Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

MHUDUMU wa baa aliyekuwa akitusi watu, akinywa pombe kupita kiasi, na kutumia dawa za kulevya, aliweza kubadili maisha yake jinsi gani? Kwa nini mwanasiasa aliyechukia dini alikubali kuwa mhudumu wa dini? Mkufunzi wa mbinu za kupigana kwa mikono katika kikosi cha polisi cha Urusi, alikabili matatizo gani ili kuwa Shahidi wa Yehova? Soma masimulizi ya watu hao.

“Sasa mimi na mama yangu tuna uhusiano mzuri.”—NATALIE HAM

MWAKA WA KULIZALIWA: 1965

NCHI: AUSTRALIA

HISTORIA: ALITUMIA DAWA ZA KULEVYA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika mji mdogo wa Robe, Australia Kusini. Wakazi wengi wa mji huo walikuwa wavuvi. Katika jamii kama hizo, watu hupenda kukutana katika hoteli ili kupiga gumzo. Wazazi hutumia muda mwingi katika hoteli hizo, hivyo watoto wao hulelewa katika mazingira ya watu wanaokunywa pombe kupita kiasi, kutumia lugha chafu, na kuvuta sigara.

Kufikia wakati nilipokuwa na miaka 12, tayari nilikuwa nikivuta sigara, nikitumia maneno mengi ya matusi, na kugombana na mama yangu kila wakati. Nilipokuwa na miaka 15, wazazi wangu walitengana na miezi 18 baadaye, nikaondoka nyumbani. Nilikunywa pombe kupita kiasi, nikatumia dawa za kulevya, na kuishi maisha mapotovu. Nilichanganyikiwa na kuwa mwenye hasira. Nilihisi ningeweza kujitunza kwa kuwa kwa muda wa miaka mitano nilijifunza mbinu za kupigana, kutia ndani mazoezi ya jinsi wanawake wanavyoweza kujilinda wasishambuliwe. Lakini nyakati nyingine nilipotulia na kutafakari kuhusu maisha yangu, nilijawa na huzuni na kuanza kusali kwa Mungu, nikimwomba anisaidie. Lakini ningemwambia, “Usiniambie niende kanisani.”

Muda fulani baadaye, nilipewa Biblia na rafiki yangu aliyekuwa mtu wa dini, ingawa hakushirikiana na kanisa lolote hususa. Kama rafiki zetu wengine, yeye pia alitumia dawa za kulevya. Hata hivyo, alisema kuwa alimwamini Mungu kutoka moyoni na akanishawishi kubatizwa. Alinipeleka kwenye ziwa lililokuwa karibu na kunibatiza. Kuanzia wakati huo na kuendelea nilihisi kuwa nina uhusiano wa kipekee na Mungu. Hata hivyo, sikupata wakati wa kusoma Biblia.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Mnamo mwaka wa 1988, Mashahidi wawili walibisha mlango wangu. Mmoja wao aliniuliza, “Unajua jina la Mungu?” Shahidi huyo alisoma andiko la Zaburi 83:18 katika Biblia yake. Andiko hilo linasema: “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Nilishtuka sana! Walipoondoka, niliendesha gari umbali wa kilomita 56 hadi kwenye duka la vitabu vya Kikristo ili nichunguze andiko hilo katika tafsiri nyingine za Biblia. Pia, nilitafuta jina hilo katika kamusi. Baada ya kujihakikishia kuwa jina la Mungu ni Yehova, nilijiuliza ni mambo mengine mangapi ambayo sijui?

Mama yangu alikuwa ameniambia kuwa Mashahidi wa Yehova si watu wa kawaida. Lakini mambo machache niliyojua kuwahusu ni kwamba hawakushirikiana na watu wengine na hawakujua jinsi ya kufurahia maisha. Nilitaka kujificha walipokuja nyumbani kwangu lakini nikabadili nia na kuamua kuwasikiliza. Niliwakaribisha na mara moja tukaanza kujifunza Biblia.

