Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

KWA nini mwimbaji maarufu aliacha uimbaji na kuwa mhudumu wa wakati wote wa dini? Na ni nini kilichomsaidia mhalifu ambaye hakimu alisema kwamba hawezi kubadilika, ageuke na kuwa raia mwema? Soma masimulizi haya ili upate majibu.

“Hakuna Anayeweza Kuwatumikia Mabwana Wawili.”​—ANTOLINA ORDEN CASTILLO

MWAKA WA KUZALIWA: 1962

NCHI: HISPANIA

HISTORIA: MWIGIZAJI NA MWIMBAJI WA ZARZUELA

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa katika kijiji kimoja kidogo cha Tresjuncos, katika eneo linaloitwa La Mancha. Familia yetu ilikuwa ya wakulima. Mama yangu alikuwa Mkatoliki, na baba yangu, Mprotestanti. Baba yangu alinifundisha kuiheshimu Biblia, na nilimwona akiisoma kila wakati. Lakini mama yangu alinifundisha imani ya kikatoliki na kunipeleka kuhudhuria Misa kila Jumapili (Siku ya Yenga).

Nilipokuwa na umri wa miaka 15, niliondoka nyumbani na kwenda kuishi katika jiji la Madrid pamoja na dada yangu mkubwa. Niliwakosa sana wazazi wangu lakini baada ya muda nikazoea hali hiyo. Nilipokuwa na umri wa miaka 17, nilipata nafasi ya kufanya kazi kwa miezi michache na kikundi kilichocheza zarzuela, mchezo wa kitamaduni wa kuimba na kuigiza wa Hispania. Nilifurahia sana maisha hayo hivi kwamba nilitaka kuwa mwigizaji. Niliacha kusomea usekretari na nikaanza kuimba pamoja na vikundi mbalimbali vya zarzuela. Wakati huo pia, nilikuwa nimeanza kuwa na uhusiano wa kimapenzi na ndugu ya mmoja wa rafiki zangu. Nilihisi kwamba nimebarikiwa kuwa na kazi nzuri, pesa, na mtu anayenipenda.

Nilianza kusafiri na vikundi mbalimbali vya zarzuela kotekote nchini Hispania na pia nchi nyingine, kama vile Ekuado, Kolombia, Kosta Rika, na Venezuela. Pia, niliimba na vikundi mbalimbali vidogo vilivyokuwa chini ya kikundi fulani maarufu cha muziki cha Madrid kilichoitwa “La movida madrileña.” Kikundi kimoja ambacho nilikuwa mwimbaji mkuu kilifanikiwa sana.

Nilipenda kazi yangu lakini sikupenda ukosefu wa maadili ulionizunguka. Hata hivyo, nikiwa mwimbaji maarufu, nilihangaikia sana jinsi watu walivyoniona. Nilianza kuwa mwangalifu sana kuhusu vyakula nilivyokula na hivyo nikapatwa na ugonjwa unaofanya mtu ajinyime chakula au kula na kujitapisha.

Hata hivyo, bado nilitamani sana kuwa mwigizaji. Mwishowe nilijiunga na shule moja jijini Madrid ili kujifunza sanaa ya uigizaji. Tulifundishwa kwamba mwigizaji anapaswa kufikiria kwa undani hisia za mtu anayemwiga na kufanya hisia hizo zitokee kihalisi. Nilipofanya hivyo, nilitambua kwamba jambo hilo lilifanya nipoteze hisia zangu kabisa. Nilikuwa mwanamke anayejifanya, na mwenye ubinafsi.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilijua kwamba ikiwa nilitaka kuwa na sifa nzuri, nilipaswa kujitahidi kuzikuza. Lakini sikujua nianzie wapi. Niliamua kwenda katika kanisa la kiinjilisti jijini Madrid ambalo niliwahi kwenda nikiwa na wazazi wangu. Nilisali kwa Mungu, nikitumia jina lake, Yehova.

