Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Tunda la Roho’ Linamtukuza Mungu

‘Tunda la Roho’ Linamtukuza Mungu

‘Tunda la Roho’ Linamtukuza Mungu

“Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mwendelee kuzaa matunda mengi.”—YOH. 15:8.

1, 2. (a) Tuna nafasi gani mbalimbali za kuwatia wengine moyo? (b) Ni zawadi gani kutoka kwa Yehova ambayo inaboresha uwezo wetu wa kumtumikia?

 FIKIRIA hali hizi mbili: Mwanamke mmoja Mkristo anagundua kwamba dada mmoja kijana anaonekana anahangaishwa na jambo fulani. Dada huyo Mkristo anafanya mipango ili kuhubiri pamoja na yule dada kijana. Wanapozungumza huku wakihubiri nyumba kwa nyumba, dada huyo kijana anaanza kumweleza kile kinachomsumbua. Baadaye siku hiyo, mwanamke huyo kijana anamshukuru Yehova katika sala kwa sababu yule dada mkomavu alimjali kwa upendo; hilo ndilo jambo alilohitaji hasa. Katika kisa kingine, wenzi wawili wa ndoa wamerudi hivi karibuni kutoka nchi ya kigeni ambako walienda kuhubiri. Kwenye tafrija fulani, wenzi hao wanaposimulia kwa msisimko mambo yaliyoonwa, ndugu mmoja kijana anasikiliza kwa makini. Baada ya miaka fulani kupita, anapojitayarisha kwenda kwenye mgawo katika nchi ya kigeni, kijana huyo anafikiria wale wenzi wa ndoa na mazungumzo ambayo yalimchochea kuwa mmishonari.

2 Labda hali hizo zinakukumbusha mtu fulani ambaye alikuchochea kufanya uamuzi wa maana katika maisha yako au mtu ambaye ulimchochea abadili maisha yake. Bila shaka, si jambo la kawaida kwa mazungumzo ya pindi moja kubadili maisha ya mtu, lakini kila siku, tuna nafasi za kuwatia wengine moyo na kuwatia nguvu. Wazia ikiwa kungekuwa na jambo fulani ambalo lingeboresha uwezo na sifa zako, na hivyo kukufanya uwe mwenye faida zaidi kwa ndugu zako na katika utumishi wa Mungu. Je, hilo halingekuwa jambo zuri ajabu? Kwa kweli, Yehova anatupatia zawadi kama hiyo, yaani, roho yake takatifu. (Luka 11:13) Roho ya Mungu inapotenda kazi katika maisha yetu, inatokeza ndani yetu sifa nzuri sana ambazo zinaboresha kila sehemu ya utumishi wetu kwa Mungu. Hiyo ni zawadi nzuri ajabu kama nini!—Soma Wagalatia 5:22, 23.

3. (a) Tunamtukuza Mungu jinsi gani tunapositawisha ‘tunda la roho’? (b) Tutachunguza maswali gani?

3 Sifa ambazo roho takatifu inatokeza zinaonyesha utu halisi wa Chanzo cha roho hiyo, yaani, Yehova Mungu. (Kol. 3:9, 10) Yesu alionyesha sababu ya msingi inayopaswa kuwafanya Wakristo wajitahidi kumwiga Mungu alipowaambia mitume wake hivi: “Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mwendelee kuzaa matunda mengi.” * (Yoh. 15:8) Tunapositawisha ‘tunda la roho,’ matokeo yanaonekana wazi kupitia jinsi tunavyosema na kutenda; na hilo linamletea Mungu wetu sifa. (Mt. 5:16) Tunda la roho linatofautiana katika njia gani na tabia za ulimwengu wa Shetani? Tunaweza kusitawisha jinsi gani tunda la roho? Kwa nini inaweza kuwa vigumu kwetu kufanya hivyo? Tutachunguza maswali au maulizo hayo tunapozungumzia sifa tatu za kwanza za tunda la roho, yaani, upendo, shangwe, na amani.

