Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

NI NINI kilichomchochea shabiki wa muziki wa roki asiyependa kuchangamana na watu aanze kupenda watu na kujitahidi kuwasaidia? Ni nini kilimchochea mwanamume fulani nchini Mexico aache mwenendo mchafu kingono? Kwa nini bingwa wa mashindano ya kuendesha baiskeli nchini Japani aliacha mashindano hayo ili amtumikie Mungu? Hebu ona mambo ambayo watu hao wanasema.

“Nilikuwa Mjeuri, Mwenye Majivuno, na Mchokozi.”—DENNIS O’BEIRNE

MWAKA WA KUZALIWA: 1958

NCHI: UINGEREZA

HISTORIA: ALIKUWA SHABIKI WA MUZIKI WA ROKI ASIYEPENDA KUCHANGAMANA na WATU

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Watu wa familia ya baba yangu ni wazaliwa wa Ireland, na nilikuwa mfuasi wa Kanisa Katoliki la Ireland tangu nilipokuwa mdogo. Mara nyingi ilinibidi kwenda kanisani nikiwa peke yangu, ingawa sikupenda kufanya hivyo. Hata hivyo, nilikuwa na njaa ya kiroho. Nilikariri Sala ya Bwana kwa ukawaida, na ninakumbuka nikifikiria maana yake nikiwa kitandani usiku. Nilitafakari sehemu mbalimbali za sala hiyo na kujaribu kufahamu maana yake.

Nilipokuwa kijana, nilijiunga na kikundi cha Marastafari. Nilipendezwa pia na harakati za kisiasa kama zile za kikundi kilichopinga mfumo wa Wanazi. Hata hivyo, nilijihusisha zaidi na harakati za kikundi cha muziki wa roki chenye mtazamo wa uasi. Nilitumia dawa za kulevya hasa bangi, ambayo nilivuta karibu kila siku. Nilikuwa na mtazamo wa kutojali chochote na nilikunywa kupindukia. Pia nilifanya mambo yaliyohatarisha maisha yangu na sikuwajali wengine. Sikutaka kuchangamana na watu wala kuzungumza nao isipokuwa tu wakati nilipoona kuwa mazungumzo hayo ni muhimu. Hata nilikataa kupigwa picha. Ninapokumbuka hayo, ninaona kwamba nilikuwa mjeuri, mwenye majivuno, na mchokozi. Nilikuwa mwenye huruma na mkarimu tu kwa rafiki zangu.

Nilipokuwa na miaka 20 hivi, nilianza kupendezwa na Biblia. Rafiki yangu aliyekuwa muuzaji wa dawa za kulevya alikuwa ameanza kusoma Biblia akiwa gerezani, na tulizungumza kwa muda mrefu kuhusu dini, Kanisa, na kazi ya Shetani ulimwenguni. Nilinunua Biblia na kuanza kuisoma peke yangu. Mimi na rafiki yangu tulikuwa tukisoma sehemu fulani za Biblia, tunakutana pamoja kuzungumzia yale tuliyosoma, kisha tunafikia mkataa fulani. Tulifanya hivyo kwa miezi mingi.

Hii ni baadhi ya mikataa tuliyofikia baada ya usomaji wetu: kwamba tunaishi katika siku za mwisho za ulimwengu huu; kwamba Wakristo wanapaswa kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu; kwamba hawapaswi kuwa sehemu ya ulimwengu huu, kutia ndani siasa zake; na kwamba Biblia ina mwongozo mzuri wa maadili. Tuliona waziwazi kuwa Biblia ni ya kweli na kwamba lazima kuwe na dini ya kweli. Lakini dini gani? Tulifikiria dini zile kubwa-kubwa na kuona kuwa zinajihusisha na siasa na pia zina mbwembwe na shamrashamra nyingi katika ibada zao, mambo ambayo Yesu hakufanya. Tulitambua kuwa Mungu hatumii dini hizo, kwa hiyo tukaamua kuchunguza dini nyingine zisizo maarufu sana.

Tulikuwa tukikutana na wafuasi wa dini hizo na kuwauliza maswali kadhaa. Tulijua Biblia inasema nini kuhusu kila swali, kwa hiyo tungeweza kujua kwa urahisi kama majibu yao yalipatana na Neno la Mungu. Baada ya kukutana nao, nilikuwa nikisali kwa Mungu na kusema, ‘Ikiwa dini ya watu hao ni ya kweli, tafadhali nichochee niwe na hamu ya kukutana nao tena.’ Lakini baada ya kukutana na wafuasi wa dini hizo kwa miezi mingi, bado sikupata dini yoyote iliyojibu maswali yetu kwa kutumia Biblia; wala sikuwa na hamu ya kukutana nao tena.

