Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Je, Yehova Anatupenda Ingawa Sisi Ni Wahindi?”

“Je, Yehova Anatupenda Ingawa Sisi Ni Wahindi?”

Barua Kutoka Mexico

“Je, Yehova Anatupenda Ingawa Sisi Ni Wahindi?”

MARA kwa mara Melesio, mwanamume anayezungumza Kio’damu, alikuwa akisafiri kutoka milimani kwenda jijini kutafuta kazi. Alihudhuria mikutano ya Kikristo na kuchukua vitabu vinavyozungumzia Biblia ili akazungumze na watu wa kwao. Aliomba mtu fulani awatembelee na kuwafundisha mengi zaidi kuihusu Biblia.

Watu wa kabila la O’damu, wanaishi mbali kwenye milima iliyo kaskazini ya kati ya Mexico, umbali wa kilomita 240 hivi kutoka kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova lililo karibu. Baadhi yetu tuliamua kuwatembelea.

Tuliondoka jijini Durango kwa lori dogo, tukiwa tumebeba mahema na mifuko ya kulalia. Pia, tulibeba chakula cha kutosha na mafuta ya gari ambayo tungetumia kwa siku tatu. Tulianza safari yetu saa kumi usiku, na tulisafiri kwa muda wa saa nane hadi mwisho wa barabara fulani ya mlimani ya vumbi. Hapo ndipo eneo la Wao’damu linapoanzia. Mbele yetu kulikuwa na bonde lenye kina kirefu na mlima.

Tuliacha gari kwenye kijiji fulani, na kutembea kwa miguu kwa muda wa saa tatu hadi sehemu ya chini ya lile bonde, huku tukiwa tumebeba mizigo yetu. Hapo tulipiga kambi, tukakusanya kuni za kutosha na kuwasha moto mkubwa ili wanyama wa mwituni wasitukaribie. Tulilala kwa zamu ya saa tatu-tatu ili kuhakikisha kwamba moto hauzimiki.

Asubuhi na mapema siku iliyofuata, tulianza kupanda ule mlima. Kulikuwa na vijia vingi, na tulipotea mara kadhaa. Mmoja wetu alizungumza Kio’damu kidogo, kwa hiyo tulizungumza kifupi kuhusu ujumbe wa Biblia na watu wanaoishi karibu na njia. Tulishangaa walipotuambia kuwa huko Los Arenales, mahali tulipokuwa tukienda, kulikuwa na watu waliojiita Mashahidi wa Yehova na walifanya mikutano ya Kikristo huko. Habari hizo zilikuwa zenye kushangaza lakini zenye kutia moyo.

Tulifika Los Arenales huku miguu yetu ikiwa na malengelenge. Nyumba katika eneo hilo zimetawanyika na zimejengwa kwa matofali ya udongo na kuezekwa kwa katoni. Hakuna shule wala umeme katika eneo hilo. Kwa kuwa watu hao wako mbali sana na watu wengine, wanaishi katika umaskini mkubwa, na chakula chao kikuu ni chapati za unga wa mahindi. Tulimpata Melesio, mwanamume kijana mwembamba aliyefurahi sana kutuona. Alitualika kwenye nyumba yake ndogo na kutuambia kwamba alikuwa akiomba kila siku ili Yehova atume Mashahidi Wake waje kuifundisha familia yake Biblia, na pia kuwafundisha Wao’damu wenzake. Aliona kuwa hawezi kuwajibu maswali yao yote.

Wao’damu ni wafuasi wa dini ya shamani. Wanatumia hirizi za manyoya na mifupa ya tai, wanaabudu nguvu za asili, na wanawaogopa viongozi wao wa kidini ambao huwatumia vibaya kujinufaisha. Melesio alitueleza kuwa alipojifunza kwenye mojawapo ya safari zake jijini kuwa Yehova ndiye Mungu wa kweli, aliharibu sanamu zake zote. Watu walifikiri kwamba miungu yao ingemuua kwa sababu ya kufanya hivyo. Lakini Melesio hakufa, hivyo wakatambua kuwa Yehova ana nguvu nyingi kushinda miungu yao. Kwa hiyo, wakaanza kuhudhuria funzo la Biblia lililokuwa linafanywa katika familia ya Melesio ambalo Melesio alikuwa akiongoza kwa kutumia vitabu vyetu.

“Niliwaambia lazima kwanza wateketeze hirizi na sanamu zao,” akasema Melesio. Wengi waliacha kuwa na woga wa kishirikina, na idadi ya waliohudhuria ikapanda hadi watu zaidi ya 80. Tulishangaa kusikia hayo, na tukaamua kufanya mkutano alasiri hiyohiyo. Tulituma wajumbe waliotumia farasi kuwapasha habari watu waliokutana kwa ukawaida nyumbani kwa Melesio. Watu 25 walihudhuria mkutano huo ingawa ilikuwa katikati ya juma na walipata habari muda mfupi tu kabla ya mkutano kuanza. Baadhi yao walitembea kwa miguu na wengine wakatumia punda.

Huku Melesio akifasiri yale tuliyosema, tuliwajibu watu hao maswali yao kwa kutumia Biblia. Waliuliza maswali kama: “Je, Yehova anatupenda ingawa sisi ni Wahindi?” “Je, anasikia sala katika Kio’damu?” Har-Magedoni itakapofika, je, Yehova atatukumbuka ingawa tunaishi mbali na majiji?” Tulifurahia kutumia Biblia kuwahakikishia watu hao wanyenyekevu kuwa Yehova anawajali wapole, hata wawe wanazungumza lugha gani au wanaishi mbali kadiri gani. Walituomba tutume mtu aende kuwafundisha mambo mengi zaidi.

Baada ya mkutano huo, tulikula chakula chetu pamoja na marafiki hao wapya. Usiku ulikuwa umefika, na kulikuwa na baridi kali huko juu milimani, kwa hiyo tulishukuru walipotupa chumba fulani kilichokuwa kinajengwa ili tulale humo. Asubuhi iliyofuata, walitusindikiza hadi kwenye gari letu kupitia njia ya mkato, na tukasafiri hadi Durango, tukiwa tumechoka, lakini wenye furaha.

Lilikuwa pendeleo kubwa sana kukutana na watu hawa wanyofu, ambao wengi wao hawawezi kusoma, kuandika, wala kuzungumza Kihispania, lakini wanaotaka kujifunza kumhusu Mungu wa kweli na kumwabudu! Tangu tuwatembelee, Mashahidi sita wamewatembelea na kukaa kwa majuma matatu. Waliwasaidia kiroho watu 45 hivi ambao wanataka kikweli kumtumikia Yehova. Wote wanahudhuria mikutano kwa ukawaida.

Kuna jambo moja ambalo hatuwezi kusahau kutaja. Huko Los Arenales kuna duka moja tu dogo, na sigara haziuzwi tena kwenye duka hilo. Sababu ni kwamba watu wengi wanajifunza Biblia na wote wameacha kuvuta sigara na wameandikisha ndoa zao pia.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Melesio na mke wake, binti zake wanne, na mama-mkwe

[Picha katika ukurasa wa 25]

Funzo la Biblia na mkutano wa Kikristo huko Los Arenales

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 25]

Servicio Postal Mexicano, Correos de Mexico