa macho—ni tata sana. Hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha kuwa kuna aina yoyote ya uhai uliojitokeza wenyewe au unaoweza kujitokeza wenyewe. Badala yake, kuna uthibitisho ulio wazi kuwa viumbe vyote vilibuniwa na mbuni mwenye akili nyingi zaidi kuliko ya wanadamu. *Waroma 1:20.

Hebu wazia ukisikiliza muziki mtamu au ukifurahia kuona mchoro wenye kupendeza au ukistaajabia jambo fulani la kitekinolojia, kisha unasisitiza kuwa hakuna mtu aliyebuni vitu hivyo. Bila shaka, hilo ni jambo lisilopatana na akili! Lakini vitu hivyo haviwezi kufikia utata, uzuri, au hata hekima iliyohusika katika kuubuni mwili wa mwanadamu. Ni jambo lisilowazika kusema kuwa mwili wa mwanadamu haukuumbwa. Zaidi ya hayo, simulizi la Mwanzo linaeleza kuwa kati ya viumbe vyote duniani, wanadamu peke yao ndio walioumbwa kwa mfano wa Mungu. (Mwanzo 1:26) Ndiyo maana ni wanadamu pekee walio na uwezo wa kubuni vitu kama afanyavyo Mungu, wakati fulani wakibuni vitu vyenye kupendeza kama muziki, sanaa, na tekinolojia. Hivyo, si ajabu kwamba Mungu ana uwezo mkubwa wa kubuni kuliko ule tulio nao.

Je, kuna ugumu wowote kumuumba mwanamke kwa kutumia ubavu wa mwanamume? * Mungu angeweza kutumia njia nyingine, lakini mbinu hii aliyotumia kumuumba mwanamke ina umaana mkubwa. Alitaka mwanamume na mwanamke wawe na uhusiano wa karibu, kana kwamba wao ni “mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Jinsi mwanamume na mwanamke wanavyokamilishana, wakifanyiza uhusiano thabiti ambao unawaimarisha wote wawili, ni uthibitisho ulio wazi kuwa kuna Muumba mwenye hekima na upendo.

Zaidi ya hayo, wataalamu wa kisasa wa chembe za urithi wamekiri kuwa yaelekea wanadamu walitokana na mwanamume na mwanamke mmoja. Kwa hiyo, je, simulizi la Mwanzo ni la kweli?

3. Je, habari kuhusu mti wa ujuzi na mti wa uzima ni hadithi tu?

Kwa kweli, simulizi la Mwanzo halionyeshi kwamba miti hiyo ilikuwa na nguvu fulani zisizo za kawaida. Badala yake, ilikuwa miti halisi ambayo Yehova aliiweka iwakilishe jambo fulani.

Je, wanadamu hawafanyi hivyo nyakati nyingine? Kwa mfano, hakimu anaweza kumwonya mtu asiidharau mahakama. Hilo halimaanishi kwamba hakimu anazuia viti, meza, nembo za taifa, kuta, na vitu vingine vilivyo ndani ya mahakama hiyo visidharauliwe, bali anataka kulinda mfumo wa kisheria unaowakilishwa na mahakama hiyo. Watawala mbalimbali wametumia fimbo ya ufalme na taji kuwa ishara ya mamlaka yao.

Hivyo, ile miti miwili iliwakilisha nini? Kumekuwa na maoni mengi yasiyoeleweka kuhusu jambo hilo. Kuna jibu la kweli na rahisi, lakini lenye umaana mkubwa sana. Mti wa ujuzi wa mema na mabaya unawakilisha pendeleo ambalo ni la Mungu pekee, yaani, haki ya kuamua yaliyo mema na yaliyo mabaya. (Yeremia 10:23) Ndio sababu lilikuwa kosa kuiba matunda ya mti huo! Kwa upande mwingine, mti wa uzima uliwakilisha zawadi ambayo Mungu pekee ndiye aliye na uwezo wa kuitoa, yaani, uzima wa milele.—Waroma 6:23.

4. Je, nyoka anayesemwa kuwa aliongea, ni hadithi tu?

Kwa kweli, huenda simulizi hilo la Mwanzo likawa gumu kueleweka, hasa ikiwa msomaji hatazingatia Biblia yote nzima. Hata hivyo, pole kwa pole Maandiko hufunua fumbo hilo lenye kutatanisha.

Ni nani au ni nini kilichomwezesha nyoka kuongea? Watu wa Israeli la kale walijua mambo mengine yaliyowasaidia kupata uelewevu zaidi kuhusu jinsi nyoka huyo alivyohusika. Kwa mfano, walijua kwamba ingawa wanyama hawaongei, kiumbe wa roho anaweza kumfanya mnyama aonekane kama anaongea. Musa pia aliandika simulizi kuhusu Balaamu. Simulizi hilo linasema kuwa Mungu alimtuma malaika amfanye punda wa Balaamu aongee kama mwanadamu.—Hesabu 22:26-31; 2 Petro 2:15, 16.

Je, roho wengine, kutia ndani wale ambao ni maadui wa Mungu, wanaweza kufanya miujiza? Musa alikuwa amewaona makuhani wa Misri wenye kufanya miujiza wakiiga baadhi ya miujiza ya Mungu, kama kugeuza fimbo iwe nyoka. Uwezo wa kufanya miujiza kama hiyo ungeweza tu kutoka kwa maadui wa Mungu walio katika makao ya roho.—Kutoka 7:8-12.

