Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kuchukua kwa Uzito Wote Utumishi Wetu kwa Yehova

Kuchukua kwa Uzito Wote Utumishi Wetu kwa Yehova

Kuchukua kwa Uzito Wote Utumishi Wetu kwa Yehova

“Mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, . . . endeleeni kuyafikiria mambo hayo.”—FLP. 4:8.

1, 2. Ni nini ambacho kimefanya watu wengi katika ulimwengu huu watafute kwanza raha maishani, na hilo linatokeza maswali au maulizo gani?

 TUNAISHI katika ulimwengu ulio na hali ngumu sana na zenye kuhuzunisha zaidi katika historia yote ya wanadamu. Ni vigumu sana kwa watu ambao hawana uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kuvumilia ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.’ (2 Tim. 3:1-5) Watu hao wanapambana na matatizo ya kila siku kwa kutegemea uwezo wao wenyewe, na mara nyingi hawapati suluhisho kamili. Ili kujaribu kuepuka kuwa na mahangaiko yanayopita kiasi ya maisha, watu wengi wanatafuta daima vitumbuizo vingi vipya vyenye kufurahisha.

2 Ili kupambana na mikazo ya maisha, mara nyingi watu wanajitahidi kutosheleza kwanza tamaa yao ya kupata raha. Wakristo wasipokuwa waangalifu wanaweza kwa urahisi kuanza kufuatia maisha ya aina hiyo. Tunaweza kuepuka jinsi gani mtego huo? Je, ni kwa kuepuka kabisa kujifurahisha au vitumbuizo? Tunaweza jinsi gani kuwa na usawaziko katika kujifurahisha na kutimiza madaraka yetu? Ni kanuni gani za Kimaandiko ambazo zinapaswa kutuongoza ili tuchukue kwa uzito mambo ya maana maishani na vilevile kuwa na wakati wa kujifurahisha?

Kuchukua Mambo kwa Uzito Katika Ulimwengu Unaopenda Raha

3, 4. Maandiko yanatusaidia jinsi gani kutambua umuhimu wa kuchukua mambo kwa uzito?

3 Ni wazi kwamba ulimwengu huu unakazia sana ‘kupenda raha.’ (2 Tim. 3:4) Hali hiyo ya kukazia sana raha na kujifurahisha inaweza kuhatarisha hali yetu ya kiroho. (Met. 21:17) Kwa hiyo, mtume Paulo alipoandika barua zake kwa Timotheo na Tito alikuwa na sababu nzuri za kutia ndani mashauri kuhusu kuchukua mambo kwa uzito. Kufuata mashauri hayo kutatusaidia kuepuka mtazamo wa ulimwengu wa kufuatia sana raha maishani.—Soma 1 Timotheo 2:1, 2; Tito 2:2-8.

4 Karne nyingi mapema, Sulemani aliandika kuhusu umuhimu wa kujinyima raha nyakati nyingine ili tuchukue kwa uzito mambo ya maana zaidi maishani. (Mhu. 3:4; 7:2-4) Kwa kweli, kwa sababu maisha ni mafupi sana, tunahitaji ‘kujitahidi sana’ ili tupate wokovu. (Luka 13:24) Hivyo, tunahitaji kuendelea kufikiria mambo yote ambayo ni ya “hangaiko zito.” (Flp. 4:8, 9) Hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kukazia sana uangalifu kila sehemu ya maisha ya Kikristo.

5. Ni jambo gani ambalo tunapaswa kuchukua kwa uzito katika maisha?

5 Kwa mfano, Wakristo wanamwiga Yehova na Yesu kwa kuchukua kwa uzito daraka lao la kufanya kazi kwa bidii. (Yoh. 5:17) Mara nyingi Wakristo hao wanasifiwa kwa sababu wana mazoea mazuri ya kufanya kazi na wanategemeka. Vichwa vya familia hasa wanajitahidi sana kufanya kazi kwa bidii ili kutegemeza familia zao. Kwa kweli, mtu asiyewaandalia mahitaji washiriki wa nyumba yake ni sawa na mtu ambaye “ameikana imani,” yaani, amemkana Yehova!—1 Tim. 5:8.

