Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Usijitenge Kamwe na Waamini Wenzako

Usijitenge Kamwe na Waamini Wenzako

Usijitenge Kamwe na Waamini Wenzako

“KWA miaka kumi, tulisisimuliwa na mambo yenye kuvutia katika ulimwengu wa biashara, na tulikuwa matajiri sana. Ingawa tulilelewa katika kweli, tulikuwa tumejitenga kabisa na Yehova na hatukuwa na nguvu za kiroho za kurudi,” anasema Jarosław na mke wake, Beata. *

Ndugu mwingine anayeitwa Marek, anakumbuka hivi: “Kwa sababu ya mabadiliko ya kijamii na kisiasa nchini Poland, nilipoteza kazi mara nyingi. Nilivunjika moyo. Niliogopa kuanzisha kampuni yangu mwenyewe kwa sababu sikuwa na uwezo au kipawa cha kufanya biashara. Mwishowe, nilishawishiwa kuanzisha kampuni yangu, huku nikifikiri kwamba jambo hilo lingenisaidia kutosheleza vizuri zaidi mahitaji ya kimwili ya familia yangu bila kupata matatizo yoyote ya kiroho. Baada ya muda, niligundua kwamba nilikuwa nimekosea kabisa.”

Katika ulimwengu ambamo gharama za maisha zinaendelea kupanda na ukosefu wa kazi unazidi kuongezeka, watu fulani wanakata tamaa na hivyo wanafanya maamuzi yasiyo ya hekima. Ndugu fulani wameamua kukubali kufanya kazi saa za ziada, kutafuta kazi zaidi ya moja, au kuanzisha biashara yao wenyewe hata ingawa hawana uzoefu wa kufanya hivyo. Wanafikiri kwamba mshahara huo wa ziada utasaidia familia na hawatapata madhara ya kiroho. Hata hivyo, matukio yasiyotazamiwa na hali ya uchumi ambayo inabadilika inaweza kuvuruga hata mipango iliyofanywa kwa nia nzuri. Matokeo ni kwamba wengine wamenaswa na mtego wa pupa na wamedhabihu mambo ya kiroho ili kufuatia vitu vya kimwili.—Mhu. 9:11, 12.

Ndugu na dada wengine wanafuatia sana mambo ya kilimwengu hivi kwamba hawana tena wakati wa funzo la kibinafsi, mikutano, au huduma. Ni wazi kwamba kupuuza mambo hayo kunaharibu hali yao ya kiroho na uhusiano wao pamoja na Yehova. Huenda pia wakapoteza uhusiano mwingine wa maana, yaani, uhusiano wao pamoja na ‘wale ambao katika imani ni jamaa zao.’ (Gal. 6:10) Wengine wanajitenga hatua kwa hatua kutoka katika undugu wa Kikristo. Fikiria kwa uzito jambo hilo.

Wajibu Wetu Kuelekea Waamini Wenzetu

Tukiwa ndugu na dada, tuna pindi nyingi za kuonyeshana upendo mwororo. (Rom. 13:8) Katika kutaniko lenu, inaelekea kwamba umewaona ‘watu wanaoteseka ambao wanalia ili wapewe msaada.’ (Ayu. 29:12) Huenda wengine hawawezi kutosheleza mahitaji yao ya msingi. Mtume Yohana alitukumbusha kuhusu nafasi tuliyo nayo ya kuwasaidia watu hao. “Yeyote aliye na riziki ya ulimwengu huu naye amwone ndugu yake akiwa na uhitaji na bado amfungie mlango wa huruma zake nyororo, ni katika njia gani kumpenda Mungu hukaa ndani yake?”—1 Yoh. 3:17.

Labda umewahi kutosheleza mahitaji ya watu kama hao na kuwasaidia wengine kwa ukarimu. Hata hivyo, hatupendezwi na undugu wetu kwa sababu tu tunataka kuwasaidia wengine kimwili. Huenda wengine wakalilia msaada kwa sababu wana upweke au wamevunjika moyo. Huenda wakahisi kwamba hawafai, wakateseka kwa sababu ya ugonjwa mbaya, au wamefiwa na mpendwa wao. Njia moja ambayo tunaweza kuwatia moyo ni kuwasikiliza na kuzungumza nao, na hivyo kujali mahitaji yao ya kihisia na ya kiroho. (1 The. 5:14) Mara nyingi kufanya hivyo kunatia nguvu zaidi kifungo cha upendo kati yetu na ndugu zetu.

Wachungaji wa kiroho wanaweza hasa kuwasikiliza kwa hisia-mwenzi, kuelewa hali yao, na kuwapa mashauri ya Kimaandiko yenye upendo. (Mdo. 20:28) Kwa njia hiyo waangalizi wanamwiga mtume Paulo, ambaye alikuwa na “upendo mwororo” kwa ajili ya ndugu na dada zake wa kiroho.—1 The. 2:7, 8.

