Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Alivumilia Licha ya Kuvunjwa Moyo

Alivumilia Licha ya Kuvunjwa Moyo

Igeni Imani Yao

Alivumilia Licha ya Kuvunjwa Moyo

SAMWELI angeweza kuhisi huzuni iliyokuwa Shilo. Watu wengi katika mji huo walikuwa wakiomboleza. Wanawake na watoto walikuwa wakilia na kuomboleza baada ya kupata habari kuhusu baba zao, waume zao, watoto wao, na kaka zao ambao hawangerudi nyumbani.Tunajua kwamba Israeli lilikuwa limepoteza wanajeshi 30,000 hivi katika pigano baya dhidi ya Wafilisti muda si mrefu baada ya wengine 4,000 kuuawa katika pigano lingine tofauti.—1 Samweli 4:1, 2, 10.

Huo ulikuwa tu mwanzo wa misiba ambayo ingewapata. Kuhani Mkuu Eli alikuwa na wana wawili waovu, Hofni na Finehasi, ambao walitoka Shilo wakiwa wamebeba sanduku takatifu la agano. Sanduku hilo lenye thamani lilikuwa wonyesho wa kuwapo kwa Mungu, na kwa kawaida liliwekwa katika patakatifu pa hema la kukutania. Hivyo, watu walienda na Sanduku hilo vitani, wakifikiri kwa upumbavu kwamba lingekuwa kama hirizi ambayo ingewasaidia kupata ushindi. Lakini Wafilisti waliliteka Sanduku hilo, na kumuua Hofni na Finehasi.—1 Samweli 4:3-11.

Kwa miaka mingi, hema la kukutania huko Shilo liliheshimiwa kwa sababu Sanduku la Agano liliweka huko. Na sasa lilikuwa limetekwa nyara. Baada ya kusikia habari hizo Eli mwenye umri wa miaka 98 alianguka kwa nyuma katika kiti chake na kufa. Binti-mkwe wake akawa mjane siku hiyo, na akafa alipokuwa akijifungua. Kabla ya kufa alisema: “Utukufu umeondoka katika Israeli kwenda uhamishoni.” Kwa kweli, mambo yangebadilika kabisa huko Shilo.—1 Samweli 4:12-22.

Samweli angeshughulika jinsi gani na mambo hayo yenye kuvunja moyo? Je, imani yake ingekuwa imara na kuweza kuwasaidia watu waliokuwa wamepoteza ulinzi na kibali cha Yehova? Nyakati fulani, sote hukabili vivunja moyo ambavyo vinaweza kujaribu imani yetu, hivyo, acheni tuone mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwa Samweli.

“Alitenda Uadilifu”

Baada ya tukio hilo, simulizi hilo la Biblia linaacha kumkazia fikira Samweli, na kuanza kulikazia fikira Sanduku takatifu, likituonyesha jinsi Wafilisti walivyoadhibiwa kwa sababu ya kuchukua Sanduku hilo, na hivyo kulazimika kulirudisha. Biblia inapomtaja tena Samweli, miaka ipatayo 20 imepita. (1 Samweli 7:2) Alikuwa akifanya nini miaka hiyo yote? Biblia inatujibu.

Tunasoma kwamba kabla ya kipindi hicho kuanza, “neno la Samweli likaendelea kuwajia Israeli wote.” (1 Samweli 4:1) Simulizi hilo linaonyesha kwamba baada ya kipindi hicho kupita, Samweli alikuwa na zoea la kuyatembelea majiji matatu ya Israeli. Aliyatembelea kila mwaka, kusuluhisha matatizo na kujibu maswali. Kisha angerudi katika mji wa kwao, Rama. (1 Samweli 7:15-17) Kwa wazi, Samweli alikuwa na shughuli nyingi katika kipindi hicho cha miaka 20.

