Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Wanaopenda Amani Watetea Jina Lao Zuri

Watu Wanaopenda Amani Watetea Jina Lao Zuri

TAARIFA KWA RAIA WA URUSI: Kwa kuchapisha habari zifuatazo, mamilioni ya watu katika nchi zaidi ya 230 watajua kuhusu kukandamizwa kwa uhuru wa kuabudu nchini Urusi bila sababu. Mnara wa Mlinzi ni gazeti linalochapishwa na kusambazwa kwa wingi zaidi ulimwenguni. Makala hii itapatikana katika lugha 188. Nakala zaidi ya milioni 40 zitachapishwa. Huenda baadhi ya watu wenye mamlaka hawatataka jumuiya ya kimataifa ijue mambo ambayo yanawapata Mashahidi wa Yehova nchini Urusi. Hata hivyo, maneno ya Yesu yatathibitika kuwa ya kweli: “Hakuna kitu kilichofunikwa kwa uangalifu ambacho hakitafunuliwa, na cha siri ambacho hakitajulikana.”—LUKA 12:2.

MNAMO Desemba (Mwezi wa 12) 2009 na Januari 2010, mahakama kuu mbili nchini Urusi zilitangaza kwamba Mashahidi wa Yehova wana msimamo mkali wa kidini. Inaonekana kama historia inajirudia yenyewe. Wakati serikali ya Sovieti ilipotawala Urusi, maelfu ya Mashahidi walishtakiwa kimakosa kwamba walikuwa maadui wa taifa. Walipelekwa uhamishoni, wakafungwa jela, na kulazimishwa kufanya kazi katika kambi za kazi ngumu. Baada ya utawala huo kuanguka, mashtaka dhidi ya Mashahidi wa Yehova yaliondolewa. Utawala huo mpya uliliondolea jina la Mashahidi lawama. * Hata hivyo, kwa mara nyingine tena, inaonekana kwamba watu fulani wameazimia kulichafua jina la Mashahidi.

Mapema mwaka wa 2009, wenye mamlaka walianza kushambulia uhuru wa kuabudu wa Mashahidi wa Yehova. Katika mwezi wa Februari (Mwezi wa 2) pekee, waendesha mashtaka walifanya uchunguzi kuhusu mambo tofauti-tofauti zaidi ya 500 kotekote nchini Urusi. Lengo la uchunguzi huo lilikuwa nini? Kuthibitisha madai ya kwamba Mashahidi wa Yehova ni wavunjaji sheria. Miezi iliyofuata, polisi walivamia mikutano iliyofanywa kwa amani katika Majumba ya Ufalme na katika nyumba za watu binafsi. Waliwanyang’anya vitabu na mali za kibinafsi. Wenye mamlaka waliwafukuza mawakili wa kigeni waliokuwa wakiwasaidia Mashahidi katika kesi yao na kuwazuia wasirudi tena katika nchi hiyo.

Mnamo Oktoba 5, 2009 (5/10/2009), maofisa wa forodha walishika shehena ya machapisho yanayotegemea Biblia mpakani, karibu na jiji la St. Petersburg. Machapisho hayo yalikuwa yamechapishwa nchini Ujerumani na yalikusudiwa kugawanywa katika makutaniko mbalimbali nchini Urusi. Kitengo maalumu cha forodha cha Urusi kinachoshughulikia bidhaa hatari zinazoingizwa kimagendo kilichunguza shehena hiyo. Kwa nini? Hati fulani ya serikali ilisema kwamba shehena hiyo “inaweza kuwa na bidhaa zilizokusudiwa kuchochea mgawanyiko wa kidini.”

Muda si muda unyanyasaji huo ulifikia kilele. Mahakama Kuu za Shirikisho la Urusi na Jamhuri ya Altay (ambayo ni sehemu ya Urusi) zilitangaza kwamba vitabu kadhaa vinavyochapishwa na Mashahidi, kutia ndani gazeti hili unalosoma, vinawachochea watu kuwa na msimamo mkali wa kidini. Mashahidi wa Yehova walikata rufaa mara kadhaa na mataifa mengi yakaeleza hangaiko lao kuhusu jinsi Mashahidi wanavyotendewa—lakini mahakama hazikubadili uamuzi wake! Kufikia sasa uamuzi huo haujabadilishwa, kwa hiyo, ni hatia nchini Urusi kuingiza au kusambaza machapisho hayo yanayotegemea Biblia.

Mashahidi wangefanya nini kuhusu jitihada hizo zinazowachafulia jina na hivyo kuzuia utendaji wao? Na uamuzi wa Mahakama unaonyesha nini kuhusu uhuru wa kidini wa kila raia wa Urusi?

Hatua ya Haraka Yachukuliwa Kukabili Hali Hiyo Inayozidi Kuwa Mbaya

Mnamo Ijumaa (Siku ya 5), Februari 26, 2010, Mashahidi wa Yehova wapatao 160,000 walianza kugawanya nakala milioni 12 za trakti ya pekee yenye kichwa Could It Happen Again? A Question for the Citizens of Russia. (Je, Itatokea Tena? Swali kwa Raia wa Urusi) Kwa mfano, huko Siberia katika jiji la Usol’ye-Sibirskoye, mamia ya Mashahidi walikusanyika katika mitaa kuanzia saa 11:30 asubuhi. Kati yao kulikuwa na wale waliokuwa wamepelekwa uhamishoni Siberia mwaka wa 1951 kwa sababu ya imani yao. Walivumilia baridi kali iliyokuwa nyuzi 40 Selsiasi chini ya sifuri ili kugawanya trakti 20,000 ambazo waligawiwa.

