Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Unaruhusu Roho ya Mungu Ikuongoze?

Je, Unaruhusu Roho ya Mungu Ikuongoze?

Je, Unaruhusu Roho ya Mungu Ikuongoze?

“Roho yako ni nzuri; na iniongoze katika nchi ya unyoofu.”—ZAB. 143:10.

1, 2. (a) Taja pindi fulani ambazo Yehova alitumia roho takatifu kuwasaidia watumishi wake. (b) Je, roho takatifu inafanya kazi katika pindi za pekee tu? Eleza.

 NI JAMBO gani linalokuja akilini unapofikiria jinsi roho takatifu inavyofanya kazi? Je, unafikiria matendo yenye nguvu ya Gideoni na Samsoni? (Amu. 6:33, 34; 15:14, 15) Labda unafikiria ujasiri wa Wakristo wa mapema au utulivu wa Stefano aliposimama mbele ya Sanhedrini. (Mdo. 4:31; 6:15) Namna gani shangwe nyingi ambayo tunaiona leo kwenye makusanyiko yetu ya kimataifa, utimilifu wa ndugu zetu ambao wamefungwa gerezani kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote, na ongezeko kubwa la kazi ya kuhubiri? Mifano hiyo yote inaonyesha waziwazi jinsi roho takatifu inavyofanya kazi.

2 Je, roho takatifu inatenda kazi katika pindi za pekee au chini ya hali fulani tu zisizo za kawaida? Hapana. Neno la Mungu linasema kwamba Wakristo ‘wanatembea kwa roho,’ ‘wanaongozwa na roho,’ na ‘wanaishi kwa roho.’ (Gal. 5:16, 18, 25) Maneno yote hayo yanaonyesha kwamba roho takatifu inaweza kuendelea kuwa na uvutano katika maisha yetu. Kila siku, tunapaswa kumsihi Yehova aongoze njia yetu ya kufikiri, kusema, na kutenda akitumia roho yake takatifu. (Soma Zaburi 143:10.) Tunapoiruhusu roho hiyo itende kazi kwa uhuru katika maisha yetu, itatokeza ndani yetu tunda ambalo linawaburudisha wengine na hilo linamletea Mungu sifa.

3. (a) Kwa nini tunahitaji kuongozwa na roho takatifu? (b) Ni maswali gani tutakayozungumzia?

3 Kwa nini ni jambo la maana tuongozwe na roho takatifu? Kwa sababu kuna nguvu nyingine ambayo inataka kututawala, nguvu inayopingana na utendaji wa roho takatifu. Katika Maandiko, nguvu hiyo inaitwa “mwili,” yaani, mielekeo mibaya ya mwili wetu wenye dhambi, urithi wa kutokamilika ambao tumepokea tukiwa wazao wa Adamu. (Soma Wagalatia 5:17.) Ni nini basi kinachohusika katika kuiruhusu roho ya Mungu ituongoze? Je, kuna hatua fulani zinazofaa ambazo tunaweza kuchukua ili kupinga uvutano mbaya wa mwili wetu wenye dhambi? Acheni tuchunguze maulizo au maswali hayo tunapozungumzia sifa sita zinazobaki za ‘tunda la roho,’ yaani, “ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.”—Gal. 5:22, 23.

Sifa ya Upole na Ustahimilivu Zinaendeleza Amani Katika Kutaniko

4. Sifa ya upole na ustahimilivu zinasaidia jinsi gani kuleta amani katika kutaniko?

4 Soma Wakolosai 3:12, 13. Katika kutaniko, sifa ya upole na ustahimilivu zinaenda sambamba ili kuendeleza amani. Sifa hizo mbili za tunda la roho zinatusaidia kuwatendea wengine kwa fadhili, kubaki watulivu tunapochokozwa, na kuepuka kulipiza kisasi wakati wengine wanaposema au kututendea mambo mabaya. Tukikosana na Mkristo mwenzetu, kuwa na ustahimilivu, au subira, kutatusaidia tusiache kushirikiana na ndugu au dada yetu na badala yake kufanya yote tunayoweza ili kurudisha amani. Je, kweli sifa ya upole na ustahimilivu zinahitajiwa katika kutaniko? Ndiyo, kwa sababu sisi sote si wakamilifu.

5. Ni jambo gani lililotokea kati ya Paulo na Barnaba, na hilo linaonyesha nini?

5 Fikiria jambo lililotokea kati ya Paulo na Barnaba. Walikuwa wametumika bega kwa bega kwa miaka mingi ili kueneza habari njema. Kila mmoja wao alikuwa na sifa nzuri. Hata hivyo, pindi moja, ‘kulitokea hasira kali kati yao, hivi kwamba wakatengana.’ (Mdo. 15:36-39) Tukio hilo linaonyesha kwamba hata watumishi waliojitoa kabisa kwa Mungu, wanakosa kuelewana nyakati fulani. Ikiwa Mkristo anakosa kuelewana na mwamini mwenzake, anaweza kufanya nini ili kuzuia hali hiyo isiwe mbaya zaidi na kusababisha ugomvi ambao unaweza kufanya uhusiano wao uharibike kabisa?