Mwenendo mpotovu na ufisadi wa wana wa Eli ulikuwa umedhoofisha imani ya watu. Inaonekana hilo lilifanya wengi wageukie ibada ya sanamu. Hata hivyo, baada ya miaka 20 ya kazi ngumu, Samweli aliwaambia watu hivi: “Ikiwa mnarudi kwa Yehova kwa mioyo yenu yote, ondoeni miungu ya kigeni iliyo katikati yenu na pia zile sanamu za Ashtorethi, nanyi mwelekeze mioyo yenu kwa Yehova bila kuyumba-yumba, mkamtumikie yeye peke yake, naye atawakomboa kutoka mkono wa Wafilisti.”—1 Samweli 7:3.

“Mkono wa Wafilisti” ulikuwa umewalemea watu. Jeshi la Israeli likiwa limeshindwa kabisa, Wafilisti waliona kwamba wako huru kuwatesa watu wa Mungu bila hofu ya kuadhibiwa. Lakini Samweli aliwahakikishia watu kwamba jambo hilo lingebadilika ikiwa tu wangemrudia Yehova. Je, walikuwa tayari kufanya hivyo? Samweli alifurahi watu hao walipoondolea mbali sanamu zao na ‘kuanza kumtumikia Yehova peke yake.’ Aliwaita watu huko Mispa, mji uliokuwa katika eneo lenye milima, kaskazini ya Yerusalemu. Hivyo, wakakusanyika, wakafunga, na kutubu dhambi yao ya kuabudu sanamu.—1 Samweli 7:4-6.

Hata hivyo, Wafilisti walisikia kuhusu kusanyiko hilo kubwa na wakataka kutumia nafasi hiyo. Hivyo, wakatuma jeshi lao huko Mispa ili liwaangamize waabudu wa Yehova. Waisraeli walipata habari kuhusu hatari hiyo iliyokuwa ikikaribia. Waliogopa sana na kumwomba Samweli asali kwa ajili yao. Alisali na kutoa dhabihu pia. Sherehe hiyo takatifu ilipokuwa ikiendelea, jeshi la Wafilisti lilikuja kuvamia Mispa. Ndipo, Yehova akajibu sala ya Samweli kwa “[kufanya] kuwe na mngurumo wa sauti kubwa siku hiyo juu ya Wafilisti.”—1 Samweli 7:7-10.

Je, tunaweza kuwazia kwamba wale Wafilisti walikuwa kama watoto wadogo ambao hujikunyata nyuma ya mama zao wanaposikia ngurumo ya radi? Hapana, hao walikuwa wanajeshi jasiri. Kwa hiyo basi, lazima mngurumo huo uwe ulikuwa tofauti kabisa na mngurumo wowote ule ambao walikuwa wamewahi kuusikia. Je, ni kwa sababu mngurumo huo ulikuwa na “sauti kubwa”? Je, ni kwa sababu ulitokea tu katika anga lisilo na mawingu, au ulikuwa ni mwangwi kutoka milimani? Vyovyote vile, mngurumo huo uliwachanganya na kuwaogopesha sana Wafilisti. Wakiwa wamechanganyikiwa kabisa, Wafilisti hao walishambuliwa badala ya kushambulia. Wanaume Waisraeli walimiminika kutoka Mispa, na kuwashinda Wafilisti, wakiwakimbiza kilomita kadhaa kuelekea kusini-magharibi ya Yerusalemu.—1 Samweli 7:11.

Vita hivyo vilileta badiliko kubwa kwa watu wa Mungu. Katika muda wote ambao Samweli alikuwa mwamuzi, Wafilisti waliendelea kushindwa. Watu wa Mungu wakaendelea kuteka tena jiji moja baada ya lingine.—1 Samweli 7:13, 14.

Miaka mingi baadaye, mtume Paulo alimtaja Samweli miongoni mwa waamuzi na manabii waaminifu ambao ‘walitenda uadilifu.’ (Waebrania 11:32, 33) Bila shaka, Samweli aliwasaidia Waisraeli kutenda yaliyo mema na yaliyo sawa mbele za Mungu. Aliendelea kuwa na matokeo mazuri kwa sababu alimngojea Yehova kwa subira, huku akitimiza kazi yake kwa uaminifu licha ya kuvunjwa moyo. Pia alionyesha roho ya shukrani. Baada ya ushindi huko Mispa, Samweli alisimamisha jiwe liwe ukumbusho wa jinsi Yehova alivyowasaidia watu wake.—1 Samweli 7:12.

