Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yesu Kristo Ni Nani Hasa?

Yesu Kristo Ni Nani Hasa?

Yesu Kristo Ni Nani Hasa?

“Basi alipoingia Yerusalemu, jiji lote likawa na msukosuko, na kusema: ‘Ni nani huyu?’ Umati ukawa ukisema: ‘Huyu ndiye nabii Yesu, kutoka Nazareti ya Galilaya!’”—MATHAYO 21:10, 11.

KWA nini kulikuwa na msukosuko wakati Yesu Kristo * alipowasili jijini Yerusalemu mwaka wa 33 W.K.? Watu wengi jijini walikuwa wamepata habari kumhusu Yesu na miujiza aliyofanya. Nao waliendelea kuwaeleza wengine kumhusu. (Yohana 12:17-19) Hata hivyo, watu hao hawakujua kwamba katikati yao kulikuwa na mtu ambaye angekuwa na uvutano mkubwa juu ya ulimwengu kwa muda mrefu hadi kufikia wakati wetu!

Fikiria mifano michache inayoonyesha kwamba Yesu amekuwa na uvutano mkubwa katika historia ya mwanadamu.

▪ Kalenda inayotumiwa sasa katika sehemu nyingi ulimwenguni inategemea mwaka ambao unawaziwa kuwa Yesu alizaliwa.

▪ Watu bilioni mbili hivi—karibu asilimia 33 ya idadi ya watu duniani—hujiita Wakristo.

▪ Dini ya Uislamu, iliyo na wafuasi zaidi ya bilioni moja duniani, hufundisha kuwa Yesu ni “nabii aliye mkuu zaidi kuliko Abrahamu, Noa, na Musa.”

▪ Semi nyingi zenye hekima zilizosemwa na Yesu sasa zinatumiwa katika njia mbalimbali na watu wengi. Kwa mfano:

‘Geuza shavu lile lingine.’—MATHAYO 5:39.

‘Msamaria mwema.’LUKA 10:33.

‘Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili.’—MATHAYO 6:24.

‘Kuna furaha zaidi katika kutoa.’MATENDO 20:35.

‘Watendee wengine yale ambayo ungependa wakutendee.’—MATHAYO 7:12.

‘Hesabu gharama.’LUKA 14:28.

Bila shaka, Yesu amekuwa na uvutano mkubwa juu ya wanadamu. Hata hivyo, watu wana imani na maoni tofauti-tofauti kumhusu. Hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Yesu Kristo ni nani hasa?’ Biblia pekee ndiyo inayotueleza alitoka wapi, aliishi jinsi gani, na kwa nini alikufa. Kujua ukweli huo kumhusu kunaweza kuwa na uvutano mkubwa katika maisha yako sasa na hata wakati ujao.

[Maelezo ya Chini]

^ “Yesu,” jina la nabii huyo kutoka Nazareti linamaanisha “Yehova Ni Wokovu.” Neno “Kristo” ni jina la cheo linalomaanisha “Mtiwa-Mafuta,” ambalo linaonyesha kuwa Yesu alitiwa mafuta, au kuwekwa na Mungu katika cheo cha pekee.