Upendo Unaotegemea Kanuni ya Juu Zaidi

4. Yesu aliwafundisha wafuasi wake wawe na upendo wa aina gani?

4 Upendo unaotokezwa na roho takatifu ni tofauti sana na upendo ambao kwa kawaida unaonyeshwa katika ulimwengu. Jinsi gani? Unategemea kanuni ya juu zaidi. Yesu alikazia tofauti hiyo katika Mahubiri ya Mlimani. (Soma Mathayo 5:43-48.) Alitambua kwamba hata watenda-dhambi wana mwelekeo wa kuwatendea wengine kama wanavyotendewa. Mtu hahitaji kujidhabihu ili aonyeshe “upendo” huo, badala yake upendo huo unaonyeshwa kwa kubadilishana zawadi. Ikiwa tunataka ‘kuwa wana wa Baba yetu aliye mbinguni,’ ni lazima tuwe tofauti. Badala ya kuwatendea wengine kama wanavyotutendea, tunapaswa kuwaona na kuwatendea wengine kama Yehova anavyowaona na kuwatendea. Hata hivyo, tunaweza jinsi gani kuwapenda maadui wetu kama Yesu alivyoamuru?

5. Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunawapenda wale wanaotutesa?

5 Fikiria mfano mmoja wa Biblia. Walipokuwa wakihubiri huko Filipi, Paulo na Sila walikamatwa, wakapigwa vikali, na kutupwa gerezani, miguu yao ikiwa imefungwa. Wakati huo, huenda pia mlinzi wa gereza aliwatesa. Walipowekwa huru bila kutazamia baada ya tetemeko la nchi, je, walishangilia kwamba sasa wangeweza kujilipizia kisasi juu ya mtu huyo? Hapana. Hangaiko lao la kutoka moyoni kwa ajili ya mtu huyo, yaani, upendo wao wa kujidhabihu, uliwachochea kumsaidia haraka, na hilo likafanya mlinzi huyo wa gereza na familia yake yote wawe waamini. (Mdo. 16:19-34) Vivyo hivyo, katika nyakati zetu, ndugu zetu wengi wamekuwa ‘baraka kwa wale wanaowatesa.’—Rom. 12:14.

6. Tunaweza kuwaonyesha ndugu zetu upendo wa kujidhabihu katika njia gani? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 21.)

6 Upendo wetu kuelekea waamini wenzetu unatia ndani mambo mengi zaidi. “Sisi tuko chini ya wajibu kuzitoa nafsi zetu kwa ajili ya ndugu zetu.” (Soma 1 Yohana 3:16-18.) Hata hivyo, mara nyingi tunaweza kuonyesha upendo wetu katika njia ndogo zaidi. Kwa mfano, tukisema au kufanya jambo ambalo linamchukiza ndugu, tunaweza kuonyesha upendo kwa kuchukua hatua ya kurudisha amani. (Mt. 5:23, 24) Namna gani ikiwa mtu fulani anatukosea? Je, tuko “tayari kusamehe,” au nyakati nyingine tuna mwelekeo wa kuweka kinyongo? (Zab. 86:5) Upendo mwingi ambao unatokezwa na roho takatifu unaweza kutusaidia kufunika makosa madogo-madogo, na kuwasamehe wengine kwa hiari au kwa kupenda ‘kama vile Yehova alivyotusamehe sisi kwa hiari.’—Kol. 3:13, 14; 1 Pet. 4:8.

7, 8. (a) Kuna uhusiano gani kati ya kuwapenda watu na kumpenda Mungu? (b) Tunaweza kufanya nini ili tumpende Yehova zaidi? (Ona picha iliyo chini.)

7 Tunaweza kusitawisha jinsi gani upendo wa kujidhabihu kwa ajili ya ndugu zetu? Kwa kumpenda Mungu zaidi. (Efe. 5:1, 2; 1 Yoh. 4:9-11, 20, 21) Nyakati tunazotumia kuwa karibu na Yehova tunaposoma Biblia, kutafakari, na kusali zinajenga mioyo yetu na kutusaidia kumpenda zaidi Baba yetu wa mbinguni. Hata hivyo, tunahitaji kununua wakati ili kumkaribia Mungu.

8 Kwa mfano: Wazia ikiwa tungeweza kulisoma Neno la Mungu, kutafakari juu yake, na kusali kwa Yehova wakati fulani tu kila siku. Je, hungekuwa makini kulinda wakati huo ili jambo lolote lisivuruge wakati wako wa kuwa pamoja na Yehova? Bila shaka, hakuna mtu anayeweza kutuzuia tusisali kwa Mungu, na wengi wetu tunaweza kusoma Biblia wakati wowote tunaopenda. Hata hivyo, huenda tukahitaji kuchukua hatua fulani ili kuzuia shughuli nyingi za kila siku zisivuruge wakati wetu wa kuwa pamoja na Mungu. Je, unanunua wakati wa kutosha kila siku kumkaribia Yehova?

