Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Baraba alitenda uhalifu wa aina gani?

Vitabu vyote vinne vya Injili vinamtaja Baraba mtu ambaye Pontio Pilato, mtawala Mroma, alimwachilia huru badala ya Yesu. Baraba anaitwa “mfungwa mwenye sifa mbaya” na pia “mnyang’anyi.” (Mathayo 27:16; Yohana 18:40) Waroma walikuwa wamemweka kizuizini huko Yerusalemu “pamoja na wachochezi, ambao katika uchochezi wao walikuwa wameua.”—Marko 15:7.

Ingawa hakuna uthibitisho kutoka katika vyanzo vya kilimwengu unaoeleza uhalifu ambao Baraba alitenda, ukweli wa kwamba anatajwa miongoni mwa wachochezi umefanya baadhi ya wasomi wamhusishe Baraba na vikundi vya wachochezi vilivyokuwapo nchini Israeli katika karne ya kwanza. Mwanahistoria Flavio Yosefo aliandika kwamba vikundi vya wahalifu vilihusika sana katika mapambano ya kijamii ya wakati huo; wahalifu hao walidai kuwa wanapigania haki ya Wayahudi wa hali ya chini waliokuwa wakikandamizwa. Uasi dhidi ya kile kilichoonwa kuwa ukandamizaji uliofanywa na Waroma na Wayahudi mashuhuri ulifikia upeo katikati ya karne ya kwanza W.K. Baadaye vikundi hivyo vya wahalifu vilifanyiza sehemu kubwa ya jeshi la Wayahudi lililowafukuza Waroma kutoka Yudea mwaka wa 66 W.K.

Kitabu The Anchor Bible Dictionary kinasema hivi: “Huenda Baraba alikuwa mshiriki wa kikundi kimoja kati ya vikundi fulani vya majambazi wa vijijini, ambavyo watu wa hali ya chini walivipenda sana kwa sababu viliwavamia watu matajiri huko Yerusalemu na kuuhangaisha utawala wa Roma.”

Katika nyakati za Waroma ni uhalifu gani ungefanya mtu auawe kama Yesu alivyouawa?

Waroma waliwaadhibu wachochezi, wahalifu, na waasi wengine kwa kuwafunga kwenye kifaa fulani cha kuwatesea watu na kuwaacha hapo wafe. Adhabu hiyo ilionwa kuwa njia mbaya zaidi ya kutekeleza hukumu ya kifo.

Kitabu Palestine in the Time of Jesus kinasema hivi kuhusu adhabu hiyo: “Ilitekelezwa hadharani nayo ilikuwa yenye kuaibisha, yenye maumivu makali, na ilikusudiwa kuwatisha watu waliojaribu kubadili utaratibu katika jamii.” Mwandishi mmoja Mroma wa nyakati za kale aliandika hivi kuhusu kuuawa kwa wahalifu: “Barabara yenye msongamano zaidi ndiyo iliyochaguliwa, mahali ambapo watu wengi wangeweza kushuhudia na hivyo kuingiwa na woga.”

Kulingana na Yosefo, mfungwa mmoja wa vita aliyekamatwa na majeshi ya Tito baada ya kuzingirwa kwa jiji la Yerusalemu mwaka wa 70 W.K. aliuawa kwa njia hiyo mbele ya kuta za jiji ili kujaribu kuwatisha walinzi wasalimu amri. Hatimaye jiji lilipoanguka, wengi waliuawa vivyo hivyo.

Mauaji makubwa zaidi kuwahi kutokea katika historia, ambayo yalitekelezwa kwa njia hiyo yalitokea mwishoni mwa uasi uliongozwa na Spartacus (73-71 K.W.K.), wakati ambapo watumwa na wapiganaji 6,000 waliuawa kando-kando ya barabara iliyotoka Capua hadi Roma.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kitabu “Give us Barabbas” cha Charles Muller, 1878