Muda mfupi baadaye, Mashahidi wa Yehova wawili walinitembelea nyumbani kwangu. Nilizungumzia Biblia pamoja nao kwa hamu kubwa, lakini pia nilipinga mambo mengi waliyokuwa wakinifundisha. Esther, Shahidi niliyejifunza naye Biblia kwa ukawaida, alikuwa mwenye subira sana. Yeye na familia yake walinionyesha upendo na fadhili nyingi sana. Nilianza kuhudhuria mikutano iliyokuwa ikifanywa na Mashahidi na muda si muda nikatambua kwamba nimepata kweli ya Biblia niliyokuwa nikiitafuta.

Nilipomaliza tu mafunzo yangu katika sanaa ya uigizaji, nilipata nafasi nyingi za kazi. Nilipata nafasi ya kushiriki katika igizo ambalo lingeonyeshwa katika jumba maarufu la michezo ya kuigiza la Madrid. Lakini pia nilitambua kwamba ili niweze kufaulu nikiwa mwigizaji, nilihitaji kujihusisha kabisa katika sanaa hiyo. Hatimaye, niliamua kutafuta aina nyingine ya kazi ambayo ingeniruhusu kukazia fikira utumishi wangu kwa Mungu. Nilitambua ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda yule mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau yule mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.” (Mathayo 6:24) Mpenzi wangu ambaye tulikuwa na uhusiano kwa miaka minane hakufurahia mambo niliyojifunza, hivyo nikaamua kukatiza uhusiano huo. Haikuwa rahisi kufanya mabadiliko hayo yote.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Sasa ninafanya kazi ambayo si ya wakati wote, kazi ya kuwatumbuiza wazee. Kazi hiyo imeniwezesha kuwa na wakati mwingi wa kuwafundisha Biblia watu wanaoongea lugha ya Kiarabu katika eneo letu. Inanibidi nijitahidi sana kujifunza lugha hiyo mpya, lakini ninafurahia sana kuwaeleza watu, ambao ni wakarimu na wanaotaka kujifunza kumhusu Mungu, mambo ambayo nimejifunza.

Hali ya kukosa hisia iliyonipata wakati nilipokuwa nikijifunza kuwa mwigizaji sasa imeisha na badala yake nina kusudi maishani. Ninahisi kwamba Yehova amenisaidia kuwa mtu bora, na mwenye furaha.

‘Nimethibitisha Kwamba Hakimu Alikosea.’​—PAUL KEVIN RUBERY

MWAKA WA KUZALIWA: 1954

NCHI: UINGEREZA

HISTORIA: NILIKUWA JAMBAZI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa Dudley, mji mkubwa wenye viwanda ulio West Midlands. Tangu nilipokuwa mtoto, baba yangu alinifanya nipende kusoma. Pia, alinitia moyo nithamini vitu vya asili, ingawa alisema vilitokana na mageuzi. Alinifundisha kwamba hakuna Mungu. Hata hivyo, wazazi wangu walinipeleka katika shule ya Jumapili ya Methodisti.

Nilipokuwa na umri wa miaka minane, nilishuhudia wavulana fulani wakiteketeza mashua kwenye kijito kimoja katika eneo letu. Polisi walikuja, lakini nikaogopa kuwaambia ukweli kwa sababu wavulana hao walikuwa wamenitisha. Nilishtakiwa isivyo haki kuhusu tukio hilo na nikakasirika sana. Hivyo nikaamua kulipiza kisasi kwa kuvamia shule, makanisa, na viwanda na kuharibu mali yenye thamani ya maelfu ya pesa. Kufikia wakati nilipokuwa na umri wa miaka kumi nilikuwa nimeanza kuvamia nyumba na maduka ili kuiba. Nilisisimuka sana kuona moto hivyo nikaanza kuteketeza kimakusudi mali za watu. Shuleni, walimu walisema kwamba mimi ni mwanafunzi mtundu sana.