Mwishowe, mimi na rafiki yangu tulikutana na Mashahidi wa Yehova. Tuliwauliza maswali yaleyale, lakini wao walitumia Biblia kutujibu. Yale waliyosema yalipatana kabisa na yale tuliyokuwa tumejifunza. Kwa hiyo, tukawauliza maswali ambayo hatukuwa tumepata majibu yake katika Biblia. Kwa mfano, tulitaka kujua maoni ya Mungu kuhusu kuvuta sigara na kutumia dawa za kulevya, na kwa mara nyingine tena, wakatumia Neno la Mungu kutujibu maswali hayo. Tulikubali kuhudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme.

Haikuwa rahisi kwangu kuhudhuria. Nilikuwa sipendi kabisa kuchangamana na watu, kwa hiyo sikutaka kukaribiwa na watu hao wote wenye urafiki na waliovalia vizuri. Nilikuwa na hakika kuwa baadhi yao walinikaribia wakiwa na nia mbaya, na sikutaka kwenda kwenye mikutano hiyo tena. Lakini kama kawaida yangu, nilimwomba Mungu ili anichochee niwe na hamu ya kukutana na watu hao tena ikiwa dini yao ndiyo ya kweli. Baada ya kusali, nilihisi nikiwa na hamu kubwa sana ya kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilijua kuwa lazima niache kutumia dawa za kulevya na haikuwa vigumu kufanya hivyo. Hata hivyo, ilikuwa vigumu sana kuacha kuvuta sigara. Nilijaribu mara kadhaa kuacha zoea hilo, lakini nikashindwa. Niliposikia kuhusu wengine ambao walitupa sigara zao na kuacha kabisa kuzivuta, nilisali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. Baada ya hapo, Yehova alinisaidia kuacha kuvuta sigara. Hivyo, nilijifunza umuhimu wa kuzungumza na Yehova waziwazi na kwa unyofu katika sala.

Pia, nilifanya badiliko lingine kubwa kuhusiana na mavazi na mapambo yangu. Nilipohudhuria mkutano mara ya kwanza kwenye Jumba la Ufalme, nywele zangu zilikuwa zimetengenezwa na kusimama kama miiba na zilikuwa na mstari uliopakwa rangi ya bluu. Baadaye, nilipaka sehemu hiyo rangi nyangavu ya machungwa. Nilivalia suruali ya jinzi na koti la ngozi lenye maandishi fulani. Sikuona uhitaji wa kufanya mabadiliko, hata ingawa Mashahidi walijaribu kunionyesha kwa fadhili sababu za kufanya hivyo. Hata hivyo, mwishowe nilifikiria andiko hili la 1 Yohana 2:15-17: “Msiwe mkiupenda ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu. Yeyote akiupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo ndani yake.” Kwa hiyo, nikaona kwamba kupitia sura yangu, nilionyesha kuwa niliupenda ulimwengu huu na kwamba ili nionyeshe upendo wangu kwa Mungu, ilikuwa lazima nibadilike. Na nilifanya hivyo.

Baadaye, nilitambua kuwa si Mashahidi tu waliotaka nihudhurie mikutano ya Kikristo. Niliona kwenye andiko la Waebrania 10:24, 25 kwamba Mungu alitaka nihudhurie mikutano. Nilipoanza kuhudhuria mikutano yote na kuwajua watu vizuri, niliamua kubatizwa ili kuonyesha kuwa nimejitoa kumtumikia Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nimechochewa sana na jinsi ambavyo Yehova huturuhusu tuwe na uhusiano wa karibu pamoja naye. Hangaiko na huruma zake zimenisukuma kumwiga na kufuata kielelezo cha Mwana wake, Yesu Kristo. (1 Petro 2:21) Nimejifunza kuwa ninaweza kusitawisha sifa za Kikristo na pia nidumishe utambulisho wangu. Nimejitahidi kusitawisha roho ya upendo na kuwajali wengine. Ninajitahidi kuwa kama Kristo kuhusiana na jinsi ninavyomtendea mke na mtoto wangu. Na ninawajali sana Wakristo wenzangu. Kumfuata Kristo kumefanya niheshimike, nijiheshimu, na kuwapenda wengine.