Hata hivyo, Mkristo akijitenga na kundi, atatimiza jinsi gani wajibu wake kuelekea waamini wenzake? Hata waangalizi wanaweza kunaswa na kishawishi cha kufuatia vitu vya kimwili. Namna gani Mkristo akinaswa na kishawishi kama hicho?

Kulemewa na Mahangaiko ya Maisha

Kama tulivyoona, kufanya kazi kwa bidii ili kutosheleza mahitaji ya msingi ya familia mara nyingi kunasababisha mahangaiko na kunaweza kutufanya tupuuze mambo ya kiroho. (Mt. 13:22) Marek, aliyetajwa mwanzoni, anaeleza hivi: “Biashara yangu ilipoporomoka, niliamua kutafuta kazi yenye mshahara mnono katika nchi za nje. Nilienda huko kwa miezi mitatu tu, kisha nikaongeza miezi mingine mitatu, na kadhalika, na nilirudi nyumbani mara kwa mara. Mke wangu ambaye si mwamini aliteseka kihisia kwa sababu hiyo.”

Maisha ya familia na pia mambo mengine yaliharibika. Marek anaendelea kusema: “Nilifanya kazi kwa saa nyingi katika joto kali sana, na zaidi ya hayo, nilifanya kazi na watu waliotumia lugha chafu ambao walijitahidi kuwakandamiza wengine. Walitenda kama majambazi. Nilishuka moyo na kuhisi nimelemewa. Sikuwa hata na wakati wa kujitunza mwenyewe, nilianza kutilia shaka uwezo wangu wa kuwatumikia wengine.”

Matokeo yenye kuhuzunisha ya uamuzi wa Marek yanapaswa kutuchochea tutue na kufikiri. Hata ikiwa inaonekana kwamba kuhamia nchi za nje kutatatua matatizo ya kifedha, je, hakutasababisha matatizo mengine? Kwa mfano, hali ya kiroho na ya kihisia ya familia yetu itakuwa namna gani? Je, hatua hiyo ya kuhama itafanya tujitenge kabisa na kutaniko? Je, haitatunyima pendeleo la kuwahudumia waamini wenzetu?—1 Tim. 3:2-5.

Hata hivyo, huenda unatambua kwamba mtu anaweza kujishughulisha sana na kazi ya kimwili hata kama hafanyi kazi katika nchi nyingine. Mfikirie Jarosław na Beata. Jarosław anasema hivi: “Tulianza kwa unyoofu kabisa. Tukiwa wenzi wapya wa ndoa, tulifungua duka dogo katika eneo zuri ili kuuza soseji zinazotiwa katika mikate. Tulipata faida kubwa sana ambayo ilituchochea kupanua biashara yetu. Lakini hatukuwa na wakati wa kutosha, kwa hivyo tulikosa mikutano ya Kikristo. Baada ya muda mfupi, niliacha upainia na pia nikaacha kutumika nikiwa mtumishi wa huduma. Tulisisimuka sana kwa sababu ya faida kubwa ambayo tulikuwa tukipata hivi kwamba tulifungua duka kubwa tukishirikiana na mtu asiye mwamini. Baada ya muda, nilikuwa nikisafiri nchi za nje ili kutia sahihi mapatano ya kibiashara yenye thamani ya mamilioni ya dola. Kwa kawaida sikupatikana nyumbani, na uhusiano wangu na mke wangu na pia binti yangu uliharibika. Mwishowe, tulijishughulisha sana na biashara hiyo iliyokuwa ikisitawi hivi kwamba tuliacha kumtumikia Yehova hatua kwa hatua. Baada ya kujitenga na kutaniko, hatukuwafikiria hata kidogo ndugu zetu.”

Tunajifunza somo gani kutokana na jambo hilo? Tamaa ya kuwa na “paradiso” ya kibinafsi inaweza kumnasa Mkristo, na kumfanya awe na mtazamo wa kutojali, hata akipoteza “mavazi yake ya nje,” yaani, utambulisho wake wa Kikristo. (Ufu. 16:15) Jambo hilo linaweza kutufanya tujitenge kabisa na ndugu zetu ambao mwanzoni tulikuwa na nafasi ya kuwasaidia.

Jichunguze kwa Unyoofu

Huenda tukafikiri hivi: ‘Hilo haliwezi kunipata. Hata hivyo, ni vizuri sisi sote tufikirie kwa uzito ni vitu vingi kadiri gani tunavyohitaji kwa kweli katika maisha. Paulo aliandika hivi: “Hatukuleta chochote katika ulimwengu, wala hatuwezi kuchukua chochote nje. Kwa hiyo, tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Tim. 6:7, 8) Ni kweli kwamba kiwango cha maisha ni tofauti katika nchi mbalimbali. Vitu ambavyo huenda vinaonekana kuwa vya msingi katika nchi iliyoendelea vinaweza kuonwa kuwa vya starehe katika nchi nyingine nyingi.

