Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fanya Maamuzi Ambayo Yanamletea Mungu Heshima

Fanya Maamuzi Ambayo Yanamletea Mungu Heshima

Fanya Maamuzi Ambayo Yanamletea Mungu Heshima

“Mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—MET. 14:15.

1, 2. (a) Hangaiko letu kuu linapaswa kuwa nini tunapofanya maamuzi yoyote yale? (b) Tutachunguza maswali au maulizo gani?

INAELEKEA kwamba tunafanya maamuzi mengi sana kila siku. Na matokeo mengi ya maamuzi hayo ni ya muda mfupi tu. Hata hivyo, maamuzi mengine yanaweza kuwa na matokeo makubwa sana katika maisha yetu. Katika maamuzi yoyote tunayofanya, yawe makubwa au madogo, hangaiko letu kuu ni kumheshimu Mungu.—Soma 1 Wakorintho 10:31.

2 Je, unaona kwamba ni rahisi au ni vigumu kwako kufanya maamuzi? Ili tufanye maendeleo na kuwa Wakristo wakomavu, ni lazima tujifunze kutofautisha kati ya yaliyo sawa na yaliyo makosa kisha tufanye maamuzi ambayo yanategemea usadikisho wetu wenyewe, wala si usadikisho wa mtu mwingine. (Rom. 12:1, 2; Ebr. 5:14) Ni sababu gani nyingine zinazotuchochea tujifunze kufanya maamuzi mazuri? Kwa nini nyakati nyingine ni vigumu sana kufanya maamuzi mazuri? Na ni hatua gani tunazoweza kuchukua ili kuhakikisha kwamba maamuzi tunayofanya yanamletea Mungu heshima?

Kwa Nini Unapaswa Kufanya Maamuzi?

3. Hatupaswi kuruhusu mambo gani yavuruge uwezo wetu wa kufanya maamuzi?

3 Tukisitasita kufanya maamuzi inapohusu viwango vya Biblia, huenda wanafunzi au wafanyakazi wenzetu wakakata kauli kwamba hatusadiki kabisa mambo tunayoamini na hivyo ni rahisi kushawishiwa. Huenda wakasema uwongo, kutumia udanganyifu, au kuiba na kisha kujaribu kutushawishi ‘tuufuate umati’ kwa kujiunga nao au kuficha mambo wanayofanya. (Kut. 23:2) Hata hivyo, mtu anayejua jinsi ya kufanya maamuzi ambayo yanamletea Mungu heshima hataruhusu woga au tamaa ya kukubaliwa na wengine imfanye ajiendeshe kwa njia inayopingana na dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia.—Rom. 13:5.

4. Kwa nini huenda wengine wakataka kutufanyia maamuzi?

4 Si watu wote wanaotaka kutufanyia maamuzi wana nia ya kutuumiza. Marafiki wenye nia nzuri wanaweza kusisitiza kwamba tufuate mashauri yao. Ikiwa tunaishi mbali na nyumbani, inaelekea kwamba watu wetu wa ukoo bado wanahangaikia sana hali yetu njema na wanaweza kuhisi kwamba wana daraka la kuendelea kutusaidia kufanya maamuzi ya maana. Kwa mfano, fikiria kuhusu matibabu. Biblia inakataza waziwazi matumizi mabaya ya damu. (Mdo. 15:28, 29) Hata hivyo, Biblia haisemi waziwazi kuhusu mambo mengine yanayohusu utunzaji wa afya na hivyo kila mmoja wetu anahitaji kujiamulia mwenyewe matibabu ambayo atakubali au kukataa. * Huenda wapendwa wetu wakashikilia sana maoni fulani kuhusu mambo hayo. Hata hivyo, tunapoamua mambo hayo, kila Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa anahitaji kubeba ‘mzigo wake mwenyewe’ wa daraka. (Gal. 6:4, 5) Hangaiko letu kuu ni kuendelea kuwa na dhamiri njema mbele za Mungu, si wanadamu.—1 Tim. 1:5.