6, 7. (a) Ni shauri gani la Kimaandiko tunaloweza kufuata kabla mazungumzo pamoja na mwamini mwenzetu hayajageuka na kuwa ugomvi mkali? (b) Kuna faida gani za ‘kuwa mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu’?

6 Maneno “kukatokea hasira kali,” yanaonyesha kwamba Paulo na Barnaba walikosana kwa ghafula na vibaya sana. Mkristo akigundua kwamba anapandwa na hasira anapozungumzia jambo fulani na mwamini mwenzake, ni jambo la hekima kutii shauri la Yakobo 1:19, 20: “Kila mtu lazima awe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu; kwa maana ghadhabu ya mwanadamu haitokezi uadilifu wa Mungu.” Ikitegemea hali, Mkristo huyo anaweza kujaribu kubadili mazungumzo, au kuzungumzia jambo hilo wakati mwingine, au anaweza kuomba kuondoka kabla mazungumzo hayajageuka na kuwa ugomvi mkali.—Met. 12:16; 17:14; 29:11.

7 Kuna faida gani za kufuata shauri hilo? Kwa kungoja hasira itulie, kusali kuhusu jambo hilo, na kwa kufikiria njia nzuri zaidi ya kujibu, Mkristo anaruhusu roho ya Mungu imwongoze. (Met. 15:1, 28) Chini ya mwongozo wa roho ya Mungu, anaweza kuonyesha upole na ustahimilivu. Hivyo, anakuwa tayari zaidi kutii shauri la Waefeso 4:26, 29: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi . . . Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu, bali neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa.” Kwa kweli, tunapovaa upole na ustahimilivu, tunachangia amani na umoja wa kutaniko.

Burudisha Familia Yako kwa Fadhili na Wema

8, 9. Fadhili na wema ni nini, na sifa hizo zina matokeo gani katika mazingira ya familia?

8 Soma Waefeso 4:31, 32; 5:8, 9. Fadhili na wema zinaburudisha kama upepo mtulivu na kinywaji baridi katika siku yenye joto. Sifa hizo zinachangia mazingira mazuri katika familia. Fadhili ni sifa yenye kuvutia ambayo inatokana na kupendezwa kikweli na wengine, na kuonyesha hivyo kwa matendo yenye faida na maneno yenye ufikirio. Wema, kama fadhili, ni sifa yenye kujenga ambayo inaonyeshwa kwa matendo yanayowafaidi wengine. Inaonyeshwa kwa kuwa na roho ya ukarimu. (Mdo. 9:36, 39; 16:14, 15) Lakini wema unatia ndani jambo lingine zaidi.

9 Wema ni kuwa na maadili au mwenendo bora. Unatia ndani si yale tu tunayofanya, bali jambo la maana hata zaidi, jinsi tulivyo. Fikiria mwanamke anayetayarisha tunda kwa ajili ya familia yake, anapolikata anachunguza kila kipande ili kuhakikisha kwamba ni tamu na limeiva lote, na halina kasoro ndani au nje. Vivyo hivyo, wema unaotokezwa na roho takatifu unaongoza kila sehemu ya maisha ya Mkristo.

10. Ni nini kinachoweza kufanywa ili kuwasaidia washiriki wa familia wasitawishe tunda la roho?

10 Katika nyumba ya Kikristo, ni nini kinachoweza kuwasaidia washiriki wa familia kutendeana kwa fadhili na wema? Ujuzi sahihi wa Neno la Mungu unatimiza sehemu ya maana. (Kol. 3:9, 10) Vichwa fulani vya familia wanaamua kujifunza pia kuhusu tunda la roho wakati wa jioni yao ya Ibada ya Familia kila juma. Si vigumu kujifunza kuhusu tunda la roho. Kwa kutumia vifaa vya kufanyia utafiti vinavyopatikana katika lugha yenu, chagueni habari kuhusu kila sifa ya tunda la roho. Mnaweza kuzungumzia mafungu machache kila juma, huku mkitumia majuma fulani kuzungumzia kila sifa. Mnapojifunza habari hizo, someni na kuzungumzia maandiko ambayo hayajanukuliwa. Zungumzieni njia za kutumia mambo mnayojifunza, na msali ili Yehova abariki jitihada zenu. (1 Tim. 4:15; 1 Yoh. 5:14, 15) Je, kweli funzo kama hilo linaweza kuwasaidia washiriki wa familia kutendeana kwa njia bora zaidi?

