Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Wafundishe Watoto Wako Kuonyesha Heshima

Wafundishe Watoto Wako Kuonyesha Heshima

Wafundishe Watoto Wako Kuonyesha Heshima

METHALI moja ya Kijerumani inasema hivi: “Mtu aliyeshika kofia mkononi, anaruhusiwa kutembea kotekote katika nchi.” Katika jamii nyingi, mtu aliyevua kofia wakati wa kuingia katika nyumba ya mtu fulani au akisalimiana alionwa kuwa mtu mwenye adabu na hivyo aliheshimiwa. Hivyo, methali iliyotajwa hapo juu inamaanisha kwamba watu wana mwelekeo wa kuwatendea kwa fadhili zaidi au kuwa na maoni mazuri zaidi kuelekea watu walio na tabia nzuri.

Ni jambo linalofurahisha kama nini kuwaona vijana wakiwa na tabia nzuri! Mwangalizi mmoja wa mzunguko huko Honduras ambaye anahubiri nyumba kwa nyumba na wahubiri wenye umri mbalimbali anasema, “Mara nyingi nimeona kwamba mtoto ambaye amezoezwa vizuri na ambaye ni mwenye heshima anagusa sana moyo wa mwenye nyumba kuliko maneno yangu.”

Katika nyakati hizi ambazo watu wasio na heshima wanazidi kuongezeka, kujua jinsi ya kuwatendea wengine ni jambo linalofaa na lenye faida. Zaidi ya hayo, Maandiko yanatuhimiza ‘tujiendeshe kwa namna inayostahili habari njema juu ya Kristo.’ (Flp. 1:27; 2 Tim. 3:1-5) Ni jambo la maana kwamba tuwafundishe watoto wetu kuwaheshimu watu wengine. Wanaweza kufundishwa jinsi gani wasionyeshe tu adabu ya kinafiki bali wawe na heshima ya kweli? *

Tabia Nzuri Inafundishwa Kupitia Mfano Mzuri

Watoto wanajifunza kwa kuiga mifano wanayoona. Kwa hiyo, njia kuu ambayo wazazi wanaweza kuwafundisha watoto wao tabia nzuri ni wazazi wenyewe kuwa na tabia nzuri. (Kum. 6:6, 7) Kuzungumza na mtoto wako kuhusu kuwa na adabu ni jambo la maana, lakini haitoshi tu kufanya hivyo. Pamoja na kumkumbusha mambo hayo, ni jambo la maana sana kuweka mfano mzuri.

Fikiria mfano wa Paula, * ambaye alilelewa katika familia ya Kikristo yenye mzazi mmoja. Baadaye, alizoea kuwaonyesha watu wote heshima. Kwa nini? Anajibu hivi: “Mama alituwekea mfano, kwa hiyo lilikuwa jambo la kawaida kwetu watoto kuwaheshimu watu.” Mkristo anayeitwa Walter aliwafundisha watoto wake wa kiume kumheshimu mama yao ambaye hakuwa mwamini. Anasema hivi: “Nilijitahidi kuwafundisha wana wangu kumheshimu mama yao kupitia mfano wangu mwenyewe, sikusema kamwe mambo mabaya kumhusu mke wangu.” Walter aliendelea kuwafundisha watoto wake Neno la Mungu, na akasali ili apate msaada wa Yehova. Mmoja wao sasa anatumika katika ofisi moja ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, na yule mwingine ni painia. Watoto wake wanawapenda na kuwaheshimu wazazi wote wawili.

Biblia inasema hivi: “Mungu si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.” (1 Kor. 14:33) Yehova anafanya kila jambo kwa utaratibu. Wakristo wanapaswa kujitahidi kuiga sifa hiyo ya Mungu na kudumisha usafi nyumbani. Wazazi fulani wamewazoeza watoto wao kutandika vitanda vyao kila siku kabla ya kwenda shuleni, kuweka nguo zao mahali panapofaa, na kusaidia kufanya kazi nyingine za nyumbani. Ikiwa watoto wataona mazingira safi na utaratibu nyumbani, inaelekea sana kwamba watahakikisha vyumba vyao na vitu vyao ni safi.

Watoto wako wana maoni gani kuhusu mambo wanayojifunza shuleni? Je, wanaonyesha kwamba wanathamini mambo ambayo walimu wao wanawafanyia? Ukiwa mzazi, je, unaonyesha kwamba unathamini mambo hayo? Inaelekea kwamba watoto wako watakuwa na maoni kama yako kuelekea kazi yao ya shuleni na walimu. Kwa nini usiwatie moyo wawe na zoea la kuwashukuru walimu wao? Kushukuru kwa sababu ya huduma fulani tunayopokea ni njia nzuri sana ya kuonyesha heshima, iwe ni huduma kutoka kwa mwalimu, daktari, muuzaji katika duka, au mtu mwingine yeyote. (Luka 17:15, 16) Vijana Wakristo ambao wanakuwa tofauti na wanafunzi wenzao kwa sababu wanajiendesha kwa adabu na kuwa na mwenendo mzuri wanastahili kupongezwa.

Washiriki wa kutaniko la Kikristo wanapaswa kuweka mfano mzuri katika kuwa na adabu. Ni jambo zuri kama nini kuona vijana ambao wanashirikiana na kutaniko wakionyesha adabu kwa kutumia maneno kama vile “tafadhali” na “asante”! Watu wazima wanapoonyesha kwamba wanamheshimu Yehova kwa kusikiliza kwa makini maagizo yanayotolewa wakati wa mikutano, vijana wanachochewa kuwaiga. Watoto wanaweza kujifunza kuwaheshimu majirani wao kwa kutazama mifano mizuri ya wale wanaoonyesha tabia nzuri kwenye Jumba la Ufalme. Kwa mfano, Andrew aliye na umri wa miaka minne tayari amejifunza kusema, “Tafadhali niruhusu nipite,” anapotaka kupita mahali palipo na watu wazima.

Ni jambo gani lingine ambalo wazazi wanaweza kufanya ili kuwasaidia watoto wao wajifunze kuwa na mwenendo mzuri? Wazazi wanaweza na wanapaswa kutenga wakati ili kuzungumza pamoja na watoto wao mambo tunayojifunza kupitia mifano mingi inayotajwa katika Neno la Mungu.—Rom. 15:4.

Fundisha Ukitumia Mifano Iliyo Katika Biblia

Inaelekea sana kwamba mama ya Samweli alimfundisha mwana wake kuinama mbele ya Kuhani Mkuu Eli. Alipompeleka Samweli kwenye maskani, huenda alikuwa na umri wa miaka mitatu au minne tu. (1 Sam. 1:28) Je, unaweza kumzoeza mtoto wako mdogo salamu kama vile “habari za asubuhi,” “habari za alasiri,” “habari za jioni,” au namna watu wanavyosalimiana mahali mnapoishi? Kama kijana Samweli, watoto wako wanaweza pia “kupendwa na Yehova na vilevile na wanadamu.”—1 Sam. 2:26.

Kwa nini usitumie masimulizi ya Biblia kuonyesha tofauti kati ya kuonyesha heshima na kukosa heshima? Kwa mfano, Mfalme Ahazia wa Israeli ambaye hakuwa mwaminifu alipotaka kumwona nabii Eliya, alimtuma ‘mkuu wa 50 na wanaume wake 50’ ili kumwita. Ofisa huyo alimwamuru nabii huyo amfuate. Hiyo haikuwa njia inayofaa ya kuzungumza na mtu ambaye alimwakilisha Mungu. Eliya alijibu jinsi gani? Alisema hivi: “Naam, ikiwa mimi ni mtu wa Mungu, moto na ushuke kutoka mbinguni, ukuteketeze wewe na 50 wako.” Na hivyo ndivyo ilivyotukia. “Moto ukashuka kutoka mbinguni, ukamteketeza yeye na wale 50 wake.”—2 Fal. 1:9, 10.