5. Tunaweza kufanya nini ili imani yetu isivunjike?

5 Kusitasita kufanya maamuzi kunaweza kutuingiza katika hatari kubwa sana. Mwanafunzi Yakobo aliandika kwamba mtu anayesitasita ‘hayuko imara katika njia zake zote.’ (Yak. 1:8) Kama mtu aliye katika mashua ambayo haina usukani katika bahari yenye dhoruba, atarushwa huku na huku na maoni ya kibinadamu yanayobadilika-badilika. Ni rahisi kama nini kwa imani ya mtu kama huyo kuvunjika na kisha awalaumu watu wengine kwa sababu ya hali yake yenye kuhuzunisha! (1 Tim. 1:19) Tunaweza kuepuka matokeo hayo jinsi gani? Ni lazima ‘tuimarishwe katika imani.’ (Soma Wakolosai 2:6, 7.) Ili tuwe imara, tunahitaji kujifunza kufanya maamuzi ambayo yanaonyesha kwamba tunaamini Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake. (2 Tim. 3:14-17) Hata hivyo, ni nini kinachoweza kudhoofisha uwezo wetu wa kufanya maamuzi mazuri?

Kwa Nini Inaweza Kuwa Vigumu Kufanya Maamuzi?

6. Woga unaweza kuwa na matokeo gani mabaya juu yetu?

6 Woga unaweza kutuzuia kufanya maamuzi—tunaweza kuogopa kufanya uamuzi usiofaa, tunaweza kuogopa kushindwa, au kuogopa kwamba wengine watatuona kuwa wapumbavu. Mahangaiko hayo yanaeleweka. Hakuna mtu anayetaka kufanya uamuzi mbaya, ambao unasababisha matatizo na labda kuleta aibu. Hata hivyo, kumpenda Mungu na Neno lake kunaweza kutusaidia kushinda woga wetu. Kwa njia gani? Kumpenda Mungu kutatuchochea sikuzote kuchunguza Neno lake na vichapo vinavyotegemea Biblia kabla ya kufanya maamuzi ya maana. Tukifanya hivyo hatutafanya makosa mengi. Kwa nini? Kwa sababu Biblia inaweza “kuwapa werevu wale wasio na uzoefu, kumpa kijana ujuzi na uwezo wa kufikiri.”—Met. 1:4.

7. Mfano wa Mfalme Daudi unaweza kutufundisha nini?

7 Je, sikuzote tutafanya maamuzi yanayofaa? Hapana. Sisi sote tunafanya makosa. (Rom. 3:23) Kwa mfano, Mfalme Daudi alikuwa mwanamume mwenye hekima na mwaminifu. Lakini, nyakati nyingine alifanya maamuzi yasiyofaa ambayo yalimfanya yeye na wengine wateseke. (2 Sam. 12:9-12) Hata hivyo, Daudi hakuacha makosa yake yamzuie kufanya maamuzi yaliyomletea kibali cha Mungu. (1 Fal. 15:4, 5) Hata ikiwa zamani tulifanya makosa, tunaweza kufanya maamuzi mazuri, tukikumbuka kama Daudi kwamba Yehova hatakazia fikira makosa yetu na atasamehe dhambi zetu. Yehova ataendelea kuwategemeza wale ambao wanampenda na kumtii.—Zab. 51:1-4, 7-10.

8. Tunajifunza nini kutokana na maelezo ya mtume Paulo kuhusu ndoa?

8 Tunaweza kupunguza woga tulio nao wa kufanya maamuzi. Jinsi gani? Kwa kutambua kwamba nyakati nyingine kuna maamuzi mbalimbali yanayofaa ambayo tunaweza kuchagua. Fikiria jinsi mtume Paulo alivyoeleza kuhusu ndoa. Aliandika hivi chini ya mwongozo wa roho takatifu: “Kama yeyote akiona kwamba anajiendesha isivyofaa kuelekea ubikira wake, ikiwa huo umepita upeo wa ujana, na hivyo ndivyo inavyopaswa kutendeka, acheni afanye lile analotaka; hafanyi dhambi. Acheni afunge ndoa. Lakini ikiwa yeyote ametulia katika moyo wake, akiwa hana uhitaji wowote, lakini ana mamlaka juu ya nia yake mwenyewe naye amefanya uamuzi huu katika moyo wake mwenyewe, kutunza ubikira wake mwenyewe, yeye atafanya vema.” (1 Kor. 7:36-38) Paulo alipendekeza useja kuwa jambo bora, lakini hilo halikuwa jambo pekee linalofaa la kuchagua.