Je, ungependa ‘kutenda uadilifu’? Ikiwa ndivyo, itakuwa vema ujifunze kuwa na subira, uvumilivu, na roho ya shukrani kama Samweli. Kila mmoja wetu anahitaji kuwa na sifa hizo. Samweli alifanya vema kusitawisha na kuonyesha sifa hizo alipokuwa bado kijana, kwa sababu alikabili vivunja moyo vikubwa zaidi katika miaka ya baadaye.

“Wana Wako Hawakutembea Katika Njia Zako”

Wakati tunaposoma tena kumhusu Samweli, nabii huyo “amezeeka.” Sasa ana watoto wawili wakubwa, Yoeli na Abiya, na amewapa jukumu la kumsaidia katika kazi ya uamuzi. Inasikitisha kwamba hawakutimiza jukumu hilo. Hata ingawa Samweli alikuwa mnyofu na mwadilifu, watoto wake walitumia madaraka yao kujinufaisha, wakipotosha hukumu na kuchukua rushwa.—1 Samweli 8:1-3.

Siku moja, wanaume wazee wa Israeli walienda kwa nabii huyo mzee na kumlalamikia wakisema: ‘Wana wako hawatembei katika njia zako.’ (1 Samweli 8:4, 5) Je, Samweli alijua kuhusu tatizo hilo? Simulizi hilo halisemi. Tofauti na Eli, kwa kweli, Samweli hakuwa baba mbaya. Yehova alikuwa amemkemea na kumwadhibu Eli kwa sababu ya kutowarekebisha watoto wake waovu na kwa kuwaheshimu watoto hao zaidi ya Mungu. (1 Samweli 2:27-29) Yehova hakumpata Samweli na makosa kama hayo.

Simulizi hilo halitaji ikiwa Samweli aliona aibu, alihangaika, au alivunjika moyo sana aliposikia kuhusu mwenendo mpotovu wa watoto wake. Hata hivyo, wazazi wengi wanaweza kuwazia jinsi alivyohisi. Leo katika ulimwengu huu mwovu, watoto wengi wanakaidi mamlaka na nidhamu inayotolewa na wazazi wao. (2 Timotheo 3:1-5) Kwa kadiri fulani, wazazi wanaokabili hali hiyo wanaweza kupata faraja na mwongozo kutokana na mfano wa Samweli. Hakuruhusu hata kidogo ukosefu wa imani wa watoto wake ubadili msimamo wake. Kumbuka kwamba, hata ikiwa maneno na nidhamu itashindwa kufikia mioyo migumu ya watoto, kielelezo kizuri cha wazazi kinaweza kugusa mioyo ya watoto wao. Na nyakati zote wazazi wana nafasi ya kumfanya Baba yao, Yehova Mungu, ashangilie kama Samweli alivyofanya.

“Tuchagulie Mfalme”

Watoto wa Samweli hawakujua pupa na ubinafsi wao ungewaathiri watu kwa kadiri gani. Wazee wa Israeli waliendelea kumwambia Samweli hivi: “Sasa tuchagulie mfalme wa kutuhukumu sisi kama mataifa mengine yote.” Je, ombi hilo lilimfanya Samweli ahisi kana kwamba wanamkataa? Kwa miaka mingi, Samweli alikuwa ametumika kama mwamuzi kwa niaba ya Yehova. Sasa walitaka mfalme awe mwamuzi wao, bali si nabii tu. Mataifa mengine yaliyowazunguka yalikuwa na wafalme, na Waisraeli walitaka mfalme pia. Samweli alionaje jambo hilo? Tunasoma hivi, “Jambo hilo lilikuwa baya machoni” pake.—1 Samweli 8:5, 6.

Ona maneno ya Yehova wakati Samweli alipomweleza jambo hilo katika sala: “Sikiliza sauti ya watu kuhusu mambo yote wanayokuambia; kwa maana hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi nisiwe mfalme juu yao.” Samweli alifarijika sana, hata hivyo, watu hao walikuwa wamemkosea sana Mungu Mweza Yote! Yehova alimwambia nabii wake awaeleze Waisraeli matokeo mabaya ya kuwa na mfalme wa kibinadamu. Samweli alipowaeleza, bado walisisitiza: “Hapana, bali mfalme atakuwa juu yetu.” Kwa kuwa nyakati zote Samweli alikuwa mtiifu kwa Mungu wake, alienda na kumtia mafuta mfalme ambaye Yehova alimchagua.—1 Samweli 8:7-19.