Kuichukua Ibada Yetu kwa Uzito Lakini kwa Shangwe

6. Tunajua jinsi gani kwamba tunapaswa kuchukua kwa uzito ibada yetu kwa Yehova?

6 Yehova hajawahi kamwe kuchukua ibada ya kweli kimchezo-mchezo. Kwa mfano, chini ya Sheria ya Musa, Waisraeli walipata matokeo mabaya sana walipoacha kumwabudu Yehova. (Yos. 23:12, 13) Katika karne ya kwanza W.K., wafuasi wa Kristo walihitaji kupambana kabisa ili kuzuia ibada ya kweli isichafuliwe na mitazamo na mafundisho mapotovu. (2 Yoh. 7-11; Ufu. 2:14-16) Leo, Wakristo wa kweli wanaendelea kuchukua kwa uzito ibada yao.—1 Tim. 6:20.

7. Paulo alijitayarisha jinsi gani kwa ajili ya huduma yake?

7 Huduma yetu ya shambani inatuletea shangwe. Hata hivyo, ili kuendelea kupata shangwe katika huduma, tunahitaji kuifikiria kwa uzito huduma hiyo na kujitayarisha mapema. Paulo alieleza jinsi alivyowahangaikia watu aliowafundisha. Aliandika hivi: “Nimekuwa mambo yote kwa watu wa namna zote, ili kwa vyovyote niwaokoe wengine. Lakini ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki hiyo pamoja na wengine.” (1 Kor. 9:22, 23) Paulo alifurahia kuwasaidia watu kiroho, naye alifikiria kwa uzito jinsi ambavyo angetimiza mahitaji hususa ya watu aliowahubiria. Kwa hiyo, alifanikiwa kuwatia moyo na kuwachochea wamwabudu Yehova.

8. (a) Tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuelekea watu ambao tunawafundisha katika huduma yetu? (b) Kuongoza funzo la Biblia kunaweza kutusaidia jinsi gani kupata shangwe zaidi katika huduma?

8 Paulo alichukua huduma yake kwa uzito jinsi gani? Alikuwa tayari ‘kumtumikia’ Yehova na pia wale ambao wangesikiliza ujumbe wa kweli. (Rom. 12:11; 1 Kor. 9:19) Tunapokubali daraka la kuwafundisha watu Neno la Mungu, iwe katika funzo la Biblia la nyumbani, kwenye mkutano wa Kikristo, au katika Ibada ya Familia, je, tunatambua kwamba tuna daraka kuelekea wale ambao tunawafundisha? Labda tunaona kwamba kuongoza funzo la kawaida la Biblia ni mzigo mzito sana kwetu kubeba. Ni kweli kwamba kwa kawaida ili kufanya hivyo tunahitaji kutenga wakati ambao tulitumia kufanya mambo yetu wenyewe na kuutumia wakati huo kuwasaidia wengine. Lakini je, si ni kweli kwamba jambo hilo linapatana na maneno ya Yesu ya kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea”? (Mdo. 20:35) Tukiwafundisha wengine njia ya kupata wokovu sisi wenyewe tutapata furaha ambayo hatuwezi kupata katika utendaji mwingine wowote.

9, 10. (a) Je, kuchukua mambo kwa uzito kunamaanisha kwamba hatuwezi kustarehe na kujifurahisha pamoja na watu? Eleza. (b) Ni nini ambacho kitamsaidia mzee kuwa mwenye kutia moyo na rahisi kufikiwa?

9 Kuchukua mambo kwa uzito hakumaanishi kwamba hatuwezi kuwa na wakati wa kustarehe na kujifurahisha pamoja na watu. Yesu aliweka mfano mkamilifu katika kutenga wakati si wa kufundisha tu bali pia wa kustarehe na kujenga mahusiano mazuri pamoja na wengine. (Luka 5:27-29; Yoh. 12:1, 2) Pia, kuchukua mambo kwa uzito hakumaanishi kwamba tunapaswa sikuzote kuonekana kuwa wakali. Kama Yesu angekuwa mtu mkali, ambaye si mwenye urafiki hata kidogo, bila shaka watu hawangevutiwa kumkaribia. Hata watoto walistarehe walipokuwa pamoja naye. (Marko 10:13-16) Tunaweza kuiga usawaziko wa Yesu jinsi gani?