9. Je, tunapaswa kuhangaika kuhusu jinsi wengine wanavyoona maamuzi yetu? Eleza.

9 Je, tunapaswa kuhangaika kuhusu jinsi wengine wanavyoona maamuzi tunayofanya? Ndiyo, tunapaswa kuhangaika kwa kadiri fulani. Ona yale ambayo Paulo alisema kuhusu kula vyakula ambavyo vilionekana kuwa vimetolewa dhabihu kwa sanamu. Alikubali kwamba si lazima uamuzi wenyewe uwe mbaya, lakini unaweza kumuumiza mtu mwingine mwenye dhamiri ambayo ni dhaifu. Paulo aliazimia nini? Aliandika hivi: “Ikiwa chakula kinamkwaza ndugu yangu, mimi sitakula nyama tena kamwe, ili nisije nikamkwaza ndugu yangu.” (1 Kor. 8:4-13) Sisi pia tunahitaji kufikiria jinsi maamuzi yetu yatavyokuwa na uvutano juu ya dhamiri za wengine. Bila shaka, hangaiko letu kuu ni matokeo ya maamuzi yetu juu ya urafiki wetu pamoja na Yehova. (Soma Waroma 14:1-4.) Ni kanuni gani za Biblia zitakazotusaidia kufanya maamuzi ambayo yanamletea Mungu heshima?

Hatua Sita za Kufanya Maamuzi Mazuri

10, 11. (a) Tunaweza kuepuka jinsi gani kuwa na kimbelembele katika familia? (b) Wazee wanapaswa kukumbuka nini wanapofanya maamuzi ambayo yanahusu kutaniko?

10 Epuka kimbelembele. Kabla ya kuamua jambo la kufanya, tunahitaji kujiuliza, ‘Je, nina mamlaka ya kufanya uamuzi huu?’ Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Je, kimbelembele kimekuja? Basi aibu itakuja; lakini wenye kiasi wana hekima.”—Met. 11:2.

11 Wazazi wanaweza kuwapa watoto wao uhuru wa kufanya maamuzi fulani, lakini watoto hawapaswi kujichukulia mamlaka hayo. (Kol. 3:20) Wake na akina mama wana mamlaka ya kadiri fulani katika familia lakini ni vizuri watambue ukichwa wa waume wao. (Met. 1:8; 31:10-18; Efe. 5:23) Vivyo hivyo, waume wanahitaji kutambua kwamba mamlaka yao ina mipaka na kwamba wako chini ya Kristo. (1 Kor. 11:3) Wazee wanafanya maamuzi ambayo yanahusu kutaniko. Hata hivyo, wanahakikisha kwamba ‘hawapiti mambo yaliyoandikwa’ katika Neno la Mungu. (1 Kor. 4:6) Pia, wanafuata kwa makini mwongozo ambao wanapokea kutoka kwa mtumwa mwaminifu. (Mt. 24:45-47) Tunaweza kujiokoa wenyewe na kuwaokoa wengine wasipatwe na mahangaiko na huzuni kubwa tukiwa wenye kiasi na kufanya maamuzi ikiwa tu tumepewa mamlaka ya kufanya hivyo.

12. (a) Kwa nini tunapaswa kufanya utafiti? (b) Eleza jinsi mtu anavyoweza kujifanyia utafiti.

12 Fanya utafiti. Sulemani aliandika hivi: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida, lakini kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huuelekea uhitaji.” (Met. 21:5) Kwa mfano, unafikiria kuanzisha biashara? Usiongozwe na hisia zako. Kusanya habari zote zinazofaa, waombe mashauri wale ambao wanajua mambo kama hayo, na uchunguze kanuni za Biblia ambazo zinahusiana na jambo hilo. (Met. 20:18) Ili utayarishe utafiti wako, andika orodha mbili, orodha moja inapaswa kuonyesha faida, na orodha nyingine hasara. Kabla ya kufanya uamuzi, ‘hesabu gharama.’ (Luka 14:28) Fikiria jinsi uamuzi wako utakavyokuwa na matokeo si juu ya hali yako ya kifedha tu bali pia juu ya hali yako ya kiroho. Unahitaji wakati na jitihada ili kufanya utafiti. Lakini ukifanya hivyo, unaweza kuepuka kufanya maamuzi ya haraka ambayo yanaweza kusababisha mahangaiko yasiyo ya lazima.

