Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Utaitamani Sana”

“Utaitamani Sana”

Mkaribie Mungu

“Utaitamani Sana”

INAUMIZA sana kumwona mtu unayempenda akiteseka na kufa. Ni jambo la kawaida kuomboleza kifo cha mpendwa. Hata hivyo, inafariji kujua kwamba Muumba wetu, Yehova Mungu anaelewa huzuni yetu. Zaidi ya hayo, anatamani kutumia nguvu zake nyingi kuwafufua wafu. Ona tumaini lililo katika maneno ya Ayubu, kwenye Ayubu 14:13-15.

Fikiria hali ilivyokuwa. Ayubu, mtu mwenye imani ya kipekee, anapatwa na majaribu makali. Anapoteza mali yake, anafiwa na watoto wake wote wapendwa, na anapatwa na ugonjwa mbaya. Akiwa katika maumivu makali anamlilia Mungu: “Laiti ungenificha katika Kaburi!” (Mstari wa 13) Ayubu anaona kuwa kaburini ni mahali anapoweza kupata kitulizo. Akiwa huko, atakuwa kama hazina ambayo Mungu ameificha na hatapatwa na matatizo wala maumivu. *

Je, Ayubu atakaa kaburini milele? Ayubu anaamini kuwa haitakuwa hivyo. Anaendelea kusali: “Laiti . . . ungeniwekea kikomo cha wakati na kunikumbuka!” Ayubu anatumaini kwa uhakika kuwa hatakaa kaburini kwa muda mrefu na kwamba Yehova hatamsahau. Ayubu analinganisha wakati atakaokuwa kaburini na “kazi ya kulazimishwa”—kipindi ambacho atalazimika kungoja. Atangoja kwa muda gani? “Mpaka kitulizo changu kije,” anasema. (Mstari wa 14) Kitulizo hicho kitamaanisha kuwa atatoka kaburini—yaani, atafufuliwa!

Kwa nini Ayubu ana uhakika kwamba atapata kitulizo? Kwa sababu anajua jinsi Muumba wetu mwenye upendo anavyohisi kuhusu watumishi Wake waaminifu ambao wamekufa. Ayubu anasema: “Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.” (Mstari wa 15) Ayubu anakubali kwamba yeye ni kazi ya mikono ya Mungu. Bila shaka, Mpaji-Uhai ambaye alimfanya Ayubu katika tumbo la uzazi, anaweza kumfufua baada ya kufa.—Ayubu 10:8, 9; 31:15.

Maneno ya Ayubu yanatusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyotupenda: Ana uhusiano wa kipekee na wale ambao kama Ayubu, hujiweka mikononi mwake na kumruhusu awafinyange ili wawe watu wenye kupendeza machoni pake. (Isaya 64:8) Yehova anawathamini sana waabudu wake waaminifu. ‘Anatamani’ washikamanifu wake waliokufa. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “-tamani” pasipo shaka ni “mojawapo ya maneno mazito zaidi ya kuonyesha hamu kubwa,” asema msomi mmoja. Ndiyo, Yehova anawakumbuka waabudu wake na pia anatamani kuwafufua.

Inafurahisha kwamba, katika kitabu cha Ayubu—kimoja kati ya vitabu vya kwanza vya Biblia kuandikwa—Yehova aliona inafaa afunue kusudi lake la kuwafufua wafu. * Anataka kukuunganisha tena na wapendwa wako waliokufa. Jambo hilo linaweza kufanya iwe rahisi kidogo kuvumilia. Tunakutia moyo ujifunze mengi zaidi kumhusu Mungu huyu mwenye upendo na jinsi unavyoweza kumruhusu akufinyange ili ustahili kuona kusudi Lake likitimia.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa Mwezi wa Machi (Mwezi wa 3):

Esta 1-9Ayubu 1-15

[Maelezo ya Chini]

^ Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kuwa neno hili la Ayubu, “ungenificha,” linaweza kumaanisha “u[ni]weke mahali salama kama akiba yenye thamani.” Kitabu kingine kinasema kwamba neno hilo linamaanisha “nifiche kama hazina.”

^ Ili kujifunza mengi zaidi kuhusu ahadi ya Biblia ya ufufuo katika ulimwengu mpya wenye uadilifu, ona sura ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.