Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Nchi Inayotiririka Maziwa Na Asali”

“Nchi Inayotiririka Maziwa Na Asali”

“Nchi Inayotiririka Maziwa Na Asali”

YEHOVA MUNGU alipowakomboa Waisraeli kutoka Misri, aliwaahidi kuwa atawapeleka “kwenye nchi nzuri na kubwa, nchi inayotiririka maziwa na asali.”—Kutoka 3:8.

Waisraeli walipoingia katika Nchi ya Ahadi, walifuga ng’ombe, kondoo, mbuzi, na hivyo wakapata maziwa mengi sana. Namna gani asali? Watu fulani wanaamini kuwa neno asali linamaanisha umajimaji mtamu uliotengenezwa kutokana na tende, tini, au zabibu. Na katika sehemu nyingi ambapo Biblia inataja asali ya nyuki, inarejelea asali ya mwituni, bali si asali ya nyuki wa kufugwa. (Waamuzi 14:8, 9; 1 Samweli 14:27; Mathayo 3:1, 4) Je, kwa kweli nchi hiyo ‘ilitiririka’ asali na maziwa?

Uvumbuzi wa hivi karibuni wa vitu vya kale katika Israeli ya kisasa unatusaidia kuelewa jambo hilo. Kuhusu uvumbuzi huo, taarifa ya chuo kikuu kimoja (Hebrew University) inasema: “Hapa ndipo mahali pa kufugia nyuki pa kale zaidi kuwahi kuchimbuliwa katika Mashariki ya Karibu ya Kale, akasema Profesa (Amihai) Mazar. Eneo hilo lilitumiwa kwa ufugaji wa nyuki kuanzia karne ya 10 mpaka mwanzoni mwa karne ya 9 K.W.K.”

Wataalamu hao wa vitu vya kale walipata safu tatu zilizokuwa na jumla ya mizinga zaidi ya 30 ya nyuki, na walikadiria kuwa eneo lote lingeweza kuwa na mizinga 100 hivi. Mizinga hiyo ilipochunguzwa, mabaki ya nyuki na molekuli za nta ya nyuki zilipatikana. Wasomi wanakadiria kuwa “asali yenye uzito wa karibu nusu tani ingeweza kukusanywa kila mwaka katika mizinga hiyo.”

Nyakati za kale, asali ilikuwa chakula kitamu, nayo nta iliyotengenezwa kutokana na masega ilitumiwa katika viwanda vya kutengenezea bidhaa za chuma na ngozi. Nta pia ilitumiwa katika mabamba ya kuandikia. Mabamba hayo yalikuwa na sehemu iliyojazwa nta na mwandikaji angeweza kuandika ujumbe juu ya nta hiyo, kisha kuiyeyusha iwapo alitaka kuandika tena. Wataalamu wa vitu vya kale wamefikia mkataa gani baada ya uvumbuzi huu?

“Ingawa Biblia haituambii chochote kuhusu ufugaji wa nyuki nchini Israeli wakati huo,” inaendelea ile taarifa ya chuo kikuu, “uvumbuzi wa eneo la Tel Rehov ambapo nyuki walifugwa, unaonyesha kwamba ufugaji wa nyuki na ukusanyaji wa asali na masega ya asali ni kazi iliyokuwa imesitawi sana mapema wakati wa kipindi cha Hekalu la Kwanza [la Sulemani]. Kwa hiyo, inawezekana kuwa neno ‘asali’ katika Biblia linamaanisha asali ya nyuki.”

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 15]

Institute of Archaeology/Hebrew University © Tel Rehov Excavations