“Walinionyesha Heshima.”—GUADALUPE VILLARREAL

MWAKA WA KUZALIWA: 1964

NCHI: MEXICO

HISTORIA: ALIKUWA NA MWENENDO MCHAFU KINGONO

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Mimi ni mmoja kati ya watoto saba, na tulilelewa jijini Hermosillo, katika jimbo la Sonora, Mexico, eneo lenye umaskini mkubwa. Baba yetu alikufa nilipokuwa mvulana mdogo, hivyo mama yetu alilazimika kufanya kazi ili kututegemeza. Mara nyingi nilitembea bila viatu kwa sababu hatukuwa na pesa za kununulia viatu. Nikiwa bado mdogo, nilianza kufanya kazi ili nisaidie kulipia gharama za familia. Kama familia nyingine nyingi, tulijazana katika nyumba ndogo.

Kwa kawaida mama yetu hakuwa nyumbani siku nzima ili kutulinda sisi watoto. Nilipokuwa na miaka 6, nilianza kutendewa vibaya kingono na mvulana mwenye miaka 15. Aliendelea kunitendea hivyo kwa muda mrefu. Kwa hiyo, nilichanganyikiwa sana kuhusu ngono. Nilifikiri ni jambo la kawaida kuvutiwa na wanaume. Nilipotafuta msaada wa madaktari au makasisi, walinihakikishia kwamba sina tatizo lolote na kwamba hisia zangu ni za kawaida.

Nilipokuwa na miaka 14, niliamua kujitambulisha kuwa shoga (mwanamume anayefanya ngono na wanaume). Niliendelea na maisha yangu ya ushoga kwa miaka 11 iliyofuata, na hata niliishi na wanaume tofauti-tofauti katika kipindi hicho. Mwishowe nilijifunza kazi ya kutengeneza watu nywele na nikafungua saluni yangu. Hata hivyo, sikuwa na furaha. Niliteseka maishani mwangu, huku nikihisi kwamba nilisalitiwa. Nilijua kwamba mambo niliyokuwa nikifanya si sawa. Nilianza kujiuliza, ‘Je, kuna watu wema na waungwana?’

Nilimkumbuka dada yangu. Alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na hatimaye akabatizwa. Alikuwa akinieleza mambo aliyokuwa akijifunza, lakini sikumsikiliza. Hata hivyo, nilivutiwa na maisha yake na ndoa yake. Niliona kuwa yeye na mume wake walipendana na kuheshimiana kikweli, na walitendeana kwa huruma. Baada ya muda, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alianza kujifunza Biblia pamoja nami. Mwanzoni, sikupendezwa sana na kujifunza. Lakini baadaye mambo yalibadilika.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Mashahidi walinialika kwenye mkutano wao mmoja, nami nikaenda. Kwenye mkutano huo, hali ilikuwa tofauti kabisa. Watu kwa ujumla walinidhihaki lakini Mashahidi hawakufanya hivyo. Walinisalimu kwa fadhili na kunionyesha heshima. Niliguswa moyo sana.

Nilivutiwa zaidi na Mashahidi nilipohudhuria kusanyiko. Niliona kwamba hata wakiwa katika vikundi vikubwa, Mashahidi walijiendesha kama dada yangu tu—walikuwa wanyofu. Nilijiuliza ikiwa labda hawa ndio watu wema na waungwana ambao nimekuwa nikiwatafuta kwa muda mrefu. Upendo na umoja wao ulinishangaza. Pia nilishangazwa na jinsi walivyotumia Biblia kujibu kila swali. Nilitambua kwamba Biblia ndiyo inayowasaidia kuwa na sifa nzuri. Pia, nilitambua kwamba nilipaswa kufanya mabadiliko mengi ili kuwa mmoja wao.

Kwa kweli, nilihitaji kubadilika kabisa kwa kuwa niliishi kama mwanamke. Nilihitaji kubadili jinsi nilivyoongea, tabia zangu, mavazi na mtindo wangu wa nywele, na pia watu niliowachagua kuwa rafiki zangu. Rafiki hao wa zamani walianza kunidhihaki wakisema: “Kwa nini unafanya hivyo? Ulikuwa sawa jinsi ulivyokuwa. Acha kujifunza Biblia. Una kila kitu.” Lakini haikuwa rahisi hata kidogo kwangu kuacha mazoea machafu kingono.