Baada ya kila funzo, nilimweleza mpenzi wangu, Craig, yale niliyokuwa nimejifunza. Mwishowe alikasirika sana na kunipokonya kitabu nilichokuwa nikijifunza na kuanza kukisoma. Baada ya majuma matatu, alifikia mkataa kwamba alikuwa amepata kweli kumhusu Mungu. Mwishowe mimi na Craig tuliacha kutumia dawa za kulevya na kunywa pombe kupita kiasi. Mimi pia niliacha kazi ya kuhudumu katika baa. Ili tuishi kupatana na kanuni za Biblia, tuliamua kufunga ndoa.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Wakati tulipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, mimi na Craig tulikuwa karibu kuachana. Leo, Craig ni mume mzuri, na tuna watoto wawili wazuri. Pia, tuna marafiki wazuri walio na imani kama yetu.

Mara ya kwanza, mama yangu alikasirika alipojua kwamba nilikuwa nikishirikiana na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, hangaiko lake lilitokana na kutowajua Mashahidi vizuri. Sasa mimi na mama yangu tuna uhusiano mzuri. Sijihisi tena kuwa sina kusudi maishani. Badala yake, nina lengo na kusudi katika maisha yangu, na ninahisi kwamba mahitaji yangu ya kiroho yanatimizwa.—Mathayo 5:3.

“Nilijifunza mambo mengi yenye kushangaza katika Biblia.”—ISAKALA PAENIU

MWAKA WA KUZALIWA: 1939

NCHI: TUVALU

HISTORIA: MWANASIASA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa katika kisiwa maridadi cha Pasifiki kinachoitwa Nukulaelae, ambacho sasa ni sehemu ya Tuvalu. Mambo yote katika kisiwa hicho yaliongozwa na makasisi ambao walipata mafunzo yao ya kidini katika chuo fulani huko Samoa. Wakaaji wa kisiwa hicho walikuwa wametwikwa jukumu la kuwalisha makasisi na familia zao, kuwaandalia makao, na hata zaidi, kuhakikisha kwamba waliwapa vitu vilivyo bora zaidi. Hata kama wakaaji hao hawakuwa na chakula cha kutosha kwa ajili yao wenyewe na familia zao, bado walipaswa kuwaandalia makasisi hao.

Kasisi wa kisiwa chetu alisimamia shule iliyokuwa kijijini mwetu, naye alifunza somo la dini, hesabu, na jiografia. Nakumbuka wakati fulani kasisi huyo aliwapiga wanafunzi mpaka wakalowa damu. Hata hivyo, hakuna mtu aliyethubutu kupinga jambo hilo, hata wazazi wenyewe. Kasisi huyo aliheshimiwa sana kana kwamba alikuwa Mungu.

Nilipokuwa na miaka kumi, niliondoka nyumbani ili kujiunga na shule pekee iliyosimamiwa na serikali katika eneo hilo, ambayo ilikuwa katika kisiwa kingine. Nilipohitimu niliajiriwa na serikali. Wakati huo, visiwa hivyo vilikuwa sehemu ya koloni la Uingereza na viliitwa Visiwa vya Gilbert na Ellice. Nilifanya kazi katika idara mbalimbali na mwishowe nikawa mhariri wa gazeti la habari la serikali lililotolewa kila juma. Niliendelea na kazi yangu vizuri hadi nilipochapisha barua kutoka kwa msomaji mmoja ambaye alishutumu jinsi ambavyo pesa zilitumiwa kufanya maandalizi kwa ajili ya ziara ya Mwana-Mfalme wa Uingereza. Mtu aliyeandika barua hiyo alitumia jina bandia, na msimamizi wangu alitaka kujua jina lake halisi. Nilikataa kumwambia na mabishano yetu yakajulikana na watu wengi.