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilipata kitabu kilichoeleza mambo ya uchawi, na nikatengeneza ubao wangu wa kufanyia uaguzi. Kwa sababu wazazi wangu hawakuamini kwamba kuna Mungu, walifikiri kwamba mazoea yangu ya kishirikina hayakuwa na madhara yoyote, na kwamba huenda yangeniepusha na matatizo. Lakini kufikia wakati nilipomaliza shule, nilikuwa nimepelekwa mara kadhaa kwenye mahakama ya watoto. Nilikuwa nimejiunga na genge watu wenye jeuri walionyoa kipara. Nilibeba wembe na mnyororo wa baiskeli kama silaha zangu. Nilipata kazi lakini nikaipoteza kwa sababu nilifungwa kwa muda mfupi. Baada ya kuachiliwa, nilianza tena kuvamia mali za watu na nikashikwa na kufungwa gerezani kwa miaka miwili. Hakimu alisema kwamba tabia yangu haiwezi kubadilika na nilikuwa mtu hatari katika jamii.

Baada ya kutoka gerezani, nilikutana tena na rafiki yangu wa kike, Anita. Tulioana, na kwa muda fulani sikuiba wala kusababisha matatizo yoyote. Hata hivyo, miaka michache baadaye nilirudia maisha yangu ya uhalifu. Nilianza kuvunja maeneo ya biashara na kuiba vitu vya thamani vilivyohifadhiwa kwenye makasha. Nilianza kutumia dawa za kulevya, kunywa pombe kupita kiasi, na kubeba bunduki. Nilishikwa tena na kupelekwa gerezani.

Maisha yangu yalifanya Anita awe na mfadhaiko mwingi sana. Daktari wake alimpa dawa za kutuliza akili, lakini akamwambia alichohitaji ni talaka ili apone. Ninafurahi kwamba Anita hakufuata ushauri huo.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Tulipokuwa tu tumeoana, Anita alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova kwa muda mfupi. Kisha nilipokuwa gerezani kwa mara ya mwisho, akatembelewa tena na Mashahidi wa Yehova. Ilitukia kwamba Anita alitembelewa siku ileile niliposali kwa Mungu nikimwambia, “Nithibitishie kama upo.”

Miezi michache baada ya kutoka gerezani, niliwasiliana na kasisi wa eneo letu na kumwomba ajifunze Biblia pamoja nasi. Alisema kwamba anaweza tu kutufundisha mambo yanayohusu imani ya kanisa na sala.

Mwishowe nilianza kusoma Biblia. Nilishangaa kujifunza kwamba Biblia inakataza mambo ya ushirikina. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Baadaye nilipata gazeti la Mnara wa mlinzi ambalo Mashahidi walikuwa wamempa Anita siku ile niliposali kwa Mungu anisaidie. Mambo niliyosoma yalinisukuma niwasiliane na Mashahidi.

Familia zetu, rafiki zetu, na watu nilioshirikiana nao katika uhalifu hawakufurahi walipojua kwamba tulikuwa tunajifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Wengine walisema kwamba nilikuwa nikipumbazwa. Lakini kusema kweli, ubongo wangu ulihitaji kusafishwa. Utu wangu ulikuwa na kasoro nyingi, dhamiri yangu ilikuwa imekufa, na zaidi ya hayo nilivuta sigara 60 hivi kila siku. Mashahidi waliotusaidia kujifunza Biblia pamoja na wale tulioshirikiana nao kutanikoni, walikuwa wenye subira na wenye fadhili. Hatimaye, nilifaulu kuacha mazoea yangu mabaya.—2 Wakorintho 7:1.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Mimi na Anita tumekuwa katika kifungo cha ndoa kwa miaka 35 sasa. Mtoto wetu mmoja na wajukuu wawili wanamtumikia Yehova pamoja nasi. Miaka ya hivi karibuni, mimi na Anita tumekuwa tukitumia muda mwingi kuwasaidia watu wengine wajifunze Biblia.

Kumtumikia Yehova kumefanya maisha yetu yawe na kusudi na yenye maana. Mnamo mwaka wa 1970, hakimu mmoja alisema kwamba tabia yangu haiwezi kubadilika. Hata hivyo, kwa msaada wa Mungu na kwa kufuata mwongozo wa Biblia, nimethibitisha kwamba hakimu huyo alikosea.