Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unabii wa 2. Njaa

Unabii wa 2. Njaa

Unabii wa 2. Njaa

“Kutakuwa na upungufu wa chakula.”—MARKO 13:8.

● Mtu fulani amekimbilia kijiji cha Quaratadji, nchini Niger. Binamu zake na pia ndugu na dada zake, wamekimbilia kijiji hichohicho kutoka sehemu za ndani za nchi hiyo ili kuepuka njaa. Lakini, mtu huyo amelala chini kwenye mkeka akiwa peke yake. Kwa nini? “Hawezi kuilisha [familia yake], hivyo hawezi kuvumilia kutazama hali yao,” anaeleza Sidi, chifu wa kijiji hicho.

MAMBO ya HAKIKA YANAONYESHA NINI? Mtu 1 hivi kati ya kila watu 7 duniani hapati chakula cha kutosha kila siku. Hali ni mbaya hata zaidi katika nchi za Afrika zilizo kusini ya jangwa la Sahara, ambako mtu 1 kati ya kila watu 3 hapati chakula cha kutosha kwa kipindi kirefu. Ili upate kuelewa jambo hilo, fikiria familia yenye baba, mama, na mtoto. Ikiwa chakula kinachopatikana kinatosha tu watu wawili kati yao, ni nani hatakula? Baba, mama, au mtoto? Huo ndio uamuzi ambao familia kama hizo zinalazimika kufanya kila siku.

NI KIPINGAMIZI GANI KINACHOTOLEWA MARA NYINGI? Dunia inatokeza chakula cha kutosha kwa ajili ya kila mtu. Kinachohitajiwa tu ni kusimamia vizuri maliasili za dunia.

JE, KIPINGAMIZI HICHO KINA MSINGI? Ni kweli kwamba wakulima wanaweza kuzalisha na kusafirisha chakula kingi zaidi kuliko zamani. Nazo serikali za wanadamu zinaweza kutatua tatizo la njaa kwa kusimamia vizuri chakula kinachozalishwa duniani. Hata hivyo, kwa miaka mingi zimejaribu kufanya hivyo, lakini zimeshindwa.

UNA MAONI GANI? Je, andiko la Marko 13:8 linatimia? Ingawa hatua kubwa zimepigwa kuhusiana na mambo ya kiteknolojia, je, upungufu wa chakula bado unawaathiri watu duniani kote?

Mara nyingi, matetemeko ya nchi na njaa ni mambo yanayotangulia matatizo ambayo yanatokana na sehemu nyingine ya ishara ya siku za mwisho.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

“Zaidi ya asilimia 33 ya watoto wanaokufa kutokana na nimonia, kuhara, na magonjwa mengine hawangekufa ikiwa wangepata lishe bora.”​—ANN M. VENEMAN, ALIYEKUWA MKURUGENZI MKUU WA HAZINA YA WATOTO YA UMOJA WA MATAIFA.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 5]

© Paul Lowe/Panos Pictures