“Shangwe ya Roho Takatifu”

9. Shangwe inayotokezwa na roho takatifu ina uwezo gani?

9 Tunda la roho linatusaidia kudumisha utulivu hata tunapopambana na matatizo. Shangwe, sifa ya pili tutakayochunguza, inaonyesha kwamba tunaweza kudumisha utulivu. Shangwe ni kama mmea ambao unaweza kusitawi hata katika mazingira magumu. Duniani pote, watumishi wengi wa Mungu ‘wamelipokea neno chini ya dhiki nyingi pamoja na shangwe ya roho takatifu.’ (1 The. 1:6) Wengine wanapambana na hali ngumu na umaskini. Hata hivyo, Yehova anawatia nguvu kupitia roho yake “ili kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.” (Kol. 1:11) Ni nini chanzo cha shangwe hiyo?

10. Ni nini chanzo cha shangwe yetu?

10 Tofauti na “utajiri usio hakika” wa ulimwengu wa Shetani, hazina za kiroho ambazo tumepokea kutoka kwa Yehova zina thamani ya kudumu. (1 Tim. 6:17; Mt. 6:19, 20) Yehova ametupatia tumaini la kuishi milele wakati ujao ambalo linatuletea shangwe. Tuna shangwe ya kuwa sehemu ya undugu wa Kikristo wa ulimwenguni pote. Zaidi ya yote hayo, shangwe yetu inategemea uhusiano wetu pamoja na Mungu. Tunahisi kama Daudi, ambaye ingawa alilazimika kuishi kama mkimbizi, alimsifu Yehova katika wimbo, akisema: “Kwa sababu fadhili zako zenye upendo ni bora kuliko uzima, midomo yangu mwenyewe itakusifu. Kwa hiyo nitakusifu muda wote wa maisha yangu.” (Zab. 63:3, 4) Hata tukipatwa na hali ngumu, tunachochewa kumsifu Mungu kwa shangwe nyingi kutoka moyoni.

11. Kwa nini ni jambo la maana kumtumikia Yehova kwa shangwe?

11 Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo hivi: “Shangilieni sikuzote katika Bwana. Mara nyingine tena nitasema, Shangilieni!” (Flp. 4:4) Kwa nini ni jambo la maana kwa Wakristo kutimiza utumishi wao kwa Yehova wakiwa na shangwe? Kwa sababu ya suala ambalo Shetani alitokeza kuhusiana na enzi kuu ya Yehova. Shetani anadai kwamba hakuna mtu anayemtumikia Mungu kwa kupenda na kutoka moyoni. (Ayu. 1:9-11) Ikiwa tungemtumikia Yehova bila shangwe ili kutimiza wajibu tu, dhabihu yetu ya sifa haingekuwa kamili. Kwa hiyo, tunajitahidi kutii himizo hili la mtunga-zaburi: “Mtumikieni Yehova kwa kushangilia. Njooni mbele zake kwa vigelegele vya shangwe.” (Zab. 100:2) Utumishi unaotolewa kwa moyo wenye shangwe, na kwa kupenda unamletea Mungu utukufu.

12, 13. Tunaweza kufanya nini ili kushinda hisia zisizofaa?

12 Kwa kweli, nyakati nyingine, hata watumishi wa Yehova waliojitoa kwake wanavunjika moyo na wanapambana ili kudumisha mtazamo mzuri. (Flp. 2:25-30) Ni nini kinachoweza kutusaidia kuvumilia nyakati kama hizo? Andiko la Waefeso 5:18, 19 linasema hivi: “Endeleeni kujazwa na roho, mkijisemesha kwa zaburi na sifa kwa Mungu na nyimbo za kiroho, mkiimba na kupiga muziki katika mioyo yenu kwa Yehova.” Tunaweza kutumia jinsi gani shauri hilo?

13 Tunapolemewa na hisia zisizofaa, tunaweza kumsihi Yehova katika sala na kujitahidi kutafakari juu ya mambo yaliyo mazuri. (Soma Wafilipi 4:6-9.) Wengine wanaona kwamba kuimba kwa sauti ya chini nyimbo zetu za Ufalme zilizorekodiwa kunawachangamsha na kuwafanya wafikiri kwa njia nzuri. Ndugu mmoja ambaye alipambana na jaribu ambalo mara nyingi lilimwacha katika hali ya kufadhaika na kuvunjika moyo, anakumbuka hivi: “Zaidi ya kusali kwa ukawaida kutoka moyoni, nilishika akilini maneno ya nyimbo chache za Ufalme. Kuimba nikiwa peke yangu kimyakimya au kwa sauti nyimbo hizo nzuri sana za kumsifu Yehova kuliniletea amani moyoni. Pia, kitabu Mkaribie Yehova kilitolewa wakati huohuo. Nilikisoma chote mara mbili mwaka uliofuata. Kilikuwa kama mafuta yenye kutuliza moyoni mwangu. Ninajua Yehova alibariki jitihada zangu.”