13. (a) Andiko la Yakobo 1:5 linatuhakikishia nini? (b) Kusali ili tupate hekima kunaweza kutusaidia jinsi gani?

13 Sali ili upate hekima. Maamuzi yetu yatamletea Mungu heshima ikiwa tu tutamwomba atusaidie kuyafanya. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” (Yak. 1:5) Hatupaswi kuona aibu kukubali kwamba tunahitaji hekima ya Mungu ili itusaidie kufanya maamuzi. (Met. 3:5, 6) Bila shaka, kutegemea tu uelewaji wetu wenyewe kunaweza kwa urahisi kutuongoza vibaya. Tunaposali ili tupate hekima na tunapochunguza kanuni za Neno la Mungu, tunaruhusu roho takatifu itusaidie kutambua nia yetu halisi ya kutaka kuchukua hatua fulani.—Ebr. 4:12; soma Yakobo 1:22-25.

14. Kwa nini tunapaswa kuepuka kungoja-ngoja kufanya uamuzi?

14 Fanya uamuzi. Usikimbilie kufanya uamuzi kabla ya kufanya utafiti na kusali ili upate hekima. Mtu mwenye hekima anachukua muda wa ‘kufikiria hatua zake.’ (Met. 14:15) Kwa upande mwingine, usiahirishe au kungoja-ngoja kufanya uamuzi. Mtu anayengoja-ngoja kufanya uamuzi anaweza kutoa visingizio vya kushangaza vya kutochukua hatua. (Met. 22:13) Lakini hata asipochukua hatua bado anafanya uamuzi, ni kana kwamba anaamua kuacha wengine waongoze maisha yake.

15, 16. Ni nini kinachohusika katika kutekeleza uamuzi?

15 Timiza au tekeleza uamuzi wako. Jitihada zetu katika kufanya uamuzi mzuri zinaweza kuwa za bure ikiwa hatufuatilii uamuzi huo na kuutekeleza kwa bidii. Sulemani aliandika hivi: “Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote.” (Mhu. 9:10) Ili ufanikiwe, ni lazima uwe tayari kutafuta vitu unavyohitaji ili kutekeleza maamuzi yako. Kwa mfano, huenda mhubiri wa kutaniko akaamua kufanya upainia. Je, atafanikiwa? Inaelekea kwamba atafanikiwa ikiwa hatatumia nguvu zake zote katika kazi ya kimwili ya ziada na vitumbuizo hivi kwamba akose wakati ambao anahitaji kutimiza huduma yake.

16 Kwa kawaida, si rahisi kutekeleza maamuzi yaliyo bora. Kwa nini? Kwa sababu “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yoh. 5:19) Ni lazima tushindane mweleka juu ya “watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Efe. 6:12) Mtume Paulo na pia mwanafunzi Yuda walisema kwamba wale ambao wanaamua kumheshimu Mungu watakuwa na pigano.—1 Tim. 6:12; Yuda 3.

17. Inapohusu maamuzi tunayofanya, Yehova anatazamia nini kutoka kwetu?

17 Chunguza tena uamuzi wako na ufanye marekebisho yanayohitajiwa. Si maamuzi yote yanayofanikiwa kama ilivyopangwa. “Wakati na tukio lisilotazamiwa” linatupata sote. (Mhu. 9:11) Hata hivyo, Yehova anatutazamia tuendelee kuvumilia matokeo ya maamuzi fulani hata tukipatwa na majaribu. Mtu hawezi kubadili uamuzi wake wa kujiweka wakfu kwa Yehova au kufanya nadhiri ya ndoa. Mungu anatutazamia tuishi kulingana na maamuzi kama hayo. (Soma Zaburi 15:1, 2, 4.) Hata hivyo, maamuzi mengi si magumu sana. Mtu mwenye hekima atachunguza mara kwa mara maamuzi ambayo amefanya. Hataacha kiburi au ukaidi umzuie kurekebisha au hata kubadili uamuzi fulani. (Met. 16:18) Hangaiko lake kuu ni kuhakikisha kwamba maisha yake yanaendelea kumletea Mungu heshima.