10 Ndugu mmoja alisema hivi kuhusu mzee fulani wa kutaniko, “Anajiwekea kiwango cha juu sana lakini hatazamii kamwe ukamilifu kutoka kwa wengine.” Je, inaweza kusemwa hivyo kukuhusu wewe? Ni jambo linalofaa kuwa na kiasi kuhusu mambo ambayo tunatazamia wengine wafanye. Kwa mfano, watoto wanafanya vyema wazazi wao wanapowawekea viwango wanavyoweza kufikia na kuwasaidia kuvifikia. Vivyo hivyo, wazee wanaweza kumtia moyo kila mtu katika kutaniko na kumpa mapendekezo yaliyo wazi kuhusu mambo anayopaswa kufanya ili akomae kiroho. Zaidi ya hayo, mzee akiwa na maoni yenye usawaziko kujihusu yeye mwenyewe, atakuwa mchangamfu na mwenye kuburudisha. (Rom. 12:3) Dada mmoja alisema hivi: “Sitaki mzee achukue kila jambo kama mzaha. Lakini ikiwa kila wakati anaonekana kuwa mkali, ni vigumu kumfikia.” Dada mwingine alisema kwamba anaona wazee fulani “wanaogopesha kwa sababu wanaonekana kuwa wakali kupita kiasi.” Wazee hawangetaka kamwe kupunguza shangwe ambayo waamini wote wanapaswa kuwa nayo wanapomwabudu Yehova, ambaye ni “Mungu mwenye furaha.”—1 Tim. 1:11.

Kutimiza Madaraka Katika Kutaniko

11. ‘Kujitahidi kufikia’ mapendeleo katika kutaniko kunamaanisha nini?

11 Paulo alipowatia moyo wanaume katika kutaniko wajitahidi kustahili kupata mapendeleo makubwa zaidi, kusudi lake halikuwa kumtia moyo mtu yeyote ajitafutie makuu. Badala yake, aliandika hivi: “Ikiwa mwanamume yeyote anajitahidi kufikia cheo cha mwangalizi, yeye anatamani kazi njema.” (1 Tim. 3:1, 4) Ili wanaume Wakristo ‘wajitahidi kufikia’ mapendeleo wanahitaji kusitawisha tamaa kubwa ya kuwa na bidii ya kukuza sifa za kiroho zinazohitajiwa ili kuwatumikia ndugu zao. Ikiwa mwaka mmoja hivi umepita tangu ndugu abatizwe na anatimiza kwa kadiri inayofaa sifa za Kimaandiko za kustahili kuwa mtumishi wa huduma ambazo zimeonyeshwa katika 1 Timotheo 3:8-13, anaweza kupendekezwa ili awekwe rasmi. Ona kwamba mstari wa 8 unasema hivi waziwazi: “Vivyo hivyo watumishi wa huduma wanapaswa kuwa wenye kuchukua mambo kwa uzito.”

12, 13. Eleza njia ambazo ndugu vijana wanaweza kujitahidi kufikia mapendeleo.

12 Je, wewe ni ndugu aliyebatizwa ambaye anachukua mambo kwa uzito na aliye katika miaka ya mwisho ya utineja? Kuna njia nyingi ambazo unaweza kujitahidi kufikia mapendeleo katika kutaniko. Njia moja ni kuboresha utendaji wako katika huduma ya shambani. Je, unafurahi kuhubiri pamoja na ndugu wenye umri mbalimbali katika utumishi wa shambani? Je, unajitahidi kutafuta mtu ambaye unaweza kujifunza naye Biblia? Ukiongoza funzo la Biblia kulingana na mapendekezo yanayotolewa katika mikutano ya Kikristo, utaboresha uwezo wako wa kufundisha. Zaidi ya hayo, utajifunza kumwonyesha hisia-mwenzi mtu ambaye anajifunza njia za Yehova. Mwanafunzi wako anapoanza kuona uhitaji wa kufanya mabadiliko, utajifunza kumsaidia kwa subira na busara kutumia kanuni za Biblia.