Muda mfupi baada ya tukio hilo, niliacha kazi ya serikali na kujiunga na siasa. Nilishinda uchaguzi katika kisiwa cha Nukulaelae na nikateuliwa kuwa Waziri wa Biashara na Maliasili. Baadaye, wakati watu wa kisiwa cha Kiribati (ambacho zamani kiliitwa Gilbert) na Tuvalu (ambacho zamani kiliitwa Ellice) walipopata uhuru kutoka Uingereza, gavana aliniomba niwe mkuu wa utawala katika eneo la Tuvalu. Lakini, sikutaka kuonekana kama nilikuwa nikishirikiana na utawala wa kikoloni. Hivyo nilikataa ombi hilo, na katika uchaguzi mkuu nikagombea cheo fulani cha juu cha kisiasa bila ufadhili wowote. Nilishindwa katika uchaguzi huo. Mwishowe, mimi na mke wangu tulirudi katika kisiwa cha nyumbani na kuamua kuishi maisha ya kawaida kijijini.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Watu wote katika kijiji chetu isipokuwa mimi, waliona siku ya Jumapili (Siku ya Yenga) kuwa siku takatifu ya Sabato. Hiyo ilikuwa siku yangu ya kusafiri baharini na kuvua samaki. Sikutaka kujulikana kama mtu wa dini. Baba yangu aliniambia jinsi yeye na watu wengine walivyohuzunishwa na matendo yangu. Lakini nilikuwa nimeazimia kutoongozwa na kanisa.

Katika mojawapo ya safari zangu kwenye kisiwa cha Funafuti—ambako mji mkuu wa Tuvalu unapatikana—ndugu yangu mdogo alinialika nihudhurie mikutano ya Mashahidi wa Yehova pamoja naye. Baadaye, Shahidi mmoja mmishonari alinipa rundo la magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ili nisome. Pia alinipa kitabu kinachofunua chanzo cha mafundisho ya kipagani ambayo yanafundishwa na dini nyingi zinazoitwa za Kikristo. Nilisoma kitabu hicho mara kadhaa. Nilijifunza mambo mengi yenye kushangaza katika Biblia, kutia ndani ukweli wa kwamba Wakristo hawako chini ya wajibu wa kushika Sabato ya kila juma. * Nilimweleza mke wangu mambo hayo, na mara moja akaacha kwenda kanisani.

Hata hivyo, bado nilikuwa nimeazimia kutoshirikiana na dini yoyote. Ingawa miaka miwili hivi ilikuwa imepita, bado nilikuwa ninakumbuka mambo niliyojifunza. Mwishowe, nilimwandikia yule mmishonari wa Funafuti, na kumwambia kuwa nilikuwa tayari kufanya mabadiliko. Alipanda mashua mara moja na kuja kunisaidia kujifunza mengi kuhusu Biblia. Baba yangu alikasirika sana alipogundua kuwa nilitaka kuwa Shahidi wa Yehova. Lakini nikamwambia kwamba Mashahidi walikuwa wamenifunza mengi kuhusu Biblia na nilikuwa nimefanya uamuzi.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Katika mwaka wa 1986, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, na mke wangu akabatizwa mwaka mmoja baadaye. Binti zetu wawili, pia walijifunza yale ambayo Biblia inafundisha na wakaamua kuwa Mashahidi wa Yehova.

Sasa nina pendeleo la kuwa katika kikundi cha kidini ambacho, kama Wakristo wa karne ya kwanza, hakina jamii mbili za watu, yaani, makasisi na watu wa kawaida. (Mathayo 23:8-12) Pia, kwa unyenyekevu wanaiga mfano wa Yesu wa kuwahubiria wengine kuhusu Ufalme wa Mungu. (Mathayo 4:17) Ninashukuru kama nini kwa kuwa Yehova Mungu ameniruhusu nijifunze ukweli kumhusu na kuwahusu watumishi wake pia!