Pia, yaelekea kuwa Musa ndiye aliyeongozwa na roho ya Mungu kuandika kitabu cha Ayubu. Kitabu hicho kinaeleza mambo mengi kumhusu adui mkubwa wa Mungu, Shetani, ambaye kwa uwongo alitilia shaka utimilifu wa watumishi wa Yehova. (Ayubu 1:6-11; 2:4, 5) Je, Waisraeli hao wa kale walikata kauli kuwa Shetani alimtumia nyoka katika bustani ya Edeni, na kumfanya aonekane kama anaongea na hivyo kumdanganya Hawa avunje utimilifu wake kwa Mungu? Huenda ikawa hivyo.

Je, Shetani ndiye aliyemfanya nyoka aseme uwongo? Baadaye Yesu alimtaja Shetani kuwa ‘mwongo na baba ya uwongo.’ (Yohana 8:44) “Baba ya uwongo” ndiye aliyesema uwongo wa kwanza kuwahi kusemwa duniani. Uwongo huo wa kwanza unapatikana katika maneno ambayo nyoka alimwambia Hawa. Akipinga onyo la Mungu kuwa kula matunda yaliyokatazwa kutasababisha kifo, nyoka alisema hivi: “Hakika hamtakufa.” (Mwanzo 3:4) Kwa wazi, Yesu alijua kuwa Shetani alimtumia nyoka kusema uwongo. Ufunuo ambao Yesu alimpa mtume Yohana unadhihirisha jambo hilo, kwa kumwita Shetani “nyoka wa zamani.”—Ufunuo 1:1; 12:9.

Je, itakuwa kupita mipaka kuamini kuwa kiumbe wa roho mwenye nguvu aliweza kumtumia nyoka na kumfanya aonekane kama anaongea? Ingawa wanadamu hawana nguvu kama viumbe wa roho, wao pia wanaweza kufanya sanamu ionekane kama inatoa sauti, kumbe ni mwanadamu anayetoa sauti hiyo.

Uthibitisho Ulio Hakika Kabisa

Je, hukubali kuwa watu wanaotilia shaka simulizi la Mwanzo hawana msingi mzuri wa kufanya hivyo? Kwa upande mwingine, kuna uthibitisho mwingi wa kwamba simulizi hilo ni historia ya kweli.

Kwa mfano, Yesu Kristo anaitwa “shahidi mwaminifu na wa kweli.” (Ufunuo 3:14) Kwa kuwa alikuwa mtu makamilifu, Yesu hakuwahi kusema uwongo wala kuipotosha kweli. Zaidi ya hayo, alifundisha kuwa alikuwapo muda mrefu kabla ya kuja duniani akiwa mwanadamu—na hata, alikuwa kando ya Baba yake, Yehova, “kabla ya ulimwengu kuwako.” (Yohana 17:5) Kwa hiyo, alikuwa hai wakati uhai ulipoanza duniani. Hivyo basi, Yesu ambaye ndiye shahidi mwenye kutegemeka zaidi ya mashahidi wote anasema nini?

Yesu aliwataja Adamu na Hawa kuwa watu halisi. Alitaja ndoa yao alipokuwa akifafanua kanuni ya Yehova kuhusu kufunga ndoa na mwenzi mmoja tu. (Mathayo 19:3-6) Ikiwa Adamu na Hawa hawakuwahi kuwapo na bustani walimoishi ilikuwa hadithi tu, basi ama Yesu alikuwa amedanganywa au alikuwa mwongo. Yesu hangeweza kudanganywa wala kusema uwongo! Yeye alikuwa mbinguni akitazama tukio hilo lenye kuhuzunisha lilipotokea katika bustani ya Edeni. Je, kunaweza kuwa na uthibitisho mwingine wenye kutegemeka zaidi ya huo?

Kwa hiyo, kutoamini simulizi la kitabu cha Mwanzo ni kukosa imani katika Yesu. Pia, kutoamini simulizi hilo kunafanya isiwezekane kuelewa baadhi ya mafundisho muhimu ya Biblia na ahadi zake zenye kufariji. Acheni tuone kwa nini inaweza kuwa hivyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Katika Biblia, jina la kibinafsi la Mungu ni Yehova.

^ fu. 7 Wazo hilo si la Kimaandiko. Biblia inafundisha kuwa kazi zote za Mungu ni kamilifu; upotovu una chanzo tofauti. (Kumbukumbu la Torati 32:4, 5) Yehova alipomaliza kuiumba dunia, alitangaza kuwa kila kitu alichoumba “kilikuwa chema sana.”—Mwanzo 1:31.

^ fu. 9 Gharika, ambayo ilisababishwa na Mungu, iliiharibu kabisa bustani ya Edeni. Andiko la Ezekieli 31:18 linadokeza kwamba kufikia karne ya saba K.W.K. “miti ya Edeni” haikuwako. Kwa hiyo, wote waliotafuta bustani ya Edeni baada ya wakati huo hawangeipata.

^ fu. 14 Ona broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 16 Jambo la kushangaza ni kwamba wanasayansi wa kisasa wa mambo ya kitiba wamegundua kwamba ubavu una uwezo usio wa kawaida wa kujirekebisha. Tofauti na mifupa mingine, ubavu una uwezo wa kukua tena ikiwa tishu inayouunganisha na uti wa mgongo haikukatwa.