11, 12. Familia mbili za Kikristo zilifaidika jinsi gani kwa kujifunza pamoja kuhusu fadhili?

11 Wenzi wa ndoa vijana ambao walitaka kufanikiwa katika ndoa yao waliamua kujifunza kwa undani kuhusu tunda la roho. Wamefaidika jinsi gani? Mke anaeleza: “Kujifunza kwamba sifa ya fadhili inatia ndani uaminifu na ushikamanifu kumetusaidia kutendeana kwa njia nzuri zaidi mpaka leo. Tumejifunza kukubali maoni ya mwingine na pia kusameheana. Na tumejifunza pia kusema ‘asante’ na ‘pole’ inapofaa.”

12 Wenzi wengine wa ndoa Wakristo, ambao walikuwa na matatizo ya ndoa, walitambua kwamba hawakutendeana kwa fadhili katika uhusiano wao. Waliamua kujifunza pamoja kuhusu fadhili. Matokeo yalikuwa nini? Mume anakumbuka: “Kujifunza sifa ya fadhili kulitusaidia kuona uhitaji wa kuaminiana na kukazia fikira sifa nzuri za mwingine badala ya kuona kwamba ana nia mbaya. Kila mmoja wetu alianza kupendezwa zaidi na mahitaji ya mwenzake. Kuwa mwenye fadhili kulitia ndani kumwomba mke wangu aeleze kwa uhuru maoni yake bila kukasirishwa na mambo aliyosema. Hilo lilimaanisha kwamba nilihitaji kuacha kuwa mwenye kiburi. Tulipoanza kutendeana kwa fadhili katika ndoa yetu, tuliacha hatua kwa hatua tabia ya kujitetea. Tulijihisi huru kwelikweli.” Je, familia yenu itafaidika kwa kujifunza kuhusu tunda la roho?

Onyesha Imani Unapokuwa Faraghani

13. Tunapaswa kulinda hali yetu ya kiroho kutokana na hatari gani?

13 Wakristo wanahitaji kuruhusu roho ya Mungu iwaongoze hadharani na faraghani. Leo katika ulimwengu wa Shetani, picha chafu sana na vitumbuizo vyenye upotovu vimeenea kotekote. Hilo linahatarisha hali yetu ya kiroho. Mkristo anapaswa kufanya nini? Neno la Mungu linatushauri hivi: “Ondoeni uchafu wote na jambo lile lenye kuzidi, yaani, ubaya, na pokeeni kwa upole upandwaji wa neno lile linaloweza kuokoa nafsi zenu.” (Yak. 1:21) Acheni tuchunguze jinsi imani, ambayo ni sifa nyingine ya tunda la roho, inavyoweza kutusaidia kubaki safi mbele za Yehova.

14. Kukosa imani kunaweza jinsi gani kumwongoza mtu kwenye mwenendo mbaya?

14 Imani inamaanisha hasa kumwona Yehova Mungu kuwa halisi. Ikiwa Mungu si halisi kwetu, tunaweza kuanguka kwa urahisi kwenye mwenendo mbaya. Fikiria jambo ambalo liliwapata watu wa Mungu katika nyakati za kale. Yehova alimfunulia nabii Ezekieli kwamba mambo yenye kuchukiza yalikuwa yakifanywa faraghani, alisema: “Je, umeona, Ee mwana wa binadamu, mambo ambayo wazee wa nyumba ya Israeli wanafanya katika giza, kila mmoja katika vyumba vya ndani vya sanamu yake ya kuchongwa? Kwa maana wanasema, ‘Yehova hatuoni. Yehova ameiacha nchi hii.’” (Eze. 8:12) Je, umeona kile ambacho kilisababisha tatizo hilo? Hawakuamini kwamba Yehova alijua mambo waliyokuwa wakifanya. Yehova hakuwa halisi kwao.

15. Imani yenye nguvu katika Yehova inatulinda jinsi gani?

15 Kinyume na hilo, ona mfano wa Yosefu. Ingawa alikuwa mbali na familia yake na watu wake, Yosefu alikataa kufanya uasherati na mke wa Potifa. Kwa nini? Alisema hivi: “Ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?” (Mwa. 39:7-9) Ndiyo, Yehova alikuwa halisi kwa Yosefu. Ikiwa Mungu ni halisi kwetu hatutatazama vitumbuizo vichafu au kufanya jambo lingine lolote faraghani ambalo tunajua linamchukiza Mungu. Tutaazimia kama mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Nitatembea katika utimilifu wa moyo wangu ndani ya nyumba yangu. Sitaweka mbele ya macho yangu kitu chochote kisichofaa.”—Zab. 101:2, 3.