“Mashahidi hawakunilazimisha kuamini mambo waliyonifundisha.” ALEXANDER SOSKOV

MWAKA WA KUZALIWA: 1971

NCHI: URUSI

HISTORIA: MKUFUNZI WA MBINU ZA KUPIGANA KWA MIKONO

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa jijini Moscow, ambalo wakati huo lilikuwa makao makuu ya Muungano wa Sovieti. Familia yetu iliishi katika jengo kubwa la makazi, na wengi wa jirani zetu walifanya kazi katika kiwanda kimoja. Ninakumbuka wakilalamika kuwa nilikuwa mtoto mtukutu na wakisema kuwa ama nitakufa mapema au kufungwa gerezani. Kufikia umri wa miaka kumi, jina langu tayari lilikuwa katika faili ya polisi.

Nilipofikia umri wa miaka 18, niliandikishwa jeshini na kuwa mlinzi wa mpakani. Nilirudi nyumbani baada ya miaka miwili na kufanya kazi katika kiwanda fulani, lakini kazi hiyo ikanichosha. Hivyo, nilijiunga na kikosi cha kupambana na ghasia cha polisi wa Moscow na nikawa mkufunzi wa mbinu za kupigana kwa mikono. Nilisaidia kukamata wahalifu jijini Moscow na nilisafiri kwenda katika maeneo mbalimbali nchini yaliyokuwa na misukosuko. Mkazo niliokuwa nao ulikuwa kama springi iliyoshindiliwa mahali fulani. Niliporudi nyumbani, mara kwa mara nilihitaji kulala kitanda tofauti na mke wangu kwa kuwa niliogopa kumuumiza nikiwa usingizini.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, nilitambua kuwa maisha ya jeuri niliyoishi hayakupatana na kanuni za Biblia. Pia niliona umuhimu wa kuacha kuvuta sigara na kudhibiti kiasi cha pombe nilichokunywa. Hata hivyo, nilifikiri kwamba singeweza kubadili kazi niliyofanya, kwa kuwa sikuwa na ujuzi mwingine wowote ambao ningeutumia kufanya kazi ili kutimiza mahitaji ya familia yangu. Pia nilihisi kuwa singeweza kwenda kuhubiri kama Mashahidi wanavyofanya.

Mwishowe, nilisaidiwa kuamini kuwa mambo yalioandikwa katika Biblia ni sahihi. Nilifarijiwa na simulizi lililo katika Ezekieli 18:21, 22. Andiko hilo linasema: “Kwa habari ya mwovu, ikiwa atageuka na kuziacha dhambi zake zote ambazo ametenda . . . , makosa yake yote ambayo ametenda—hayo hayatakumbukwa juu yake.”

Nilifurahi kwamba Mashahidi hawakunilazimisha kuamini mambo waliyonifundisha lakini walinisaidia kuona sababu ya kuamini mambo hayo. Nilichukua rundo la magazeti 40 au zaidi waliyonipa na kuyasoma kwa muda wa majuma matatu. Mambo niliyojifunza yalinithibitishia kuwa nilikuwa nimeipata dini ya kweli.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Kabla ya kuanza kujifunza Biblia nilikuwa karibu kutalikiana na mke wangu. Sasa ndoa yetu imekuwa bora. Mimi na mke wangu tulianza kujifunza Biblia wakati mmoja na tukaamua kumtumikia Yehova pamoja. Sasa familia yangu ina furaha zaidi. Pia, niliweza kupata kazi ambayo haipingani na kanuni za Biblia.

Nilipoanza kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba, ningepandwa na hasira nyingi—ningehisi kama nilivyohisi zamani kabla ya kuwavamia wahalifu. Sasa nina hakika kuwa ninaweza kuwa mtulivu hata mtu akijaribu kunichokoza. Baada ya muda, nilijifunza kuwa mwenye subira kuelekea watu. Ninasikitika nilipoteza muda mwingi maishani, lakini sasa ninahisi kwamba maisha yangu yana kusudi kwelikweli. Ninafurahi kutumia nguvu nilizo nazo kumtumikia Yehova Mungu na kuwasaidia wengine.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 24 Kwa habari zaidi, ona makala yenye kichwa “Je, Unapaswa Kushika Sabato ya Kila Juma?” iliyochapishwa katika Mnara wa Mlinzi wa Februari 1, 2010 (1/2/2010), ukurasa wa 11-15.