Kifungo Chenye Kuunganisha cha Amani”

14. Amani inayotokezwa na roho takatifu inatokeza jambo gani la pekee?

14 Katika makusanyiko yetu ya kimataifa, wajumbe wenye malezi mbalimbali wanafurahia kushirikiana na ndugu na dada zao Wakristo. Ushirika kama huo wenye kufurahisha unaonyesha amani ambayo watu wa Mungu wanafurahia leo, yaani, umoja wa ulimwenguni pote. Mara nyingi watazamaji wanashangaa wanapoona watu ambao wanatazamia wawe maadui ‘wakijitahidi sana kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.’ (Efe. 4:3) Kwa kweli umoja huo ni wa pekee kwa sababu ya mambo ambayo wengi wao wamelazimika kushinda.

15, 16. (a) Petro alikuwa na malezi gani, na malezi yake yalimletea tatizo gani? (b) Yehova alimsaidia Petro jinsi gani kurekebisha mtazamo wake?

15 Si jambo rahisi kuwaunganisha watu wa malezi mbalimbali. Ili tuelewe vizuri mambo tunayohitaji kushinda ili kuwa na umoja huo, acheni tuchunguze mfano wa mtume Petro katika karne ya kwanza. Mtazamo wake kuwaelekea Watu wa Mataifa wasiotahiriwa unaweza kuonekana katika maneno yake yafuatayo: “Ninyi mnajua jinsi ilivyo kinyume cha sheria kwa Myahudi kujiunga na mtu wa jamii nyingine au kumkaribia; na bado Mungu amenionyesha sipaswi kumwita mtu yeyote kuwa najisi au si safi.” (Mdo. 10:24-29; 11:1-3) Akifuata maoni yaliyokuwa yameenea wakati huo, inaonekana kwamba tangu utotoni Petro aliamini kwamba Sheria ilimlazimisha kuwapenda Wayahudi wenzake tu. Huenda Petro alifikiri kwamba ni jambo la kawaida kabisa kuwaona Watu wa Mataifa kuwa maadui ambao walipaswa kuchukiwa. *

16 Hebu wazia jinsi Petro alivyohisi vibaya alipokuwa akiingia ndani ya nyumba ya Kornelio. Je, mtu aliyekuwa hapo zamani na maoni yasiyofaa kuhusu Watu wa Mataifa ‘angeunganishwa kwa upatano’ pamoja nao katika “kifungo chenye kuunganisha cha amani”? (Efe. 4:3, 16) Ndiyo, kwa kuwa siku chache mapema, roho ya Mungu ilikuwa imefungua moyo wa Petro, ikamwezesha kuanza kurekebisha mtazamo wake na kushinda maoni yake ya ubaguzi. Kupitia maono, Yehova alimwonyesha Petro wazi kwamba maoni ya Mungu kuhusu watu hayaamuliwi na jamii au taifa lake. (Mdo. 10:10-15) Hivyo, Petro alimwambia Kornelio hivi: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Mdo. 10:34, 35) Petro alibadilika, na akaungana kikweli na “ushirika mzima wa akina ndugu.”—1 Pet. 2:17.

17. Kwa nini umoja ambao watu wa Mungu wanafurahia ni wa pekee?

17 Kisa cha Petro kinatusaidia kuthamini mabadiliko makubwa ambayo yanafanyika kati ya watu wa Mungu leo. (Soma Isaya 2:3, 4.) Mamilioni ya watu “kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha” wamerekebisha njia yao ya kufikiri ili kuipatanisha na “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Ufu. 7:9; Rom. 12:2) Zamani, wengi wa watu hao waliongozwa na chuki, uadui, na migawanyiko ya ulimwengu wa Shetani. Lakini kwa kujifunza Neno la Mungu na kwa msaada wa roho takatifu, wamejifunza ‘kufuatilia mambo yanayofanya kuwe na amani.’ (Rom. 14:19) Umoja huo unamletea Mungu sifa.

18, 19. (a) Kila mmoja wetu anaweza kuchangia jinsi gani amani na umoja wa kutaniko? (b) Tutazungumzia nini katika habari inayofuata?

