Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unabii wa 5. Kuharibiwa kwa Dunia

Unabii wa 5. Kuharibiwa kwa Dunia

Unabii wa 5. Kuharibiwa kwa Dunia

‘Mungu atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’—UFUNUO 11:18.

● Bw. Pirri ni mgemaji wa pombe ya mnazi huko Kpor, Nigeria. Biashara yake imeharibiwa na mafuta mengi yaliyomwagika kwenye delta ya Mto Niger. “Mafuta hayo yanaua samaki wetu, yanaharibu ngozi yetu, na kuchafua mito yetu,” Pirri anasema. “Sina njia nyingine ya kupata riziki.”

MAMBO ya HAKIKA YANAONYESHA NINI? Wataalamu fulani wanasema kwamba tani milioni 6.5 za takataka huingia baharini kila mwaka. Asilimia 50 hivi ya takataka hizo ni vifaa vya plastiki ambavyo vitaelea baharini kwa mamia ya miaka kabla ya kuoza. Kando na kuchafua dunia, wanadamu wanamaliza maliasili za dunia kwa kiwango kikubwa sana. Uchunguzi unaonyesha kwamba dunia huhitaji mwaka mmoja na miezi mitano ili kutokeza tena maliasili ambayo wanadamu hutumia kwa mwaka mmoja. “Ikiwa idadi ya watu na matumizi ya maliasili yatazidi kuongezeka, basi tutahitaji kuwa na Dunia mbili kufikia mwaka wa 2035,” linaripoti gazeti Sydney Morning Herald la Australia.

NI KIPINGAMIZI GANI KINACHOTOLEWA MARA NYINGI? Wanadamu wana akili na wanaweza kutatua matatizo yao kwa njia nzuri.

JE, KIPINGAMIZI HICHO KINA MSINGI? Vikundi mbalimbali na pia watu mmoja-mmoja wamejitahidi sana kuwaeleza watu umuhimu wa mazingira. Hata hivyo, dunia inaendelea kuchafuliwa kwa kiwango kikubwa sana.

UNA MAONI GANI? Je, kuna uhitaji wa Mungu kuingilia kati na kuiokoa dunia isiharibiwe—kama ambavyo ameahidi kufanya?

Kwa kuongezea mambo hayo matano ambayo yamezungumziwa kuhusu unabii, Biblia pia ilitabiri mambo mazuri ambayo yangetokea siku za mwisho. Ona mfano mmoja katika unabii wa sita.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

“Ninahisi kana kwamba nimepoteza paradiso na badala yake kumiliki rundo la takataka zenye sumu.”​—MANENO YA ERIN TAMBER, MKAAJI WA PWANI YA MAREKANI, KUHUSU MADHARA YA MAFUTA YALIYOMWAGIKA KWENYE GHUBA YA MEXICO, 2010.

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

Je, Tumlaumu Mungu?

Kwa kuwa Biblia ilitabiri hali mbaya tunazoona leo, je, hilo linamaanisha kuwa tunaweza kumlaumu Mungu kwa sababu ya hali hizo? Je, yeye ndiye anayesababisha mateso yanayotupata? Unaweza kupata majibu yenye kuridhisha ya maswali hayo katika sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]

U.S. Coast Guard photo