13 Ninyi ndugu vijana mnaweza kujitolea kuwasaidia kwa njia yoyote inayowezekana ndugu wenye umri mkubwa zaidi katika kutaniko. Mnaweza pia kupendezwa na hali ya Jumba la Ufalme, na kusaidia kulisafisha na kulitunza. Mnapojitolea kusaidia kwa njia yoyote ile mnayoweza, roho yenu ya kujitolea inaonyesha kwamba mnachukua huduma yenu kwa uzito. Kama Timotheo, mnaweza kujifunza kujali kwa unyoofu mahitaji ya kutaniko.—Soma Wafilipi 2:19-22.

14. Ndugu vijana wanaweza ‘kujaribiwa juu ya kufaa’ jinsi gani ili watumike katika kutaniko?

14 Enyi wazee, muwe tayari kuwapa migawo ndugu vijana ambao wanajitahidi ‘kukimbia tamaa zinazotukia ujanani’ na ambao wanafuatilia “uadilifu, imani, upendo, amani,” pamoja na sifa nyingine nzuri. (2 Tim. 2:22) Kwa kuwapa vijana migawo katika kutaniko wanaweza ‘kujaribiwa juu ya kufaa’ kubeba madaraka, ili ‘maendeleo yao yawe wazi kwa watu wote.’—1 Tim. 3:10; 4:15.

Kuchukua Mambo kwa Uzito Katika Kutaniko na Katika Familia

15. Kulingana na andiko la 1 Timotheo 5:1, 2, tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunawachukua wengine kwa uzito?

15 Kuchukua mambo kwa uzito kunatia ndani kuwaheshimu ndugu na dada zetu. Paulo alitaja uhitaji wa kuwatendea wengine kwa heshima katika shauri ambalo alimpa Timotheo. (Soma 1 Timotheo 5:1, 2.) Hilo ni jambo la maana hasa tunaposhughulika na watu wa jinsia tofauti. Mfano wa Ayubu katika kuwaheshimu wanawake, hasa mwenzi wake wa ndoa, unastahili kuigwa. Alijitahidi kabisa kutomtazama mwanamke mwingine kwa kumtamani. (Ayu. 31:1) Kuwachukua ndugu na dada zetu kwa uzito kunamaanisha kuepuka kuwachezea kimapenzi au kufanya jambo lolote ambalo linaweza kumfanya ndugu au dada asifurahie kuwa karibu nasi. Kuwaheshimu wengine ni jambo la maana hasa wakati watu wawili wanapositawisha uhusiano wa kimapenzi kwa kusudi la kufunga ndoa. Mkristo anayechukua mambo kwa uzito hawezi kamwe kuchezea hisia za mtu wa jinsia tofauti.—Met. 12:22.

16. Eleza tofauti iliyopo kati ya maoni ya watu fulani katika ulimwengu kuhusu daraka la mume na baba na maelezo ya Biblia kuhusu daraka lake.

16 Tunahitaji pia kuwa waangalifu ili tuendelee kuchukua kwa uzito madaraka ambayo tumepewa na Mungu katika familia. Ulimwengu wa Shetani unadhihaki daraka la mume na baba. Michezo ya watumbuizaji au wachekeshaji inadharau kichwa cha familia kwa kuonyesha kwamba anastahili tu kudhihakiwa na hapaswi kuheshimiwa. Hata hivyo, Maandiko yanaonyesha kwamba mume ana madaraka mazito, na kwamba yeye ndiye “kichwa cha mke wake.”—Efe. 5:23; 1 Kor. 11:3.

17. Eleza jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunachukua madaraka yetu kwa uzito tunaposhiriki katika ibada ya familia.