Linda Moyo Wako kwa Kuwa na Sifa ya Kujizuia

16, 17. (a) Kama inavyoelezwa katika kitabu cha Methali, “kijana ambaye amepungukiwa moyoni” alianguka jinsi gani katika dhambi? (b) Kama inavyoonyeshwa kwenye ukurasa wa 26, jambo kama hilo linaweza kutokea jinsi gani leo bila kujali umri wa mtu?

16 Kujizuia au kujidhibiti, sifa ya mwisho ya tunda la roho, inatuwezesha kukataa mambo ambayo Mungu analaumu. Inaweza kutusaidia kulinda moyo wetu. (Met. 4:23) Fikiria hali inayoelezwa katika andiko la Methali 7:6-23, kuhusu jinsi “kijana ambaye amepungukiwa moyoni” anavyoanguka katika kishawishi cha kahaba mmoja. Ananaswa na mtego baada ya ‘kupita barabarani, karibu na pembeni kwa mwanamke huyo.’ Labda alikuwa akitanga-tanga karibu na nyumba ya kahaba huyo kwa udadisi tu. Kwa ghafula, anakosa kutambua kwamba anaongozwa katika njia ya upumbavu na kwamba “nafsi yake mwenyewe inahusika.”

17 Kijana huyo angeepuka jinsi gani kosa hilo hatari? Kwa kutii onyo hili: “Usipotee na kuingia katika barabara zake.” (Met. 7:25) Hapa tunaweza kujifunza somo fulani: Ikiwa tunataka roho ya Mungu ituongoze, tunahitaji kuepuka kujiingiza wenyewe katika hali zenye kushawishi. Njia moja ambayo mtu anaweza kutanga-tanga kwenye njia ya upumbavu ya yule “kijana ambaye amepungukiwa moyoni” ni kwa kutazama-tazama bila kusudi vituo mbalimbali vya televisheni au kwenda huku na huku kwenye Intaneti. Iwe mtu anakusudia au hakusudii, anaweza kuona kwa ghafula picha zinazoamsha hamu ya ngono. Hatua kwa hatua anaweza kusitawisha zoea chafu la kutazama ponografia (picha au habari za ngono), na hivyo kuharibu kabisa dhamiri yake na uhusiano wake pamoja na Mungu. Anaweza pia kupoteza uhai wake.—Soma Waroma 8:5-8.

18. Mkristo anaweza kuchukua hatua gani ili kulinda moyo wake, na hatua hizo zinahusiana jinsi gani na kujizuia?

18 Bila shaka, tunaweza na tunapaswa kuonyesha sifa ya kujizuia kwa kuchukua hatua papo hapo picha chafu inapotokea kwa ghafula. Lakini itakuwa vizuri zaidi tukiepuka hali hiyo mapema! (Met. 22:3) Kujizuia kunatia ndani kujilinda kwa njia mbalimbali zinazofaa na kushikamana na njia hizo. Kwa mfano, kuweka kompyuta mahali panapoonekana wazi kunaweza kutulinda. Wengine wanaona ni vizuri kutumia kompyuta au kutazama televisheni ikiwa tu kuna watu wengine nyumbani. Wengine wameamua kutotumia Intaneti. (Soma Mathayo 5:27-30.) Basi na tuchukue hatua zozote za lazima ili kujilinda wenyewe na kuilinda familia yetu ili tuweze kumwabudu Yehova tukiwa na “dhamiri njema na kutokana na imani bila unafiki.”—1 Tim. 1:5.

19. Kuna faida gani za kuiruhusu roho takatifu ituongoze?

19 Tunda linalotokezwa kupitia utendaji wa roho takatifu linaleta faida nyingi. Sifa ya upole na ustahimilivu zinachangia amani katika kutaniko. Fadhili na wema zinaendeleza furaha katika familia. Kuwa na imani na kujizuia kunatusaidia kubaki karibu na Yehova na kuwa safi mbele zake. Zaidi ya hayo, andiko la Wagalatia 6:8 linatuhakikishia hivi: “Yeye anayepanda kwa roho atavuna uzima wa milele kutokana na roho.” Ndiyo, kwa msingi wa fidia au dhabihu ya ukombozi ya Kristo, Yehova atatumia roho takatifu ili kuwapa uzima wa milele wale ambao wanaruhusu roho takatifu iwaongoze.

Ungesema Nini?

• Sifa ya upole na ustahimilivu zinaendeleza jinsi gani amani katika kutaniko?

• Ni nini kinachoweza kuwasaidia Wakristo kuonyesha fadhili na wema nyumbani?

• Kuwa na imani na kujizuia kunaweza jinsi gani kumsaidia Mkristo kuulinda moyo wake?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 24]

Unaweza jinsi gani kuzuia mazungumzo yasigeuke na kuwa ugomvi mkali?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kujifunza kuhusu tunda la roho kunaweza kuifaidi familia yako

[Picha katika ukurasa wa 26]

Tunaepuka hatari gani kwa kuwa na imani na kujizuia?