Hata hivyo, Samweli alionyesha utii wake jinsi gani? Kwa kinyongo, bila kujali? Je, aliruhusu vivunja moyo viathiri moyo wake, na kuwa mwenye uchungu? Watu wengi wangefanya hivyo, lakini si Samweli. Alimtia Sauli mafuta na kusema kuwa huyo ndiye ambaye Yehova amemchagua. Alimbusu kama ishara ya kumkaribisha na ya ujitiisho kwa mfalme huyo mpya. Kisha, akawaambia watu: “Je, mmemwona yule ambaye Yehova amemchagua, kwamba hakuna yeyote kama yeye kati ya watu wote?”—1 Samweli 10:1, 24.

Samweli hakukazia kasoro, bali sifa nzuri za mtu huyo aliyechaguliwa na Yehova. Na kwa upande wake, alikazia fikira rekodi yake ya utimilifu kwa Mungu badala ya kutafuta kukubaliwa na watu wasio na msimamo. (1 Samweli 12:1-4) Pia, alitimiza mgawo wake kwa uaminifu, akiwashauri watu wa Mungu kuhusu hatari za kiroho walizokabili na kuwatia moyo waendelee kuwa waaminifu kwa Yehova. Shauri lake liliwafikia mioyo, nao wakamsihi Samweli asali kwa niaba yao. Aliwapa jibu hili zuri: “Kwa upande wangu, ni jambo lisilowaziwa, kwamba nimtendee Yehova dhambi kwa kuacha kusali kwa ajili yenu; nami nitawafundisha ninyi katika njia iliyo njema na iliyo sawa.”—1 Samweli 12:21-24.

Je, umewahi kuvunjika moyo kwa sababu mtu mwingine alichaguliwa kwa ajili ya daraka au pendeleo fulani? Mfano wa Samweli unatukumbusha kwamba hatupaswi kuruhusu wivu wala uchungu utawale mioyo yetu. Mungu ana kazi nyingi zenye kuridhisha kwa ajili ya kila mtumishi wake mwaminifu.

“Ni Mpaka Wakati Gani Utamwombolezea Sauli?”

Samweli alikuwa sahihi kuona sifa nzuri za Sauli, kwa sababu Sauli alikuwa mtu wa pekee. Kando na kimo chake na sura yake yenye kuvutia, mwanzoni Sauli alikuwa jasiri, hodari na mwenye kiasi. (1 Samweli 10:22, 23, 27) Zaidi ya sifa hizo, Sauli alikuwa na zawadi yenye thamani—hiari, yaani, uwezo wa kuchagua jinsi ya kutumia maisha yake na kufanya maamuzi yake mwenyewe. (Kumbukumbu la Torati 30:19) Je, alitumia zawadi hiyo vizuri?

Kwa kusikitisha, mtu anapopata pendeleo jipya, jambo hilo linaweza kumfanya apoteze sifa ya kiasi. Muda si muda Sauli alianza kuwa na kiburi. Aliamua kutotii maagizo ya Yehova ambayo Samweli alimpa. Wakati fulani Sauli alikosa subira na kutoa dhabihu ambayo ilipaswa kutolewa na Samweli tu. Samweli alimshauri vikali na kutabiri kwamba ufalme hautabaki katika familia ya Sauli. Badala ya kujifunza kutokana na nidhamu hiyo, Sauli aliendelea kutotii hata zaidi.—1 Samweli 13:8, 9, 13, 14.

