Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Gehena Ni Mahali pa Moto wa Mateso?

Je, Gehena Ni Mahali pa Moto wa Mateso?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Gehena Ni Mahali pa Moto wa Mateso?

▪ Katika masimulizi ya vitabu vya Injili, Yesu anawaonya wanafunzi wake kuhusu hukumu ya Gehena. Ni wazi kuwa Yesu alitaka onyo hilo lichukuliwe kwa uzito. Hata hivyo, je, Yesu alikuwa akirejelea mahali penye moto ambapo watu wanateswa milele?—Mathayo 5:22.

Kwanza, na tuchunguze neno Gehena. Neno la Kigiriki Geʹen·na linalingana na neno la Kiebrania geh Hin·nomʹ, linalomaanisha “bonde la Hinomu,” au kwa jina kamili geh veneh-Hin·nomʹ, “bonde la wana wa Hinomu.” (Yoshua 15:8; 2 Wafalme 23:10) Eneo hilo ambalo leo linaitwa Wadi er-Rababi, ni bonde jembamba lenye kina kirefu, lililo upande wa kusini na kusini-magharibi mwa Yerusalemu.

Katika siku za wafalme wa Yuda, kuanzia karne ya nane K.W.K., eneo hilo lilitumiwa kwa ibada za kipagani, kutia ndani kuwatoa watoto kama dhabihu kwa kuwateketeza motoni. (2 Mambo ya Nyakati 28:1-3; 33:1-6) Nabii Yeremia alitabiri kuwa bonde hilo lingekuwa mahali ambapo Wababiloni wangewaua Wayudea, hiyo ikiwa hukumu kutoka kwa Mungu kwa sababu ya uovu wao. *Yeremia 7:30-33; 19:6, 7.

Kulingana na msomi Myahudi David Kimhi (m. 1160-m. 1235 W.K.), baadaye bonde hilo liligeuzwa kuwa mahali ambapo wakaaji wa jiji la Yerusalemu walitupa takataka. Moto katika bonde hilo uliwaka wakati wote na ulitumiwa kuteketeza takataka hizo. Chochote kilichotupwa humo kiliteketea kabisa na kuwa majivu.

Watafsiri wengi wa Biblia wameamua wenyewe tu kutafsiri neno Geʹen·na kuwa “motoni.” (Mathayo 5:22, Habari Njema kwa Watu Wote) Kwa nini? Kwa sababu walihusianisha imani ya kipagani kuwa waovu hupatwa na hukumu ya moto baada ya kifo, na moto halisi uliokuwa kwenye lile bonde la kuteketezea takataka, nje ya jiji la Yerusalemu. Hata hivyo, Yesu hakuhusianisha Gehena na mateso.

Yesu alijua kuwa wazo la kuwateketeza watu wakiwa hai linamchukiza Baba yake wa mbinguni, Yehova. Kuhusu matumizi ya Gehena katika siku za nabii Yeremia, Mungu alisema: “Wamejenga mahali pa juu pa Tofethi, palipo katika bonde la mwana wa Hinomu, ili kuwateketeza wana wao na binti zao katika moto, jambo ambalo sikuamuru wala halikuingia moyoni mwangu.” (Yeremia 7:31) Isitoshe, wazo la kutesa wafu linapingana na sifa ya Mungu ya upendo na pia fundisho la Biblia lililo wazi kuwa wafu “hawajui lolote kamwe.”—Mhubiri 9:5, 10.

Yesu alitumia neno “Gehena” kuonyesha uharibifu wa milele utakaotokana na hukumu kali ya Mungu. Hivyo, neno “Gehena” lina maana sawa na “ziwa la moto,” linalotajwa katika kitabu cha Ufunuo. Maneno Gehena na ziwa la moto yanafananisha uharibifu wa milele, bila tumaini la ufufuo.—Luka 12:4, 5; Ufunuo 20:14, 15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kitabu kimoja cha marejeo (New Catholic Encyclopedia) kinasema hivi kuhusu unabii huo: “Wakati wa kuharibiwa kwa Yerusalemu, wakaaji wake wengi wangeuawa na maiti zao kutupwa, bila kuzikwa, kwenye bonde ili zioze au ziteketee.”