17 Huenda mume akaandalia familia yake mahitaji ya kimwili. Lakini asipotoa mwongozo wa kiroho, ataonyesha kwamba hana busara na hekima. (Kum. 6:6, 7) Hivyo, andiko la 1 Timotheo 3:4 linasema kwamba ikiwa wewe ni kichwa cha familia na unajitahidi kufikia mapendeleo zaidi katika kutaniko, ni lazima uwe “mwanamume anayeisimamia nyumba yake mwenyewe kwa njia nzuri, mwenye watoto wanaojitiisha pamoja na kuchukua mambo kwa uzito wote.” Kuhusu jambo hilo, jiulize hivi: ‘Je, ninatenga kwa ukawaida wakati wa kuwa na ibada ya familia katika nyumba yangu?’ Wake fulani Wakristo wanalazimika kuwasihi sana waume wao ili waongoze katika mambo ya kiroho. Kila mume anapaswa kuchunguza kwa uzito jinsi anavyoliona daraka hilo. Bila shaka, mke Mkristo anapaswa kuunga mkono mpango wa Ibada ya Familia na kushirikiana na mume wake ili kuufanikisha.

18. Watoto wanaweza jinsi gani kujifunza kuchukua mambo kwa uzito?

18 Watoto pia wanatiwa moyo wafikirie kwa uzito maisha yao. (Mhu. 12:1) Hakuna ubaya kwa watoto wadogo kujifunza kufanya kazi kwa bidii nyumbani kulingana na umri na uwezo wao. (Omb. 3:27) Mfalme Daudi alipokuwa kijana mdogo, alijifunza kuwa mchungaji mwema. Pia, alijifunza kuwa mwanamuziki na mtungaji wa nyimbo, ustadi ambao ulimwezesha kumtumikia mtawala wa Israeli. (1 Sam. 16:11, 12, 18-21) Bila shaka, akiwa kijana mdogo, Daudi alijua kucheza michezo mbalimbali, lakini pia alijifunza ustadi wenye thamani sana ambao alitumia baadaye kumsifu Yehova. Ustadi wake akiwa mchungaji ulimsaidia kuliongoza taifa la Israeli kwa subira. Ninyi vijana, mnajifunza ustadi gani mbalimbali wenye faida ambao utawasaidia kumtumikia Muumba wenu na kuwatayarisha kutimiza madaraka wakati ujao?

Kuendelea Kuwa na Maoni Yenye Usawaziko

19, 20. Umeazimia kuendelea kuwa na mtazamo gani wenye usawaziko kujihusu wewe mwenyewe na ibada yako?

19 Sote tunaweza kujitahidi kuwa na maoni yenye usawaziko kujihusu sisi wenyewe, na kutojiona kuwa watu wasiotaka mzaha wowote. Hatungetaka kamwe kuwa ‘waadilifu kupita kiasi.’ (Mhu. 7:16) Ucheshi kidogo unaweza kuondoa hali ya wasiwasi nyumbani, kazini, au tunaposhughulika na ndugu na dada zetu Wakristo. Washiriki wa familia wanapaswa kuwa waangalifu ili wasiwachambue-chambue wengine kupita kiasi na hivyo kuvuruga amani na utulivu unaopaswa kuwa nyumbani. Katika kutaniko, wote wanaweza kujifunza kucheka pamoja na kufurahia ushirika, huku wakizungumza na kufundisha mambo mazuri yenye kujenga.—2 Kor. 13:10; Efe. 4:29.

20 Tunaishi katika ulimwengu ambao haumthamini Yehova au kuchukua sheria zake kwa uzito. Kinyume chake, watu wa Yehova wanahangaikia sana kumtii Mungu wao na kuwa washikamanifu kwake. Inafurahisha kama nini kuwa sehemu ya ushirika huo mkubwa wa watu ambao wanamwabudu Yehova “kwa uzito wote”! Na tuazimie kuendelea kuchukua kwa uzito maisha na ibada yetu.

Ungesema Nini?

• Kwa nini tunapaswa kuepuka mtazamo wa ulimwengu wa kutafuta kwanza raha maishani?

• Tunaweza jinsi gani kuwa wenye shangwe na wakati huohuo kuchukua kwa uzito huduma yetu?

• Maoni yetu kuhusu kukubali mapendeleo yanaonyesha jinsi gani ikiwa tunachukua mambo kwa uzito au hapana?

• Eleza kwa nini kuwaheshimu ndugu zetu na washiriki wetu wa familia ni jambo zito sana.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ni lazima mume aiandalie familia yake mahitaji ya kimwili na ya kiroho