Ili kutangaza kampeni hiyo ya siku tatu, Mashahidi wa Yehova waliandaa mkutano na waandishi wa habari huko Moscow, mji mkuu wa Urusi. Kati ya wale waliokaribishwa kuzungumza ni Bw. Lev Levinson, mtaalamu kutoka katika Taasisi ya Kutetea Haki za Kibinadamu. Kwa ufupi alieleza jinsi Mashahidi wa Yehova walivyonyanyaswa na kuteswa na Wanazi huko Ujerumani na katika Muungano wa Sovieti, na hatua ya serikali ya kuondoa mashtaka dhidi ya Mashahidi. Pia alisema hivi: “Rais Yeltsin alitangaza kwamba waumini wa dini zote ambao waliteswa wakati wa utawala wa Sovieti waliondolewa lawama. Na walipaswa kurudishiwa kila kitu walichopoteza. Mashahidi wa Yehova hawakumiliki chochote wakati wa utawala wa Muungano wa Sovieti, lakini jina lao zuri liliondolewa lawama.

Kwa mara nyingine tena jina hilo zuri limo hatarini. “Katika nchi ileile ambayo ilionyesha kwamba inasikitishwa na yaliyotokea zamani,” akasema Bw. Levinson, “watu hawa wanateswa bila sababu yoyote.”

Watu Waguswa na Kampeni

Je, kampeni ya kugawanya trakti ilitimiza lengo lake? Bw. Levinson alisema, “Nilipokuwa nikija katika mkutano huu wa waandishi wa habari niliona watu katika gari moshi ambao walikuwa wameketi wakisoma trakti ambayo Mashahidi wa Yehova wanagawanya kotekote nchini Urusi leo. . . . Watu wameketi na kusoma trakti hiyo, na wanaisoma kwa makini.” * Kwa mfano, ona mambo yaliyoonwa yafuatayo.

Mwanamke mmoja mzee katika eneo lenye Waislamu wengi la Urusi ya kati alikubali trakti hiyo na kuuliza inazungumzia nini. Alipoambiwa inazungumzia haki za binadamu na uhuru nchini Urusi, alisema hivi: “Hatimaye mtu fulani ameyakazia uangalifu masuala haya! Kuhusu hayo, Urusi imekuwa ikirudia enzi za Muungano wa Sovieti. Asanteni sana. Mnafanya kazi nzuri!”

Mwanamke mwingine huko Chelyabinsk aliyeonyeshwa trakti hiyo alisema: “Tayari nimeipata na kuisoma. Ninawaunga mkono kabisa. Sijui kama kuna dini nyingine inayoweza kutetea imani yake kwa utaratibu kama dini yenu. Ninapenda jinsi mnavyovaa, na jinsi mnavyotumia busara nyakati zote. Ni wazi kwamba mnaamini kabisa mambo mnayofundisha. Ninaona kwamba Mungu yupo pamoja nanyi.”

Huko St. Petersburg, mwanamume mmoja ambaye alisema kwamba tayari amepata trakti aliulizwa kama alipendezwa na mambo aliyosoma. Alijibu, “Ndiyo. Nilipokuwa nikiisoma trakti hiyo, nilisisimuka na kutokwa na machozi. Nyanya yangu alikandamizwa [wakati wa utawala wa Sovieti] na aliniambia mengi kuhusu wale aliofungwa pamoja nao. Kulikuwa na wahalifu wengi, lakini pia kulikuwa na wale ambao hawakuwa na hatia lakini walifungwa kwa sababu ya imani yao. Ninafikiri kila mtu anapaswa kujua kilichotokea, hivyo, mnafanya jambo zuri.”

Hali Itakuwa Namna Gani Wakati Ujao Nchini Urusi?

Mashahidi wa Yehova nchini Urusi wanathamini uhuru ambao wamefurahia kwa miaka 20 iliyopita. Hata hivyo, wanajua kwamba wanaweza kunyang’anywa uhuru huo wakati wowote. Iwe kampeni ya hivi majuzi ya kuwachafulia Mashahidi jina inaonyesha kwamba Urusi inarudia kipindi kingine cha ukandamizaji au la, tutasubiri tuone.

Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wameazimia kuendelea na kazi yao ya kuhubiri ujumbe wa Biblia wa amani na tumaini, hata hali iwe namna gani. Trakti hiyo ya pekee inamalizia azimio lao hivi: “Ukandamizaji hautafanikiwa. Hatutaacha kusema kwa busara na kwa heshima kumhusu Yehova Mungu na Neno lake, Biblia. (1 Petro 3:15) Hatukuacha kufanya hivyo tulipokabili ukatili wa Ujerumani ya Nazi, wala hatukuacha wakati wa kipindi kigumu zaidi cha ukandamizaji katika nchi yetu, na hatutaacha wakati huu.—Matendo 4:18-20.”

^ fu. 13 Saa kadhaa kabla ya ule mkutano na waandishi wa habari, makutaniko ya Mashahidi wa Yehova huko Moscow yalikuwa yameanza kugawanya trakti hiyo.