Hata tuwe tunaishi katika eneo lenye kiwango gani cha maisha, fikiria maneno yafuatayo ya Paulo: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu.” (1 Tim. 6:9) Mtego unafichwa hivi kwamba mnyama anayewindwa hawezi kuuona. Unakusudiwa kunasa windo kwa ghafula. Tunaweza kuepuka jinsi gani kunaswa na mtego wa ‘tamaa zenye kudhuru’?

Kujua mambo ya kutanguliza kunaweza kutuchochea kutafuta wakati zaidi wa kufanya mambo ya Ufalme, kama vile funzo la kibinafsi. Kusali na kujifunza kibinafsi kunaweza kumsaidia Mkristo awe na “uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili” ili kuwasaidia wengine.—2 Tim. 2:15; 3:17.

Katika muda wa miaka michache, wazee wenye upendo walijitahidi kumjenga na kumtia moyo Jarosław. Alichochewa kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yake. Anasema hivi: “Pindi moja tulipokuwa na mazungumzo yenye kugusa moyo, wazee walitaja mfano wa Kimaandiko wa kijana mmoja tajiri ambaye alitaka kuishi milele lakini hakuwa tayari kuacha vitu vyake vya kimwili. Kisha wazee hao wakaniuliza kwa busara ikiwa habari hiyo inanihusu. Jambo hilo lilinifungua macho nikaona marekebisho niliyohitaji kufanya!”—Met. 11:28; Marko 10:17-22.

Jarosław alichunguza kwa unyoofu hali yake akaamua kuacha kujishughulisha na biashara kubwa. Katika muda wa miaka miwili, yeye na familia yake walirudia hali yao nzuri ya kiroho. Sasa anawatumikia ndugu zake akiwa mzee. Jarosław anasema hivi: “Ndugu wanapojishughulisha sana na mambo ya kibiashara na kupuuza hali yao ya kiroho, ninatumia mfano wangu kuwaonyesha kwamba si jambo la hekima kufungwa nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini. Si rahisi kushinda vishawishi vyenye kuvutia na kuepuka mazoea yasiyo ya unyoofu.”—2 Kor. 6:14.

Marek pia alijifunza somo fulani kwa njia ngumu. Ingawa alipata kazi yenye mshahara mnono katika nchi ya nje ambayo ilisaidia familia yake kifedha, uhusiano wake pamoja na Mungu na ndugu zake uliharibika. Baada ya muda, alibadili mambo ambayo alikuwa akitanguliza. “Kwa miaka mingi, hali yangu ilikuwa kama ya Baruku wa zamani ambaye ‘aliendelea kujitafutia makuu.’ Mwishowe, nilifunua moyo wangu, nikamwambia Yehova mahangaiko yangu, na sasa ninahisi kwamba nimepata tena usawaziko wa kiroho.” (Yer. 45:1-5) Sasa Marek anajitahidi kufikia “kazi njema” ya kuwa mwangalizi katika kutaniko.—1 Tim. 3:1.

Marek anawaonya hivi wale ambao huenda wanafikiria kwenda nchi za nje ili kutafuta kazi yenye mshahara mnono: “Ukiwa katika nchi ya nje, ni rahisi sana kuanguka katika mitego ya ulimwengu huu mwovu. Kutojua vizuri lugha ya wenyeji kunakuzuia kuwasiliana na wengine. Huenda ukarudi nyumbani ukiwa na pesa, lakini pia unapata vidonda vya kiroho ambavyo vinaweza kuchukua muda mrefu kupona.”

Kudumisha usawaziko kati ya kazi yetu ya kimwili na wajibu wetu kuelekea ndugu zetu kutatusaidia kumpendeza Yehova. Na tunaweza kuwawekea wengine mfano halisi ambao unaweza kuwachochea wafanye uamuzi wenye hekima. Wale ambao wamelemewa wanahitaji kutegemezwa, kuhurumiwa, na kuwekewa mfano mzuri na ndugu na dada zao. Wazee wa kutaniko na Wakristo wengine wakomavu wanaweza kuwasaidia waamini wenzao kudumisha usawaziko na kuepuka kulemewa na mahangaiko ya maisha.—Ebr. 13:7.

Ndiyo, tusijitenge kamwe na waamini wenzetu kwa kujishughulisha sana na kazi yetu ya kimwili. (Flp. 1:10) Badala yake, acheni tuwe ‘matajiri kwa Mungu’ tunapotanguliza mambo ya Ufalme katika maisha yetu.—Luka 12:21.

[Maelezo ya Chini]

^ Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Je, kazi yako ya kimwili inakuzuia kuhudhuria mikutano?

[Picha katika ukurasa wa 23]

Je, unathamini nafasi ulizo nazo za kuwasaidia ndugu na dada zako wa kiroho?