18 Kila mmoja wetu anaweza kuchangia jinsi gani amani na umoja wa watu wa Mungu? Makutaniko mengi yana watu kutoka nchi za kigeni. Huenda wengine wakawa na desturi tofauti au hawazungumzi lugha yetu vizuri. Je, tunajitahidi kuwajua? Neno la Mungu linatutia moyo tufanye hivyo. Akiliandikia kutaniko la Roma, ambalo lilikuwa na waamini Wayahudi na Watu wa Mataifa, Paulo alisema hivi: “Mkaribishane, kama vile Kristo pia alivyotukaribisha sisi, kwa kusudi la kumpa Mungu utukufu.” (Rom. 15:7) Je, kuna mtu yeyote katika kutaniko lenu ambaye unaweza kujitahidi kumjua vizuri zaidi?

19 Tunaweza kufanya jambo gani lingine ili kuruhusu roho takatifu ifanye kazi katika maisha yetu? Habari inayofuata itajibu swali hilo tunapozungumzia sifa zinazobaki za tunda la roho.

[Maelezo ya Chini]

^ Tunda ambalo Yesu alitaja linatia ndani ‘tunda la roho’ na “tunda la midomo” ambalo Wakristo wanamtolea Mungu kupitia kazi ya kuhubiri Ufalme.—Ebr. 13:15.

^ Andiko la Mambo ya Walawi 19:18 linasema hivi: “Usilipize kisasi wala usiwe na kinyongo juu ya wana wa watu wako; nawe mpende mwenzako kama wewe mwenyewe.” Viongozi wa dini ya Kiyahudi waliamini kwamba maneno “wana wa watu wako” na “mwenzako” yaliwahusu Wayahudi tu. Sheria iliwaagiza Waisraeli wajitenge na mataifa mengine. Hata hivyo, sheria haikuunga mkono maoni yaliyoenezwa na viongozi wa kidini wa karne ya kwanza, ya kwamba watu wote ambao hawakuwa Wayahudi walikuwa maadui na hivyo walipaswa kuchukiwa wakiwa mtu mmoja-mmoja.

Ungesema Nini?

• Tunaweza kuonyesha jinsi gani upendo wa kujidhabihu kuelekea ndugu zetu?

• Kwa nini ni jambo la maana kutimiza utumishi wetu kwa Mungu tukiwa wenye shangwe?

• Tunaweza kuchangia jinsi gani amani na umoja wa kutaniko?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

“Hawa Ndio Wakristo wa Kweli”

Kitabu kimoja (Between Resistance and Martyrdom—Jehovah’s Witnesses in the Third Reich) kina maelezo ya mfungwa mmoja kijana Myahudi, anayesema jinsi alivyokutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza baada ya kuwasili katika kambi ya mateso ya Neuengamme:

“Mara tu baada sisi Wayahudi kutoka Dachau kuwasili katika kambi hii, Wayahudi wengine walianza kuficha kila kitu walichokuwa nacho ili wasishiriki vitu vyao pamoja nasi. . . . Tulipokuwa nje [ya kambi ya mateso], tulikuwa tukisaidiana. Lakini hapa, katika hali ya kufa na kupona, jambo ambalo kila mmoja anahangaikia kwanza ni kujiokoa na kuwasahau wengine. Lakini fikiria jambo ambalo Wanafunzi wa Biblia walikuwa wakifanya. Wakati huo, walilazimika kufanya kazi ngumu sana ya kurekebisha mabomba fulani ya maji. Kulikuwa na baridi na walisimama siku nzima katika maji ya barafu. Hakuna mtu aliyeelewa jinsi walivyovumilia hali hiyo. Walisema kwamba Yehova anawapa nguvu za kuvumilia. Walihitaji sana mkate kama vile tulivyouhitaji, kwa sababu walikuwa na njaa. Lakini walikuwa wakifanya nini? Walikusanya mikate yote ambayo walikuwa nayo, wakala nusu ya mikate hiyo, na nusu iliyobaki wakawapa waamini wenzao ambao walikuwa wametoka tu kufika kutoka Dachau. Na waliwakaribisha na kuwabusu. Kabla ya kula, walisali. Baadaye, wote walikuwa wameshiba na walikuwa na furaha. Walisema kwamba hawakuwa na njaa tena. Unaona, huo ndio wakati nilipofikiria hivi: Hawa ndio Wakristo wa kweli.”

[Picha katika ukurasa wa 19]

Je, unanunua wakati kila siku kutoka kwa shughuli nyingine ili kumkaribia Yehova?