Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mwisho” Ni Nini?

“Mwisho” Ni Nini?

“Mwisho” Ni Nini?

“. . . na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—MATHAYO 24:14.

HIVI karibuni kumekuwa na mazungumzo mengi kuhusu mwisho wa dunia. Katika vitabu, sinema, na magazeti kuna habari zenye kuchekesha na hata za kisayansi zinazoonyesha kwa njia mbalimbali misiba itakayotokea katika siku ya maangamizi. Misiba hiyo inatia ndani uharibifu utakaotokana na vita vya nyuklia, kugongana kwa sayari ndogo, virusi hatari, mabadiliko makubwa ya hali ya hewa, au wavamizi kutoka sayari nyingine.

Maoni ya dini pia yanatofautiana. Dini nyingi zinafundisha kwamba “mwisho” utakomesha uhai wote duniani. Akizungumzia kuhusu Mathayo 24:14, mwanatheolojia mmoja aliandika maneno haya yenye kuogopesha: “Huu ni mmoja kati ya mistari muhimu zaidi katika Neno la Mungu . . . Kizazi chetu kinakabili maangamizi ya kiwango kikubwa sana hivi kwamba ni wachache kati yetu wanaojaribu kuwazia jinsi hali itakavyokuwa.”

Kwa kawaida, wenye maoni hayo hupuuza jambo hili muhimu: Yehova Mungu ‘aliifanya dunia ikiwa imara,’ yeye “hakuiumba tu bila sababu, [bali] aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Hivyo, Yesu alipozungumza kuhusu “mwisho,” hakumaanisha kwamba dunia itaharibiwa; wala hakumaanisha kuwa wanadamu wote wataangamizwa. Alimaanisha kwamba waovu—wale ambao kwa kiburi wanakataa kuishi kulingana na mwongozo wenye upendo wa Yehova—wataharibiwa.

Fikiria mfano huu: Tuseme unamiliki nyumba nzuri na unawaruhusu watu waishi humo bila malipo. Baadhi yao wanaishi na wengine kwa amani na wanaitunza nyumba yako vizuri. Hata hivyo, wengine wanasababisha vurugu, wanapigana, na kuwaonea wale wakaaji wazuri. Wanaharibu nyumba yako na kwa kiburi wanakataa kukusikiliza unapojaribu kuwazuia wasifanye hivyo.

Ungefanya nini ili kurekebisha mambo? Je, ungeibomoa nyumba yako? Yaelekea hungefanya hivyo. Labda ungewaondoa wale wakaaji wabaya na kurekebisha uharibifu ambao umefanywa.

Yehova atafanya vivyo hivyo. Alimwongoza mtunga-zaburi kuandika: “Watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia. Na bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:9-11.

Mtume Petro alizungumza kuhusu jambo hilohilo. Aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Mbingu zilikuwapo tangu zamani za kale na dunia ikisimama imara kutoka katika maji na katikati ya maji kwa neno la Mungu; na kwa njia hizo ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji.” (2 Petro 3:5, 6) Hapa mtume alikuwa akirejelea Gharika ya siku za Noa. Ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu uliharibiwa, lakini dunia yenyewe haikuharibiwa. Gharika hiyo iliyoikumba dunia nzima ‘iliweka kielelezo kwa watu wasiomwogopa Mungu juu ya mambo yatakayokuja.’—2 Petro 2:6.

Kisha Petro akaongeza: “Mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto.” Ikiwa tungesoma sehemu hiyo tu, huenda tungekosa maana ya mstari mzima. Hata hivyo, ona kwamba mstari huo unaendelea kusema: “Na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.” Huo si uharibifu wa dunia, bali wa watu wasiomwogopa Mungu. Ni nini kinachofuata? Petro aliandika: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya [Ufalme wa Kimasihi wa Mungu] na dunia mpya [jamii ya wanadamu waadilifu], na humo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:7, 13.

Unabii wa Biblia pia unaonyesha kwamba “mwisho” utafika hivi karibuni. Soma Mathayo 24:3-14 na 2 Timotheo 3:1-5 ili uone mambo yanayothibitisha kwamba maneno hayo ni ya kweli. *

Je, inashangaza kuwa watu wengi wamechanganyikiwa kuhusu Mathayo 24:14, andiko ambalo hata mtoto mdogo anaweza kulielewa? Kuna sababu za kuchanganyikiwa. Shetani amepofusha watu wasielewe kweli zenye thamani zinazopatikana katika Neno la Mungu. (2 Wakorintho 4:4) Pia, Mungu ameficha makusudi yake yasijulikane na watu wenye kiburi lakini ameyafunua kwa watu wanyenyekevu. Kuhusiana na hilo, Yesu alisema: “Ninakusifu wewe hadharani, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umewaficha mambo haya wenye hekima na wenye akili na umeyafunua kwa watoto.” (Mathayo 11:25) Ni pendeleo kubwa kama nini kuwa miongoni mwa watu wanyenyekevu wanaoelewa vizuri Ufalme wa Mungu ni nini, na wanaoweza kuwa na tazamio la kupata baraka ambazo wale wanaounga mkono Ufalme huo watapata!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kwa habari zaidi, ona sura ya 9 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ufalme utaondoa uovu wote duniani