Mkuu mwingine wa 50 alitumwa ili amlete Eliya. Yeye pia alijaribu kumwamuru Eliya amfuate. Kwa mara nyingine tena, moto ulishuka kutoka mbinguni. Lakini, mkuu mwingine wa tatu alimjia Eliya. Mwanamume huyo alionyesha heshima. Badala ya kumwamuru Eliya, alipiga magoti na kusihi: “Ewe mtu wa Mungu wa kweli, tafadhali acha nafsi yangu na nafsi ya hawa watumishi wako 50 iwe na thamani machoni pako. Tazama, moto ulishuka kutoka mbinguni, ukawateketeza wale wakuu wawili wa kwanza wa 50 na wale 50 wao, lakini sasa acha nafsi yangu iwe na thamani machoni pako.” Je, nabii wa Mungu angeita moto ushuke juu ya mtu ambaye huenda alikuwa mwoga lakini aliyezungumza kwa heshima hivyo? Hilo lingekuwa jambo lisilowazika! Badala yake, malaika wa Yehova alimwambia Eliya aende pamoja na ofisa huyo. (2 Fal. 1:11-15) Je, hilo halikazii kwamba ni jambo la maana kuonyesha heshima?

Mtume Paulo alipokamatwa na askari-jeshi Waroma katika hekalu, hakutenda kana kwamba alikuwa na haki ya kuzungumza. Kwa heshima, alimuuliza ofisa mkuu hivi: “Je, ninaruhusiwa kukuambia jambo fulani?” Kwa sababu hiyo, Paulo alipewa nafasi ya kujitetea.—Mdo. 21:37-40.

Alipokuwa akihojiwa, Yesu alipigwa kofi kwenye uso. Hata hivyo, alijua njia inayofaa ya kujitetea, alisema hivi: “Ikiwa nimesema vibaya, toa ushahidi kuhusu ubaya wenyewe; lakini ikiwa nimesema sawasawa, kwa nini unanipiga?” Hakuna mtu ambaye angepata kosa lolote katika maneno hayo ya Yesu.—Yoh. 18:22, 23.

Neno la Mungu pia lina mifano inayoonyesha jinsi tunavyoweza kutenda tunaporekebishwa kwa ukali na jinsi tunavyoweza kukubali kwa heshima makosa fulani tuliyofanya zamani au kukubali kwamba tulipuuza mambo fulani. (Mwa. 41:9-13; Mdo. 8:20-24) Kwa mfano, Abigaili aliomba msamaha kwa sababu mume wake, Nabali, alikuwa amemtendea Daudi kwa dharau. Zaidi ya kuomba msamaha, alimpa Daudi zawadi ya chakula kingi. Daudi alifurahishwa sana na mambo ambayo Abigaili alifanya hivi kwamba baada ya kifo cha Nabali alimchukua Abigaili awe mke wake.—1 Sam. 25:23-41.

Wafundishe watoto wako kuonyesha watu heshima, iwe chini ya hali ngumu au iwe tu ni kuonyesha adabu. ‘Kuacha nuru yetu iangaze mbele ya watu’ katika njia hiyo ‘kunampa utukufu Baba yetu aliye mbinguni.’—Mt. 5:16.

[Maelezo ya Chini]

^ Bila shaka, wazazi wanahitaji kuwasaidia watoto wao kuona tofauti kati ya kuwaheshimu watu wazima na kujinyenyekeza kwa mtu ambaye huenda anataka kuwaumiza. Ona gazeti Amkeni! la Oktoba (Mwezi wa 10) 2007, ukurasa wa 3-11.

^ Baadhi ya majina yamebadilishwa.