Kupitia Samweli, Yehova alimwambia Sauli apigane vita dhidi ya Waamaleki. Maagizo ya Yehova yalitia ndani amri ya kumuua mfalme wao mwovu, Agagi. Hata hivyo, Sauli alimhifadhi Agagi na kuchukua nyara nzuri zilizopaswa kuharibiwa. Samweli alipoenda kumrekebisha, Sauli alionyesha jinsi alivyokuwa amebadilika. Badala ya kukubali shauri kwa unyenyekevu, Sauli alijitetea na kujaribu kupunguza uzito wa matendo yake. Aliepuka jambo lililokuwa likizungumziwa, na kujaribu kuwaelekezea watu lawama. Sauli alipojaribu kukataa nidhamu aliyopewa akidai kwamba baadhi ya nyara zingetumika katika kumtolea Yehova dhabihu, Samweli alisema maneno haya maarufu: “Tazama! Kutii ni bora kuliko dhabihu.” Kwa ujasiri, Samweli alimkemea Sauli na kumweleza uamuzi ambao Yehova alikuwa ameuchukua: Ufalme utararuliwa kutoka kwa Sauli na kupewa mtu mwingine bora.—1 Samweli 15:1-33.

Samweli alihuzunishwa sana na makosa ya Sauli. Alimlilia Yehova usiku kucha kuhusu jambo hilo. Hata alimwombolezea Sauli. Samweli alikuwa ameona kuwa Sauli angeweza kuwa mfalme mzuri, mwenye sifa nzuri, lakini sasa hakuwa na matumaini tena. Mtu ambaye alimfahamu awali sasa alikuwa amebadilika, alikuwa amepoteza sifa zake nzuri na kumwacha Yehova. Samweli alikataa kumwona Sauli tena. Hata hivyo, kwa upole Yehova aliurekebisha mtazamo wa Samweli kwa kumshauri hivi: “Ni mpaka wakati gani utamwombolezea Sauli, huku mimi, kwa upande mwingine, nimemkataa asitawale akiwa mfalme juu ya Israeli? Jaza pembe yako mafuta, nawe uende. Nitakutuma kwa Yese Mbethlehemu, kwa maana nimejipatia mfalme kati ya wanawe.”—1 Samweli 15:34, 35; 16:1.

Kusudi la Yehova halitegemei wanadamu wasio wakamilifu ambao hawadumishi uaminifu wao nyakati zote. Ikiwa mtu mmoja anakosa uaminifu, Yehova atamtafuta mwingine ili kutimiza mapenzi Yake. Hivyo, mzee Samweli akaacha kumwombolezea Sauli. Kwa mwelekezo wa Yehova, Samweli alienda nyumbani kwa Yese huko Bethlehemu, ambako alikutana na vijana wenye kuvutia. Hata hivyo, tangu mwanzo Yehova alimkumbusha Samweli hivi: “Usiangalie sura yake wala urefu wa umbo lake . . . Kwa kuwa Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona jinsi moyo ulivyo.” (1 Samweli 16:7) Mwishowe Samweli akaletewa Daudi, mwana wa mwisho wa Yese, huyo ndiye ambaye Yehova alikuwa amemchagua!

Katika miaka yake ya mwisho-mwisho, Samweli alikuja kuelewa kwa nini Yehova aliamua kumwondoa Sauli na kumweka Daudi. Sauli akawa na wivu uliomfanya atake kumuua Daudi na pia akawa mwasi-imani. Hata hivyo, Daudi alionyesha sifa nzuri kama vile ujasiri, uaminifu, utimilifu, imani, na ushikamanifu. Kadiri Samweli alivyokaribia kufa, ndivyo imani yake ilivyozidi kuwa imara. Alikuja kuona kwamba Yehova anaweza kushughulikia, kurekebisha, au hata kubadili hali yenye kuvunja moyo iwe baraka. Hatimaye Samweli alikufa, akiwa amejiendesha vizuri kwa karibu karne moja. Haishangazi kuwa Waisraeli wote walimwombolezea mtu huyo mwaminifu! Hata leo, watumishi wa Yehova wanapaswa kujiuliza, ‘Je, nitaiga imani ya Samweli?’

[Picha katika ukurasa wa 25]

Samweli angeweza kuwasaidia jinsi gani watu wake wakabiliane na hali ya kuvunjika moyo?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Samweli alikabiliana jinsi gani na kuvunjwa moyo na watoto wake waliokuwa waovu?