Hata hivyo, nilijua kuwa ningeweza kufanya mabadiliko makubwa, kwa kuwa andiko hili la 1 Wakorintho 6:9-11 lilinigusa moyo: “Kwani! Je, hamjui kwamba watu wasio waadilifu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msipotoshwe. Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume wanaolala na wanaume . . . hawataurithi ufalme wa Mungu. Na bado wengine wenu mlikuwa hivyo. Lakini mmeoshwa mkawa safi.” Yehova aliwasaidia watu wa nyakati hizo kufanya mabadiliko, na alinisaidia pia. Niling’ang’ana kwa miaka kadhaa kuacha mazoea hayo, lakini upendo na mwongozo wa Mashahidi ulinisaidia sana.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Leo, mimi ninaishi maisha ya kawaida. Nimeoa, na mimi na mke wangu tunamfundisha mtoto wetu kufuata kanuni za Biblia. Nimeacha kabisa mazoea yangu ya zamani, na ninafurahia manufaa na mapendeleo mengi ya kiroho. Mimi ni mzee wa kutaniko, na nimeweza kuwasaidia wengine kujifunza kweli ya Neno la Mungu. Mabadiliko niliyofanya maishani mwangu yalimfurahisha sana mama yangu hivi kwamba alikubali kujifunza Biblia na sasa yeye ni Mkristo aliyebatizwa. Dada yangu aliyeishi maisha machafu kingono pia amekuwa Shahidi wa Yehova.

Hata baadhi ya watu waliojua maisha yangu ya zamani sasa wanatambua kwamba nimefanya mabadiliko na kuwa mtu bora. Na ninajua kilichonichochea kufanya mabadiliko hayo. Zamani nilitafuta msaada wa wataalamu, lakini nikapata mashauri mabaya. Hata hivyo, Yehova alinisaidia kwelikweli. Ingawa nilijihisi kuwa sifai, alinijali na kunionyesha upendo na subira. Niliguswa moyo sana kujua kuwa Mungu kama huyo mwenye hekima, upendo, na mwema, alinijali na alitaka niwe na maisha bora.

“Nilikuwa Mpweke, na Nilikosa Uradhi na Kusudi Maishani.”—KAZUHIRO KUNIMOCHI

MWAKA WA KUZALIWA: 1951

NCHI: JAPANI

HISTORIA: ALIPENDA SANA MASHINDANO YA KUENDESHA BAISKELI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika mji wenye bandari usio na shughuli nyingi katika Wilaya ya Shizuoka, nchini Japani. Familia yetu ya watu wanane iliishi katika nyumba ndogo. Baba yetu alikuwa na duka la baiskeli. Tangu nilipokuwa mdogo, alikuwa akinipeleka kwenye mashindano ya kuendesha baiskeli na akafanya nipendezwe na mchezo huo. Kisha, akaanza kunitayarisha kuwa mwendeshaji wa baiskeli wa kulipwa. Nilipokuwa katika shule ya msingi, alianza kunizoeza kwa bidii. Katika shule ya sekondari, nilishinda mataji matatu katika mashindano ya kitaifa ya kila mwaka. Nilikataa mwaliko wa kujiunga na chuo kikuu, na badala yake nikajiunga na shule ya kuzoeza washiriki wa mashindano ya kuendesha baiskeli. Nilipokuwa na miaka 19, nikawa mmoja wa waendeshaji wa baiskeli wa kulipwa.

Kufikia wakati huo, lengo langu maishani lilikuwa kuwa mwendeshaji wa baiskeli bora zaidi nchini Japani. Nilipanga kuchuma pesa nyingi ili familia yetu iwe na maisha salama na matulivu. Nilianza kufanya mazoezi kwa bidii sana. Nilipojihisi ninalemewa na mazoezi makali au sehemu fulani ya mashindano iliyokuwa ngumu, ningejikumbusha tena na tena kwamba nilizaliwa niwe mshiriki wa mashindano ya kuendesha baiskeli na ilinipasa kuendelea na mazoezi tu! Nilifanya hivyo, na bidii yangu ikaanza kuzaa matunda. Katika mwaka wangu wa kwanza, nilishinda mashindano ya wanafunzi wapya. Katika mwaka wangu wa pili, nilifanikiwa kushiriki katika mashindano yanayoamua mwendeshaji wa baiskeli aliye bora zaidi nchini Japani. Nilikuwa wa pili katika mashindano sita niliyoshiriki.

