Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Wanaohubiri Habari Njema?

Ni Nani Wanaohubiri Habari Njema?

Ni Nani Wanaohubiri Habari Njema?

“ . . . itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.”—MATHAYO 24:14.

HABARI njema inahubiriwa ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova. Wanafanya hivyo katika njia tofauti-tofauti. Njia moja ni kwa . . .

Kuzungumza na Watu. Kama Yesu na wanafunzi wake, Mashahidi wa Yehova wanawatembelea watu ili kuwahubiria habari njema. (Luka 8:1; 10:1) Mashahidi hawangoji watu wawatafute. Kuwahubiria watu kuhusu Ufalme wa Mungu ni kazi inayofanywa na Mashahidi wote, ambao ni zaidi ya milioni saba. Wanahubiri nyumba kwa nyumba, barabarani, kwa simu, na kwa njia nyingine. Mwaka uliopita, Mashahidi walitumia zaidi ya saa bilioni moja na nusu katika kazi hiyo.

Wanawafundisha wengine kuhusu Ufalme wa Mungu na pia kuhusu ‘mambo yote ambayo Yesu aliwaamuru.’ (Mathayo 28:20) Wanaongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya milioni nane bila malipo.

Mashahidi wanahubiri ulimwenguni pote—katika nchi 236. Wanawahubiria watu wa aina zote. Wanahubiri vijijini na hata mijini, katika misitu ya Amazoni, misitu mikubwa ya Siberia, majangwa ya Afrika, na katika Milima ya Himalaya. Hawalipwi kwa kufanya kazi hiyo, bali wanaifanya kwa kutumia wakati na gharama zao wenyewe. Wanachochewa na upendo wao kwa Mungu na jirani. Pia, wanahubiri habari njema kupitia . . .

Machapisho. Gazeti hili, ambalo jina lake kamili ni Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova, sasa linachapishwa katika lugha 185 likiwa na jumla ya nakala zaidi ya milioni 42 kwa kila toleo. Gazeti la Amkeni!, ambalo pia linatangaza kuhusu Ufalme, linachapishwa katika lugha 83 likiwa na jumla ya nakala milioni 40 hivi kwa kila toleo.

Vitabu, broshua, trakti, CD/MP3, na DVD ambazo zinafafanua mafundisho ya Biblia zinapatikana katika lugha 540 hivi. Katika kipindi cha miaka kumi tu iliyopita, Mashahidi wametayarisha na kugawanya vifaa zaidi ya bilioni 20. Hiyo ni sawa na vifaa vitatu hivi kwa kila mtu anayeishi duniani!

Mashahidi wa Yehova pia wamechapa au kuagiza uchapaji wa tafsiri mbalimbali za Biblia. Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ambayo imetafsiriwa, kuchapwa, na kusambazwa na Mashahidi, sasa inapatikana ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 96. Zaidi ya nakala milioni 166 zimesambazwa. Mashahidi pia wanahubiri habari njema ya Ufalme . . .

Kwenye Mikutano ya Kikristo. Mikutano inayofanywa kila juma katika Majumba ya Ufalme si utaratibu tu wa ibada za kidini; inakusudiwa kuelimisha watu. Hotuba hutolewa kulingana na kichwa fulani cha Biblia, na watu hujifunza Biblia wakitumia gazeti la Mnara wa Mlinzi na machapisho mengine. Katika mikutano hiyo, pia Mashahidi hujifunza jinsi ya kuwa na matokeo zaidi wakiwa watangazaji wa habari njema.

Mashahidi hujifunza habari ileile katika makutaniko zaidi ya 107,000 ulimwenguni pote. Jambo hilo linachangia umoja wao. Watu wote wanakaribishwa kwenye mikutano hiyo. Hakuna sadaka zinazokusanywa. Bila shaka, yote hayo hayangekuwa na maana yoyote ikiwa Mashahidi wangeshindwa kuishi kulingana na yale wanayohubiri. Hivyo basi, wanajaribu kupendekeza habari njema . . .

Kwa Mfano Wao Mzuri. Wanajitahidi kuweka mfano mzuri kuhusiana na mwenendo wao wakiwa Wakristo, wakifanya kadiri wanavyoweza kuwatendea wengine kwa njia ambayo wao wenyewe wangependa watendewe. (Mathayo 7:12) Ingawa hawajakamilika na nyakati nyingine wanakosea, bado wao wanatamani kwa unyofu kuwatendea watu wote kwa upendo, si kwa kuwahubiria habari njema tu, bali pia kwa kuwasaidia katika njia nyingine inapowezekana.

Mashahidi wa Yehova hawajaribu kuugeuza ulimwengu kupitia kazi yao ya kuhubiri. Yehova atakaporidhika kuwa kazi hiyo imefanywa vya kutosha, ndipo mwisho utakapokuja kama Yesu alivyotabiri. Hilo litamaanisha nini kwa dunia na watu?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Habari njema inahubiriwa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote