Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuishi Milele Katika Paradiso Kutachosha?

Je, Kuishi Milele Katika Paradiso Kutachosha?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Kuishi Milele Katika Paradiso Kutachosha?

▪ Biblia inatoa tumaini la kwamba tunaweza kuishi milele katika Paradiso hapa duniani. (Zaburi 37:29; Luka 23:43) Je, kuishi milele katika mazingira makamilifu kutachosha?

Hilo ni swali la maana sana. Wachunguzi wamegundua kwamba mtu anapochoshwa na jambo fulani kwa muda mrefu, anaweza kuanza kuhangaika, kuvunjika moyo, na hata kushawishika kufanya mambo yanayoweza kuhatarisha uhai wake. Watu wasio na kusudi maishani au ambao wamechoshwa na mambo wanayofanya kila siku, huenda wakaanza kuchoka na maisha. Je, watu watakaoishi katika Paradiso watakosa kusudi? Je, mambo watakayokuwa wakifanya kila siku yatakuwa yenye kuchosha?

Kwanza, kumbuka kwamba ni Yehova Mungu, Mtungaji wa Biblia, anayetoa ahadi hiyo ya uzima wa milele. (Yohana 3:16; 2 Timotheo 3:16) Sifa kuu ya Mungu ni upendo. (1 Yohana 4:8) Yehova anatupenda sana na ametupa vitu vyote vizuri tunavyofurahia sasa.—Yakobo 1:17.

Muumba wetu anajua kwamba ili tuwe na furaha, tunahitaji kufanya kazi tukiwa na kusudi. (Zaburi 139:14-16; Mhubiri 3:12) Katika Paradiso watu wataishi maisha yenye kusudi na yenye kufurahisha. Kazi watakayofanya itawanufaisha wao wenyewe na wapendwa wao. (Isaya 65:22-24) Ikiwa ungekuwa na kazi ya wakati wote, yenye kupendeza, na yenye kuchangamsha, je, ungechoshwa na maisha?

Pia, kumbuka kwamba Yehova Mungu hataruhusu mtu yeyote tu aishi katika Paradiso. Anatoa zawadi ya uzima wa milele kwa wale tu wanaomwiga Mwana wake, Yesu. (Yohana 17:3) Alipokuwa duniani, Yesu alifurahia kufanya mapenzi ya Baba yake. Aliwafundisha wafuasi wake kwa maneno na kwa matendo kuwa furaha ya kudumu inatokana zaidi na kutoa kuliko kupokea. (Matendo 20:35) Katika Paradiso hiyo itakayorudishwa, watu wote wataishi kupatana na zile amri mbili kuu, yaani, kumpenda Mungu na kumpenda jirani. (Mathayo 22:36-40) Wazia ukiwa umezungukwa na watu wasio na ubinafsi, wanaokupenda, na wanaopenda kazi zao! Je, unafikiri utachoka kuishi na watu kama hao?

Maisha katika Paradiso yatahusisha mambo gani mengine? Kila siku tutaweza kujifunza jambo jipya kumhusu Muumba wetu. Tayari watafiti wamevumbua mambo mengi yenye kustaajabisha kuhusu uumbaji wa Yehova. (Waroma 1:20) Hata hivyo, kufikia sasa ni mambo machache tu tunayofahamu kuhusu uumbaji wa Yehova. Miaka mingi iliyopita, mwanamume mwaminifu Ayubu alichunguza mambo aliyojua kuhusu uumbaji wa Mungu, na mkataa aliofikia bado ni wa kweli. Ayubu alisema hivi: “Hizo ndizo kingo za njia zake, nao ni mnong’ono ulioje wa jambo lililosikiwa juu yake! Lakini kuhusu mngurumo wake wenye nguvu ni nani anayeweza kuonyesha uelewaji?”—Ayubu 26:14.

Hata tukiishi milele, hatutaweza kujua kila kitu kuhusu kazi za Yehova Mungu. Biblia inasema kwamba Mungu ameweka tamaa ya kuishi milele katika mioyo yetu. Lakini pia inasema kwamba hatutaweza “kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.” (Mhubiri 3:10, 11) Je, unafikiri utachoshwa na kujifunza mambo mapya kumhusu Muumba wako?

Hata leo, ni mara chache ambapo watu walio na shughuli nyingi za kuwasaidia wengine na kumletea Mungu utukufu, huhisi kuwa wamechoka. Tunaweza kuwa na hakika kwamba tukiwa na shughuli nyingi katika kazi kama hiyo, hatutawahi kuhisi tumechoshwa na maisha—hata kama tutaishi milele.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 27]

Earth: Image Science and Analysis Laboratory, NASA-Johnson Space Center; Galaxy: The Hubble Heritage Team (AURA/​STScI/​NASA)