Niliendelea kuwa mmoja kati ya washindani bora, na nikaanza kuitwa miguu yenye nguvu ya Tokai, eneo fulani la Japani. Nilipenda sana kushindana. Baada ya muda, nilianza kuogopwa kwa kuwa sikuwajali wengine katika mashindano. Pesa ziliongezeka na ningeweza kununua chochote nilichotaka. Nilinunua nyumba yenye chumba cha mazoezi kilichokuwa na vifaa bora sana. Pia nilinunua gari kutoka ng’ambo ambalo bei yake ilikuwa karibu sawa na bei ya nyumba. Ili niwe salama kifedha, niliingia katika biashara ya kununua na kuuza hisa na nyumba.

Hata hivyo, bado nilikuwa mpweke, na nilikosa uradhi na kusudi maishani. Kufikia wakati huo nilikuwa na mke na watoto watatu, lakini mara nyingi nilikosa subira niliposhughulika na familia yangu. Nilikuwa nikiwakasirikia mke na watoto wangu kuhusu mambo madogo-madogo. Kwa hiyo, walianza kuchunguza uso wangu kwa wasiwasi ili kuona kama nimekasirika.

Hata hivyo, baadaye mke wangu alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Jambo hilo lilileta mabadiliko mengi. Alisema kuwa alitaka kuhudhuria mikutano ya Mashahidi, hivyo nikaamua tuhudhurie sote tukiwa familia. Bado ninakumbuka usiku ambapo mzee fulani wa kutaniko alinitembelea nyumbani kwangu na kuanza kujifunza Biblia pamoja nami. Mambo niliyojifunza yalinigusa moyo sana.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Sitasahau jinsi andiko la Waefeso 5:5 lilivyonigusa moyo. Linasema: “Hakuna mwasherati au mtu asiye safi au mtu mwenye pupa—maana yake ni kuwa mwabudu-sanamu—aliye na urithi wowote katika ufalme wa Kristo na wa Mungu.” Niliona kuwa mashindano ya kuendesha baiskeli yalihusisha kucheza kamari na kwamba yalimchochea mtu kuwa na pupa. Dhamiri yangu ilianza kunisumbua. Nilihisi kuwa ikiwa nilitaka kumpendeza Yehova Mungu, nilihitaji kuacha mashindano hayo. Lakini huo ulikuwa uamuzi mgumu sana kwangu.

Nilikuwa nimemaliza tu mwaka niliokuwa nimefanikiwa zaidi, na nilitamani kupata mafanikio zaidi. Hata hivyo, niliona kwamba kujifunza Biblia kuliniletea amani na utulivu wa akili—hali tofauti kabisa na roho niliyohitaji kusitawisha ili kushinda! Nilishiriki mashindano mara tatu tu baada ya kuanza kujifunza, lakini katika moyo wangu sikuwa nimeamua kabisa kuacha mashindano hayo. Pia sikujua jinsi ambavyo ningeitegemeza familia yangu. Nilihisi nimekwama—singeweza kusonga mbele wala kurudi nyumba, nao watu wangu wa ukoo wakaanza kunipinga kwa sababu ya imani yangu mpya. Baba yangu alikata tamaa sana. Sikujua la kufanya, hivyo nikawa na mfadhaiko mkubwa na hata nikapatwa na kidonda cha tumbo.

Kilichonisaidia kuvumilia wakati huo mgumu ni kwamba niliendelea kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, na hatua kwa hatua, imani yangu ikaimarika. Nilimwomba Yehova asikilize sala zangu na kunisaidia kuona kuwa anasikiliza. Mfadhaiko wangu ulipungua zaidi pale mke wangu aliponihakikishia kwamba haikuwa lazima aishi katika nyumba kubwa ili kuwa na furaha. Hivyo, pole kwa pole nikafanya maendeleo ya kiroho.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nilitambua kwamba maneno ya Yesu katika Mathayo 6:33 ni ya kweli kabisa. Alisema: “Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” Hatujawahi kukosa “vitu vingine” ambavyo Yesu alirejelea, yaani, mahitaji muhimu maishani. Ingawa mapato yangu sasa ni kidogo yakilinganishwa na wakati nilipokuwa nikishiriki katika mashindano ya kuendesha baiskeli, mimi na familia yangu hatujapungukiwa na chochote katika miaka 20 iliyopita.

Isitoshe, ninapofanya kazi au kuabudu pamoja na waamini wenzangu, ninapata furaha na uradhi ambao sijawahi kupata. Siku zinapita tu. Hali katika familia yangu imekuwa nzuri sana. Watoto wangu watatu pamoja na wake zao wamekuwa watumishi waaminifu wa Yehova.