Kuwazoeza Wengine Kufanya Maamuzi Yanayomletea Mungu Heshima

18. Wazazi wanaweza kuwazoeza watoto wao jinsi gani kufanya maamuzi mazuri?

18 Wazazi wanaweza kuwasaidia sana watoto wao kujifunza kufanya maamuzi yanayomletea Mungu heshima. Moja kati ya njia bora zaidi za kuwafundisha wengine ni kupitia mfano wetu. (Luka 6:40) Inapofaa, wazazi wanaweza kuwaeleza watoto wao hatua ambazo wao wenyewe walichukua ili kufanya uamuzi fulani. Wakipenda, wanaweza pia kuwaruhusu watoto wao wajifanyie maamuzi fulani na kisha wawapongeze wakati maamuzi hayo yanapofanikiwa. Hata hivyo, namna gani mtoto akifanya uamuzi mbaya? Mwanzoni, huenda mzazi akawa na mwelekeo wa kumzuia mtoto asipatwe na matokeo mabaya ya uamuzi wake, lakini nyakati nyingine kufanya hivyo huenda kusimsaidie mtoto. Kwa mfano, mzazi anaweza kumruhusu mtoto kuchukua leseni au kibali cha kuwa dereva. Tuseme kwamba mtoto huyo anavunja sheria za barabarani na kutozwa faini. Mzazi anaweza kuamua kulipa faini hiyo. Hata hivyo, ikiwa mtoto anaagizwa afanye kazi na kulipa faini hiyo, inaelekea sana kwamba atajifunza kuwa mwangalifu kuhusu jinsi anavyotenda.—Rom. 13:4.

19. Tunapaswa kuwafundisha wanafunzi wetu wa Biblia nini, na tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

19 Yesu aliwaambia wafuasi wake wawafundishe wengine. (Mt. 28:20) Moja kati ya masomo ya maana zaidi ambayo tunaweza kuwafundisha wanafunzi wa Biblia ni jinsi ya kufanya maamuzi mazuri. Ili kufanya hivyo kwa matokeo, ni lazima tuepuke mwelekeo wa kuwaambia jambo la kufanya. Itakuwa vizuri zaidi tukiwafundisha kutafakari kuhusu kanuni za Biblia ili waweze kujiamulia jinsi ya kutenda. Kwa kweli, “kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Rom. 14:12) Kwa hiyo, sisi sote tuna sababu nzuri za kufanya maamuzi yanayomletea Mungu heshima.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kwa mazungumzo zaidi kuhusu habari hii, ona nyongeza yenye kichwa “Nina Maoni Gani Kuhusu Visehemu vya Damu na Matibabu Yanayohusisha Damu Yangu Mwenyewe?” iliyochapishwa katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Novemba (Mwezi wa 11) 2006, ukurasa wa 3-6.

Ungesema Nini?

• Kwa nini tunahitaji kujifunza jinsi ya kufanya maamuzi?

• Woga unaweza kuwa na matokeo gani mabaya juu yetu, na tunaweza jinsi gani kushinda woga wetu?

• Ni hatua gani sita tunazoweza kuchukua ili kuhakikisha kwamba maamuzi yetu yanamletea Mungu heshima?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 16]

Hatua za Kufanya Maamuzi Mazuri

1 Epuka Kimbelembele

2 Fanya Utafiti

3 Sali ili Upate Hekima

4 Fanya Uamuzi

5 Timiza au Tekeleza Uamuzi Huo

6 Chunguza Tena na Ufanye Marekebisho

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mtu anayesitasita kufanya uamuzi ni kama mtu aliye katika mashua ambayo haina usukani katika bahari yenye dhoruba